Search This Blog

Friday, October 28, 2022

NENDA NA MOYO WANGU - 1

 

     





    IMEANDIKWA NA : STALLONE JOYFULL



    *********************************************************************************



    Simulizi : Nenda Na Moyo Wangu

    Sehemu Ya Kwanza (1)





    Ninachokumbuka ni mlio wa simu, ambao ulinikumbusha kuivua suruali kisha

    viatu; nilivyotaka kulala navyo bila kuvua kutokana na pombe nyingi

    nilizokunywa. Ulikuwa ni mlio ulioashiria ujumbe mfupi wa maneno uliingia

    katika simu yangu, hata hivyo sikushuhurika nayo nikajitupa kitandani

    kivivu. Siku hiyo sikuoga wala kukumbuka chakula.



    Mara nikiwa katikati ya usingizi, ghafla simu ikaita kwa sauti ya juu.

    Hapana!

    Ilikuwa ni sauti ndogo ya kawaida ila kwa kuwa niliilalia kwa sikio langu,

    ndio maana niliisikia kuwa ilikuwa ikitoa sauti kali mno. Kwa hasira

    sikutazama aliyekuwa akipiga wala aliyenitumia meseji ile, nikaizima.

    Usingizi mzito ukanibeba kwenye usiku ule wa manane mpaka nilipoamka

    asubuhi majira ya saa 4:25 asubuhi. Niliandaa maji ya moto ya kuoga huku

    simu yangu nikiwa nimeiweka chaji. Nikiwa nayasubiri maji yachemke,

    nilikihisi kichwa changu kizito kutokana na pombe nilkizokunywa, nikaanza

    kuikumbuka siku ya jana nikiwa nimekaa kitandani, kiunoni n'na taulo zito

    jeupe kifua wazi tayari kwa kuoga.

    ....



    NIKIIKUMBUKA SIKU YA JANA JINSI ILIVYOKUWA:- Jana ilikuwa ni jumatatu, kama

    jumatatu nyingine zenye pilikapilika nyingi tofauti. Hiyo ilikuwa ni

    kuanzia asubuhi mpaka ilipotimu majira ya jioni, jumatatu hiyo ikabadilika

    kwetu na kuwa sawa na wikiendi. Katikati ya hoteli ya Lamada kwenye bustani

    murua yenye ukijani uliokolea, tulijumuika katika tafrija ya tukio maalumu

    la kuvishana pete mimi na mpenzi wangu Beatrice.

    Tuliwaalika ndugu jamaa na rafiki zetu wa karibu, kushuhudia tukio hilo la

    kipekee. Kila mmoja alikuwa na uso wa furaha kwa kushuhudia tukio lile

    likitimia. Mimi na Beatrice tulifurahi zaidi kwa kuwa ndoto zetu

    ziliendelea kutimia tangu tulipoanza uhusiano wetu tukiwa chuo.

    "Nakupenda sana Beatrice"

    "Hakuna mwingine zaidi yako Ramon"

    Kisha tukapeana papi zetu, huku ndimi zetu zikipigana kwa furaha kwakitendo

    cha badilishana lita kadhaa za mate midomoni mwetu. Sherehe iliendelea,

    watu wakafurahi wakala wakashiba, walevi wakanywa wakalewa nikiwa mmoja wao

    kati yao, huku Beatrice akiwa ameshika chupa yake ya tatu ya soda akinywa

    taratibu.

    Ilikuwa yapata saa 6:45 usiku, ndio tuliondoka baada ya Beatrice kunifuata

    katikati ya meza niliyokaa na Michael pamoja na rafiki zetu wengine, mara

    baada ya sherehe kuisha na watu kadhaa kuondoka akiwemo mama yangu, baba

    akiwa na wazazi wa Beatrice wakinywa kwa furaha.

    "Tunachelewa baby, saa saba kasorobo sa' hivi"

    Aliniambia huku akitazama saa kwenye simu yake. Nikawaaga rafiki zangu

    kisha tukaenda kuwaaga wazazi waliozama katika vicheko. Nikamsindikiza

    Beatrice mpaka nyumbani kwake Mikocheni ambapo alishaacha kuishi na wazazi

    wake waliokuwa wakiishi Bunju.

    kisha mimi nilirudi nyumbani kwangu kijichi.

    ....

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mlio wa kitufe kilichofyatuka kutoka katika birika la kuchemshia maji, ndio

    ulinitoa katika mawazo hayo ya siku ya jana na kunirudisha tena chumbani

    kwangu. Nikazima ukutani na kuyamwaga maji yale ya moto kwenye ndoo ya

    kuogea, kisha nikabeba sabuni pamoja na mswaki niliouweka dawa nikaingia

    bafuni nikiwa nimeshajaza maji mengine ya baridi ya kuyapooza yale ya moto.

    Nilipomaliza kupiga mswaki baada ya kuvua taulo huku nikipiga mluzi

    niliokuwa nikiimba wimbo fulani wa "Msondo Ngoma" nikakumbuka jambo. Jana

    usiku nilipigiwa simu, na nani? Meseji pia? Atakuwa nani? Nilikumbuka

    kutazama kweli? Si kwenda kuangalia mpaka nilipomaliza kuoga na dakika kumi

    zilitosha kufanya hivyo.



    Nikamaliza kuoga na kutoka bafuni huku nikijifuta maji kwa taulo.

    Saa iliyopo juu ya meza ya chumbani kwangu ilionesha kuwa imetimu Saa 5:58

    zilibaki dakika mbili itimie saa 6 mchana. Nikaiwasha simu yangu kuangalia

    ni nani aliyekuwa akinipigia simu. Nikafungua sehemu ya simu ambazo

    hazijapokelewa, alikuwa ni mpenzi wangu Beatrice. Nikaipiga simu yake,

    haikupokelewa. Mara ya pili haikupokelewa, ya tatu vivyo hivyo.

    Nikakumbuka kuwa jana usiku ilianza kuingia meseji kabla ya simu kupigwa,

    nikaenda upande wa meseji, alikuwa ni Betrice pia. Nilipousoma ujumbe wake,

    moyo ulinilipuka vuuup!! Kama taa ya kandili inayoanza kuishi mafuta yake,

    nikaanza kuhisi joto kali licha ya upepo mkali wa feni ulioendelea kupuliza

    ndani ya chumba changu.

    Meseji hiyo iliandikwa "KWANINI UMENIUWA RAMON?"...

    Nilijaribu tena kuipiga simu ya Beatrice lakini nilichojibiwa, kilikuwa ni

    kile kile nilichoambiwa mara ya kwanza na sauti ya mwanamke wa huduma kwa

    wateja "simu unayopiga haipokelewi, bonyeza..." Nikaikata na hapo nikahisi

    naanza kuchanganyikiwa. Sikujua Beatrice alimaanisha nini mpaka aseme kuwa

    ninamuuwa. Nikaamua nimpigie rafiki yangu Michael ambaye alimfahamu vizuri

    Beatrice, Michael hakuwa akipatikana.

    Nikaamua kwenda mwenyewe hadi Mikocheni anapoishi Beatrice.

    Niliwasha gari yangu na kushusha kilima cha kijichi kisha nikaibukia kwa

    buruda na kupita misheni nikaitafuta barabara ya kilwa road nije kuibukia

    azikiwe niitafute barabara ya mwai kibaki baada ya mwendo wa speed kali

    ulionichukua zaidi ya dakika 45 mpaka kukatisha katika mtaa anaoishi

    Beatrice.

    Nilisimamisha gari mara baada ya kufika getini kwake na kupiga honi nyingi,

    lakini sikuona dalili za kufunguliwa. Nikaizima gari yangu na kushuka,

    niseme ukweli kuwa nilikuwa n'na hasira kwa kuwa nilijua ni utani wa

    Beatrice lakini wasiwasi ulinijia kila nilipowaza itakuwaje kama ni kweli

    amepatwa na matatizo?

    Nikaitazama kwa dakika kadhaa kamera ya ulinzi pale getini, lakini haikuwa

    ikitazama tena getini kama nilivyozoea. kitu cha ajabu na kilichonitia

    mashaka niliona kuwa ilinyofolewa kwa makusudi au bahati mbaya na mtu awaye

    yeyote, lakini sikutambua. Nikaamua kugonga hodi mara kadhaa na kuona

    kimya, nikaamua kulisukuma geti lile likafunguka bila ajizi. Mshangao

    mwingine, haikuwa kawaida kwa Beatrice kuacha mlango wazi.

    Nilipoingia ndani mara baada ya kuvuka geti lile, nyumba ilikuwa kimya huku

    mlinzi Baraka akiwa hayupo eneo lake la lindo.

    Nikapiga hatua chache mpaka kwenye nyumba kubwa ya Beatrice, moyo wangu

    ukapiga pah! Ukutani mwa nyumba ya Beatrice karibu na ulipo mlango wa

    kuingilia, niliona alama ya kiganja kilicholowa damu na kushika eneo hilo

    la ukuta.

    Miguu yangu ilianza kutetemeka na kuwa kama inayogongana huku kengele ya

    hatari ikipiga kichwani mwangu. Ukweli ni kwamba sasa matumaini ya kumkuta

    mpenzi wangu akiwa hai yalikuwa madogo kuliko nilivyokuwa nikitoka

    nyumbani. Nilianza kuona ukweli wa meseji yake lakini wasiwasi ulisukuma

    zaidi mapigo yangu ya moyo, kwanini aandike mimi ndiye ninayemuuwa? Ukimya

    ule ulinitisha zaidi kuliko alama ya kiganja cha damu juu ya ukuta wa

    nyumbani kwa Beatrice.

    Nikaingia ndani ya nyumba hiyo, pale mlangoni nikalakiwa na mburuzo wa mtu

    aliyekuwa akivuja damu kutoka mwanzo wa mlango mpaka katika moja ya mlango

    wa kuingilia chumba ambacho Beatrice alifanya kama stoo.

    Nilipofungua chumba hicho, nilichokikuta hakielezeki. Kichwa

    kilitenganishwa na mwili wala kichwa chake hakikuonekana na hadi leo sijuhi

    kiko wapi. Tumboni kulikuwa na shimo kubwa lililoacha sehemu kubwa ya

    utumbo kutoka nje na kuleta picha iliyotisha zaidi.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    "Baraka!!!" Niliita kwa hofu huku nikiziba sura yangu kwa uoga na machozi

    yakanibubujika.

    Nilijaribu kutaka kukimbia na kuingia chumbani kwa Beatrice huku nikimuita

    Beatrice. Beatrice hakuitika bali nikapokelewa na utelezi ulionifanya

    niisalimie sakafu na kuibusu ardhi ya chumbani kwa Beatrice na kunifanya

    niilambe damu iliyoganda pembeni ya mwili ulio uchi huku macho yakinitazama

    na mdomo kama unaonizomea wa mpenzi wangu Beatrice.

    "Mamaa weee!!" Kwa wahka nilipiga kelele za kuchanganyikiwa, nilipomsogelea

    Beatrice nikamsukasuka huku nikimuita "Beatrice, Beatrice amka mama. Nini

    kimekukuta jamani Beatrice, amka mama"

    Bisu kubwa lilizama tumboni kwake huku kwenye sehemu ya koromeo lake ikiwa

    imekatwa hivyo kuweka kama mfereji fulani uliotisha kuutazama. Nilikuwa

    nikitazama mwili wa Beatrice na si Beatrice mwanamke niliyekuwa naye jana

    usiku.

    Nikiwa katika kulia huko? Nikasikia mchakato wa nyayo za mtu zikitembea

    kuja ndani ya nyumba ya Beatrice.

    "Wauwaji!!"

    Akili yangu ikaninong'oneza. Nilinyanyuka upesi kuelekea sebuleni,

    nikajificha nyuma ya kochi ili niweze kuwaona waliokuwa wakiingia. Tulikuwa

    tumepishana sekunde chache kwani mara baada ya kuzama nyuma ya kochi lile,

    wale waliokuwa wakija wakawa wamesimama eneo la stoo karibu na kochi

    nililojificha mimi. Nilipoinua kichwa changu kuchungulia ni watu wa aina

    gani? Nikawa nimefanya kosa, walikuwa ni askari sita, wa kike wakiwa wawili

    kila mmoja akiwa amevaa gloves wanne wakiwa na silaha mikononi mwao huku

    wawili wakiwa hawajavaa nguo za kipolisi bali mikononi walibeba simu za

    upepo.

    "Muuwaji!" Alikuwa ni askari mmoja mweusi wa kiume, aliyeshika bastola yake

    ndogo kiukakamavu akaropoka huku akinielekezea silaha ile. Mwingine

    akaropoka kwa sauti yake thabiti.

    "Mikono juu ya kichwa usijiguse popote ukikiuka maagizo haya tunakutoa

    ubongo. Usijaribu kufanya ujanja wowote" Ilikuwa ni sauti isiyo na mzaha

    hata kidogo

    Niliogopa sana kuoneshwa mdomo wa bastola kama mtu mwenye makosa. Ila

    kukutwa ndani ya nyumba yalipofanyika mauaji, hakika sikuwa na ujanja.

    "Mimi sihusiki!?"

    Nilijaribu kujitetea kwa sauti ya kitetemeshi lakini haikusaidia. Mmoja wa

    askari wale akaangua kicheko cha fedheha na kunitazama katikati ya miguu

    yangu. Nikaushusha uso wangu pia kutazama kilichomfanya askari yule

    kucheka, nikaishusha mikono yangu haraka kuiziba sehemu ile. Kumbe ile hali

    ya ubaridi uliokuwa ukipenya katikati ya miguu yangu ni mikojo

    iliyonichuruzika kutokana na uoga.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Mikono juu, pumbavu" askari yule aliyekuwa akicheka akabadilika ghafla na

    uso wake ukawa ule wa kuudhi. Mmoja kati yao akawa amenisogelea na

    kunifunga pingu kwa nyuma katika mikono yangu. Kisha nikatolewa ndani ya

    nyumba ile na kuwekwa katika gari ya polisi kwa mateke huku nikiwa

    nimekwidwa kwa nyuma kwa style ya tanganyika jerk(suruali kukamatwa kwa

    nyuma ya makalio na kufanya miguu kuelea juu juu) kisha walikaa ndani huku

    nikiachwa na askari wengine watatu wenye bunduki aina ya Ak-47 wakinilinda

    zaidi ya dakika 40.

    Nikiwa nimefungwa pingu zile huku nikitazama askari waliokuwa wakinilinda

    huku wale wengine wakitoka na kuingia ndani ya nyumba ya Beatrice na

    mwingine akipiga piga picha kiganja kile ukutani na mburuzo ule mimi nikawa

    najiuliza. Nilianza kujiuliza meseji niliyoipokea kutoka kwa Beatrice

    "kwanini unaniuwa Ramon?" Kisha nakuta maiti mbili katika nyumba yake!

    Inawezekana Baraka ndiye aliyemuua? Sasa kwanini aseme mimi ninamuuwa?

    Ilianza meseji kisha ikafuata simu, inamaana aliyekuwa akinipigia simu ni

    Beatrice au aliyemuuwa? Kwanza aliyemuuwa ni nani? Na hawa polisi, nani

    amewataarifu mapema hivi kuwa ndani kuna mauaji yametokea? Hiki ni

    kitendawili na huu ni mtihani wa aina yake niliokutana nao. Kwa sababu kama

    nitadhani ni Baraka ndiye alimuua Beatrice na je yeye ni nani alimuua? Na

    mbwa wako wapi?

    Baada ya askari wale kutoka ndani ya nyumba ya Beatrice walinifunga

    kitambaa cheusi machoni pangu na hivyo sikuweza kuona chochote mbele yangu.

    Wakawasha gari na msafara wa kwenda kusikojulikana ukaanza. Akili yangu

    ikawa na hopfu na kule ninakopelekwa. Sasa kama ni askari na ninapelekwa

    mahabusu kwanini nizibwe na kitambaa cheusi? Nikaogopa zaidi.

    Ulikuwa ni umbali mrefu ambao siwezi kukadiria tulitumia dakika ngapi au

    kilometa ngapi mpaka kufika katika jumba hili kubwa lenye giza nene.

    Nilitolewa ndani ya gari na kufunguliwa kitambaa na kisha taa zikawashwa,

    kumbe tulikuwa tumeingia gereji nikapitishwa katika mlango mdogo wa

    kuingilia katika nyumba hiyo. Ilikuwa ni nyumba kubwa sana, nyumba ambayo

    haikuonesha dalili ya kuwa ni makazi ya mtu labda ni ofisi fulani. Kama ni

    ofisi, kwanini niletwe ofisini na sio nipelekwe mahabusu nizijuazo?

    Nikapelekwa katika chumba fulani kidogo chenye meza fulani ndogo na viti

    viwili vikitazamana. Nikawekwa katika kiti kimoja huku taa yenye mwanga

    mkali ikining'inia. Nikatolewa zile pingu kisha nikaachwa peke yangu.

    Nilikitazama kile chumba kile pemnbe na kuziona kamera nne katika kila

    pembe ya ukuta. Mbele yangu kulikuwa na kioo kipana ambacho hakikuwa na

    tofauti na vile ambavyo huwa naviona kwenye picha za wazungu katika vyumba

    vya mahojiano kama hiki.

    Sikujua kuna siku na mimi nitakuwa katika mazingira kama haya.

    Nilikaa kwa dakika kumi na tano mpaka mlango ulipofunguliwa na kuingia

    kijana mrefu mwenye mwili uliokomaa kimazoezi na misuli iliyojazia. Alikuwa

    ana kipara kichwani mwake na sauti nadhifu iliyombana.

    "Habari yako Ramon?" Alinisalimu mtu yule. Nikajiuliza amenijuaje?

    "Salama tu!" Sauti yangu ilitoka kwa shida kutokana na hofu ya hapo nilipo.

    Kwanza nilianza kuhisi huenda wauaji waliomuua mpenzi wangu ndio

    walionichezea mchezo huu na kujifanya wao ni askari. Sikujua ilikuwaje

    walifahamu ndani ya nyumba ile kumetokea mauaji na iweje waje dakika chache

    tu mara baada ya mimi kwenda katika nyumba ile na vipi huyu sasa anitaje

    jina langu? Nini hiki kinaendelea?http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Unavuta sigara?"

    Nilimuona yule mtu ambaye bado hakuwa amejitambulisha kwangu, akitoa kasha

    la sigara aina ya embassy na kuiwasha moja ya kwake baada ya kuitupia

    mdomoni. Aliivuta mikupuo miwili mimi nilipokataa kisha akarudisha kete ya

    maongezi mezani.

    "Naitwa Jafari Hiza ningependa unifahamu hivyo kwa sasa mpaka hapo baadaye"

    akanyamaza kwa tuo, kisha akavuta mkupuo mwingine wa sigara na moshi wake

    ukaelea angani kisha akaizima sigara ile. "Nakufahamu wewe ni Ramon na ni

    mpenzi wake Beatrice, Sivyo?"

    "Ndivyo, Lakini..."

    Alininyooshea kiganja chake kilichokomaa na kuinamisha uso wake kama kwamba

    hakutaka kunisikiliza nilichotaka kuzungumza.

    "Sihitaji uongee kitu ambacho sijakuuliza" alinyamaza kwa muda kama

    anayetafakari jambo, kisha akaendelea. "Umefanya kosa kubwa sana mdogo

    wangu. Kumuuwa mtoto wa kigogo wa umoja wa mataifa? Unajiamini nini?"

    "Mimi...?"

    Akanikatisha tena

    "Mimi sijauuwa!" nikajitetea bila matumaini

    "mimi sijamuuwa" Akaniigiza kwa kubana pua kisha akacheka kwa kebehi. "Na

    ile meseji aliyokutumia kuwa kwanini unamuuwa, aliituma saa ngapi? Ulimuuwa

    na kuondoka zako kisha wakati anakata roho ndio akapata nafasi ya kukuuliza

    swali lililotia simanzi kiasi kile au meseji ile alikutumia wakati gani?"







    "Mimi sijauuwa"

    "Hujauwa? Jana usiku wa manane haukuwa naye? Mlisimama getini ukiwa na gari

    yako aina ya Funcargo ukiwa umevaa shati nyeusi ya polo iliyokubana? Labda

    nikuulize, ulirudi saa ngapi tena kufanya mauaji yale?"

    Nikapatwa na ubaridi wa unyevunyevu fulani wa uchungu ulionitiririsha

    machozi kama chemchem kutoka juu ya maporomoko na kwenda chini ya ardhi.

    Nikalia sana kwa kuwa sifahamu chochote kuhusu mauaji ya Beatrice lakini

    kila anachozungumza kilikuwa ni kweli na kuweza kunitia hatiani katika

    mauaji hayo. Nilimuona akisimama na kuweka cd kwenye deki na kuiwasha tv

    iliyopo pembeni yetu. Nikatumbua macho kushuhudia nini alikuwa anaenda

    kunionesha.

    Cd iliyowekwa ilikuwa ikionesha giza, lakini kwa msaada kidogo wa taa

    niliweza kujiona mimi pamoja na Beatrice. Wajihi alioutaja huyu mtu

    aliyejitambulisha kwangu kama Jafary Hiza ndio ule niliouona kwenye cd ile.

    Hapo nikagundua kuwa waliitazama kwanza kabla hawajanihoji chochote.

    Nikajiuliza sana hawa ni watu gani? Kwanini nisipelekwe polisi basi kama

    n'natuhumiwa kwa mauaji na niletwe katika chumba hiki ? Hakika niliumia

    sana nafsi. Jafary Hiza alinitazama na kuniambia

    "Nimekuonesha cd hii kukuambia kuwa vithibitisho vyote vya wewe kuwa umeuwa

    tunavyo sasa sielewi utakataa nini? Na pia labda nikuulize swali"

    akanyamaza kiasi kisha akaendelea "hivi nyinyi vijana kwanini unapomchoka

    mwenzio unamfanyia jambo la kinyama kiasi kile? Na yule mlinzi wa watu

    amekukosea nini? Ndio kupoteza ushahidi? Wale mbwa uliowapa sumu je! Ndio

    walianza au ni Baraka alianza kufa? Kwanini umeamua kufanya mauaji ya

    kutisha kiasi hiki Ramon?"

    Nikanyanyua mdomo wangu kwa mshangao wa ajabu baada ya kusikia kuwa mbwa

    wale waliokuwa wakimlinda Beatrice kuwa wameuwawa kwa sumu "Mimi sihusiki

    na mauaji hayo Jafary sihusiki chochote na sifahamu chochote kuhusu mauaji

    hayo"http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kabla Jafary Hiza hajazungumza alichotaka kuzungumza, kuna sauti ilitoka

    kutoka katika chombo fulani pale mezani.

    "Namba 3 kuna mwanasheria anahitaji kuzungumza na mtuhumiwa"

    Jafary Hiza akajibu "Sawa nimekuelewa namba 1 mfungulie mlango niwaache

    wazungumze"

    Kisha niliuona mlango ambao aliingilia Jafary Hiza ukifunguka na kuingia

    mwanamke mmoja mrembo sana. Kiukweli mwanamke yule alikuwa ni mrembo

    kuanzia alivyovaa hata sura pamoja na umbo lake. Alivaa suruali ya kitambaa

    iliyonyooshwa vyema na kutiwa upanga mkali kisha na koti lake la kitambaa

    kinachofanana na suruali ile aina ya linen ya kahawia, usoni akiwa

    amebandika miwani nyeupe. Hata mwendo wake mwanamke huyu, ulikuwa ni ule wa

    kujitupa tupa kama wa walimbwende waoneshao mavazi au kugombania taji la

    umisi.





    ITAENDELEA 

0 comments:

Post a Comment

Blog