Search This Blog

Friday, October 28, 2022

BEYOND PAIN - 2

 









    Simulizi :Beyond Pain

    Sehemu Ya Pili (2)





    “Karibu….Kar…karibuni…” Akatamka Chris huku akionekana kuogopa kwa namna nilivyomuangalia.Skumjibu kitu nikaendelea kumtazama.Sikutazamia kama ningepatwa na hasira za namna ile baada ya kumuona mtu ambaye awali alikuwa ni rafiki yangu mkubwa .Beka alitambua kwa haraka jinsi nilivyopandwa na hasira akanishika mkono na kuniketisha sofani.

    Hakuna mtu aliyeitikia salamu ya Chris.Wote tukaingia sebuleni na kukaa kimya kimya.Emmy alikuwa ameinama hakutaka kututazama usoni.

    “jamani karibuni sana..Chris akasema huku akiwa bado amesimama na mwenye wasi wasi mwingi.

    “Mnatumia vinywaji gani? Chris akasema huku akiliendea friji

    “Kijana hebu tulia na ukae chini.Hatujaja hapa kutumia vinywaji”

    Baba mkwe akasema kwa ukali.Chris akaenda kuketi sofani karibu na Emmy halafu akazima kabisa luninga ile iliyokuwa mle sebuleni kukawa kimya.Baraka akaja na kusimama pembeni yangu.nadhani kuna kitu alikuwa amekihisi.Hakutaka kukaa mbali nami.Akanishika mkono kwa nguvu.

    “Habari za siku nyingi wayne? Chris akasema baada ya kuona sebule iko kimya huku akijilazimisha kutabasamu.Sikumjibu kitu bali nikaendelea kumtazama.Baba mkwe akakohoa kidogo halafu akasema

    “Kijana ,wewe ndiye Chris? Baba mkwe akauliza

    “Ndiye mimi mzee” Chris akajibu

    “Vizuri. Nadhani kabla hatujaendelea ningetoa utambulisho mfupi.Mimi ni baba yake mzazi Emmy.Yule pale ni mama yake mzazi Emmy.Yule mzee pale ni Mzee wa kanisa na mwalimu wa dini wa Emmy na Wayne.Yule pale anaitwa ndugu…nani jina lako ndugu” baba mkwe akamuuliza Beka.

    “naitwa beka”

    “Exactly.Anaitwa ndugu Beka ni rafiki wa Emmy na Wayne .Wale pale nadhani unawajua ni wasimamizi wa ndoa ya Wayne na Emmy.Wa mwisho sina haja ya kumtambulisha kwa sababu unamfahamu fika kwa sababu ni rafiki.. I mean alikuwa rafiki yako.Kwa kukumbusha jina lake anaitwa Wayne ni mume wa ndoa wa Emmy ”

    Baba mkwe akanyamaza kidogo halafu akaendelea.

    “Chris nadhani mpaka hivi sasa umekwisha elewa ni kwa nini tuko hapa.Sina haja ya kutoa maelezo marefu sana kwa sababu hivi unavyotuona tumetoka katika kikao kizito na mambo mengi tayari tumekwisha yaongea huko.kwa ufupi ni kwamba tulipigiwa simu na wayne akatuomba tuonane jioni.Jioni ya leo kama alivyokuwa ametuomba tumeitika wito tukakusanyika bila kufahamu ni jambo gani alilokuwa akituitia.Baadae alitueleza jambo alilotuitia ,jambo ambalo kwa mtu mwenye moyo mwepesi unaweza ukaanguka na kufariki mara tu ukihadithiwa.Ni jambo lenye kuumiza na kusikitisha sana.Kwa mujibu wa maelezo ya wayne ni kwamba wewe na mkewe Emmy mna mahusiano ya kimapenzi.Wewe uliwahi kuwa rafiki mkubwa wa wayne na hata kulipotokea matatizo kati ya wayne na Emmy mara ya kwanza ni wewe ndiye uliyekuwa mstari wa mbele katika kutafuta suluhu.Baada ya Emmy na wayne kuelewana ni wewe ndiye uliyekuwa kiongozi wa jopo lililofanikisha sherehe za harusi yao.Sielewi ni shetani gani alikuingia hadi ukaamua kuwa na mahusiano ya kimapenzi na mke wa rafiki yako.si tu rafiki yako bali rafiki yako mkubwa na wa karibu.Hilo lilikuwa dogo,kubwa zaidi ikabainika kwamba katika mahusiano hayo baina yako na Emmy mlipata mtoto ambaye Wayne alijua ni wa kwake kumbe mtoto huyu ni wako wewe .Hili ni jambo baya sana na halivumiliki.Umemtendea vibaya sana rafiki yako na vile vile umemtendea vibaya sana mwanao Baraka.Nadhani akiwa mkubwa na kuufahamu ukweli kiundani atakuchukia katika maisha yake yote kwa kitendo ulichokifanya.Baada ya kuligundua hilo Wayne alimtaka Emmy wakafanye kipimo cha DNA ili kubaini kama ni kweli Baraka ni mwanae au si mwanae.kwa ujeuri kabisa Emmy alikataa kata kata.Wayne alifunga safari hadi dar es salaam na kufanya kipimo hicho ambapo ilidhihirika kwamba ni kweli Baraka hakuwa mwanae wa damu.Hebu pata picha ni maumivu kiasi gani aliyoyapata mwenzio baada ya kugundua kwamba mtoto aliyemlea na kumpenda na kumthamini kuliko kitu chochote kumbe si mwanae wa damu.Namshukuru sana wayne kwa sababu ni kijana mwenye roho ya ujasiri sana ambaye siku zote anaongozwa na mwenyezi Mungu kutokufanya maamuzi mabaya.Kama si kwa maongozi ya mwenyezi Mungu hivi sasa tungekuwa tukiongea mambo mengine kabisa.Lakini kama hiyo haitoshi bado Emmy aliamua kuondoka nyumbani na kuja kuishi kwako kwa kiburi bila ruhusa ya mumewe.Linaumiza sana jambo hili.Wayne alivumilia mwishowe akaona hataweza kuvumilia suala hili zaidi ya hapa lilipofikia hivyo akatuita na kuamua kuliweka wazi suala hili ikiwa ni pamoja na maamuzi yake.Katika kikao tulichokaa,mbele ya wazazi wake,mume wake,mzee wa kanisa pamoja na mashahidi wao wa ndoa emmy alitamka kwa ulimi wake kwamba hataki tena kuishi na Wayne na kwamba wewe Chris ndiye mwanaume wa maisha yake.Anataka aishi na wewe ili mumlee mtoto wenu Baraka.Kama mzazi nilipaswa kuhakikisha kwamba watoto hawa wanamaliza tofauti zao na kuendelea kuishi kwa amani na kujenga familia iliyo bora.Sikuweza kulifanya hilo kwa sababu Emmy kwa kiburi kabisa alisema kwamba hana haja na masuluhisho ya namna yoyote ile.yeye anachohitaji ni kupewa nafasi ya kuishi na wewe.Niliyatazama macho yake na nikabaini kwamba hakuwa hata na chembe ya mapenzi kwa Wayne tena kwa hiyo hata kama tungewasuluhisha ingekuwa ni kumuongezea matatizo wayne.”

    Baba mkwe akanyamaza kidogo akatutazama wote halafu akasema

    “bwana Chris,nimekuja hapa mimi kama baba wa Emmy nikiwa na mama yake Emmy na mashahidi wao Nataka mbele yao utamke wazi kwamba ni kweli Baraka ni mtoto ambaye umezaa na emmy halafu masuala mengine yafuate.”

    Baba mkwe akasema huku amemkazia macho Chris. ambaye alikuwa ameinama asijue afanye nini.Jasho lilikuwa likimtiririka.Nilikumbuka jinsi urafiki wetu ulivyokuwa mkubwa na wala sikutegemea kama ingetokea siku angenifanyia kitu kama hiki.Ni wazi ulimi ulikuwa mzito kutamka lolote.

    “Chris tunakusubiri wewe.hebu ongea haraka bado tuna mambo mengi ya kuongea”

    Usoni kwa Chris kulikuwa na michirizi ya machozi ambayo sikujua kama alikuwa akilia kwa kulijutia kosa lake au yalikuwa ni machozi ya uongo.

    “baba..na mama naombeni mnisamehe..Nimek…..” Alisema Chris lakini kabla hajaendelea mbele zaidi baba mkwe akadakia

    “Chris usipoteze wakati wetu.Ninachotaka kusikia ni kauli yako kwamba ni kweli umezaa na Emmy.Just short and clear” baba mkwe akasema kwa ukali

    “baba ni kweli,nimezaa na Emmy” Chris akasema huku akitazama chini kwa aibu.

    Kwa fundo nililokuwa nalo moyoni nilitamani niichukue chupa ile ya mvinyo iliyokuwa mezani nimtwange nayo kichwani.Nilianza kujilaumu kwa kuamua kuja huku kwa sababu kuja kwangu huku kumeyaamsha upya mateso na maumivu yote aliyonisababishia Emmy.Awali nilijipa moyo kwamba maumivu yale ni ya kupita na tayari nimekwisha yazoea lakini kumbe nilikuwa najidanganya.maumivu yale hayakuwa yakizoeleka wala kuvumilika.

    “Nadhani nyote mmmesikia kwa kauli yake kwamba ni kweli amezaa na emmy mtoto ambaye ni huyu Baraka.” Baba mkwe akasema halafu akanyamaza na kumkazia macho Emmy halafu akamtazama Baraka aliyekuwa amesimama pembeni yangu amenishika mkono.Hakutaka kuuachia mkono wangu.

    “Chris ,baada ya kukiri wewe mwenyewe kwa ulimi wako kwamba Baraka ni mwanao ,kitu cha kwanza tunachokifanya hapa usiku huu ni kukukabidhi mtoto wako baraka ili umtunze na kumlea kama baba yake mzazi .Baadae taratibu za kisheria na kidini zitafuata ili tuone ni jinsi gani tunaweza kulibadilisha jina la mtoto ili liweze kuendana na jina la baba yake mzazi.Tungeweza kumzuia mtoto huyu abaki kwa Wayne na asikutambue wewe kama baba yake,lakini kwa kufanya hivyo tungekuwa bado hatumtendei haki mtoto mdogo kama huyu ambaye ana haki ya kumfahamu baba yake mzazi.Kwa hiyo kuanzia usiku huu utakuwa na mwanao Baraka na utamtunza na kumlea kwa jinsi unavyoona inafaa kama baba yake.Tunasikitika sana kwa sababu mateso anayoyapata mtoto huyu kwa hivi sasa ni makubwa .”baba mkwe akasema

    Baraka ambaye alikuwa amesimama pembeni yangu amenishika mkono kwa nguvu akawa akitokwa na machozi na kuniambia kwa sauti ndogo

    “Baba mimi sitaki kubaki hapa.Tunaondoka wote” Sebule nzima ikawa kimya wote wakimtazama Baraka na kumuonea huruma malaika yule anayeteseka bila sababu.Iliniuma sana kumpoteza mtoto kama yule niliyekuwa nikimpenda kupita maelezo.Sikuwa na jinsi zaidi ya kumuachia aende kwa baba yake mzazi.Nilihisi kama vile nilikuwa naadhibiwa kwa kosa ambalo silijui kwa maumivu yaliyokuwa ndani ya moyo.

    “baraka baba njoo hapa.” Baba mkwe akamwita Baraka

    “Babu mi sitaki.mi sibaki hapa nitarudi kwetu na baba” Baraka akasema huku akilia.

    Baba mkwe akasimama,akamshika mkono Baraka na kwenda kukaa naye sofani.

    “Baraka najua bado u mtoto mdogo lakini tayari una akili ya utambuzi.Nadhani mpaka sasa hivi unamfahamu baba yako ,si ndiyo? Baba mkwe akauliza na baraka akaitika kwa kichwa

    “Good boy.baba yako anaitwa nani” Baba mkwe akauliza tena huku akitabasamu

    “baba yangu anaitwa wayne” baraka akajibu

    “Vizuri sana . Sasa Baraka kuna kitu kimoja ambacho tunataka ukifahamu Ni kwamba Wayne si baba yako mzazi.baba yako mzazi ni yule pale anaitwa Chris.Kwa hiyo kuanzia leo wewe utaishi hapa kwa baba yako mzazi pamoja na mama yako.Umesikia Baraka? Baba mkwe akasema na kumfanya Baraka akaangue kilio.Ikanibidi nimchukue na kumbembeleza.

    “Sikia baraka utabaki hapa kwa baba,mama yako pia atabaki hapa.Nitakuwa nakuja kukuangalia na kukuletea zawadi kila jumamosi.”

    “baba mimi sitaki kubaki hapa” Baraka akapiga kelele

    “baraka utabaki na mama yako”

    “Mimi simpendi mama.nakupenda wewe baba” Baraka akasema huku akilia na kuwaacha watu wote midomo wazi.

    Nilishindwa kuyazuia machozi kunitoka kwa kauli ile ya Baraka.Ni wazi aliufahamu ukatili wa mama yake .

    “baba ,itakuwa ngumu sana kwa baraka kubaki hapa.naombeni mniruhusu nirudi naye nikaendelee kuishi naye ili hata kama ni kumkabidhi kwa baba yake basi tumfanyie maandalizi ya kutosha ya kisaikolojia lakini si hivi tunavyotaka kufanya.Tunamuumiza mtoto bure.” Nikasema

    Emmy akainuka pale sofani na kuja kumchukua Baraka kwa nguvu

    “Nimeshasema mtoto wangu haendi popote.Hapa ni kwa baba yake na ataishi hapa atake asitake.” Emmy akanyanyua Baraka na kuondoka naye huku mtoto akipiga kelele nyingi.

    Baada ya muda akarejea bila baraka.nadhani alikuwa amekwenda kumfungia chumbani.

    Baba mkwe akaendelea baada ya Emmy kuirejea.

    “ Bwana Chris baada ya zoezi la kwanza kukamilika kitu kingine kinachofuata ni kukukabidhi rasmi Emmy”

    Chris akastuka sana kwa kauli ile ya baba mkwe akataka kuongea jambo baba mkwe akamuonyeshea ishara anyamaze.

    “kaa kimya kabisa na sitaki unijibu chochote.Huna nafasi ya kunijibu lolote.” Baba mkwe akasema kwa ukali.

    “Chris naomba usistuke kwa sababu Emmy kwa mdomo wake ametamka kwamba hataki kuendelea kuishi na Wayne na anataka kuja kuishi na wewe ili mumlee mtoto wenu baraka.Tokea mwanzo ulifahamu fika kwamba Emmy ni mke wa mtu tena mke wa rafiki yako wa karibu lakini ukadiriki kuwa na uhusiano naye na hatimaye mkazaa mtoto.Nina imani ulikwisha jiandaa kwa lolote litakalotokea.Ulikuwa ufahamu nini kitatokea baada ya mambo yote haya kuwekwa bayana.Niwazi ulitegemea ndoa ya Wayne na Emmy kuvunjika na wewe kupata nafasi ya kuwa na Emmy.Imetokea kama ulivyokuwa umekusudia.Ndoa kati ya Emmy na wayne naweza sema kwamba haipo tena.Sababu kubwa ya kutokuwepo kwa ndoa hii kati ya Wayne na Emmy ni wewe.Kwa hiyo Bwana Chris nimekuja hapa mimi pamoja na hawa wote unaowaona ili nikukabidhi rasmi Emmy.Kuanzia sasa chochote kitakachomtokea Emmy kitakuwa ni jukumu lako.Mimi kama baba mzazi wa Emmy pamoja na mama yake wote kwa pamoja tumekwisha nawa mikono,hatutahusika tena na jambo lolote linalomuhusu .Kwa sasa wewe ndiye utakuwa baba na mama yake.Kitendo mlichokifanya si kitendo cha kibinadamu na hakistahili kuvumilika.Tokea sasa Emmy yuko mikononi mwako.Mlee na kumtunza jinsi unavyotaka wewe Mimi nimemaliza.” Akasema Baba mkwe na taratibu nikauona uso wa Chris ulivyokuwa umelowa jasho.Hakuwa ametegemea mambo haya kufika hapa yalipokuwa yamefika.Nilimsikitikia sana Emmy kwa ujinga aliokuwa ameufanya kwa sababu Chris ninamfahamu fika kwamba hakuwa na lengo lolote naye.Chris tabia yake ndiyo hiyo ya kuchezea wanawake na kisha kuwatelekeza.Siwezi elezea uchungu unaonipata kila nikimuwaza mtoto Baraka.Ni wazi alikuwa katika wakati mgumu mno licha ya umri wake kuwa mdogo.

    “Jamani kuna mtu ana jambo la kuongeza? Baba mkwe akauliza baada ya ukimya mkubwa kutanda mle ndani.Macho ya watu wote mle ndani yakanigeukia mimi .Wote walijua labda nilihitaji kusema machache.Nilikuwa na mengi ya kuongea lakini kila nilipojaribu kutaka kusema neno kuna kitu kilikuwa kimenikaba koo kiasi cha kushindwa kutamka neno.Fundo la hasira lilikuwa limenikaa.Niliutumia mkono wangu kuwafanyia ishara kwamba sina lolote la kuongea.

    “Nadhani hakuna yeyote mwenye jambo la kuongea.Tunaweza kuondoka” Baba mkwe akaamuru.Wakati tukiinuka kwa ajili ya kuondoka Chris akasimama na kusema jambo

    “Baba samahani naomba mkae kidogo .Hata mimi nina mambo ya kuongea.Mbona hamjanipa nafasi ya kuongea? Hivi mnavyonifanyia si vizuri.Haiwezekani mje mnimwagie mtu hapa ndani katika mfumo huu.Tafadhalini jamani naomba na mimi nisikilizwe japokuwa nimekosea..” Chris akasema huku akiwa ameifumbata mikono yake kifuani kwake na sauti yake ilikuwa ni yenye kukwama kwama.
    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Tumekumwagia mtu? Baba mkwe akauliza kwa ukali

    “Unadiriki kusema tumekumwagia mtu? Kweli kijana huna haya.Baada ya mambo yote haya uliyoyafanya bado unadiriki kusema kwamba una kitu cha kuongea? Huna nafasi wala kitu chochote cha kuongea baradhuli wewe.Ulitegemea nini baada ya kuivuruga ndoa ya rafikiyo? Ulichokuwa umekitegemea ndicho hicho umekipata.Emmy sasa ni mke wako halali.Na kwako Emmy,kwa kuwa umemkana mumeo wa ndoa mbele yetu na kutamka kwa ulimi wako kwamba hutaki kuishi naye tena,na sisi hatutaki kukuona tena nyumbani kwetu.na hatukutambua kama mwanetu.Lolote litakalokupata kuanzia sasa ,baba na mama yako ni huyu mwenzio ambaye leo hii amekuwa ni mtu wa maana sana kwako.Usitutambue kwa lolote lile.Na ninakwambia wazi wazi kwamba kitendo ulichomfanyia mwenzio na wewe kitakurudia.Utafanywa kama ulivyomfanyia mwenzio”. baba mkwe akafoka

    “lakini baba…..” Chris akataka kusema jambo lakini kabla hajaendelea akazuiwa na Emmy.

    “Chris usiseme chochote.kwa kuwa wamekwisha nikataa kuwa mimi si mtoto wao sasa ya nini uendelee kuwabembeleza? Achana nao Chris.Let them go.”

    Nilimtazama Emmy kwa hasira.Alikuwa akiongea kwa kiburi sana.Sikutegemea kama ni kweli Emmy niliyemfahamu leo hii anadiriki kutamka maneno yale kwa kiburi kikubwa na tena mbele ya wazazi wake.Baba mkwe hakutaka kuongea tena neno lolote akatuongoza tukatoka nje.Nilimuona Chris akiwa amesimama pale sebuleni akiwa haamini kilichokuwa kimetokea.

    “Wayne baba, nenda nyumbani kapumzike.Tutaongea zaidi kesho.Ninachokuomba usiwaze sana kuhusu haya yaliyotokea.Hii ni mitihani ya dunia na huna budi kuishinda.Ninachokusihi jitahidi sana kuomba Mungu ili aweze kukupa nguvu ya kuweza kuyashinda majaribu haya.Muda si mrefu mambo haya yatakwisha na utasahau kabisa” baba mkwe akaniambia huku akinipiga piga mgongioni wakati tukijiandaa kuingia katika magari yetu .Sikujibu kitu nilikuwa nimeinama chini nikitafakari..Sikutegemea kama mwisho wangu na Emmy ungekuwa namna hii.



    “Wayne anayosema baba yako mkwe ni ya kweli kabisa.Jipe moyo na Mungu atakusaidia.Jitahidi sana kudumu katika maombi na Mungu atakusikia.Inawezekana Mungu ana mpango mwingine na wewe.Mimi binafsi nitakuombea sana kila siku ili upate nguvu uweze kuendelea na maisha yako.Ila kesho nitaonana na baba Paroko na kumweleza kuhusu suala hili ili tuone ni kitu gani anaweza akafanya kwa sababu kwa mahali ndoa yako ilipofikia ni pagumu sana.” Mwalimu wangu wa kanisa naye akasema machache.Niliwashukuru sana wazee wale kwa nasaha zao na kwa jinsi walivyoniunga mkono ,tukaingia magarini na kuondoka zetu.

    “Beka sikutegemea kama mwisho wangu na Emmy ungekuwa namna hii.mwanamke niliyempenda na kumthamini leo amenifanyia kitendo kama hiki du ! sikutegemea kabisa.Nilikuwa mjinga sana kwa kumuamini Emmy kupita kiasi .Alinitenda mara ya kwanza nikamsamehe na kurudiana naye tena.Nilifanya kosa kubwa sana kuamua kurudiana naye baada ya kosa lile la kwanza.Nimepoteza muda mwingi katika kulihudumia penzi lisilokuwa na matunda yoyote zaidi ya maumivu kila kukicha.” Nilisema kwa hisia kali wakati tukiendelea na safari ya kurudi nyumbani.Nilikuwa na uchungu mwingi.

    “Wayne najua ni jinsi gani ulivyoumizwa na suala hili.Hata mimi ninapata wakati mgumu sana kuamini kama ni kweli yametokea haya.Ni kweli kama mambo haya ameyafanya Emmy ninayemfahamu mimi.kama nisingeshuhudia mwenyewe kwa macho yangu nisingeamini katu kama Emmy angeweza kufanya mambo kama yale.Kitu cha msingi ni kukubali kilichotokea.Jipe moyo na maisha yaendelee.Jipange na uanze maisha mapya.Msahau kabisa Emmy katika maisha yako.Bado hujachelewa Wayne katika kuyapanga upya maisha yako.Jipange vizuri na mwisho wa siku utasahau kila kitu kuhusu Emmy” beka akasema.

    “Beka hakuna mtu anayeweza kuyaongelea au kupima maumivu niliyoyapata kwa kitendo hiki cha Emmy.Amenisababishia majeraha makubwa moyoni ambayo si rahisi kufutika mapema.Itanichukua muda mrefu sana kumsahau Emmy na mambo yote aliyonitendea.Kinachoniuma zaidi ni ukatili alioufanya kwa mtoto Baraka.Inaniwia vigumu kuamini kwamba mtoto yule si mwanangu.Bado ninampenda kupita maelezo na sijui hata nifanye kitu gani ili niweze kuyaondoa maumivu haya makali kuhusiana na mtoto huyu .” Nikasema huku Beka akikanyaga mafuta na kuongeza mwendo wa gari

    “Huwezi kumsahau kwa haraka namna hiyo Wayne.Nakushauri uchukue likizo ndefu na uende mbali na hapa ukae huko kwa muda .Utakapokuwa mbali na mazingira haya utajifunza ni jinsi gani ya kuanza maisha mapya.Nadhani hii itakuwa njia bora sana ya kuweza japo kwa asilimia chache kukusahaulisha na mkasa huu wa kuumiza.” Beka akasema.Ushauri wa Beka ulikuwa mzuri nikauona unafaa

    “nakubaliana nawe Beka.Hilo ni wazo zuri.Itanibidi nilifanyie kazi mapema iwezekanavyo.I need to go far away from here.I need to forget everything.” Nikasema.Wazo lile la Beka lilikuwa ni wazo zuri ambalo hata mimi nilikuwa bado sijalifikiria.Ni kweli ,ningezidi kuumia sana kama ningeendelea kukaa ndani ya nyumba ambayuo kila siku kumbu kumbu ya Emmy na baraka zingekuwa zinanijia.

    Beka alinipeleka nyumbani akaniacha pale na yeye kuondoka.Nikaingia ndani na kukaa sebuleni.Ukutani kulikuwa na picha kubwa niliyopiga na Emmy siku ya harusi yetu.Niliiangalia picha ile kwa umakini mkubwa .Emmy alikuwa amejaa tabasamu zito,alikuwa amependeza sana.Ni kipindi ambacho tulikuwa katika mapenzi makubwa.Tulikuwa katika mahaba mazito sana.Ni katika kipindi hicho nilikuwa ni mmoja kati ya wanaume wenye furaha kubwa duniani.Sikutaka tena kuendelea kuiangali a picha ile,nikaitoa na kuiweka chini,nikaanza kukusanya vitu vyote ambavyo vitanisababisha nimfikirie Emmy .Nilikusanya kila kitu chenye uhusiano na Emmy kuanzia picha hadi vyombo nikavifunga pamoja katika boksi kubwa na kwenda kuvihifadhi stoo.Saa nane za usiku nikapanda kitandani na kulala.



    * * * *



    Niliamka saa nne za asubuhi.Kichwa kilikuwa kizito sana.Nyumba yote ilikuwa kimya kabisa.Nilizoea kuamka asubuhi na kuikuta nyumba ikiwa imechangamka kwa muziki ,maongezi na vicheko lakini leo hii hali ilikuwa tofauti kabisa.Hakukuwa na sauti yoyote iliyokuwa inasikika.Mtu pekee niliyeamini angekuwapo ndani muda ule ni mtumshi wa ndani .Kwa kuwa nilikuwa nimedhamiria kuchukua likizo ndefu na kuondoka kabisa Arusha niliamua kumpa likizo binti yule wa ndani akapumzike hadi hapo nitakapomuhitaji tena.Nilijizoa zoa pale kitandani nikaenda nje na kumkuta Sharifa akifua nguo.

    “Shikamoo kaka” akanisalimu kwa adabu.

    “marahaba Sharifa hujambo?

    “Sijambo kaka” akajibu msichana yule mwenye adabu nyingi.Msichana yule aliyekuwa akitokea mkoani Singida nimeishi naye kwa muda mrefu na ninamchukulia kama mmoja kati ya ndugu zangu.

    “Sharifa kuna jambo ninataka kuongea na wewe” Nikamwambia na kumfanya astuke na kuacha kazi aliyokuwa akiifanya.

    “Sharifa nadhani unafahamu kila kitu kilichotokea hapa nyumbani.Hali hapa nyumbani si shwari.Dada yako ameondoka na kwa sasa niko mwenyewe hapa nyumbani.Kutokana na mambo yaliyotokea hata mimi nimeamua kuchukua likizo na kusafiri ,kwa maana hiyo nimeona nikupe likizo uende nyumbani ukapumzike kwa muda halafu nitakaporudi nitakuita tena..Kwa hiyo leo ungejiandaa na kesho uanze safari” Nilimpatia kiasi cha shilingi laki tatu kwa ajili ya maandalizi ya kwenda nyumbani kwao.Ingawa hakuwa na pingamizi lakini niliamini moyoni hakuwa amependezwa na suala lile la kumtaka arudi nyumbani kwa muda hadi hapo nitakapomuita tena.Sikulijali hilo .Baada ya kuoga nikapata kifungua kinywa halafu nikarudi tena chumbani kwangu kulala.Sikuwa na hamu ya kwenda mahala popote.Niliutumia muda huo kutafakari mustakabali mzima wa maisha yangu yaliyopita na yajayo.Nilijaribu kuitumia nafasi hiyo katika kuyapanga maisha yangu yajayo bila ya kuwa na Emmy na Baraka.

    Saa kumi za jioni niliamua kutoka na kwenda sehemu tulivu kwa ajili ya kupata upepo na kupunguza mawazo.Sikutaka kwenda sehemu zenye mkusanyiko mkubwa wa watu.Nilihitaji kwenda mahala ambako ni tulivu ,nitakapopata wasaa wa japo muda mfupi kuyasahau maisha yangu ya nyuma.Arusha tulivu garden ni moja kati yua sehemu tulivu sana kama lilivyo jina lake.Ni sehemu ambayo imekuwa inapendwa sana na wageni toka nchi mabalimbali.nafikiri mahala hapa panapendwa kutokana na utulivu wake na mandhari ya kuvutia mno.Ninaifahamu sehemu hii na ndiyo maana nikachagua kuja huku kwa sababu ni sehemu pekee niliyoamini ingeweza kunisaidia kunisahaulisha na dhahama iliyonikumba japo kwa masaa machache

    Niliwasili katika geti la sehemu hii tulivu na kuingia ndani.Nilikuwa nikitabasamu kwa mandhari safi na tulivu ya mahala hapa.Ndani ya bustani hii tulivu kulikuwa na sura nyingi za wageni ambao kama nilivyosema wanapapenda sana mahala hapa.Niliegesha gari na kushuka nikatafuta mahala nikaketi.Ukimya ulikuwa umetawala sehemu hii.Ni milio ya ndege na muziki laini wa ala ndivyo vilivyokuwa vikisikika.Hakika nilipafurahia mno mahala hapa.Muhudumu aliyevalia nadhifu,suti safi nyeusi na tai nyekundu akafika na kwa adabu akanikaribisha na kuniuliza kile ambacho ningependa kutumia.Nilimuomba aniletee wine safi aina ya Lion hills.Mkononi nilikuwa na kitabu cha hadithi tamu ya kusisimua nilichokinunua majuma kadhaa yaliyopita,kitabu kilichoandikwa na mmoja kati ya waandishi wa riwaya ninaopenda kusoma riwaya zao kiitwacho “Before I die” Kwa siku hii niliamua kutumia muda huu niliouapata kwa ajili ya kuisoma hadithi hii tamu na ya kusisimua.Nilikuwa nikisoma huku nikiendelea kupiga mafunda kadhaa ya wine ile nzuri.Nilijisikia furaha sana kwa muda ule niliokuwa pale.

    “habari yako kaka” Nilistuliwa na sauti tamu na nzuri ya mwanamke.Kwa kuwa nilikuwa nimezama katika simulizi nzito ya kitabu hiki cha “before I die” nilionesha kama kustushwa kidogo na sauti ile.Nikainua kichwa na kukutana na sura ya mwanamke mmoja mrembo sana aliyekuwa amesuka nwele zake katika mtindo wa rasta zilizokuwa zimemkaa vyema.Alikuwa mwembamba wa wastani na mwenye sura nzuri .

    “Nzuri dada habari yako” Nikasema huku nikimtazama mwanadada yule .

    “habari yangu nzuri. Naruhusiwa kukaa? Akauliza dada yule mwenye sauti tamu .

    “Hakuna shida unaweza kukaa” Nikasema na dada yule akavuta kiti na kuketi.Mara moja muhudumu akafika dada yule akamuomba amletee kinywaji chake alichokiacha katika meza aliyokuwa amekaa.

    “Sahamani kaka kama nimekusumbua ,nilikuwa nimekaa kule peke yangu lakini nikaona ninazidi kuboreka.Nimekuona muda mrefu uko hapa mwenyewe nikaona nisogee hapa walau nione kama ninaweza kupata mtu wa kuongea naye mawili matatu.Sahamani kama nimekukwaza.” Akatamka dada yule na kunifanya nitabasamu kutokana na adabu na ustaarabu wake

    “Bila samahani dada yangu.Mimi mwenyewe nilikuja hapa kwa ajili ya kupumzika na kupoteza mawazo lakini kwa kuwa sikuwa na mtu yeyote wa kuweza kubadilishana naye mawazo nikaamua kujisomea kitabu changu hiki cha hadithi ilimradi siku iende” Nikasema huku nikikifunika kitabu changu nilichokuwa nakisoma na kukiweka mezani.

    “Wow ! “before I die” ! Nimesikia kwamba kitabu hiki kimetoka.Nilikuwa nakitafuta sana.Napenda sana riwaya za huyu kaka.mara nyingi nisomapo riwaya zake huwa nahisi msisimko wa ajabu sana” Akasema dada yule.

    “Kumbe hata wewe ni mpenzi wa mtunzi huyu? Nikauliza huku nikitabasamu.

    “Mimi ni shabiki wake mkubwa.Kinachonifurahisha ni kwamba amekuwa akiandika simulizi tamu ambazo mara nyingi ni vitu vinavyotokea katika jamii yetu.Kuna kitabu aliwahi kukitoa kinaitwa Malaika wa Valentine,kwa kweli kitabu kile kila ninapokisoma huwa ninatoa machozi kwa sababu hadithi ile inanigusa mno kwani mambo yaliyomo katika kitabu kile yaliwahi kunitokea hata mimi.Tokea wakati huo siachi kusoma hadithi yake hata moja.” Akasema mwanadada yule ambaye tayari muhudumu alikwisha mletea kinywaji chake alichokuwa anakitumia.Nilipotazama alikuwa akitumia Miami 24 whisky.Nilistuka kidogo kwa sababu kutokana na umbo lake na jinsi alivyo sikutegemea kama angeweza kutumia kinywaji kikali kama kile.Nilipatwa na shauku ya kutaka kumfahamu zaidi yule dada.Akamimina mvinyo kidogo katika glasi halafu akanywa yote akainua kichwa na kunitazama.

    “Nimefurahi sana kumpata shabiki mwingine wa simulizi za Patrick.” Nikasema huku nikitabasamu.

    “Hata mimi ninafurahi sana kila ninapokutana na mtu ambaye anapenda kusoma hadithi za watunzi mbali mbali.Itabidi tufanye mpango wa kuanzisha klabu ya wasomaji wa riwaya ,wewe mwenyekiti mimi katibu ,au unasemaje? Akauliza na kufanya wote tuangue kicheko kikubwa.Hiki kilikuwa ni kicheko changu cha kwanza toka nimekumbwa na masahibu ya Emmy.

    “Hiloni wazo zuri sana.Tunaweza tukaanzisah kitu cha namna hiyo ambacho kinaweza kusaidia sana kuamsha ari ya usomaji vitabu hapa nchini.Katibu wewe unaitwa nani? Nikauliza na kumfanya dada yule acheke kicheko kikubwa kinachosababisha na mimi nicheke.Akatoa kitambaa katika pochi yake ndogo na kujifuta machozi yaliyotokana na kucheka.

    “naitwa Clara.na wewe mwenyekiti wangu unaitwa nani? Akauliza

    “Mimi naitwa wayne”

    “Ouh Jina zuri sana wayne.Nafurahi mno kukufahamu.” Akasema Clara huku akitabasamu.

    “Wayne wewe ni mkaazi wa hapa Arusha? Akauliza.

    “Haswaa.Mimi nimkaazi wa hapa hapa Arusha.Ninaishi maeneo ya Majengo.wewe unaishi wapi?

    “Kwa sasa mimi makazi yangu ni Pretoria afrika kusini japokuwa wazazi wangu wanaishi Dar es salaam.Hapa Arusha nimekuja kwa siku chache kwa ajili ya kutoa mada katika semina ya mitindo na mavazi inayoendelea katika hoteli ya Naura spring.Siku ya leo nimeamua kuja hapa kwa ajili kupata hewa safi na kutuliza kichwa.” Clara akasema.

    “Ouh kumbe unajishughulisha na masuala ya mitindo na mavazi? Nikauliza

    “ ndiyo .Ninajishughulisha na mambo ya ubunifu na mitindo kwa ujumla.” Akajibu.

    “Nilipokuona nilijua ni lazima ungekuwa mwanamitindo” Nikasema na kumfanya atabasamu.

    “Unaionaje fani ya mitindo na mavazi hapa Tanzania ukilinganisha na afrika ya kusini? Nikauliza. Clara akamimina mvinyo katika glasi akanywa halafu akasema.

    “Kwa hapa Tanzania fani hii ya mitindo bado iko chini japokuwa kuna wanamitindo wazuri na wabunifu wazuri.Wenzetu wamepiga hatua kubwa sana.Kuna kila sababu ya kuongeza juhudi ili kuweka kufikia hatua waliyopiga wenzetu kama afrika kusini .Wenzetu wakojuu sana.Ninachokifanya kwa sasa ninajaribu kuwatafutia wanamitindo na wabunifu wa kitanzania nafasi katika majukwaa makubwa ya kimataifa na kuwafanya wajulikane.Ni kazi kubwa lakini tunajitahidi na maendeleo si mabaya” Clara akasema.

    “ Nimefurahi sana kusikia hivyo Clara.Unajua hata mimi hapo awali nilikuwa na ndoto za kuwa mbunifu lakini baadae nikajikuta nikiingia katika masuala mengine kabisa na kuamua kuachana na mawazo ya kuwa mbunifu” Nikasema

    “Unayoyasema ni kweli kabisa Wayne.Wengi wanakuwa na ndoto za kuwa watu Fulani lakini si wote wanaoweza kuzifanya ndoto zao kuwa kweli.Mimi sikuwa na wazo la kuwa mwanamitindo na wala sikuwahi kuota kwamba iko siku nitajulikana katika majukwa makubwa ya mitindo na mavazi.Kitaaluma mimi ni daktari lakini kwa sasa nimeachana na shughuli za udaktari na kuamua kujikita zaidi katika mitindo.Ilikuwa mwaka juzi wakati nikiwa katika mapumziko nchini afrika kusini nilipokutana na mtu ambaye alinishawishi nijaribu fani ya mitindo kwani aliona nina vigezo vyote vya kuwa mwanamitindo.Nilikuwa nataka kuyabadili maisha yangu kwa hiyo nikaona niingie katika mitindo.Nashukuru Mungu kwani baada tu ya kuingia katika mitindo maisha yangu yalibadilika na mpaka sasa ni mmoja kati ya wanamitindo wanaofahamika na kuheshimika sana nchini afrika kusini.” Clara akasema na kuzidi kuniongezea udadisi juu yake.

    “amesema alitaka kuyabadili maisha yake? Kwa nini alitaka kuyabadili maisha yake? Lazima kuna sababu iliyomlazimu afanye vile Aliwezaje kufanikiwa kuyabadili maisha yake? Hata mimi ninahitaji kuyabadili maisha yangu na kuyasahau maisha yangu yaliyopita.Natakiwa kuwa karibu na Clara ili aweze kunisaidia kuyabadili maisha yangu kama yeye alivyofanikiwa” Nikawaza huku nikimuangalia Clara usoni.

    “ Kwa hiyo wayne usishangae kwamba ulikuwa na ndoto za kuwa mbunifu lakini ukajikuta ukifanya kazi nyngine tofauti kabisa na ubunifu .” Clara akasema na kunifanya nitabasamu

    “Una bahati sana Clara .Umeweza kufanikiwa katika fani ambayo hukuwahi hata kuota kama siku moja ungekuwa mmoja kati ya wanamitindo wakubwa.” Nikasema

    “Nashukuru Wayne.Niliweza kufanikiwa kwa sababu nilikuwa najituma sana na nilikuwa nahitaji kufanya kitu ambacho kingenifanya niyasahu maisha yangu ya nyuma na kuanza maisha mapya.Hii ndiyo sababu iliyonifanya nijitume mno kitu kilichopelekea kufanikisha ndoto zangu.” Akasema

    “nafurahi jinsi ulivyojituma na ukafanikiwa.Ila ninachofurahi zaidi katika jitihada zako za kuyasahu maisha ya nyuma kama unavyodai , hujasahau nyumbani” Nikasema na wote tukaangua kicheko kikubwa.

    “You are so funny wayne..Siku zote nyumbani kutabaki nyumbani.Nilizaliwa Tanzania ,nimekulia Tanzania.Afrika ya kusini nimekwenda miaka minne iliyopita.Kwa hiyo Tanzania ni nyumbani na siwezi kusahau nyumbani na ndiyo maana unaniona niko hapa mida hii.Niko nyumbani” Clara akasema huku akitabasamu.Natamani ungesikia mrembo huyu akiongea.Hutatamani amalize kuongea.Alijua kupangilia maneno na sauti Kama angekuwa mtangazaji katika redio au televisheni nina imani angejizolea maelfu ya wapenzi.

    “ Ulitaka kusahau kitu gani Clara? Nikauliza kwa umakini na kumfanya Clara acheke kwa sauti.Kitu kingine alichojaaliwa mrembo huyu ni ucheshi.Kwa muda huu mchache niliokaa naye nimegundua kwamba ni mmoja kati ya wasichana wachache wenye mafanikio na ambao hawana ile silica ya kujivuna au kujiona wao ni bora zaidi kuliko wengine.Clara ni mcheshi na mchangamfu sana.

    “Wayne hilo swali la kichokozi” akasema huku akiendelea kucheka.

    “Si vibaya kufahamu Clara kwa sababu unapoamua kufanya mabadiliko fulani basi ni lazima kuwe na sababu fulani .Wewe ni sababu gani zilikupelekea kuamua kuyabadili maisha yako na kuanza maisha mapya? Nikauliza na kumfanya acheke tena.

    “wayne wewe ni mwandishi wa habari? “ akauliza na kunifanya na mimi nicheke.

    “Hapana Clara mimi si mwandishi wa habari” Nikajibu.

    Clara akatoa kitambaa chake cha mkononi na kujifuta macho halafu akaniangalia

    “Ni hivi Wayne,katika haya maisha tunapitia mambo mengi sana .Kuna nyakati tunapitia mambo ambayo kwa kweli yanatusababishia tuweze kuyachukia maisha ,kuichukia dunia na watu waliomo ndadni yake.Kuna nyakati vile vile tunaamua kuyabadii maisha yetu na kuamua kuwa wapya tena kutokana na maisha tuliyoishi huko nyuma..Kwa sasa mimi ni mtu mwenye furaha na amani maishani mwangu tofauti na maisha niliyokuwa nikishi hapo awali.Kuhusu ni kitu gani kilipelekea mimi kuamua kubadili maisha yangu..its uhh…something personal.I’m sorry for that” Clara akasema

    “Usijali Clara.Ila nakubaliana nawe kwamba kuna mambo yanayotutokea katika maisha na ambayo yanatulazimu kuachana kabisa na maisha yetu ya nyuma na kuishi maisha mapya.” Nikasema na mara kumbukumbu za Emy zikanijia kichwani na kunifanya nikae kimya ghafla.

    “Wayne are you ok? Clara akanistua.

    “Yah I’m ok “Nikajibu.

    “Unaonekana kama umezama katika mawazo ghafla” Clara akasema.Sikujibu kitu nikatabasamu

    “Thinking of your wife? Akauliza tena.Nikamtazama usoni na kusema

    “I don’t have a wife” Clara akanikazia macho na kuniuliza.

    “whats that ring for?

    “A ring? Nikauliza kwa mshangao.Ni kweli katika kidole changu cha mkono pete ya ndoa bado ilikuwa iko kidoleni.Nilighafirika sana baada ya kugundua ujinga niliokuwa nimeufanya wa kumdanganya mrembo yule.Midomo ilikuwa ikinitetemeka na kunifanya nishindwe kutamka neno.





    Clara akaona jinsi nilivyobadilika ghafla akasema

    ‘Usijali Wayne ,its ok.Sikuuliza kwa ubaya” Picha za Emmy zilikuwa zikija kwa kasi kichwani kwangu

    “baba mimi nimekwisha sema siwezi tena kuishi na Wayne.hakuna haja ya kupoteza wakati kwa usuluhishi.Yeye amekwishanipa ruhusa niende kwa hiyo hakuna kitu cha kuendelea kujadili hapa.hata mkisema nini mimi siwezi kurudiana na Wayne.”

    Ni maneno ambayo aliyatamka Emmy mbele ya wazazi wake,yalinifanya nikae kimya na fundo kunijaa rohoni.Siwezi kuyasahau maneno yale yaliyojaa kiburi.Nikakumbuka pia siku niliyompigia simu na kumtaka afike nyumbani kwa ajili ya kikao alinijibu majibu ambayo sintaweza kuyasahu kama yalitoka kwa aliyekuwa mke wangu wa ndoa.

    “Tuongee nini tena? Hatuna cha kuongea wayne.tayari ukweli unaufahamu kwa hiyo sioni kama kuna kitu tunatakiwa kuongea mimi na wewe.Umeshatambua Baraka siyo mwanao kwa hiyo hata mimi si mkeo.Sifikirii tena kuishi na wewe .Nimechoka mimi maisha ya kubanwa banwa na kufugwa fugwa ndani kama njiwa.Nahitahi maisha ya uhuru,maisha ya kufanya nitakacho.Naomba uniache Wayne.Mimi sifai kuwa mkeo.Unahitaji mwanamke bora wa kuishi naye na si mimi.”

    Uchungu na maumivu niliyokuwa najaribu kuachana nayo vikarudi upya.

    “Nilizama katika penzi la mtu asiyependeka.Nilikuwa kipofu.Nilipoteza muda kupalilia penzi ambalo halikuwa na faida wala manufaa yoyote.She was right.may be I wasn’t a man enough for her.I wasn’t her choice.Its time to let her go.Its time to forget her” Nikawaza.Nikaui

    nua mkono na kuitazama pete ile ambayo toka emmy amenivisha siku tunakula kiapo cha ndoa yetu haijawahi kutoka mkononi mwangu.Nilisikia uchungu mwingi kwa jinsi alivyoweza kuivunja ahadi aliyoiweka mbele ya madhabahu ya Mungu.Aliahidi kunipenda katika kila hali lakini ameshindwa kutimiza ahadi yake.hakuwa na thamani yoyote tena kwangu.Bado niliendelea kuitazama pete ile kwa uchungu huku machozi yakinitoka.Sikuona tena ulazima wa kuendelea kuivaa pete ile kidoleni.Tarati

    bu nikaanza kuizungusha na kuitoa kidoleni kwangu.Niliitoa kidoleni na kuishika mkononi.Clara alikuwa amenitumbulia macho asiamini alichokuwa amekiona.Niliitazama pete ile kwa hasira nikainuka na kelekea moja kwa moja lilipokuwa bwawa kubwa ambalo ndani yake kulikuwa na bata wazuri weupe wakiogelea.Nikaishika mkononi pete ile nikaitazama na kunong’ona

    “ I have t do this to forget you Emmy.As from today I erase every memory of you in my heart.You ‘ll have no chance in my heart. From today I don’t know you,..from today I never married you…from today you are out of my life.I’m moving forward with my life” Nilisema maneno yale kwa uchungu mwingi huku machozi yakinitoka.Nikainua mkono na kuirusha pete ile mbali kati kati ya bwawa.Niliitaza

    ma pete ile ikidumbukia kati kati ya bwawa lile.Nilibaki nimeishikilia nguzo iliyokuwa pembeni ya bwawa kwa dakika kadhaa.Bado machozi yalikuwa yakinitoka.

    “Wayne its ok.” Ilikuwa ni sauti ya upole ya Clara aliyekuwa akinitazama kwa wasi wasi.Alinishika mkono na kuniongoza kunirudisha mahala tulipokuwa tumekaa.

    “Calm down Wayne ,its gonna be fine” akasema Clara kwa sauti ya upole huku akinisugua bega.

    “Whysky please” Nikasema na kulisogeza glasi karibu na Clara ili animimie mvinyo

    Clara akanitazama kwa mshangao.Akanimiminia mvinyo katika glasi nikaunywa wote kwa mara moja.

    “One more please” Nikasema.Clara akanimiminia tena mvinyo katika glasi nikanywa na kuweka glasi mezani.

    “I’m sorry Wayne” Clara akasema

    “Usijali Clara,ni mambo ya kwaida.”

    Kimya kikapita cha dakika mbili hivi halafu nikasema

    “Clara samahani kwa hali ilivyobadilika ghafla,lakini nimeshindwa kuvumilia.I feel so much pain inside.This is beyond pain Clara.” Nikasema kwa uchungu mwingi huku Clara akinisugua sugua

    “Its ok Wayne.You are gonna be fine.You are gonna be ok” Akasema Clara.

    “I don’t think so Clara.No body knows how I feel inside.” Nikajibu.Kikapita kimya kidogo Clara akauliza

    “Wayne what happened? Can you tell me? “

    “Clara sijui hata nikueleze kitu gani.Lets not talk about it now.Lets not ruin our evening.Tumekuja hapa kupoteza mawazo na si kuongeza mawazo.Lets drink and have fun” Nikasema na kujimiminia mvinyo katika glasi nikanywa.Clara naye akamimina mvinyo akanywa..

    Muda ulizidi kwenda na kiza kikaanza kuingia.Tulikuwa tukiongea na kucheka kwa furaha sana .Kwa mara ya kwanza toka matatizo ya Emmy yamenikuta nilikuwa na furaha iliyopitiliza.Tuliongea mambo mengi huku tukicheka na kupata mvinyo.Ilikuwa ni siku nzuri . Kwa muda wa masaa haya machache nilisahau kabisa kama muda mfupi uliopita nilikuwa nimezama katika dimbwi la matatizo.Nilistaajabia uwezo wa Clara wa kuweza kunisahaulisha japo kwa masaa machache machungu yote yaliyonisibu .Mwanamke huyu alikuwa na uwezo wa ajabu sana.Alikuwa miongoni mwa wale watu wachache mno ambao wana uwezo wa kutamka neno moja likasababisha mabadiliko makubwa katika maisha ya watu.Nilivutiwa mno kuwa karibu na Clara .Japokuwa hapo kabla niliweka ahadi kwamba kwa jinsi alivyonitenda Emmy sintathubutu kuwa na mwanamke mwingine tena maishani .Nilikuwa nikiamini kwamba wanawake wote ni sawa.Baada ya kukutana na Clara msimamo wangu umeanza kutetereka na nimeanza kuamini bado wapo wanawake wazuri na wenye kunifaa na mmoja wao ni huyu mrembo aliyekaa nami mezani,ambaye amenisahaulisha machungu yote niliyoyapata .Clara alikuwa mwanamke mcheshi,mkarimu

    ,na mwenye uelewa wa mambo wa kiasi cha juu mno.Ni mwamanke msomi,mzuri na mwenye ndoto za kufanya kazi kwa bidii na kufikia malengo aliyojiwekea.Ni

    lipata shauku ya kutaka kumfahamu Clara kiundani zaidi .Sikufichi ndugu msomaji nilikuwa nimevutiwa mno na Clara.Mvuto huu haukutokana na ya pombe tulizokuwa tunakunywa lakini nilihisi kuna kitu kipo moyoni ambacho ni vigumu kukielezea.Nilihisi kuna kitu kipo kati yetu sisi wawili .Nilikuwa na hisia na furaha ya ajabu sana ambayo sijawahi kuipata wakati nikiwa na Emmy.

    “Nilipoteza muda mwingi kwa Emmy na kumbe wako wanawake wengine wazuri wenye kujiheshimu “ niliwaza huku nikimuangalia Clara usoni.

    “Wayne nimekuona unaniangalia sana usoni kwa muda mrefu sasa.Whats wrong? Clara akauliza baada ya kugundua kwamba nilikuwa nikimuangalia usoni.Ni kweli nilikuwa nikimuangalia.Sikuisha hamu ya kuitazama sura ile nzuri .

    Nilitabasamu na kujibu

    “Clara imenibidi nikuangalie tena na tena usoni ili nithibitishe kama mwanamke niliyenaye mezani ni binadamu wa kawaida au ni roho.” Nikasema na kumfanya Clara acheke kwa sauti.

    “Kwa nini unasema hivyo Wayne? Clara akauliza

    “Its ..uhhmm …I feel something strange with you…kwa muda wa masaa haya machache tuliyokaa pamoja hapa najiona kama mtu mpya.Najisikia huru na mwenye furaha kupita kiasi.Kwa muda huu mfupi nimeweza kuyasahau matatizo yangu yote niliyonayo.Kwa muda huu mfupi ninajiona ni kama vile ninaishi katika dunia isiyokuwa na matatizo ya aina yoyote..I feel like you have some power..a magic power which makes people forget their problems.”Nikasema huku Clara akiwa hana mbavu kwa kucheka.Alicheka sana na kunifanya nami nicheke pia.Akachukua kitambaa na kujifuta machozi yaliyotokana na kucheka.

    “Wayne umenifurahisha sana leo.Sijawahi kukutana na mtu aliyenifurahisha kama wewe.Hebu leta mkono wako hapa” Clara akasema nami bila kukawia nikaunyoosha mkono wangu akaushika na kuupeleka katika bega lake.

    “Hiki umeshika ni kitu gani? Akauliza

    “Hili ni bega” Nikajibu.

    “Una hakika umeshika bega?

    “Ndiyo Clara hili ni bega”

    “Ok Good..kama una hakika kwamba hili ni bega basi mimi si mzimu.Mzimu ni roho na hauna nyama and above all mzimu haunywi mvinyo” Akasema Clara na wote tukajikuta tukiangua kicheko kikubwa.

    “I wish like I could be this happy everyday” Nikasema

    “Me too” akasema Clara huku akitabasamu.

    “Bado nina muda wa wiki nzima wa kuwapo hapa Arusha.Kama na wewe utakuwa na muda wa kutosha bado tunaweza kuendelea kukutana na kuwa na furaha kila siku.Siwezi kukataa Wayne kwamba leo nimefurahi sana. I had a very great time with you.Nimeipenda kampani yako” Nilitabasamu kuisikia kauli ile ya Clara .Akainua mkono wake na kuitazama saa

    “wayne inakaribia saa tano za usiku.Nikiendelea kukaa na wewe hapa tunaweza tukafika asubuhi.Its time to go now.I had a very great time Wayne.” Clara akasema kwa sauti ya chini ambayo ilionyesha wazi ni kwamba alipenda kuendelea kukaa nami.

    “Clara sipati neno la kukushukuru kwa jinsi ulivyoifanya siku yangu ya leo kuwa yenye furaha .Nashukuru sana Clara.” Nikasema huku nikimalizia mvinyo uliokuwa ndani ya glasi.

    “Hapa arusha umefikia wapi? Nikauliza

    “Nimefikia SEAN 11 Lodge wewe unaishi maeneo gani?……” Akasema

    “.Mimi ninaishi Majengo” Nikasema huku nikisimama

    “Nashukuru kukufahamu Wayne.You are such a wonderfull guy…” Clara akasema na kunipa mkono.

    “Hata mimi nafurahi sana kukufahamu Clara.Sikutegemea kama siku ya leo ingeisha nikiwa na furaha ya ajabu namna hii.uhhm .if its ok with you can you give me your phone number ? Nikasema.

    “Nipe wewe namba yako kwa sababu bado sina namba ya simu ya Tanzania.Nitakupigia mimi” Clara akasema.Nikamuandikia namba zangu na kumpa.

    “Kesho tutaonana wapi? Nikamuuliza.

    “Ratiba yangu ya kesho inaonyesha nitakuwa na shughuli nyingi lakini nitakutaarifu kama nitapata nafasi ama vipi” Clara akasema huku akianza kupiga hatua kuondoka na mimi nikiwa pembeni yake.Nilihisi msisimko wa ajabu kutembea na mlimbwende yule.Mwendo wake wa maringo ulinifanya nijione kama ninatembea na malaika.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Are you sure you can drive? Kama hujisikii kuendesha let me take you to a hotel” Nikamuuliza

    “No thank you Wayne.I’m a bit drunk but I can manage”

    Nilimsindikiza Clara katika gari lake akaingia na kuliwasha.Sikuondoka pale hadi alipoligeuza na kuliweka tayari kwa kuondoka.Akashusha kioo na kunipungia mkono.

    “Good night Wayne” Akasema .

    “Good Night Clara” Nikajibu .Clara akafunga kioo na kuliondoa gari.Nililitupi

    a macho gari lile likiondoka hadi lilipopotea kabisa machoni pangu.Nikaelekea katika gari langu nikaingia na kukaa nikiwa nimeuinamia usukani

    “What a wonderfull woman…sidhani kama atakuwa binadamu wa kawaida yule..si mzimu kweli yule? Lakini hapana, nimeushika mkono wake na kuhakikisha ni binadamu wa kawaida.Mwanamke huyu mbona ameuteka moyo wangu ghafla namna hii? Gosh hizi ni hisia za kweli au ni hizi pombe nilizokunywa?…N

    ikawaza.”

    “Yeroo…..Mbona unainamia sukani..umesidiwa tukupeleke sipitali?” Sauti ya mlinzi wa kimasai aliyekuwa akilinda eneo lile ndiyo inanistua katika mawazo .

    “Ouh Rafiki..niko mzima siumwi kitu” Nikawasha gari na kuondoka

    **********

    Saa tisa za usiku bado nilikuwa sijapata usingizi.Toka nimerudi nimekuwa nikihangaika kitandani kujaribu kutafuta usingizi bila mafanikio.Sikuelewa sababu ilikuwa ni pombe nilizokunywa au ni mawazo niliyokuwa nayo.Mawazo mengi sana yamekuwa yakinijia kichwani .Kubwa ilikuwa ni kumbukumbu ya mambo yaliyotokea jioni ya siku iliyotangulia.Kumbukumbu hii ilikuwa ikijirudia kichwani kama filamu na kunifanya nitabasamu.

    “Clara…” Nilisema kwa sauti ndogo huku nimekaa kitandani

    “You are such an amazing woman.” Nikasema huku nikitabasamu.

    “ hatimaye nimekutana na mwanamke wa ndoto zangu.Clara is a perfect woman for me.Ana kila kitu ninachokihitaji kwa mwanamke wa ndoto zangu” Nikajilaza tena kitandani.

    “ I think like I’ve lost her.Itakuwaje kama sintaonana naye tena? Vipi kama hatanipigia simu tena? Ouh Mungu wangu ninakufa na mawazo ya huyu mwanamke.”

    Nikainuka kitandani na kwenda kuketi sofani.

    “Sintasafiri tena kama nilivyokuwa nimepanga.Kuonana na Clara kumenifanya nimsahau Emmy ghafla.Nilazima nionane tena na Clara.Siwezi kukubali kumpoteza.Nitam

    saka dunia nzima hadi nimpate……..” Nikawaza huku nikiwa nimejilaza sofani.

    Sikumbuki saa ngapi usingizi ulinichukua .Nilistushwa na mvumo wa simu iliyokuwa pembeni yangu.Nikafumbua macho yaliyokuwa mazito kutokana na usingizi.Nikaichukua simu na kuangalia mpigaji.Alikuwa ni baba mkwe.

    “baba shikamoo” Nikamsalimu.

    “marahaba Wayne habari za leo?

    “nzuri tu baba habari za kwenu?

    “Huku kwema.Nimekupigia ili nijue unaendelea vipi “ baba mkwe akauliza

    “Ninaendelea vizuri baba Nashukuru” Nikajibu

    “Ok Nashukuru sana kama unaendelea vizuri.Ukiwa na tatizo lolote lile tafadhali tupigie simu sisi wazee wako tupo tutakusaidia”

    “Sawa baba nashukuru” Nikajibu na baba mkwe akakata simu.

    Niliyafikicha macho ili niweze kuona vizuri.Nilitazama saa ilipata saa tatu za asubuhi.Haikuwa kawaida yangu kulala kwa muda mrefu namna hii .Nadhani hii ilitokana na pombe tulizokuwa tumekunywa jana yake.Tulimaliza chupa nzima ya mvinyo mkali.Mvinyo ule tuliokunywa jana yake ukanifanya niikumbuke sura ya kuvutia yenye nuru na tabasamu muda wote,sure yenye macho mazuri meupe ambayo ungependa yakuangalie muda wote,sura yenye midomo laini na mizuri ambayo kila anapotasamu huanikiza meno meupe yaliyojipanga vyema kinywani,ni sura ya mwanamke wa kipekee kabisa Clara ambaye toka nimekutana naye jana yake amenikosesha usingizi na kunifanya usiku mzima nikeshe nikimuwaza yeye.

    Niliipekua simu ili kuangalia kama Clara alipiga wakati nikiwa usingizini au alituma ujumbe wa maneno lakini hakukuwa na simu yoyote iliyopigwa wala ujumbe toka kwa Clara.Nikaitupa simu pembeni.

    “Laiti kama ningezifahamu namba za simu za hoteli aliyofikia ningempigia walau kumjulia hali.Nina hamu ya kutaka kuisikia tena sauti yake nzuri.Lakini bado mapema ndiyo kwanza saa tatu.Ni lazima atanipigia .Kwa namna nilivyokuwa nimemgusa ni lazima atanipigia.Ngoja niendelee kusubiri” Nikawaza.

    Mwili ulikuwa mzito kuinuka pale kitandani.Nilihisi njaa kali.Nikaenda jikoni nikatazama katika friji lakini sikupata chochote cha kuweza kula..Nikaamua nioge halafu nitoke kwenda kutafuta supu safi.Kisha oga niliigia garini na kuondoka kwenda kutafuta chochote cha kutia tumboni asubuhi ile hususan supu .Bado sura ya Clara ilikuwa ikinijia akilini kila mara na kuniweka katika fikara nzito.

    “This is what they call love at first sight.Yaani kumuona jana tu tayari ameniteka akili namna hii.Sina shaka na hisia zangu.Ninaamini moyo wangu haunidanganyi kwamba Clara ndiye mwanamke anayenifaa maishani.” Nikawaza huku nikipata supu.

    Mpaka saa nne za usiku Clara hakuw amenipigia simu kama alivyokuwa ameahidi.Niliumia sana kwa kitendo hiki.Mishale ya saa ilizidi kusonga kwa kasi hadi ilipofika saa sita za usiku lakini sikuwa nimepokea simu yoyote au hata ujumbe wa maneno toka kwa Clara.Kichwa kilijaa mawazo mengi.Mwishowe nikaamua kulala.

    Siku ya pili ikakatika bila ya kupokea tena simu toka kwa Clara.Nilijiuliza maswali mengi kulikoni asipige simu wakati alikwisha ahidi kunipigia? Nini kimetokea? Ndugu msomaji nilikuwa na mawazo mengi mno kwa Clara kushindwa kunipigia simu.Nilianza kupatwa na mawazo pengine hakuwa na nia ya kweli ya kunipigia simu na aliongea vile kwa ajili ya kuniridhisha.Ni

    lianza kukata tamaa ya kuonana tena na Clara .Nilijiona kama ni mtu nisiyekuwa na bahati katika suala la urafiki na watoto wakike.





    Siku ya alhamisi saa tatu za usiku nikiwa nimepumzika nyumbani nikiangalia filamu,mara simu yangu ikaita.Nikaichu

    kua na kutazama mpigaji.Zilikua ni namba ngeni katika simu yangu.Nikabonyeza kitufe cha kupokelea simu.

    “Hallo” Nikasema

    “Hallo naongea na Wayne? Sauti ya kike ikauliza ambayo moja kwa moja niliitambua ilikuwa ni sauti ya Clara.Nikapatwa na furaha ya ghafla.

    “yah hapa unaongea na Wayne.Nani mwenzangu? Nikauliza huku nikijifanya kutoifahamu sauti ile .

    “Unaweza ukaikumbuka sauti hii? Akauliza Clara huku akicheka kicheko cha chini chini kama kawaida yake

    “yah …nadhani…uhhm hii itakuwa ni sauti ya Clara..” Nikasema halafu Clara akacheka kicheko kikubwa.

    “Nilitegemea utakuwa umeshaisahau sauti hii” Clara akasema huku akicheka

    “katika sauti zote za dunia hii sauti hii sintaweza kuisahau hata sekunde moja.hata Ukiwa katika kundi la watu elfu moja sauti yako nitaitambua tu kwa sababu ni sauti ya kipekee sana….” Nikasema huku sura yangu ikiwa imepambwa na tabasamu zito.Clara akaendelea kucheka

    “Wayne habari za toka tulipoonana?

    “habari nzuri Clara.Sijui wewe.Niliona kimya kingi nikajua pengine umeshazipoteza namba zangu” Nikasema

    “Ouh No Wayne..siwezi kuipoteza namba yako.Nilishindwa kukupigia nilikuwa nimebanwa mno na ratiba.Unajua siku zenyewe ni chache na mambo yalikuwa mengi sana kwa hiyo ikanibidi kufanya kazi hadi usiku wa manane kila siku.Nasuhukuru Mungu tunamalizia leo” Clara akasema kwa sauti tulivu

    “Ouh kumbe mnamaliza leo?

    “Ndiyo Wayne leo tunamaliza .Lakini kesho kutakuwa na sherehe za kuchangia kituo cha watoto wanaoishi katika mazingira magumu cha Future generation Hafla hiyo itafanyika kuanzia saa moja za usiku.Ninaomba kama utakuwa na nafasi twende wote”

    “Clara nitakuwa na nafasi ya kutosha hivyo usihofu tutakwenda wote.”

    “Nashukuru sana kwa kukubali kwenda nami katika hafla hiyo.Nitakutegemea unipitie hapa hotelini kwangu saa kumi na mbili za jioni.” Clara akasema

    “Hakuna tatizo Clara nitafika hapo hotelini kwako mida hiyo uliyosema.”

    “Ok Wayne goodnight”

    “Goodnight Clara” Nikajibu na simu ikakatwa.Nilipatwa na furaha ya aina yake.Nilikwisha kata tamaa ya kuonana tena na Clara.Simu hii aliyopiga ilinirudishia furaha na matumaini ya kumuona tena mrembo yule.

    * * * *

    Saa kumi na mbili juu ya alama ilinikuta katika geti la kuingilia SEAN 11 LODGE alikofikia Clara.Sikutaka kuchelewa miadi na mrembo huyu wa kutukuka.Nilishuka katika gari nikajiangalia na kujiona niko safi kabisa kwa ajili ya shughuli ya usiku huu.Nilikuwa nimependeza kupita maelezo.Nilikuwa nimevaa suti kali nyeusi .Ukiwa umeambatana na mrembo kama huyu inakubidi na wewe uwe umependeza isivyo kawaida ili muendane.Nilitembea kwa mikogo hadi mapokezi.Nikawasalimu akina dada wawili waliokuwa pale wenye nyuso za furaha.Nikawaomba wamtaarifu Clara kwamba mgeni wake amekwisha fika.dada mmoja akachukua simu akapiga halafu akaiweka simu chini akaongea na mwenzake ambaye akaja akanichukua na kunipeleka katika ukumbi.Nilionyeshwa meza moja iliyokuwa na viti viwili ambayo ilikuwa pembeni kabisa mwa ukumbi ule uliokuwa na mwanga hafifu na watu wachache.Muhudumu yule akanivutia kiti na kunikaribisha.

    “Clara amesema ukae hapa utumie chochote kile unachoona kitakufaa kwa muda huu unapomsubiri.yeye bado anajiandaa.” Akasema dada yule mwenye lafudhi ya kichaga

    Nilimwambia aniletee mvinyo mwepesi .Nilikuwa na mawazo mengi juu ya Clara.Niliwaza jinsi muonekano wake utakavyokuwa usiku wa leo ,niliwaza jinsi tutakavyoongozana katika shughuli hiyo.Niliwaza mambo mengi sana.Dakika ishirini toka nifike pale mara kwa mbali nikamuona mtu akija kwa mwendo wa madaha mno.Toka kwa mbali niliweza kumtambua alikuwa ni Clara.Mrembo yule alikuwa aking’aa usiku huu.Kadiri alivyopkuwa akisogelea pale mezani ndivyo moyo wangu ulivyoongeza kasi ya mapigo yake. Alikuwa amevaa gauni refu jekundu lililokuwa likingaa kila limulikwapo na mwanga wa taa.Shingoni alikuwa amevaa mkufu mdogo wa dhahabu wenye kung’aa na mkononi alikuwa na pochi ndogo nyekundu.Chini alikuwa amevaa viatu virefu vyekundu.kwa ujumla alikuwa amependeza isivyo kawaida.

    “Waoo !! Wayne you are amazing tonight….samahani sana kwa kuchelewa” Akasema Clara akiwa amesimama pembeni ya ile meza huku akinipa mokono.

    “Bila samahani Clara.You look like a heaven angel tonight ” Nikajibu huku nikitabasamu.Clara akacheka na kusema

    “Angels don’t wear high hills ” Tukacheka wote kicheko kikubwa.

    “nadhani tunaweza kuondoka..” akasema Clara.Tukatoka na kuingia katika gari langu tukaondoka kuelekea katika hafla ya uchangiaji wa kituo cha watoto wanaoishi katika mazingira magumu.

    “Nimefurahi sana kukuona tena Clara” Nikaanzisha mazungumzo ndani ya gari.

    “ I missed you Wayne…did you miss me? Akauliza Clara .

    “I missed you so badly.Siku zilivyokuwa zikikatika bila ya kupata simu yako nilikuwa na mawazo mengi mno.Niliwaza pengine labda umepoteza namna yangu,au pengine …….”

    “Pengine nini” akauliza Clara huku akitabasamu

    “pengine labda hukujisikia kunipigia kwa kuogopa usumbufu wa namna moja au nyingine”

    “Pole sana Wayne kwa usumbufu huo ulioupata .Sikufanya makusudi kutokukupigia simu.Nilikuwa nimebanwa sana na ratiba ndiyo maana sikuweza kupata muda wa kukaa na wewe.mambo yalikuwa mengi na siku zilikuwa kidogo.”

    Tuliendelea na maongenzi na kutaniana huku tukicheka kwa furaha na hatimaye tukafika mahala inapofanyikia hafla hiyo.Hapo nje palikuwa na magari mengi ya watu waliokuwa wamekuja katika kuchangia.

    Tuliposhuka garini Clara akaukamata mkono wangu na kisha tukaanza kuingia ukumbini kama wapenzi.

    “Do you mind? Akaniuliza iwapo nitajali kwa kitendo kile cha kunikamata mkono.Sikujibu kitu nikatabasamu naye akatabasamu .Nilikuwa nimefurahi moyoni kupita kiasi kwa kitendo kile cha kuingia ukumbini huku tumeshikana mikono kama wapenzi.Yeyote ambaye angetuona angefikiri kwamba sisi ni wapenzi tena tunaopendana mno.Nilifarijika mno kwa kitendo kile.Nilijiona ni mwanaume mwenye thamani tena.

    Watu walikuwa ni wengi ndani ya ukumbi huu mkubwa.Watu walikuwa wakitukodolea macho wakati tukipita kutafuta meza.Wengine walikuwa wakinong’onezana.Sikuelewa ni kwa nini ilitokea vile.labda ni namna tulivyokuwa tumependeza.Ghafla bila kutegemea niliona kitu ambacho sikuwa nimekitegemea kukiona mahala pale.Katika meza moja nilimuona Emmy akiwa amekaa na Chris pamoja na watu wanaofanya kazi kampuni moja na Chris ambao baadhi yao niliwafahamu kupitia kwa Chris.Macho yangu na Emmy yakagongana.Niliuona mstuko wa wazi uliompata.Akainamisha kichwa chake chini kukwepa macho yangu.Chris alistuka baada ya kuona jinsi mpenzi wake alivyo badilika ghafla.Alipogeuka kuangalia tukagonganisha macho.Amani ikamtoweka ghafla.Sikuwajali nikamshika mkono Clara tukaendelea kwenda mbele katika meza zilizokuwa wazi.

    Sikuwa nimefikiria kama ningeweza kuonana na Emmy mapema namna hii.Niliamini kwamba kwa sasa mwanamke yule hayuko moyoni mwangu kwa sababu pamoja na kugonganisha macho katu sikuwa na mstuko wowote .Nilijisikia amani kubwa moyoni.Hiki kilikuwa ni kipimo tosha kwamba tayari hana nafasi yoyote tena moyoni mwangu.Kilichokuwa kikinijia mara kwa mara na kunipa mawazo mengi ni sura ya Baraka.Sikujua mpaka sasa hivi atakuwa katika hali gani.Nilizoea kucheza naye kila siku,nilikumbuka jinsi tulivyokuwa tukikaa bustanini hasa nyakati za usiku tukipiga magitaa yetu na kuimba.Zilikuwa ni nyakati za furaha sana.Sikutegemea kama huko aliko alikuwa akipata furaha kama aliyokuwa akiipata alipokuwa na mimi.Sikuwa na namna ya kufanya ili niweze kuonana naye tena.Sikutaka kuwa karibu na Emmy kwa namna yoyote ile.Sikutaka kumbughudhi katika maisha yake mapya.Nilichokifanya ni kuomba Mungu siku moja anikutanishe na Baraka japo kwa dakika mbili ili niweze kufurahi naye tena.

    “Wayne mbona huagizi vinywaji? Akauliza Clara baada ya kurudi toka katika meza ya jirani alikokuwa amekwenda kuwasalimia wanamitindo wenzake.

    “Ninakusubiri wewe ili tuagize kwa pamoja” Nikasema na mara muhudumu akafika tukaagiza vinywaji.

    “Nilikuwa nawasalimia marafiki zangu.” Akasema Clara.

    “Nimewaona.They are so pretty” Nikatania.

    “Shhhhhhh!!! Don’t ever say that to me Wayne.I’m so jelousy…don’t talk to any woman tonight..I wont allow any woman to steal you from me tonight ..I’m gona kill the one who try” Clara akasema huku akicheka kwa nguvu sana na mimi pia nikacheka.

    “Kusema ukweli umependeza sana Wayne.You are the cutest man tonight.Naogopa nisije nikaibiwa” Clara akasema huku akiendelea kucheka.Kama hujamfahamu Clara unaweza ukadhani labda amekwisha lewa lakini hivi ndivyo alivyo.Ni mtu mcheshi ,mchangamfu na mwenye utani mwingi.Manenoyale ya utani aliyoyaongea yanazidi kunipandisha joto la mwili.Nilitamani kama angekuwa akimaanisha kile alichokuwa anakisema.Nilitmani kuwa na Clara muda wote.Ni mwanamke ambaye ana heshima,mstaarabu ,mwenye kujipenda,mwenye kujali watu,mcheshi na mkarimu.Sifa zote hizi zilinifanya nivutike kutaka kuwa naye muda wote.

    “Ok here’s the deal.I’m not going to talk to any woman and you don’t talk to any man..deal?

    “Deal” akajibu Clara huku akicheka kicheko kikubwa.Watu waliokuwa meza za karibu walikuwa wakitushangaa kwa jinsi tulivyokuwa tunafurahi.

    “mwanaume yeyote akikaribia meza hii ninamtoa kwa makofi” Nikasema na tukaendelea kucheka.

    “Wayne umeshawahi kupigana katika maisha yako”

    “Yes ! “ nikajibu kwa ufupi

    “Sura yako ya upole haionyeshi kama ni mtu wa vurugu.” Akasema huku akitabasamu

    Sherehe zilifunguliwa na mgeni rasmi aliyekuwa mbunge wa jimbo la Arusha mjini.Baadae shughuli za uchangiaji zikaanza.Baadhi ya makampuni yaliyokuwa yamealikwa yalikuwa yametuma wawakilishi wao kuleta michango yao ambao walikuwa wakipita mbele na kukabidhi kiasi kilichotolewa na kampuni husika.Kampuni zilikuwa ni nyingi na mara nikasikia kampuni anayofanyia kazi Chris ya Amazora safari ikitajwa.Chris ndiye aliyekuwa akiongoza kundi la wafanyakazi wa Amazora safari kwenda kukabidhi michangoya kampuni .Miongoni mwao alikuwepo Emmy.Sikutaka kuwatazama tena nikayarudisha macho na mawazo yangu mezani.

    Michango bado iliendelea kutolewa Makampuni na watu mbali mbali walikwisha toa michango yao na ndipo muongoza shughuli akachukua kipaza sauti na kumkaribisha muandaaji wa shughuli ile mama Blandina chokasi ambaye alifika pale mbele akakabidhiwa kipaza sauti ili aweze kuongea jambo.Ukumbi wote ukakaa kimya ili kumsikiliza mama yule.

    “Ndugu mgeni rasmi,mheshimiwa mbunge wetu wa Arusha mjini,wawakilis

    hi wa makampuni mbali mbali,ndugu wageni waalikwa mabibi na mabwana ninapenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru kwa namna mlivyojitokeza kwa wingi kuchangia kituo hiki cha watoto wanaoishi katika mazingira magumu cha future generation.Kuji

    tokeza kwenu kunaonyesha ni jinsi gani nyote mnavyoguswa na matatizo ya watoto hawa ambao wengi wao hawana wazazi au wazazi wao hawana uwezo wa kuwatunza.Najua nyote mna majukumu mengi lakini mmejibana na kutoa kile mlichokuwa nacho kwa ajili ya kuwasaidia watoto hawa masikini.Sisi hatutaweza kuwalipa chochote il tunawaombea kwa Mungu awazidishie wote mara mbili ya mlicho nacho na awape moyo wa kuweza kujitolea zaidi kwa ajili ya watu masikini na wasio na uwezo.” Akatulia na ukumbi wote ukalipuka kwa makofi na vigere gere halafu akaendelea.

    “Ndugu wageni waalikwa mabibi na mabwana,bado shughuli yetu inaendelea lakini nimesimama hapa kwa ajili ya jambo maalum kabisa.Nimesimama hapa kwa ajili ya kutoa shukrani za kipekee kwa mtu ambaye kampuni yake ndiyo imefanikisha jambo hili muhimu la leo.Ni mwanadada wa kitanzania ambaye kazi zake za mitindo na urembo zimevuka mipaka ya nchi yetu na kufika mbali .Kwa sasa mwanadada huyu anafanya kazi za mitindo na ubunifu nchini afrika ya kusini.Ni mbunifu mkubwa wa kimataifa na kampuni yake inafahamika kote duniani.Amekuwa akishiriki katika matamasha na majukwaa mbali mbali makubwa ya urembo duniani.Mbunifu huyu amekuwa akifanya juhudi kubwa katika kuhakikisha kwamba wabunifu na wanamitindo wa kitanzania wanafahamika duniani.Kupitia kampuni yake ya Black angels amekwisha wasaidia wanamitindo zaidi ya 30 kupata mikataba na kufanya kazi na makampuni makubwa ya urembo duniani,vile vile amefanikisha kuwatangaza wabunifu wa kitanzania katika majukwaa makubwa ya mitindo duniani.Mbunifu huyu amekuwa na mchango mkubwa sana katika umoja wa wabunifu na wanamitindo wa Tanzania.Mara kwa mara amekuwa akija na kutoa semina kwa wabunifu na wanamitindo wachanga.Kwa muda wa wiki mbili sasa tumekuwa naye hapa Arusha akiendesha semina ya mambo haya ya ubunifu na urembo.Kwa kuifanya fani hii ya mitindo na urembo izidi kukua hapa nchini aliona haitakuwa vizuri kama semina ile itaisha hivi hivi ,akabuni lifanyike jambo hili la kuichangia jamii.Kila mwaka tutakuwa tunafanya kitu kama hiki na kuichangia jamii yetu katika matatizo mbali mbali iliyokuwa nayo.Mabibi na mabwana naomba sasa nimtambulishe kwenu rais wa kampuni ya Black angels Bi Clara msikongo.Kokote uliko tafadhali Clara simama uwasalimu wageni waalikwa.”

    Clara akasimama na kupunga mikono,ukumbi wote ukalipuka kwa makofi na vigere gere.Nilikuwa nimestuka sana.Sikujua kama nimekaa na mtu mkubwa na maarufu namna ile.Nilimtazama Clara akiwapungia mikono wageni mle ukumbini huku akiwa na tabasamu zito Sikuamini macho yangu.

    “Clara tafadhali naomba upite uje huku mbele ili uongee neno lolote kwa hadhira hii iliyokusanyika hapa usiku huu” mama Blandina akasema.

    Clara akachukua pochi yake pale mezani halafu akanisogelea akaniinua mkono.Nilielewa alikuwa akitaka niinuke pale kitini.Moyo ulikuwa ukinienda mbio sana.Alitambua kwamba nilikua mzito kusimamam akaniinamia na kuninong’oneza sikioni.

    “Don’t be nervous..smile” akasema.Nikainuka na kuanza kutabasamu.Akanishika mkono tukaanza kutembea kwa madaha kuelekea jukwaani.Makofi na vigere gere vilikaribia kulichana paa la ukumbi ule mkubwa.Miguu ilikuwa ikinitetemekaSi

    kuelewa hofu ile ilikuwa imetoka wapi.Tulipanda jukwaani nikasimama pembeni ya Clara ambaye akapewa kipaza sauti ili aongee machache

    “mabibi na mabwana habari zenu.”

    “Nzuriiii” Ukumbi wote ukaitikia huku makofi yakipigwa.

    “Awali ya yote napenda kuwashukuru sana kwa kuitika mwito wetu.Japokuwa ilikuwa ni taarifa ya muda mfupi lakini mmeweza kujitokeza kushirikiana nasi katika kuchangia jambo ili muhimu.Kila siku tunashuhudia ongezeko la watoto wanaoishi mitaani katika mazingira magumu.Kama wana jamii tuna jukumu la kuwasaidia watoto hawa ambao wengi wao hawana wazazi au kama wana wazazi basi ni masikini sana.Ni jukumu la kila mwanajamii kuhakikisha kwamba anatoa kile kidogo alicho nacho kwa ajili ya kuwasaidia watoto hawa .Kuna makundi mengi yanayohitaji msaada kama vile wanawake wenye maradhi ya Fistula,wanawake wanaosumbuliwa na kansa ya matiti n.k Sisi kama jukwaa la wanamitindo tumeamua kuanza kwanza na kundi hili la watoto hawa na kisha tutachangia makundi mengine.” Clara akatulia na ukumbi wote ukalipuka kwa makofi

    “Ndugu zangu uwingi wenu usiku huu wa leo umenipa faraja sana kwamba sasa fani hii ya urembo imeanza kueleweka katika jamii kwamba si uhuni kama ilivyokuwa ikidhaniwa hapo awali bali ni kazi kama kazi nyingine zozote.Fani hii ya urembo kama ikitiliwa mkazo inaweza kuwa ni mkombozi wa ajira kwa vijana wetu wengi.Tunaiomba serikali iitazame fani hii kwa upana wake kwa sababu ni fani ambayo inaweza ikatutangaza sana kimataifa kama tunavyojitahidi kufanya hivi sasa japokuwa mchango wa serikali bado ni mdogo mno.Ndugu zangu sitaki kuchukua muda mrefu wa kuongea kwa sababu bado kuna mambo mengine yanaendelea.napenda kabla ya kumaliza niseme kwamba pamoja na kwamba mimi ni mmoja wa waandaaji wa shughuli hii lakini mimi na mwenzangu hapa tunao mchango wetu ambao tunautoa kwa ajili ya watoto hawa.Kwa pamoja tunatoa cheki yenye thamani ya fedha za kitanzania shilingi millioni hamsini.” Ukumbi wote ukalipuka kwa kelele za shangwe.Nilistuka sana.Sikuwa nimeongea na Clara kuhusu jambo lolote lile kuhusiana na fedha zile alizosema tumetoa kwa pamoja mimi na yeye.Clara akatoa cheki akaikabidhi huku makofi na vigere gere vikizidi.



    “Kabla hatujaondoka nadhani mwenzangu hapa na jambo la kusema” Clara akasema akiwa na maana ya mimi.Sikuwa nimejiandaa kusema lolote na sikujua niseme nini.Nilihisi kutetemeka.Sikuwa na uzoefu wa kuongea mbele ya hadhira kubwa kama ile iliyobeba watu mashuhuri na matajiri.Clara akanipa kipaza sauti huku akitabasamu.Nilikipokea japo mikono ilikuwa ikinitetemeka.Nilikishika kipaza sauti nikakisogeza karibu na mdomo wangu.Clara akaniangalia kwa tabasamu.Sijui nilipata wapi nguvu na uwezo wa kuongea ghafla nikajikuta nikisema

    “Mabibi na mabwana,sina mengi ya kuongea kwa sababu mengi amekwisha yaongea mwenzangu hapa.Ninachotaka kukisema ni kwamba kadiri muda ulivyokuwa ukienda mimi binafsi nimejikuta nikizidi kuguswa na maisha ya watoto hawa.Nimejikuta nikitaka kuchangia tena na tena lakini uwezo unakuwa hauruhusu.Kwa namna nilivyoguwa naomba kama mimi nitoe ahadi ya kuchangia tena shilingi millioni thelathini pesa ambayo nitaitoa kesho.” Ukumbi wote ukalipuka kwa shangwe .Nikatabasamu baada ya kuiona furaha ile ya watu.Nikamrudishia Clara kipaza sauti lakini kabla hajakikabidhi kwa mama Blandina akaniomba nisogee karibu yake.Nikasogea akauinua mkono wake na kuuzungusha shingoni kwangu akaniangalia kwa tabasamu na kusema.

    “Mabibi na mabwana na mimi naongeza tena shilingi millioni ishirini .Jumla mimi na mwenzangu hapa tunatoa shilingi za kitanzania millioni mia moja.Ahsanteni sana” Ukumbi ukalipuka kwa kelele za shangwe.Clara akanishika mkono tukaanza kushuka ngazi huku ukumbi wote ukiwa umesimama ukitushangilia .Nilihisi kama miguu inagongana wakati tukirudi katika meza yetu.Sikuwa nimetegemea kitu kama kile kutokea.Mambo yale makubwa yalitokea kwa haraka sana.Niliona ni kama ndoto vile.

    “You did great..I didn’t expect you could be such a smart guy….Wayne you are amazing..congraturations” Clara akaninong’oneza sikioni wakati tukikaa kwenye viti vyetu.Sikujibu kitu nilikuwa nikitabasamu.Nikatoa kitambaa na kujifuta jasho lililokuwa likinitoka kama nimemwagiwa maji.

    Mambo yaliyokuwa yametokea pale ukumbini yalikuwa ni kama ndoto .Sikuwa nimetarajia kuwa mambo yangekuwa kama vile.Siwezi kuelezea ni jinsi gani nilivyokuwa nimefurahi moyoni.

    Baada ya kushuka toka jukwaani meza yetu ilikuwa haikauki watu waliokuja kutupa mikono ya pongezi..Huu ulikuwa ni usiku wa kipekee sana kwangu.Nilifura

    hia sana kwa namna Clara alivyonifanya niyasahau masahibu yote yaliyokuwa yamenikumba .Kila nilipomtazama Clara usoni nilishindwa kuamini kama ni yeye kweli ndiye aliyeweza kunifanya nikawa na furaha kubwa namna ile.Katika usiku ule nilikuwa nimepata heshima kubwa na ya kipekee kwanza kwa kuongozana na mwanamke mwenye sifa kubwa kama Clara, na pili kitendo cha kusimama jukwaani na kuongea na hadhira ile kubwa ya watu na kuwafanya wote walipuke kwa shangwe kilinipa heshima kubwa mno ambayo sikuwa nimetarajia kuipata.Emmy alinidharau na kuniona si mtu mbele ya watu lakini leo Clara amenirudishia heshima yangu iliyopotea..Nilipokumbuka kwamba Emmy naye alikuwepo pale ukumbini nikatabasamu Sikujua nimshukuruje Clara kwa namna alivyoirudisha tena furaha yangu iliyopotea.

    “Ninaamini Clara ndiye mwanamke ambaye Mungu ameniandalia.Moyo wangu umekuwa rahisi mno kumkubali na kumpa nafasi kubwa.Sina shaka na moyo wangu kwani naamini safari hii haunidanganyi kama ulivyofanya kwa Emmy.Lakini Clara si kama Emmy.Utofauti wao ni kama ardhi na mbingu.Safari hii sitaki kufanya makosa.Nitaenda naye taratibu na mpaka niuteke moyo wake.Ninachotakiwa kukifanya kwa sasa ni kuanza kumfahamu kiundani Natakiwa niwe na subira kwa sababu iwapo nitaanzisha masuala ya mapenzi mapema namna hii ninaweza kumpoteza malaika huyu.Natakiwa nianze kwa kujenga urafiki mkubwa na baadae ndipo masuala ya mapenzi yafuate.Sitaki kumpoteza mtu muhimu kama huyu.” Niliwaza huku nikimtazama Clara kwa kuibia akiwa anazungumza na wanamitindo wenzake.

    Saa saba za usiku ndipo tulipopata nafasi ya kuondoka pale ukumbini.Hatukuweza kuondoka mapema kutokana na Clara kuwa na maongezi na watu wengi ambao wengi wao walikuwa ni wanamitindo na wabunifu.Mpaka anaingia garini bado walikuwepo wasichana waliokuwa wanamfuata ili kujaribu kupata walau namba yake ya simu kwa sababu hawakujua ni wapi wangeweza kumuona tena baada ya semina ile kumalizika.

    “Pole na kazi nzito” Nikasema wakati tukiondoka maeneo yale

    Clara akaniangalia na kusema huku akitabasamu

    “ahsante sana Wayne.Sikutegemea kama watu wangekuwa wengi namna hii.Nasikitika muda umekuwa mdogo sana na sijaweza kuonana na wote waliokuwa wakihitaji kuniona.Nitatafuta muda nirudi tena Arusha.Nimepapenda sana”

    “Kwa hiyo unategemea kuondoka lini ? Nikauliza

    “Kesho kutwa natakiwa niwe nimeondoka Tanzania.Kuna shughuli moja muhimu natakiwa kwenda kuifanya afrika kusini” Clara akasema na kunifanya nistuke na ninyong’onyee ghafla.Katika mawazo yangu nilitegemea kwamba pamoja na semina kumalizika lakini angeendelea kubaki arusha kwa siku kadhaa .Laiti kama ningekuwa na uwezo ningeweza kumzuia asiondoke kwa sababu bado nilihitaji kuwa naye.

    “Mbona kimya hivyo Wayne” Clara akauliza.Nadhani aligundua kwamba nilikuwa kimya ghafla.Kwa kweli kutoka moyoni sikutaka Clara aondoke,lakini uwezo wa kumzuia asiondoke sikuwa nao.

    “ Nilidhani baada ya kumaliza semina ile ungebaki Arusha japo kwa siku mbili tatu.Nilikuwa nimepanga nikupeleke ukatembelee hifadhi ya Ngorongoro.” Nikasema .Clara akanitazama halafu akasemahttp://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Wayne hata mimi sikuwa nimepanga kuondoka mapema namna hii.Nilipanga kuwa na siku kadhaa za mapumziko baada ya semina kumalizika lakini nilipigiwa simu jana usiku na mmoja wateja wangu wakubwa kuwa kuna kazi moja muhimu sana ambayo natakiwa kwenda kuifanya.I’m sorry Wayne kwa kuikosa ofa hii ya kwenda kutembea Ngorongoro lakini usijali nitatafuta nafasi nitakuja tena Arusha.Nimepapenda sana .Kuna hewa safi,warembo wazuri and above all I’ve met with so wonderfull people especially you Wayne.Toka siku tumekutana umekuwa ni mmoja kati ya watu wangu muhimu sana japokuwa hatujapata muda mwingi wa kukaa na kufurahi pamoja.Wayne naomba ufahamu kwamba uko katika orodha ya watu wangu muhimu wanaonifanya niwe na furaha katika maisha haya.You are so wonderfull.I’ll miss you a lot but don’t worry I’ll come back I promise” Clara akasema kwa ile sauti yake nzuri yenye kuvutia.Nilifarijika mno kwa maneno yale ya Clara.Kuwa miongoni mwa watu wake ambao yeye anawaita ni wa muhimu ilikuwa ni faraja kubwa kwangu.Japokuwa hakunifahamu kiundani lakini alitokea kuniamini na kunweka miongoni mwa watu muhimu.Ulikuwa ni mwanzo mzuri ambao sikutaka kuuharibu.

    “Usijali Clara.Siku yoyote ukitaka kuja Arusha naomba unitaarifu tafadhali ili nikufanyie maandalizi kama mwenyeji wako” Nikasema na kumfanya Clara acheke kicheko kikubwa.

    “hakuna haja ya maandalizi Wayne.Hapa ni kama nyumbani.Hata nikija bila taarifa nafahamu nina watu wangu wa muhimu.” Clara akasema huku akicheka

    “Kwa hiyo Clara kama umepanga kuondoka kesho kutwa,siku ya kesho utakuwa na kazi gani? Nikauliza ili kujua kama ninaweza kupata walau nafasi ya mwisho ya kuwa na mwanamke huyu mrembo.

    “kesho nitaondoka na ndege ya saa saba mchana kwenda kuwaaga wazazi Dar es salaam halafu kesho kutwa ndiyo nitaondoka kuelekea South Afrika.”Akajibu.

    Nilimpeleka Clara hadi katika hoteli aliyokuwa amepanga.Nilimsindikiza hadi katika chumba chake akanikaribisha ndani,sikujivunga nikaingia ndani na kuketi sofani.

    “Clara kwa kuwa muda umekwenda sana na kesho unatakiwa kusafiri ,mimi naomba nikuage ili nikupe nafasi ya kujiandaa kwa safari ya kesho.” Nikasema huku nikijiandaa kuinuka.

    “Wayne please sit down.” Clara akasema ,nikakaa chini.

    “Mbona una haraka namna hiyo? Kesho ninaondoka lakini zitapita siku nyingi kabla hatujaonana tena ,Don’t you like to spend sometimes with me? Don’t you wanna talk about it? Clara akauliza

    “about what? Nikauliza na mimi

    “about what happened at the party” akasema Clara na kunifanya nicheke .

    “Please Wayne just for tonight,stay with me and we can have wine,talk,laugh and have fun.I know after I’m gone I’ll miss someone to laugh with.” Clara akasema Hakujua ni jinsi gani nilivyokuwa nimefurahi kwa kuniomba niendelee kukaa pale.

    “Ok Nitabaki kwa saa moja au mawili halafu nitaondoka” Nikasema

    “Thank you so much Wayne.It means a lot to me.Now wait there and I’ll be back in a second” Akasema Clara huku akifungua mlango na kuingia katika chumba cha kulala.Baada ya kama dakika mbili akarudi akiwa amevaa suruali ndefu ya kitambaa chepesi pamoja na koti jeusi lenye manyoya laini.Akalifungua friji na kutoa chupa za mvinyo akazipanga mezani.

    “Nina furaha ya ajabu sana leo Wayne.Naomba tunywe na tufurahi mpaka tuchoke” Akasema Clara.Tulipoanza kunywa Clara akasema

    “Wayne naomba nichukue nafasi hii kukuomba samahani kwa kilichotokea pale ukumbini”

    “Nothing wrong happened Clara” Nikasema

    “Najua utasema hakuna kilichotokea lakini nilikupandisha jukwaani bila ridhaa yako.Haukuwa umepanga kuongea na hadhira kubwa kama ile.najua vile vile hata zile fedha ulizochangia hukuwa umepanga kuzitoa kwa hilo usijali nitakurudishia zile fedha zote…..”

    “no no no Clara” Niliingilia kati kabla hajamaliza sentensi yake.

    “Nimetoa fedha zile kwa moyo mmoja na wala sihitaji unirudishie.Uliponiomba niambatane nawe katika uchangiaji wa kituo kile nilikwisha andaa mchango wangu kama mshiriki.Tafadhali Clara mchango ule niliutoa kwa moyo wangu wote kwa ajili ya watoto hawa wenye mazingira magumu,na kuhusu kunipandisha jukwaani yah ! I was a bit nervous lakini kwa kuwa karibu nawe nilipata ujasiri mkubwa hata nikaweza kuongea na umati ule mkubwa wa watu.” Nikasema kwa msisitizo na kumfanya Clara atabasamu,akaniangalia kisha akasema

    “Wayne you are amazing.Nilifanya makusudi kukuomba nipande nawe jukwaani.Lengo langu lilikuwa kukupima ni jinsi gani unavyojiamini.I know you were nervous but what you did was wonderfull.Nimefurahi sana Wayne kwa sababu hukuweza kuniangusha.Kwa dakika kadhaa tuliweza kuziteka akili za kila mmoja pale ukumbini.Wayne sijawahi kuwa na furaha kama siku ya leo.Na furaha yote hii imechangiwa na wewe.You made my evening.” Clara akasema huku akiinua glasi yake tukagonganisha maglasi yetu

    “cheers!! Tukasema kwa pamoja.

    Kitu kimoja ambacho sikuwa na uwezo nacho ni kusimamisha muda uliokuwa ukienda kwa kasi ya ajabu.Nilitaka niendelee kubaki na mrembo yule asiyechosha kuwa naye.Nilihisi kuipata furaha ya ajabu ambayo sikuwa nimeipata kwa miaka mingi.

    “Wayne mbona kimya? Unawaza nini? “ .akauliza Clara baada ya kuniona nikiwa kimya ghafla nikimtazama

    “Nothing Clara” Nikajibu

    “Wayne do you have a family? Clara akauliza.Sikujibu swali lile kwa haraka.Sikujua nimpe jibu gani.Swali lile likanikumbusha mateso aliyonipa Emmy ,papo hapo nikamkumbuka mtoto Baraka.

    “Not anymore” Nikajibu kwa sauti iliyoonyehsa kuwa na chembe za hasira ndani yake

    “You had one? Clara akauliza tena.

    “Clara it’s a very log story.Nisingependa kuiongelea hadithi hii kwa usiku huu wenye kila aina ya furaha,sipendi kuufanya usiku huu mzuri uwe ni usiku wa simanzi” Nikasema huku nikiongeza mvinyo katika glasi

    “can you be strong enough to tell me? Clara akaendelea kusisitiza.

    “Clara I’m sorry but its not a nice story to hear tonight.There is nothing interested in it.It’s a beyond pain story.So why don’t we skip this and talk some other sweet things like nice places in South Africa..your handsome boyfriend..”

    “Hahahahaaaa…….hahahaa…….” Clara akacheka kicheko kikubwa mara tu nilipomaliza sentensi yangu.

    “Boyfriend? .. akauliza

    “yes you boyfriend,Don’t you have one” Nikauliza na kumfanya acheke tena kicheko kikubwa.Sikushangaa kwa sababu toka nimemfahamu nimegundua kwamba Clara anapenda mno kucheka.

    “Wayne unamaanisha nini unaposema boyfriend? Akauliza huku akipiga funda la mvinyo

    “I mean someone you love,someone whom your heart belong to…………” sikumalizia sentensi yangu Clara akaanza tena kucheka

    “wayne unanifurahisha sana.I don’t have a boyfriend or believe in love.Kama unamaanisha mpenzi,mpenzi wangu mimi ni kazi yangu ninayoifanya kwa mapenzi yote toka moyoni.After what I got from men,I don’t think I will ever love again.Ninaishi maisha yangu ya furaha,I have lots of friends,I have a job,I do whatever I want to do,I drink,I dance I sing and I’m happy.so what do I need a man for? ………Clara akasema huku akiinuka na kwenda katika friji kuchukua vipande vya barafu.Maneno yale yalikuwa mazito sana kiasi kwamba nilianza kukata tamaa kama ningeweza kumpata mwanamke kama yule maishani.Maneno

    yale yalionyesha wazi kwamba aliwahi kutendwa huko nyuma na kumfanya asione tena thamani ya mapenzi.Kwa sasa alikuwa na maisha yake mazuri yaliyojaa furaha na amani hivyo hakutaka kupata tena matatizo.Kwa upande Fulani nilikubaliana na mawazo yake kwa sababu hata mimi kwa jinsi nilivyokuwa nimetendwa na Emmy sikutaka tena kujiingiza katika masuala ya mahusiano kwa sababu niliamini wanawake wote ni sawa.Sielewi ni kitu gani kilichonikutani

    sha na Clara ambaye kwa muda mfupi niliokutna naye ameweza kuufuta mtazamo huo kichwani kwangu na kunijengea mtazamo mpya kwamba wanawake wote si sawa.kwa mbali nilisikia kitu kama sauti ikininiambia nisikatishwe tamaa na maneno yale ya Clara.

    “ You can have all that Clara,money,fri

    ends job,cars and everything,but are you happy?” Nikamuuliza Clara.Akachukua glasi yake,akapiga funda kubwa la mvinyo akaliweka chini na kukaa kimya kwa sekunde kadhaa akiniangalia.

    “Mbona hunijibu? Nikamwambia Clara.Akanitazama na kusema

    “Sorry Wayne, this conversation brings me lots of things in my mind..Uliniuliza swali gani?.” Clara akasema .Nilimtazama usoni nikagundua kuna mambo aliyokuwa akiyawaza.

    “Nilikuuliza kwamba ,unasema una kila kitu,pesa,marafiki,kazi na kila kitu unachokitaka unakipata.Lakini je una furaha moyoni mwako?

    “Furaha ipi unayoizungumzia Wayne” Clara akauliza

    “nazungumzia furaha ya moyo.Pamoja na kuwa na vitu vyote hivyo maishani lakini moyo wako una furaha? Nikauliza

    “Wayne nina furaha.Kwa sababu kila kitu ninachokitaka ninakipata Nina furaha.Kikubwa kinachonifanya niwe na furaha maishani ni kwamba niko huru,moyo wangu una amani.Nina uhuru wa kufanya chochote nikitakacho.Hebu niambie kuna furaha zaidi ya hiyo? Clara akauliza

    “Nafahamu hilo Clara ,nazungumzia ndani ya moyo wako una furaha? Nikauliza tena

    “Wayne nimeshakwambia nina furaha moyoni mwangu” Clara akajibu akanitazama na kusema

    “Please Wayne can we change the subject.Can we talk of something else like..uhhm tell me of your love life,about your girfriend” Clara akasema huku akitabasamu,akainua glasi yake na kupiga funda la mvinyo.Nilifikiri kidogo nimweleze nini nikaamua kusema ukweli

    “ I don’t have a girlfriend.”

    Clara akanitazama kwa makini usoni baada ya kauli ile na kusema

    “Wayne ,tell me what happened? Kila ninapokutajia kuhusu masuala ya mahusiano yako unabadilika ghafla.Kitu gani kimekutokea? Tafadhali naomba uniambie.Nitakusaidia” Clara akasema kwa msisitizo huku amenikazia macho

    Nilivuta pumzi ndefu na kusema

    “Clara ni hadithi ndefu sana na nisingependa kuongelea masuala hayo kwa sasa”

    “C’mon Wayne mimi ni rafiki yako.naomba uniamini.Nieleze nini kilikutokea ? Usiponieleza leo utanieleza lini? Clara akauliza

    “Sawa Clara kwa vile umesisitiza kutaka kujua ukweli ,nitakueleza ukweli.”

    Nilimweleza Clara kila kitu toka tulipoanza mahusiano yetu mimi na Emmy na hadi tulipokuja kuachana..Nilip

    omaliza kumsimulia mkasa ule ulionipata niliona michirizi ya machozi machoni pa mrembo yule.

    “Wayne hadithi yako imenichoma moyo sana.Kwa nini binadamu wengine wanakuwa na ukatili wa namna hii? Pole sana wayne.Nafahamu kwa sasa uko katika wakati mgumu mno.Jipe moyo na yatakwisha” Clara akasema huku akifuta machozi

    “Usijali Clara,nimemwachia Mungu ndiye atakayenilipia.Sihitaji kulipa ubaya kwa Emmy..Nashukuru hata hivyo kwa kukutana nawe kwa sabahu umenifanya kwa siku hizi chache tulizofahamiana niwe mtu mwenye furaha na kusahau yote yaliyonipata.Nakiri kwamba wewe ni mwanamke wa pekee sana.Mwanaume atakayekuwa nawe atakuwa na bahati kubwa mno”

    Clara akacheka sana baada ya kuongea vile.

    “Wayne kila mara unaongelea kuhusu mwanaume.Ninayafurahia maisha yangu bila mwanaume kwa hiyo sifikirii kuwa na mume” Clara akasema

    “what about children? Nikauliza.Clara akakaa kimya akafikiri kwa muda na kusema

    “Kids ?

    “Yes.Hujawahi kufikiri kuwa na watoto siku moja?

    “I love children and I’d like to have two .Nafikiri furaha yangu itakamilika siku nikiwa na mtoto wangu”

    “Good . kama ni hivyo utawapataje hao watoto bila kuwa na mume? Nikauliza

    “Ouh Wayne please just forget about that..lets talk of something else..” Clara akasema akionyesha wazi kulikwepa swali langu.Lengo langu lilikuwa kutaka kufahamu undani wake kuhusu maisha yake ya kimapenzi.Toka nimekutana naye Clara amekuwa mgumu sana kunieleza kuhusu maisha yake ya kimapenzi.Kila ninapoanzisha mazungumzo hayo huwa anapenda tubadilshe maongezi.Nilisi

    mama,nikamsogelea karibu na kumshika bega lake la kulia kwa mkono wangu

    “Nisikilize Clara,pamoja na kwamba umekiri kuwa una furaha ya kutosha maishani,lakini ukweli ni kwamba hauna furaha ya moyo.Kusema kwamba haufikirii kuwa na mpenzi hauutendei haki moyo wako.Moyo wako unahitaji upate mwenza na hivyo kuufanya uwe na furaha maishani.Clara you are a great woman.You deserve to be loved and be happy.You need someone who can complete your happiness.Don’t lie to yourself Clara that you have happiness.You don’t..Utakuwa mwanamke mwenye furaha pindi utakapompata mwanaume wa maisha yako.Tafadhali naomba usilisahau hilo”





    Nilimwambia Clara ambaye alikuwa ametulia akinisikiliza.Akachukua glasi yake ya mvinyo akapiga funda moja akainama na kufikiri kisha akasema

    “Wayne katika wanaume niliowahi kukutana nao,sijawahi kukutana na mwanaume aliyeniambia maneno yaliyonigusa kama uliyoniambia leo hii.Maneno yako yamenigusa sana moyo.Umeamsha kitu kipya ambacho sikuwa nikikifikira katika maisha yangu.Namkabidhi Mungu ndiye atakayejua hatima ya maisha yangu .Kama itampendeza mimi kupata mwanaume wa maisha yangu na iwe hivyo” Clara akasema taratibu akiwa ameinamisha kichwa.Nilitabasamu baada ya kuisikia kauli ile.

    Nilitazama saa na kukuta ni saa tisa za usiku.

    “Clara muda umekwenda sana.Nahitaji kukuacha upumzike na ujiandae kwa safari ya kesho” Nikasema huku Clara akinitazama

    “No Wayne you cant go now and leave me alone.Stay with me just for tonight..” Clara akaomba.Niimtazama machoni na kugundua kwamba alikuwa akimaanisha alichokisema.Hakujua ni furaha kiasi gani nilikuwa nayo kwa kuniomba nibaki naye usiku ule kitu nilichokuwa nikikiomba kila siku.Nilitabasamu na kumsogelea,akas

    imama na kunishika shingo yangu kwa mikono yake laini.

    “I’ll stay with you tonight” Nikasema kwa sauti ya tayatibu yenye kukwama kwani nilihisi msisismko wa ajabu baada ya kuguswa shingo yangu na mrembo yule.Msisimko ule ukanifanya niichukue mikono yangu na kuizungusha kiunoni mwake na kumfanya astuke ghafla na kuanza kuhema kwa kasi.

    “Wayne what do you want from me tonight? Clara akauliza kwa sauti laini

    “I just want a wonderfull night with you..unforgetable night” Nikasema na kwa kasi ya ajabu akanivuta kwake na kunipiga mabusu mfululizo.Nilihisi kama napaa mawinguni kwa mpasuko wa furaha nilioupata.Ulikuwa ni usiku wa aina yake.Kwa miaka mingi sikuwa nimepata usiku niliohisi kama niko peponi kama huu.

    * * * *

    “Wayne you are amazing” Ilikuwa ni sauti ya laini ya Clara iliyonistua toka usingizini.Niliyafumbua macho na kujikuta nikiwa pembeni ya mrembo mwenye uzuri uliotukuka.Nilijihisi kama vile niko ndotoni.Kiumbe aliyekuwa amelala pembeni yangu alifanana na wale wanaopatikana katika simulizi mbali mbali au kwenye picha za kuchora.

    “Wayne..thank you for the wonderfull night “ Akasema Clara na kunitoa katika fikra kuwa nilikuwa ndotoni.Sikuwa nikiota.Ni kweli nilikuwa nimelala na Clara.Nilimtazama Clara ambaye alikuwa amenigeukia akinitazama usoni huku macho yake mazuri yakifanya mwili wangu uhisi msisimko wa ajabu

    “Wayne sikutegemea kama ningekuja kukutana na mwanaume ambaye angenipa furaha kama uliyonipa usiku wa kuamkia leo.Katika maisha yangu sijawahi kukutana na mwanaume wa shoka kama wewe.Nilichokipata katika maisha yangu ya kimapenzi ni karaha na mateso kiasi kwamba niliwachukia wanaume wote na kuwaona ni wanyama,wabinafsi na hakuna mwanaume ambaye angeweza kunipa raha niliyokuwa nikiihitaji.Wayne naomba nikiri kwamba umenibadilisha mtazamo wangu.Umenifanya niamini kwamba bado wako wanaume ambao Mungu amewajaalia uwezo mkubwa wa kuwaridhisha wanawake.Wayne you are one of those few men hard to find in this world.I don’t know what I should do to make you forever mine.Sikujua kama itatokea siku nitatokea kumuhusudu mwanaume kama ilivyonitokea kwako.Wayne naomba usinielewe vibaya lakini toka nimekutana nawe nimejikuta nikiwa tofauti sana na nilivyokuwa awali.Nimejikuta nikiwa na furaha ya ajabu kitu ambacho hakijawahi kunitokea hapo kabla.Nimejikuta nikitoka nje ya msimamo wangu kwa mara ya kwanza na kuhisi kwamba ninahitaji kuwa na mtu wa kunifanya niendelee kuipata furaha hii ya ajabu niipatayo sasa.Wayne sihitaji kuwa mbali nawe tena kuanzia sasa.Kwa mara ya kwanza toka nimezaliwa ninathubutu kupiga magoti na kuomba nafasi ndani ya moyo wa mtu.Wayne tafadhali naomba unipe nafasi ndani ya moyo wako.Sintakuumiza kama alivyokufanya mwanamke uliyekuwa naye.Nitakupenda na kuwa nawe daima kwa sababu you are so special Wayne.” Clara akashindwa kuendelea akakiangusha kichwa chake kifuani kwangu.Nilihisi joto la ghafla.Nilihisi ile ilikuwa njozi na si kitu cha kweli.Clara mwanamke mrembo anayeupeleka mbio moyo wangu toka nimekutana naye leo hii kwa mdomo wake anatamka kwamba anahitaji kuwa nami maishani.Niliona ni kama muujiza mkubwa ulionitokea.

    Sikuwa na kitu cha kujivunga tena.Sikuwa na kipingamizi wala sababu yoyote ya kukataa ombi lile la Clara.Niliamini yale yalikuwa ni majibu ya maombi yangu niliyomuomba Mungu baada ya kutendwa na Emmy.

    Siku mpya ikaanza kwa penzi zito kati yangu na Clara.

    “ Wayne nasikitika sana kwa sababu sitaki kubanduka pembeni yako lakini kazi hii inayonilazimu kwenda afrika kusini leo ni muhimu mno.Itanilazimu kwenda na baada ya muda mfupi nitarejea.Nahisi miguu mizito kuondoka hapa lakini sina namna nyingine ya kufanya.Wayne umeniteka ghafla kiasi kwamba sijielewi.nini kimenitokea.Kabla sijaondoka ningependa nikapafahamu nyumbani kwako ili nikija kwa mara nyingine nisifikie tena hotelini” Clara akasema .

    Sikuwa mbishi kwa kila alichokuwa akikiongea Clara.Nilimsikiliza kama malkia wangu.Kwa kuwa alikuwa na safari mchana wa siku hiyo,hatukuwa na muda wa kupoteza tukaingia garini na kuelekea nyumbani kwangu.

    Tulifika nyumbani kwangu na kwa ghafla nilipatwa na mstuko wa ajabu kwa nilichokiona katika geti la kuingilia ndani .Nilisimamisha gari na kushuika kwa haraka. Katika geti la nyumbani kwangu alikuwepo Baraka amekaa juu ya tofali.Nilimwinua na kumkumbatia kwa furaha kubwa.

    “baraka umekuja saa ngapi? Nikamuuliza

    “Nimekuja asubuhi ,nimekuta geti limefungwa kwa kufuli nikajua haupo nikaamua kukaa hapa nje nikusubiri” Baraka akajibu

    “Mama na baba wamekuruhusu uje huku asubuhi hii?

    “hapana hawajaniruhusu.Nimetoroka nyumbani.Simtaki uncle Chris.Kila siku ananilazimisha nimuite yeye baba.Nataka kuendelea kukaa na wewe.Sitaki tena kurudi kule kuishi na mama.Nataka kuishi na wewe.” Baraka alisema huku akitoa machozi.Mtoto huyu aliniumiza sana na kukitonesha tena kidonda kilichoanza kupona.Niliendelea kumlaani Emmy kwa kitendo alichokifanya na kumfanya mtoto mdogo kama yule kuteseka namna ile.

    “basi usilie baraka.Tutakaa wote siku ya leo halafu jioni nitakupeleka nyumbani na kama mama yako atakubali uishi huku basi tutaishi wote.” Nilimwambia Baraka ambaye alionyesha wazi kutokuridhika na uamuzi wangu wa kumrudisha nyumbani kwao jioni.Nilimtambulisha Baraka kwa Clara,akamshika mkono nikaingiza gari ndani.Kwa muda mfupi Clara na Baraka wakazoeana na kuwa marafiki .Dakika zile chache za kuwa pamoja zilileta furaha kubwa miongoni mwetu.

    Tukiwa bado katika maongezi na vicheko pale sebuleni mara ghalfa mlango unafunguliwa na anaingia Emmy akiwa ameongozana na askari wanne .Alikuwa amefura kwa hasira.Wote tukapigwa na butwaa kwa hali ile.Moja kwa moja Emmy akaninyooshea kidole mimi na mmoja wa wale askari akanikaribia.

    “Ndugu wewe ndiye Wayne?”

    “Ndiye mimi.Kuna nini afisa? Nikauliza kwa mshangao

    “Wayne tunakuhitaji kituoni.Unatuhu

    miwa kumchukua mtoto aitwaye Baraka bila ridhaa ya wazazi wake.Tafadhali tunaomba tuongozane kwenda kituoni kwa ajili ya maelezo zaidi.”

    Mwili wote ukajikuta ukilowa jasho na midomo kunitetemeka kwa hasira.

    “Afande nafahamu kwamba mko kazini lakini naomba mnieleweshe ninakamatwa kwa kosa lipi? Sielewi nimefanya kosa gani “ Nikawaambia wale askari ambao walionyesha hawakuwa na muda wa kupoteza.

    “ Bwana Wayne,huyu mama unamfahamu? Akauliza yule askari aliyeonekana ndiye kiongozi wa msafara ule

    “Ninamfahamu.Alikuwa mke wangu” Nikajibu huku nikimtazama Emmy kwa macho makali

    “Huyu mama ndiye mlalamikaji ,na ameleta malalamiko kwamba mtoto wake amepotea na moja kwa moja akakuhisi wewe kwamba ndiye uliyemchukua mtoto huyo bila ridhaa ya wazazi wake kitu ambacho ni kosa kisheria.Tumekuja hapa na kumkuta mtoto huyo anayedaiwa kupotea yuko hapa kwako.Kwa hiyo tunakuhitaji hapa tuende wote kituoni ili ukatoe maelezo yako kuhusiana na suala hili” akasema afande yule ambaye sikuweza kuzisoma namba zake kwa sababu ya sweta alilokuwa amevaa.Niliuma meno kwa hasira nikawatazama wale maaskari kisha nikasema

    “naomba tusikilizane maafande.Mimi siwaelewi mnaongea kitu gani kwa sababu mimi ndiyo kwanza nimefika hapa nyumbani sina hata nusu saa,sasa huyo mtoto nimemuiba saa ngapi? Isitoshe nimefika hapa na kumkuta Baraka amekaa getini.Nikamuuliza amefikaje fikaje hapa akaniambia kwamba ametoroka nyumbani kwao basi nijkamchukua na kuingia naye ndani.Kama hamuamini ninachokisema hebu muulizeni mtoto huyu hapa yeye mwenyewe atasema ukweli” Nikasema kwa msisitizo

    “Afande msimuamini huyo.Amemuiba mtoto wangu na kuja kumficha huku.Tafadhali afande tusizidi kupoteza muda mchukueni tuelekee kituoni,atajite

    tea mahakamani” Emmy akasema akiwa amefura kwa hasira.Nilitamani nimrukie na kumpa kipigo kikali mwanamke yule lakini nikajitahidi kujizuia ili nisifanye jambo kama hilo japokuwa nilikuw ana hasira zisizomithilika..

    “Afande samahani naomba na mimi niongee kidogo” Clara aliyekuwa ameduwaa akiangalia mambo yanavyokwenda akafunguka na kusema

    “Nyamaza kimya hasidi wewe….” Emmy akasema kwa ukali akimwambia Clara lakini afande akamzuia

    “Emmy hebu nyamaza tumsikilize na mwenzio anataka kusema nini.Endelea mama…” afande akampa ruhusa Clara aongee

    “Afande mimi sioni kosa ambalo Wayne anatuhumiwa nalo.Nimekuwa na Wayne toka jana jioni,tulihudhuria wote hafla ya uchangishaji fedha za kusaidia kituo cha watoto wanaoishi katika mazingira magumu.Tumetoka pale ukumbini na kuelekea hotelini kwangu.Nimekuwa na Wayne usiku mzima na hakurejea nyumbani kwake.Asubuhi hii tumeongozana wote kuja hapa kwake na tulipofika getini tumemkuta mtoto amekaa,Wayne akamuuliza kama ameruhusiwa kuja huku na mama yake ,Baraka akasema kwamba hakuruhusiwa na mtu yeyote kuja huku ila ametoroka yeye mwenyewe baada ya kutokuridhishwa na maisha anayoyaishi huko kwao.Nimeona niongee ukweli kwa sababu inaonekana huyu mwanamke hana uhakika na anachokiongea.” Clara akasema na ghafla Emmy akakurupuka na kutaka kumvaa Clara,akazuiwa na askari.

    “Niacheni nimfundishe adabu huyu mwanamke naona bado hajanifahamu mimi ni nani.nakuonya wewe mwanamke usiingilie mambo yasiyokuhusu.kama unahitaji mtoto zaa wa kwako na si kusubiri wengine wakuzalie ili uibe.Ninakwambia wewe na huyu baradhuli mwenzio mtanikoma mwaka huu.” Emmy akaongea kwa sauti kali.Niliitazama sura ya Clara nikaona ni jinsi gani alivyoumizwa na maneno yale ya Emmy.Hasira zikanipanda nikashindwa kujizuia nikataka kumvaa Emmy na kumpa kipigo lakini askari wakafanya kazi yao na kunizuia.

    “Afande sintakubali hata siku moja mwanamke huyu akaja na kuanza kuporomosha matusi ndani ya nyumba yangu. Kama ni kutukana anitukane mimi na hata siku moja asije akamgusa Clara.Hahusiki na kitu chochote .”Nikasema kwa ukali.

    “Anhaa kumbe huyu ndiye anayekupa kiburi,basi nitakula naye sahani moja.Yeye si ndiye anayeona fahari kuchukua mabwana za watu, nakwambia nitamfundisha adabu.Nitamuonyesha mimi ni nani.Wayne fahamu kwamba wewe bado ni mume wangu halali wa ndoa na ninakuonya kwamba sintakupa muda wa kupumzika.Nitakufundisha adabu” Emmy akaongea kwa kujiamini sana.Chuki ya wazi wazi ikajidhihuirisha machoni pake.Sikuelewa nini sababu ya chuki ile kubwa na ya dhahiri aliyokuwa nayo Emmy kwangu.Alitaka kuwa huru na nikamruhusu aende anakotaka kwenda .Kwa ulimi wake alitamka kwamba hanitaki tena katika maisha yake sasa kwa nini aanze kunifuatilia maisha yangu wakati kila mmoja amekwisha anza maisha yake? Nilikasirika sana

    “jamani hapa hatukuja kwa ajii ya kugombana.Sasa sikilizeni.Wayne na mwenzio,wote tunaelekea kituoni kwa ajili ya kupata maelezo ya kina juu ya suala hili lenye utata.Mambo yote yatajulikana huko huko kituoni” Afande akasema.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Sawa hakuna shida afande.Lakini huyu mwenzangu Clara naomba mumuache aende zake kwa sababu kwanza hahusiki kwa namna yoyote na masuala haya na pili ana safari ya kwenda Dar es salaam saa tano asubuhi ya leo kwa ndege na tayari amekwisha kata tiketi.” Nikawaomba wale maaskari lakini kwa haraka Clara akasema

    “wayne usijali nitakuwa nawe mpaka mwisho.Siwezi kukuacha peke yako katika tuhuma ambazo si za kweli.Safari yangu ninaweza kwenda siku yoyote ile lakini sintakubali kuona ukinyanyaswa na mijitu yenye roho za kishetani” Clara akasema huku ameukunja uso wake kwa hasira.Moyoni nilisikitika sana kwa kumuingiza Clara katika matatizo yangu na Emmy,mwanamke mwenye roho ya shetani.Maneno yale ya Clara yalionyesha kumchoma moyo Emmy ambaye alibetua midomo na kusonya kisha kwa ghadhabu akamuendea Baraka aliyekuwa sofani akilia ,akamchukua kwa nguvu.

    “hebu twende ,wewe ndiye unayesababisha mpaka mimi natukanwa namna hii” Emmy akaongea kwa hasira huku akimvuta mkono baraka ambaye alikuwa akipiga kelele akigoma kuondoka.

    “Bwana wayne tafadhali ingia garini wewe na mwenzio twende kituoni ” Afande akaniamuru nipande gari la polisi lililokuwa imeegeshwa pale nje kwangu.

    “Afande sijakataa kwenda kituoni.Nimetii bila shuruti na ninaomba niruhusiwe kuongoza kituoni mimi mwenyewe na gari yangu.Siwezi kupanda gari moja na huyo mwanamke” Afande akanitazama na kukubaliana nami kwamba nitumie gari langu.Mimi na Clara tukaingia katika gari langu na kuongoza kuelekea kituoni.Clara alikuwa kimya na hakuongea kitu chochote.Ni wazi alikuwa ameumizwa sana na kitendo alichokifanya emmy.Nilikuwa nikimtazama kwa kuibia .

    “Clara samahani sana kwa yote yaliyotokea.Sifahamu nini sababu ya mwanamke yule kunifanyia mambo kama haya..Kama uhuru nimekwisha muachia na anaishi na mtu ambaye yeye mwenyewe alitamka kwamba ndiye anayempa furaha maishani sasa iweje tena aanza kunifuatilia katika maisha yangu? Ameniumiza sana lakini nitamuonyesha mimi ni nani” Nikasema

    “Wayne tafadhali usiendelee kugombana na yule mwanamke kichaa.Utajikuta ukipoteza muda mwingi kwa mambo yasiyokuwa na maana yoyote.Kitu cha msingi jaribu kujipanga na kuangalia maisha yako ya mbeleni.Mtu kama yule usimuweke katika akili yako.Ukisema upambane naye utapoteza muda wako bure.Nakushauri achana naye kabisa na wala usijishughulishe naye hata kidogo” Clara akasema huku akiweka mkono mmoja begani kwangu

    “Vipi kuhusu safari yako ya Afrika kusini? Itakuwaje iwapo hautaonekana? Nikauliza

    “Usijali kuhusu hilo wayne.safari yangu si muhimu kwama ulivyo wewe.Mimi ninafahamu thamani yako kwangu na ndiyo maana niko tayari kufanya lolote lile kwa ajili yako.Niko tayari kwenda hadi mwisho wa dunia kwa ajili yako.Kwa hiyo kuhusu hilo la safari lisikupe shida kabisa Wayne.” Maneno yale yakanifanya nitabasamu .Clara alimaanisha alichokuwa amekisema.Aliiona thamani yangu kwake na hivyo kuwa tayari kufanya chochote kile kwa ajili yangu.Niliapa moyoni kufanya kila niwezalo kwa ajili ya kuwa na mwanamke kama huyu ambaye ananijali na kunithamini .

    Tulifika kituoni na kushuka kisha tukawasubiri askari wale wafike kwa sababu tulikuwa tumewatangulia kufika.Walipofika tukaongozana wote hadi ndani ambako nilichukuliwa maelezo.Nilipomaliza Clara naye akaomba atoe maelezo yake kama nyongeza kwa yale ya kwangu akakubaliwa.

    Baada ya masaa manne ya mjadala mkali baina yetu na maafisa wa polisi ikaonekana wazi kwamba sikuwa na kosa lolote nililolifanya ila zilikuwa ni hila za Emmy kutaka kunichafua.Alipewa onyo kali kwanza kwa kusumbua chombo cha dola na pili kwa kutaka kunichafua.Vile vile ikaamriwa kwamba aniombe radhi mimi pamoja na Clara kwa usumbufu aliotusababishia na mwisho akakanywa kwamba kama tumeachana asijaribu tena kuyafuatilia maisha yangu.

    Baada ya kikao kile tukaagana na maafisa wa polisi tukatoka na kuelekea lilipo gari letu huku tumeshikana mikono.Nikamfungulia Clara mlango aingie garini lakini kabla hajaingia nikamuona Baraka akija mbio kule kwenye gari letu.

    “daddy naomba usiniache nirudi tena kwa mama.naomba tuondoke wote” Baraka akasema huku akilia.Nilimuonea huruma sana mtoto yule kwa namna alivyokuwa akiteseka lakini sikuwa na jinsi ya kumsaidia.Nilibaki nikimtazama.Clara akainama na kumbembeleza

    “Baraka nenda kwa mama .Mimi na baba yako tutakuja kuomba kwa mama yako ili akuruhusu ukae nasi..” Clara akamwambia Baraka ambaye akanigeukia na kuniuliza

    “Eti daddy ni kweli ?

    “kweli Baraka.Tutakuja kuongea na mama yako ili akuruhusu uje kukaa kule kwetu” Nikajibi na ghafla akatokea Emmy na kumnyakua Baraka kwa nguvu toka kwa Clara

    “Nakwambia hivi wewe mwanamke,lazima nikuonyeshe kazi.Nitakufundisha adabu.Wewe ndiye unayempa kiburi huyu kunguru,basi jiandae kupambana na mimi” Emmy akasema kwa shari.Clara akamtazama na kutabasamu kisha akanisogelea akanikumbatia na kunipa busu moja zito.

    “Let’s get out of here darling.She is crazy” Clara akasema huku akicheka kichini chini kisha tukaingia garini na kuondoka tukimuacha Emmy amevimba kwa hasira.

    “Darling ,sababu iliyopelekea wewe ukaachana na yule mwanamke ni ile ile uliyonieleza au kuna sababu nyingine? Clara akauliza tukiwa garini

    “Kwa nini umeuliza hivyo Clara?

    “Kwa sababu naona chuki aliyokuwa nayo yule mwanamke ni kubwa sana na ya wazi.Ni kama vile anataka kukuangamiza kabisa.Ni kama vile anataka kulipiza kisasi kwa jambo baya ulilomfanyia” Clara akasema na kunifanya nitabasamu

    “Clara yule mwanamke sijui anachokitafuta kwangu ni kitu gani.Kama ni chuki nilipaswa kuwa nayo mimi kwa sababu yeye ndiye aliyenifanyia mambo ya ajabu sana.Mimi sijamfanyia jambo lolote lile baya na wala hastahili kuwa na chuki na mimi.Alihitaji uhuru na nikampatia uhuru sasa tatizo liko wapi? Clara nakuomba umpuuze hayawani yule.Hana chochote cha kukufanya” Nikasema na kumfanya Clara atabasamu,akanisogelea karibu na kubusu





    Niliendelea kumshukuru Mungu kwa kunisaidia kushinda tuhuma zile nzito alizokuwa ameziibua Emmy.Bado sikuelewa ni kwa nini Emmy alikuwa na chuki ya namna ile kwangu.Sikufahamu nilimkosea jambo gani baya kiasi cha kumfanya anichukie namna ile.Kama ni kuachana na mimi yeye ndiye aliyetaka tuachane sasa ni kwa nini anifanyie vile? Kwa nini aliahidi kuendelea kupambana na mimi? Pengine labda kile kitendo cha kuniona niko na Clara kilimuuma sana .Yawezekana alikuwa akiugulia moyoni kwa wivu.Lakini wivu wa nini kwa sababu ni yeye ndiye aliyeyaanzisha mambo yote haya.

    Mawazo haya yaliendelea kuniumiza kichwa sana na mara Clara akanistua

    “wayne unawaza nini?

    “Mambo mengi Clara.Nawaza ni namna gani ulivyoumia moyoni kwa jambo alilolifanya Emmy.Nawaza ni namna gani nitakuomba msamaha kwa jambo la aibu kama lile.Ni siku yetu ya kwanza tu kuwa pamoja halafu unakutana na jambo kama lile na kupelekea ukafika hadi polisi na kikubwa zaidi amekufanya uahirishe hadi shughuli zako muhimu.Kila nikifikiria suala hili ninaumia sana Clara”

    Clara akanitazama akatabasamu na kuunyoosha mkono wake ,akasugua sugua shingo yangu kidogo huku akisema

    “Wayne naomba usikwazike kwa kitendo alichokifanya Emmy.Kwangu mimi sikuumia kwa mambo aliyoyafanya bali nilimuonea huruma sana kwa sababu hana amani moyoni kwa mambo aliyoyafanya.Kama hatabadilika basi hatakuwa na amani maishani mwake hadi siku yake ya mwisho.Mimi sina tatizo naye hata kidogo na nina imani kwamba hawezi kunifanyia kitu chochote kibaya kama alivyoahidi.Yale yalikuwa ni maneno ya kujipa moyo.Ninachokushauri kwa sasa inabidi uondoke hapa Arusha kwa muda wa mwezi mmoja au zaidi ili umsahau kabisa Emmy.Utakapofanya hivyo utakuwa umempa nafasi hata yeye mwenyewe ya kuweza kuendelea na mambo mengine yanayomuhusu kwa sababu kila atakapokuwa akijaribu kukutafuta hatakupata.”

    “wazo lako zuri Clara.Hata hivyo nilikuwa na mawazo kama hayo toka zamani na niliahirisha baada ya kukutana nawe.”

    “Uliahirisha safari kwa ajili yangu? Clara akauliza

    “Ndiyo Clara .Nilikwisha andaa safari ya kuelekea Zanzibar mahala ambako niliamini ni sehemu nzuri na ambayo ingenifanya nisahau kabisa yote yaliyonitokea lakini nilipokutana nawe siku ile mipango yote ikavurugika.”

    Clara akacheka kicheko kikubwa kama kawaida yake halafu akasema

    “kama uliahirisha safari kwa ajili yangu,na mimi leo nimeahirisha safari kwa ajili yako.Ngoma droo” wote tukacheka kicheko kikubwa.

    “Ulikuwa umepanga kwenda Zanzibar? Clara akaniuliza

    “Ndiyo Clara nilikuwa nimepanga kwenda kupumzika Zanzibar.Nilitaka nikaishi mbali kabisa na hapa na nikaona kwamba Zanzibar ni sehemu nzuri na salama sana kwa mapumziko.”

    “hata mimi sijawahi kufika Zanzibar.Unaonaje kama tukienda wote kupumzika Zanzibar? Clara akauliza.Nikamtazama na kusema.

    “Kokote utakakotaka twende ,nitakuwa tayari.hata ukisema leo hii tunywe sumu tufe wote mimi niko tayari” Nikasema na kumfanya Clara acheke sana .Akafunua pochi yake na kutoa kitambaa cha mkononi na kufuta machozi yaliyotokana na kucheka

    “Wayne unanifurahisha sana.You make me feel a very special woman in this world.Najisikia furaha sana.You are very special to me”

    Sikujibu kitu zaidi ya kutabasamu ,halafu nikapunguza mwendo wa gari na kukata kona ya kuelekea nyumbani kwangu.

    “Wayne naomba usinielewe vibaya kwa haya nitakayokwambia “ akasema Clara tukiwa tumejipumzisha kitandani nyumbani kwangu

    “Nakusikiliza Clara” Nikamwambia huku nikilisugua bega lake la kulia kwa mkono wangu

    “Ni muda mrefu sana nimeishi maisha yangu nikiwa mwenyewe bila kuwa na mpenzi na niliweka nadhiri kwamba sintakuwa na mtu aitwaye mpenzi katika dunia hii hadi kifo changu.Nilikuwa nikiwachukia wanaume.Niliamini wanaume wote baba yao mmoja kwa hiyo wote wako sawa.Wayne sifahamu kilinitokea kitu gani lakini baada ya kukutana na wewe nimejikuta nikiivunja nadhiri yangu.Nimejikuta nikibadili msimamo na matazamo wangu.Kilichoto

    kea hata mimi bado nashangaa.Hata marafiki zangu wakifahamu kuhusu uhusiano wetu huu watanishangaa sana kwa sababu walielewa fika ni jinsi gani nilivyokuwa nikiwachukia wanaume.Wayne nimevunja nadhiri yangu ya kutokuwa na mwanaume na nimeamua kukukabidhi moyo wangu wewe pekee kwa kuamini kwamba uko tofauti sana na wengine.Nimekupa moyo wangu kwa sababu nakupenda sana.Nakukabidhi moyo na mwili wangu uvitunze.Nakuahidi nitakupenda hadi mwisho wa maisha yangu.Nitakuwa mwaminifu kwako hadi kifo kitutenganishe.Nitaishi nawe katika kila hali ,iwe masika kiangazi,kwenye jua na mvua.Ugonjwa na faraja sintakuacha Wayne.Pamoja na hayo yote nakuomba kitu kimoja tu”

    Clara akasema kwa hisia kali huku macho yake yamejaa machozi

    “Chochote utakachoomba Clara nitakutimizia.” Nikasema taratibu huku nikishika mikono yake.

    “Wayne don’t ever make me cry. Promise me that you’ll never hurt me.Promise me that you’ll make me a happiest woman” Clara akasema huku amenikazia macho.Nilimtazama mrembo yule mwenye macho ya kimalaika.Macho yake yalinieleza kila kitu kilichokuwamo moyoni mwake.Nikamshika mikono yake na kumsogeza zaidi kwangu.Nikambusu na kusema

    “Clara My angel naomba nikueleze ukweli kwamba hadi sasa najihisi kama vile niko ndotoni kwa sababu sikutegemea kama wanawake kama wewe bado wanaishi katika dunia hii.Baada ya kutengana na Emmy niliumia sana na sikufichi kwamba niliwachukia wanawake kupita kiasi.Kila mwanamke niliyemuona nilijenga picha kwamba ana tabia kama za Emmy.Siku ile nilipokutana nawe nilijikuta nikibadili kabisa mtazamo wangu kuhusu wanawake.Nilijikuta nikipata furaha ya ajabu na kusahau kama nilikuwa nimeumizwa muda mfupi uliopita.Toka siku ile nilikuwa naota ni namna gani ningeweza kuwa na furaha kama ningekuwa na mwananke kama wewe.Nilisali na kumuomba Mungu anirejeshee tena furaha yangu iliyopotea na leo hii amesikia sala zangu na niko nawe hapa kitandani.Clara nakupenda na ninakuahidi kwamba nitakuheshimu na kukutunza kwa sababu wewe ni kitu cha thamani kubwa maishani mwangu .Thamani yako inazidi hata ile ya Lori zima la almasi.Siku zote nitakuwa nawe na kukuenzi kama malkia wangu.Sintakuumiza na wala kukutoa machozi.nakuahidi hivyo ” Clara akanivuta kwake na kunikumbatia kwa nguvu..

    Tulishinda nyumbani kwangu hadi jioni ,nikampeleka Clara hotelini alikofikia akabadili mavazi kisha tukaelekea katika klabu moja ya usiku ambako kulikuwa na muziki wa bendi.Tulicheza na kufurahi hadi saa nane za usiku kisha tukarejea hotelini kwa Clara tukalala hadi asubuhi.Sikuwahi kupata raha za namna hii katika maisha yangu.Nilimuona Clara kama malaika aliyeshushwa ili kunipa furaha maishani mwangu.

    Asubuhi ya siku iliyofuata tulirejea nyumbani kwangu kwa ajili ya kubadili nguo kisha tuelekee matembezini.Tul

    ipanga tukatembee katika bustani ya nyoka .Clara alikuwa akisikia kwamba kuna nyoka wanafugwa na hivyo alihitaji kwenda kuangalia. .

    Baada ya kuingia chumbani kwangu nilihisi kama vile chumba hakikuwa sawa.Sikutilia maanani sana nikalifungua kabati na kutoa nguo nikavaa.Nikiwa naendelea kuvaa simu yangu ikaita.Nikaangalia namba za mpigaji,zilikuwa ni namba ngeni kabisa katika simu yangu.

    “hallow” Nikasema baada ya kuipokea simu ile

    “hallow Wayne.Ni mimi Emmy”

    “Bastard ! unanitafutia nini wewe baradhuli ? Nikajikuta nikisema kwa ukali.Nilipatwa na hasira za ghafla

    “Ama kweli umenichoka.Umefikia hatua ya kuniita baradhuli ? Akasema Emmy

    “Emmy nakuonya . Acha kabisa kunifuata fuata katika maisha yangu.Naomba hii iwe ni mara ya mwisho kuisikia sauti yako ”

    “ Nafurahi kusikia hivyo Wayne.Nafahamu sihitaji kukusumbua tena katika maisha yako.Nakuacha ule raha na mwanamitindo wako.Sintakupig

    ia tena simu lakini nadhani wewe ndiye utakayenipigia simu na kunitafuta.Kabla sijakata simu na kuachana nawe kabisa kuna jambo naomba nikueleze ”

    “unataka kunieleza nini wewe mwanamke ? nikauliza

    “usiwe na haraka hivyo Wayne.Mimi ndiye niliyekupigia simu na ninaomba unisikilize.Nakuomba tafadhali unisikilize kwa makini kwa mara ya mwisho.Nafahamu una shilingi millioni mia moja na arobaini katika benki ya kimataifa ya European Africa Bank.Nafahamu ni jinsi gani ulivyozipata fedha zile na ninaufahamu mtandao wenu wote.Sitaki kukuchosha sana lakini ninakupa masaa ishirini na manne uhamishe shilingi millioni mia moja katika akaunti yangu benki ya Stanbic. Iwapo hautatekeleza hilo fahamu kwamba utakwenda mahakamani na ninakuhakikishia kwamba ni lazima utafungwa kifungo kirefu gerezani kwa sababu ushahidi wote ninao.kama huamini angalia kabati lako unalohifadhi kumbukumbu zako.Kumbuka masaa ishirini na nne Wayne ama la utafia gerezani na utamuacha mrembo wako akiponda raha na wanaume wenzako.hahahahahaa bye Wayne”

    Nilikuwa nimepigwa na butwaa nikashindwa hata kufunga mkanda wa suruali nikaiacha ikaanguka chini.Jasho lilianza kunitoka.

    “wayne whats wrong” Akasema Clara ambaye alistuka kutokana na mabadiliko yangu ya ghafla.

    “Documents !! documents ! ……” Nikasema huku nikilivuta kabati kubwa la nguo na kwa nyuma yake nikaanza kubonyeza namba za sefu ambalo huwa natunzia kumbu kumbu zangu muhimu.Sefu hili huwa linafunguliwa na namba maalum na kwa bahati mbaya Emmy alikuwa akizifahamu

    Nilitamani ardhi ipasuke niingie ndani baada ya kulifungua sefu langu na kukuta nyaraka zangu muhimu hazimo.

    “damn you Emmy..” Nikaishiwa nguvu na kukaa chini.

    Clara alistuka sana kwa hali niliyokuwa nayo akanisogelea na kuniuliza

    “Wayne whats wrong? Sikumjibu kitu .Akakimbia na kuniletea glasi ya maji

    “Kunywa maji Wayne.” Nikaishika glasi ile nikanywa maji kisha akaniinua na kunipeleka kitandani.

    “My documents” Nikasema kwa uchungu

    “what documents? Clara akauliza

    Niliendelea kutikisa kichwa kwa hasira

    “wayne document zipi hizo? Clara akaendelea kuuliza

    “She was here..that bastard was here last night !! Nikasema kwa sauti kali

    “Wayne nani alikuja hapa? Clara akauliza

    “ Emmy” Nikajibu na kumfanya Clara astuke

    “Emmy ?

    “Ndiyo Emmy alikuja hapa jana usiku na amechukua nyaraka zangu muhimu sana”

    “Ouh Emmy why are you doing this to me? Nikasema huku nikiuma meno kwa uchungu.

    “Calm down Wayne.” Clara akasema huku akinipiga piga mgongoni.

    “Wayne nyaraka hizo zilikuwa zinahusu nini? Akauliza Clara.Nilishindwa nimjibu nini.akanitazama tena na kuuliza

    “Wayne hebu niambie nyaraka hizo zilikuwa zinahusu nini?

    “mshenzi yule alifahamu mahala nilipokuwa naweka nyaraka zangu muhimu na amekuja kuzichukua” Nikasema

    “wayne please answer me.Nyaraka hizo zilikuwa ni za nini? Pengine ninaweza kukusaidia kuzipata”

    “Clara nyaraka hizo ni za muhimu sana na kama nikifanya mchezo ninaweza kufungwa.” Clara akastuka na kuniangalia kwa macho makali

    “Kufungwa ?” akauliza

    “Ndiyo Clara.Ninaweza kufungwa” Nikajibu

    “Ufungwe kwa kupoteza nyaraka ? Clara akauliza

    “Its not simple as you think Clara.This is something very serious” Nikasema huku nikiinuka pale kitandani na kwenda kusimama dirishani.Nilikuwa nikihema kwa kasi kutokana na hasira nilizokuwa nazo.

    “Wayne kama amekuja Emmy na kuingia ndani mwako bila ruhusa yako na kisha akachukua nyaraka zako,basi tunaweza kusema kwamba mtu huyo ni mhalifu.Amevunja na kuiba.Twende tukamshitaki polisi haraka ili wamkamate” Clara akasema

    “No Clara hili si suala la polisi.Ndiyo maana amenipigia simu na kunifahamisha kwamba nyaraka zangu anazo kwa sababu anafahamu kwamba sintaweza kwenda polisi kushitaki.”

    “Why Wayne? Kwa nini usiende kumshitaki polisi wakati ameingia nyumbani kwako ,akachukua nyaraka zako na kuondoka.Huo ni uhalifu.Lets report her to the police.That’s the best way to teach her a lesson.Huwezi kumuacha mtu kama huyu .Huyu ni mhalifu na huwezi kujua anaweza hata akakuua.Ouh Wayne I’m so sacred.lets go to police” Clara akasema.Uso wake ulionyesha wasi wasi.

    “hapana Clara .Hili si suala la kwenda kushitaki polisi.Hili ni suala langu mimi na yeye”

    “Wayne tell me why ?? kwa nini tusimshitaki polisi ili achukuliwe hatua?

    “ No Clara we cant do that” Clara akanisogelea na kusema

    “Wayne niambie ni kwa nini Emmy asichukuliwe hatua kwa kosa alilolifanya? Sikujibu kitu nikainama chini

    “Whats going on Wayne? Don’t tell me you are scared of her.” Nilinyamaza kimya na kumtazama Clara ambaye alianza kupata mashaka.Niliogopa kumweleza ukweli kwa sababu ilikuwa ni mapema sana kuanza kukumbana na mambo kama haya.hakupaswa kuanza kuumizwa na masuala yangu kwa muda huu mfupi.Nilimchukia Emmy kupita kiasi kwani sasa niliamini lengo lake lilikuwa ni kunifanya niishi maisha magumu .Nikiwa nimezama katka dimbwi la mawazo nikastukia bega langu likiguswa na Clara.Nikainua kichwa na kumtazama

    “Wayne do you real love me? Clara akauliza

    “Clara I love you more than you think” Nikajibu

    “kama kweli unanipenda Wayne tell me the truth.Whats going on here.If you love and trust me tell me the truth and I’ll understand you.Hata kama umeua mtu,niambie ukweli.As far as I love you I will understand.” Clara akasema huku akinitazama usoni.

    Nilimtazama usoni,nikajisikia vibaya sana.Clara hakustahili kuteseka kwa ajili yangu.macho yake yalikuwa yakitoa machozi ,nikamuonea huruma nikaamua kumweleza ukweli.

    “Clara nitakueleza ukweli” Nikasema huku nikimshika mkono na kumpeleka kitandani,.Tukaa na kutazamana.

    “I’m listening Wayne.” Clara akasema.Nikakohoa kidogo kusafisha koo langu kisha nikasema

    “Hapo awali nilikuwa nafanya kazi katika halmashauri ya jiji la Arusha nikiwa katika kitengo cha ukarabati wa miundombinu.Mimi ndiye niliyekuwa nikiratibu shughuli zote za ukarabati wa miundombinu mbalimbali ya halmashauri ya jiji kama vile barabara n.k.Miaka mitatu iliyopita aliletwa mkurugenzi mpya ambaye kwa sasa ni marehemu.Mkurug

    enzi huyu ambaye naweza kusema kwamba ndiye aliyenifundisha namna ya kubuni miradi hewa na kuingiza mfukoni pesa ya halmashauri.Akiwa kama kiongozi ,aliunda mtandao wa watu ambao kwa pamoja tulishirikiana katika kubuni miradi mingi ambayo haikuwepo au kama ilikuwepo basi ilikarabatiwa au kujengwa kwa kiwango cha chini sana tofauti na gharama zilizoainishwa katika taarifa za mradi.Tulitengeneza fedha nyingi sana.Tulibuni miradi mingi iliyogharmu mabilioni ya shilingi lakini mingi kati ya hiyo haikuwepo na au ilikuwa ya kiwango cha chini sana.Haikuwa rahisi kugunduliwa kwa sababu mkaguzi mkuu wa ndani wa halmashauri na wahasibu wote walikuwa katika mtandao wetu hivyo kila ripoti za ukaguzi zilipohitajika zilipelekwa ripoti nzuri na za kufurahisha.Ilitokea bahati mbaya mkaguzi wetu wa ndani alihamishwa na kuletwa mkaguzi mwingine ambaye hakuweza kushirikiana na sisi hivyo kutaka kutibua mambo.Ili kulizima sakata hilo ikatulazimu kuwanyamazisha huyo mkaguzi pamoja na mkurugenzi .Baada ya hapo nikaacha kazi halmashauri na kutafuta kazi mahala kwingine.Wakati mambo yote haya yanafanyika nilimshirikisha Emmy kama mke wangu katika kila kitu.Alichokifanya Emmy ,jana usiku amekuja na kuchukua nyaraka zangu zote muhimu na anazo kwa sasa.Alikuwa akifahamu kwamba nina shilingi millioni mia moja na ishirini benki ambazo nilizipata wakati ninafanya kazi halmashauri.Anataka nihamishie shilingi milioni mia moja katika akaunti yake ya benki na nisipofanya hivyo ataripoti suala hili polisi.Amenipa saa ishirini na nne niwe nimetekeleza hilo agizo”

    Nilimaliza kumweleza ukweli Clara ambaye akainuka na kushika kichwa chake kwa mikono yake miwili.

    “Ouh my god ! what a scandal.Why me? “ Clara akasema kwa hali ya kukata tamaa.Nilihisi kuchanganyikiwa.

    Clara akavuta pumzi ndefu akaenda kukaa kitandani,akainama na kujishika kichwa kwa mikono yake miwili.Sikuelew

    a alikuwa akiwaza kitu gani lakini ni wazi alikuwa katika hali ya kukata tamaa.Aliumizwa mno na maneno niliyomwambia.Nilimtazama kwa makini huruma ikaniingia.Clara alikuwa akiishi maisha yake kwa raha mustarehe na hakuwa na matatizo .Aliogopa kuingia katika mahusiano tena baada ya kutendwa katika uhusiano wake wa awali.Japokuwa hajawahi kunieleza ni kitu gani kilimtokea hapo kabla kiasi cha kumfanya awachukie wanaume lakini ni wazi kitu alichofanyiwa kilimuumiza sana kiasi cha kumfanya awachukie wanaume wote .Baada ya miaka kadhaa kupita ameamua kumuamini na kumpa mwanaume mwingine nafasi katika moyo wake,mwanaume huyo ni mimi.Siku mbili tu tangu awe na mimi amekutana na mambo ambayo yametonesha donda lililokwisha pona muda mrefu.Clara amejikuta akiuumiza tena moyo wake.Jana nilituhumiwa kumchukua mtoto Baraka bila ridhaa ya wazazi wake kitu kilichopelekea kushikiliwa na polisi kwa masaa kadhaa tukihojiwa.Kutokana na sakata hilo Clara aliahirisha safari yake ya muhimu sana.Leo hii limeibuka tena jambo jingine jipya.Sikuhitaji kumuumiza Clara namna ile lakini sikuwa na namna nyingine ya kufanya zaidi ya kumueleza ukweli.Sikuona umuhimu wa kumficha kitu kwa sababu hata kama ningeficha ingekuja kufahamika tu.



    Clara alikuwa akitoa machozi na kwa mbali nilisikia kilio cha chini chini.Nafikiri alikuwa akilia kwa mambo niliyoyafanya kwa sababu ni kinyume kabisa cha maadili ya mfanyakazi wa umma.Niliiba fedha ya serikali ambayo ni kodi za wananchi.Fedha zile nyingi zingeweza kutumika katika miradi ya maendeleo kama zahanati na kununua vifaa vya shule n.k. Kwa mara ya kwanza nilihisi uchungu kwa kuliibia taifa namna ile.Nilisikia uchungu mkubwa moyoni.Kingine nilichohisi kinamliza Clara ni namna jina lake litakavyochafukhttp://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    a.Clara ni mtu mwenye jina na heshima kubwa sana katika jamii kwa hiyo kitendo cha Emmy kulipeka suala lile mbele ya sheria na yeye kuonekana nami ni wazi kingelichafua jina lake zuri lenye heshima kubwa ndani na nje ya nchi.Roho iliniuma nikamuonea huruma mrembo yule aliyekuwa ameketi kitandani akilia kwa kwikwi.

    “Kama ni kuchafuka ni bora nichafuke mimi na Clara abaki na heshima yake .Kwa mambo niliyoyafanya sistahili kuwa karibu na mtu kama Clara.Itakuwa vizuri kama nikibaki mwenyewe na kuendelea kuubeba msalaba wangu mwenyewe.” Nikawaza na kuanza kupiga hatua za taratibu na kumsogelea Clara.Nilikuwa na wasi wasi mwingi ni jinsi gani ningeweza kuongea naye .Kwa sasa sikutegemea kama angetaka hata kuzungumza nami.Nikajikaza na kumshika bega.

    “Clara “ Nikamuita taratibu akainua uso wake uliokuwa umelowa machozi.Nikamtazama nikasikia uchungu mwingi .Nilimuahidi Clara kwamba sintamliza lakini leo hii uso wake umelowa machozi kwa sababu yangu.

    “Clara najua sistahili hata kuongea na wewe tena lakini tafadhali naomba unisikilize japo kwa dakika chache ” Nikasema na kutulia kidogo,nikamtaz

    ama Clara aliyekuwa ametulia kimya .

    “Clara nakumbuka nilikuahidi kwamba sintathubutu hata siku moja kukutoa chozi na wala kuumiza moyo wako. Ahadi niliyokupa nimeshindwa kuitimiza na tazama sasa hivi uso wako umejaa machozi,na moyo wako umeumia kwa sababu yangu.Nimesikia uchungu sana kukuona ukitoa machozi kwa jambo ulilolisikia.Kwa mara ya kwanza ninajutia kitu nilichokifanya.Chozi lako ulilomwaga limenifanya nisikie uchungu mwingi na kuuona ujinga nilioufanya.Kitu nilichokifanya nitakijutia katika maisha yangu yote yaliyobaki kwa sababu kimenifanya nikampoteza mwanamke niliyempenda kwa moyo wangu wote.”

    Clara akaonyesha mstuko baada ya kutamka maneno yale ya mwisho.

    “ Clara narudia tena kukiri kwamba nilifanya kosa kubwa sana kuchukua fedha zile za serikali ambazo ni kodi na majasho ya wanachi wanyonge. Fedha ile ingeweza kufanya shughuli mbali mbali za maendeleo .Chozi ulilolimwaga limenifanya nitambue kosa langu.Ninastahili kufikishwa mbele ya sheria na kupata adhabu.Ni kweli ninastahili adhabu kwa kosa hili.Clara wewe ni mtu safi uliyezitumia nguvu na vipaji vyako hadi ukafika hapa ulipo sasa hivi.Jina lako ni kubwa na heshima yako katika jamii ni kubwa sana.Siko tayari kuona jina lako likichafuliwa kwa sababu yangu.Japokuwa inaniuma kusema lakini ni lazima niseme kwamba kutokana na hali halisi ilivyo siko tayari kuyakubali matakwa ya Emmy.Siko tayari kumpatia kiasi hicho cha pesa anachokitaka.Kama alivyokuwa ametishia kwamba endapo nisipotimiza matakwa yake ni lazima atanifikisha katika vyombo vya sheria.Niko tayari kwa hilo..Kwa mambo niliyoyafanya napenda kukiri kwamba sistahili kuwa na mtu kama wewe.Ninaomba uhusiano wetu Clara uishie hapa ili niweze kuyakabili mambo haya mimi mwenyewe bila kumuhusisha mtu yeyote .Hii itakuwa njia pekee ya kukuepusha na aibu hii kubwa na kulilinda jina lako safi.” Nikasema na kutulia kidogo.Clara akafuta machozi na kunitazama kisha akanivuta mkono na kunifanyia ishara niketi kitandani.

    “Wayne tafadhali usiseme hivyo.Ukisema hivyo unazidi kunifanya niumie zaidi “Clara akasema

    “ Inaniuma kusema hivyo Clara lakini huo ndio ukweli halisi ambao lazima tuukubali siko tayari kuona jina lako likichafuka kwa ufisadi nilioufanya..Ni

    nastahili kuubeba msalaba wangu mwenyewe”

    “Wayne naomba unisikilize.” Akasema Clara na kuinama chini kidogo akatafakari.

    “Ni kweli nimeumia sana.Siwezi kuelezea ni kwa kiasi gani lakini nimeumia mno.Ni muda mfupi sana tumekuwa pamoja lakini kwa muda huu mfupi yameanza kujitokeza mambo ambayo yamesababisha uhusiano wetu kutetereka.Wayne siku zote nilikuwa nikikwepa kujiingiza katika mahusiano kwa kuogopa kuumiza moyo wangu kwa mara nyingne tena.Pamoja na yote yaliyotokea lakini kuachana si suluhisho.Haya yote ni majaribu ambayo hatuna budi kuyashinda.Mimi siwezi kukuacha hata uniambie kitu gani.Tayari nimekwisha ufungua moyo wangu na kuuruhusu upende tena kwa hiyo siwezi kurudi nyuma.Niko tayari kusimama na wewe katika sakata hili.Sintajali kama jina langu litachafuka ama la.Ninachokijua ni kwamba niko na wewe na moyo wangu unahitaji kuwa na wewe pekee.kwa hiyo sahau suala la kuachana kwa sababu siyo suluhisho la tatizo hili.Nikikuacha leo hii mimi ndiye nitakayeumia zaidi .” Clara akasema na kunivuta kwake ,akanikumbatia halafu akaniachia na kusema

    “Pamoja na yote uliyoyafanya Wayne lakini bado hayanizuii mimi kukupenda au kuwa na wewe.Wote tunafanya makosa katika maisha yetu na tujapogundua baadae makosa tuliyoyafanya huwa tayari tumeshachelewa.Wayne nafurahi kama umeligundua kosa lako na kulijutia.Kinac

    hotakiwa kwa sasa ni kuangalia namna tutakavyoweza kulimaliza suala hili” Clara akasema.Nikamtazama mrembo yule na kumwambia

    “Kuna jambo nimekuwa nikilifikiria pengine labda linaweza likasaidia ili suala hili libaki kama lilivyo”

    “jambo gani hilo Wayne? Clara akauliza

    “nafikiria kukubaliana na matakwa ya Emmy.” Nikasema na kumfanya Clara astuke

    “Yaani kumpatia Emmy pesa zote kama alivyotaka?

    “Ndiyo Clara.Nadhani hii itakuwa njia pekee itakayomfanya anyamaze na asilipeleke suala hili katika vyombo vya usalama”

    “Wayne hapana.Huwezi fanya hivyo.Hutakiwi kukubaliana na matakwa ya Emmy.Kukubali anachokitaka kutaonyesha ni jinsi gani ulivyo dhaifu na atautumia udhaifu huo kukufanyia kila aina ya vituko.Leo atataka ufanye hiki,kesho atakuambia ufanye kile.Usikubali kamwe kumpa hiyo nafasi.Unachotakiwa kukifanya ni kumpigia simu na kumtaarfu kwamba hauko tayari kukubaliana na vitisho vyake na kwamba hutampatia hata senti moja katika zile fedha.Muonyeshe kwamba uko imara na hauko tayari kuyumbishwa na kama anataka kupeleka nyaraka hizo katika vyombo vya kisheria mpe ruhusa afanye hivyo.” Clara akasema na kunifanya nizidi kumshangaa.

    “Unashangaa nini Wayne? Chukua simu na umpigie sasa hivi na umweleze hayo niliyokwambia halafu nitakueleza nini kitafuata.” Nikachukua simu na kupiga namba zile alizonipigia Emmy.

    “hallo Wayne.Mbona umenipigia simu mapema namna hii? Umeshanitumia hizo fedha kama nilivyokuambia? Akasema Emmy baada ya kupokea simu.

    “Emmy tafadhali naomba unisikilize” Nikasema huku uso wangu umekasirika.

    “Nakusikiliza Wayne” Akasema Emmy

    “Nimekupigia simu kukuonya kwamba iwe ni mwanzo na mwisho kunipigia simu na kunipa amri.Naomba ufahamu kwamba siko tayari kuendeshwa na mwanamke mwenye upeo finyu kama wewe.Ninakupa masaa kumi na mbili ,nyaraka zote ulizoziiba hapa nyumbani kwangu ziwe zimerudi na kama hutatekeleza utanitambua mimi ni nani.Nimechoshwa nawe Emmy...” Nikasema kwa ukali.Emmy akacheka na kusema

    “Wayne,kumbe kuna nyakati huwa unakuwa jasiri namna hii? Hahahaaa nafurahi kuona huyo mwanamitindo wako anakupa ujasiri wa namna hiyo.Mpe salamu zangu .Na wewe kwa kuwa umeonyesha kiburi basi naomba tupambane mimi na wewe na tuone ni nani atakayechukua ushindi.Bado nakusisitizia kwamba masaa ishirini na manne yakipita bila fedha niliyokwambia kuingia katika akaunti yangu basi ujue kwamba mwisho wako utakuwa ni gerezani na pesa yote nitabaki naimiliki mimi.Kwa hiyo wakati bado una nafasi tafadhali fanya vile nilivyokuamuru.

    Jambo la mwisho nakuomba usinipigie simu kama huna kitu cha maana cha kuniambia.” Emmy akasema kwa jeuri na kukata simu

    Nilipandwa na hasira kasi kwamba kama angekuwa karibu ningemshushia kipigo kikali.Nilikuwa nikihema mfululizo kwa hasira nilizokuwa nazo.Sikuelewa sababu ya Emmy kuwa na uadui mkubwa na mimi kiasi kile.

    “You did great” akasema Clara huku akinipiga piga mgongoni

    “Kwa sasa hata yeye atakuwa akijiuliza ni kwa nini umekuwa jasiri namna ile.Hata kama alikuwa na wazo la kwenda katika vyombo vya sheria itambidi ajiulize mara mbili.”

    “Clara nina wasi wasi baradhuli huyu anaweza akakusababishia matatizo makubwa.”

    “Usijali kuhusu hilo Wayne kwa sababu huyu mtalaka wako anaonekana bado ana akili za kitoto na haniwezi mtu kama mimi.Sasa sikiliza Wayne.Mimi nitakusaidia katika kulitatua tatizo hili kwa sababu bado liko ndani ya uwezo wangu kulimaliza.Nitalimaliza suala hili lakini naomba unipe ahadi kwamba baada kumalizika hautajihusisha tena na masuala ya uhujumu wa uchumi wala aina yopyote ya ufujaji wa fedha za umma au kujipatia fedha kwa njia isiyo halali.”

    “Clara ninajutia kosa nililolifanya na ninataka kuyabadili maisha yangu na kuishi maisha mazuri ya kujitafutia fedha za halali.” Nikasema na kumfanya Clara atabasamu

    “Nafurahi kusikia hivyo.Kwa sababu nakupenda nimeamua kulibeba mimi suala hili.Mpango mzima utasomeka kwamba mimi na wewe ni washirika wa kibiashara toka muda mrefu na una kiasi Fulani cha hisa katika kampuni yangu ya mavazi kwa hiyo fedha zile zilitoka katika kampuni yangu.Nitawasiliana na wahasibu wa kampuni yangu ili waandae nyaraka ambazo zitakuonyesha kwamba wewe ni mshirika wangu kibiashara na kwamba kwa nyakati tofauti ulipokea fedha toka katika kampuni yangu.Vile vile nitawaelekeza waingize leo kiasi fulani cha pesa katika akaunti yako yenye fedha anazozitaka Emmy ili ionekane ni kweli umekuwa unapokea fedha toka kampuni yetu.Kokote atakakokwenda Emmy ataonekana mwongo na tutamtaka athibitishe hilo analolisema na itakuwa ni aibu kubwa kwake.”

    “Ouh Clara sijui hata nikushuruje kwa msaada huu mkubwa unaonisaidia.” Nikasema huku nikimkumbatia

    “Bado sijamaliza Wayne.Kuna jambo ambalo ninataka kuliweka sawa.Nina uhakika suala hili litamalizika kwa sababu litasimamiwa na wanasheria wangu ambao ni wanasheria wakubwa na wenye uzoefu .Baada ya suala hili kumalizika nitakuwa nimeingia katika dhambi kubwa.Nimeshiriki katika kufunika uovu.Kwa maana hiyo sintakuwa na amani daima.Ninachotaka kukisema hapa ni kwamba fedha ile yote uliyoichukua inabidi tuirudishe kwenye jamii. Sina maana ya kufanya mkutano na waandishi wa habari na kusema kwamba ulichukua fedha za serikali na unataka kuzirudisha bali tutazitumia katika mradi wowote wa maendeleo.Tunaweza tukazitumia fedha hizo kujenga darasa au kuchimba kisima cha maji katika sehemu ambayo kuna shida ya maji au kununua vitabu mashuleni ili mradi tufanye kitu chochote chenye faida kwa jamii kupitia fedha ile.Iwapo utakubaliana nami kuhusu suala hilo nitaamini kwamba ni kweli unajutia kosa lako na kwamba una lengo la dhati la kubadilika na kuanza kuishi maisha mapya kabisa .Je uko tayari kwa hilo? Clara akauliza

    Lilikuwa ni swali gumu sana kulijbu kwa haraka. Nikatafakari kwa sekunde chache ili nione nitamjibu nini. Ni kweli nilikuwa na mamilioni ya fedha ambazo zote zilitokana na ufisadi tulioufanya mimi na wenzangu kwa fedha ya walipa kodi wa Tanzania.Swali lile lilikuwa ni mtego wa mimi kuchagua ama fedha ama clara.Kwa sasa Clara ndiye aliyekuwa kila kitu kwangu .Fedha zote nilizokuwa nazo hazitakuwa na maana kama nitaikosa furaha hii ya maisha yangu.Nikakata shauri ni bora nikose fedha lakini niwe na Clara.

    “Clara nashukuru sana kwa kukutana nawe kwani ni wewe pekee ambaye umenifanya nifahamu nini nimefanya na nini ninapaswa kufanya .Nimejifunza kitu kikubwa sana toka kwako.Kwa moyo wote nakuahidi kwamba baada ya mambo haya yote kuisha fedha zile zote tutazirudisha kwa wananchi.” Nikasema na kumfanya Clara atabasamu ,akanikumbatia

    “Nimefurahi sana kusikia hivyo Wayne.Basi usiumize kichwa tena na huyu kichaa Emmy .Vaa nguo zako tutoke na kuendelea na siku yetu kama tulivyokuwa tumepanga.Wakati ukijiandaa naomba niitumie nafasi hii kuwasiliana na watu wa kampuni yangu pamoja na wanasheria ili waanze kulishughulikia suala hili haraka.” Clara akasema akanibusu na kutoka mle chumbani.Nilibaki nimesimama kwa dakika tatu nikitafakari kisha nikaanza kuvaa nguo tayari kwa kutoka.Baada ya muda Clara akaingia tena chumbani.

    “Kuwa na amani mpenzi wangu,usiumizwe kichwa na Emmy.Mimi nimeamua kulisimamia suala hili na litakwisha.Naomba uniamini.” Clara akaniambia huku akilirekebisha shati nililokuwa nimevaa.

    “Clara sioni hata nitamke neno gani kukushukuru kwa namna ulivyoamua kunisaidia katika suala hili.Nina deni kubwa ambalo ninahitaji kukulipa” nikasema na kumfanya Clara atabasamu ,akanisogelea karibu zaidi akanibusu.

    “Wayne ni kweli una deni kwangu na nitakuomba unilipe kitu kimoja tu”

    “Clara niko tayari kukulipa kitu chochote kile utakachoomba.Niambie unahitaji kitu gani na sinta sita kukupatia.Niko tayari kufika hadi pembe ya mwisho wa dunia kwa ajili ya kukutafutia kitu unachokihitaji.Niambie tafadhali unataka nikulipe nini?

    Clara akanitazama kwa macho yake mazuri na kunifanya nisisimkwe mwili

    “Una uhakika utanipatia ninachokihitaji? Akauliza Clara

    “Nina uhakika Clara.Nitakupatia chochote kile unachokihitaji.” Nikajibu kwa kujiamini

    “nafurahi kusikia hivyo Wayne.Kitu ninachotaka toka kwako ni kidogo sana na ambacho hakikulazimu kwenda hadi mwisho wa dunia kukipata.Ninachohitaji ni nafasi ndani ya moyo wako.”

    Nikamuangalia Clara na kutabasamu baada ya kutamka vile.Nikamvuta karibu yangu zaidi nikamuangalia usoni na kumwambia.

    “Clara huna haja ya kuomba nafasi ndani ya moyo wangu.Toka siku nimezaliwa tayari nafasi yako ilikwisha wekwa moyoni mwangu.Moyo wangu umejazwa na sura yako pekee.hakuna tena mwanamke mwingine anayeweza kuipata nafasi hii iliyojazwa nawe.Mapenzi yangu yote yameishia kwako pekee Sina mapenzi tena kwa mwanamke mwingine .” Nikasema na kumbusu Clara ambaye alikilaza kichwa chake kifuani kwangu na kunikumbatia kwa mahaba mazito.

    “Wayne naomba uelewe kwamba ninakupenda kuliko kitu chochote katika dunia hii.Wewe ndiye kila kitu kwangu.tafadhali nahitaji nafasi ya kudumu ndani ya moyo wako.Nataka uwe wangu peke yangu.Nahitaji muda wako uliobakia wa kuishi hapa duniani uumalize ukiwa na mimi.Nataka tuishi pamoja,nataka tuzae watoto na kutengeneza familia yenye furaha na upendo.Nnakuhitaji Wayne katika maisha yangu” Mrembo huyu adhimu alikuwa akiongea toka nani kabisa mwa moyo wake.Ni kweli alikuwa akinipenda na hata mimi nilikuwa nikimpenda kupita kiasi.Nilijilaumu sana kwa kupoteza muda mwingi kwa mtu kama Emmy mwanamke asiye na shukrani ambaye katika kipindi cha maisha niliyoishi naye amenisababishai maumivu ambayo naweza kusema ni zaidi ya maumivu ya kawaida.

    “Clara my angel.Nakuhakikishia kwamba wewe ni wangu pekee,na mimi niwako pekee.Sijui nitampa nini Mungu kama shukrani zangu kwake kwa kuniletea furaha hii kubwa ya maisha yangu.Amenirudishia furaha ya maisha iliyokwisha toweka.Clara nitakupenda milele na milele na ninakuahidi kwamba hakuna mtu yeyote katika dunia hii atakayeweza kututenganisha.Ni kifo pekee kitakachoweza kututengansiaha mimi na wewe.Nitaishi nawe na kukupenda hadi katika pumzi yangu ya mwisho “ maneno yale yakamfanya Clara ashindwe kujizuia kudondosha machozi.

    “tafadhali usilie Clara.Huu ni wakati wa kufurahi na si wakati wa kudondosha machozi” nikamwambia huku nikimfuta machozihttp://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Wayne ninalia kutokana na furaha niliyonayo.Nimekaa miaka mingi nikijihisi ni mwenye furaha lakini sikuwahi hata mara moja kuipata furaha kubwa kama niipatayo sasa kwa kuwa nawe.Ni wewe ndiye uliyenipa furaha hii kubwa maishani.” Akasema Clara.na kuniangalia usoni.

    “Darling twende tukaendelee na ratiba yetu ya siku.Tuna kila sababu ya kufurahi” Tukatoka na kuingia garini tukaelekea eneo la meserani ambako kuna hifadhi ya nyoka.Mimi si mpenzi kabisa wa nyoka na ni moja kati ya vitu ninavyoviogopa sana katika hii dunia lakini niliamua kwenda huko kwa sababu Clara alipenda kwenda kutazama nyoka wa aina mbali mbali wanaofugwa.Amek

    uwa akisikia hifadhi hii ya nyoka na alipanga siku moja aitembelee na sasa ameipata nafasi hiyo hakutaka kuipoteza.







    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog