Search This Blog

Friday, October 28, 2022

ZARI LA NDOA - 1

 

     





     IMEANDIKWA NA : RAMAAH MZAHAM



    *********************************************************************************



    Simulizi : Zari La Ndoa

    Sehemu Ya Kwanza (1)







    UTANGULIZI







    Simba hakuwa ni mzungumzaji sana kwa kuwa



    hakuwa amejiandaa kwa tukio ambalo lilitokea kwa ghafla



    bali aliwashukuru sana wote waliofanikisha shughuli ile.



    Upande wa mke alisimama Matwiga



    ambae alitumia muda mwingi mno kumsifu kijana mwenzie



    kwa uvumilivu mkubwa alio uonyesha



    hadi leo wanakutana kwenye…







    NDOA YA ZARI!















    Mjini Songea kwenye kata ya Bombambili, kijana Sungura Masamaki, akiwa amekutana na Zainab Mapunda, binti ambae waliwahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi wakiwa Shule ya sekondari Mahenge, leo wanakutana tena baada ya kupotezana kwa takriban miaka miwili.



    Walitenganishwa na masomo baada ya Sungura kuchaguliwa kuendelea na masomo ya kidato cha 5 kwenye shule ya Sekondari Tosamaganga iliyopo Iringa. Zainab yeye hakuendelea na masomo na hakuwa tu akitaka kusoma.



    Furaha iliwatawala sana kwa kukutana kwa mara nyingine baada ya kupotezana kwa kipindi kirefu, kipindi chot hicho hawakuwa na mawasiliano yoyote, sasa Zainab alionekana ni Zainab kweli, alipendeza sana na umbo zuri la kike lilionekana bila kificho.



    Alimkumbatia Sungura aliekuwa na tabasamu pana usoni wakiwa wameshikana mikono kama watu wanaocheza ukuti. Baada ya kujuliana hali na kuulizana habari za siku nyingi, Sungura na Zainab wakaondoka kuelekea maeneo ya kati kati mwa kata yao ya Bombambili.



    Kila mmoja alikuwa na lake la kusema hivyo waliutumia muda ule kwa kuongea na kila mtu kuonesha hisia zake kwa mwenzie. Lakini Zainab alikuwa anaonekana kama akimlaumu sana Sungura kutokana na ukimya wake kwa kipindi chote akiwa shule.



    Nae Sungura hakuwa nyuma kwenye suala la kujitetea, alimwambia akiwa kule shule hakuwa na uwezo wa kumiliki simu na hata kama angekuwa nayo, asingeruhusiwa kuitumia na zaidi, kwa pale ilipo shule, mtandao ni shida mno. Pamoja na hayo akamuomba msamaha mpenzi wake nae akamuelewa na kumsamehe.



    Walininunua mahitaji yao kama walivyokuwa wakihitaji kila mmoja na mahitaji yake na kuanza kurudi makwao. Sungura alikuwa akiishi na kaka yake aitwae Simba. Wazazi wao tayari walifariki kitambo sana wakiwaacha wakiwa na umri wa wastani wa kuweza kujielewa.



    Ahadi waliyoweka wakati wakiagana ni kwamba watawasiliana baadae hasa muda wa jioni na kueleke nyumbani kuanza kupika chakula cha mchana ili pindi kaka yake atakaporejea akute tayari kafanya mambo.



    Bahati yake akamkuta ndani anasoma gazeti, Simba akamshangaa mdogo wake kwa kurejea akiwa na furaha tele. Akamuuliza vije. Sungura akamwambia kuwa amekutana na Zainab muda ule alipokuwa kienda sokoni na kwenda pamoja nae na wamerejea pia pamoja na kuachana mlangoni Zainab akielekea kwao.



    Simba kamuuliza hasa hiyo ndio sababu ya furaha ile aliyonayo? Sungura akajibu haswaa hiyo ndio sababu ya furaha yake, wala hana sababu nyingine yoyote tofauti, kwani anampenda sana Zainab na katu hatamani kumkosa kwa sababu sasa nae amejua kwamba Zainab nae anampenda sana.



    Tabasamu likamvaa Simba usoni na kumuuliza mdogo wake kuwa ni kigezo gani alichokitumia kujua kwamba Zainab anampenda kwa dakika hizo chache alizokuwa nazo.



    "Kaka, furaha aliyoipata baada ya kuniona huwezi kuamini... Alinirukia shingoni, ni vile tu mimi mwenyewe mdogo wako nipo vizuri kwenye upande wa mazoezi, lah sivyo ndugu yangu, sote tungekwenda chini chali..." Aliongea huku akionesha ishara ya kuanguka.



    Wakacheka na Simba akaongeza huku akikunja gazeti lake alilokuwa akilisoma



    "Na hivi sikuwepo mimi, hata kama umeongeza chumvi ni lazima niamini tu kile ukisemacho," Sungura nae akatabasamu
    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    "Wewe niamini nduguyo, tena baadae anakuja, lakini wewe ulikuwa ukimuona kipindi cha nyuma ambacho mimi sikuwepo, hebu niambie Bro, ilikuwaje?" Alimuuliza kaka yake huku akimsogelea.



    "Sasa mie nikwambie nini mdogo wangu ikiwa wewe mwenyewe tayari umeisha ona dalili zote za mapenzi?" Alihoji Simba huku akimtazama mdogo wake kwa jicho la udadisi.



    "Kaka Simba wanawake hawa, ohoo! mtu anaweza kuigiza bila mwingine yoyote kujua ila tu yule alie karibu yake," alisema Sungura akiwa na nia ya dhati ya kutaka kujua.



    "Sasa unamaanisha mie nipo karibu nae?"



    "Si hivyo, lakini tambua mimi sikuwepo hapa kwa miaka miwili, hivyo hata sijui chochote kilichojiri kwa kipindi hicho chote ambacho mie ckuwepo." Simba alitikisa kichwa kukubali



    "Ni kweli mdogo wangu, lakini wewe ndio una muda bado wa kujua kilichojiri kwa kipindi chote ambacho hukuwepo," alimtoa shaka mdogo wake, nae akahoji



    "Kivipi sasa?"



    "Una marafiki wengi hapa na bado hujakaa nao na hata huyo Zainab hujakaa nae mkaongea ninaamin kabisa utaujua tu ukweli wenyewe."



    "Kaka kama vile kuna kitu unakijua hivi, ila unanificha, hutaki kuniambia."



    "Acha hisia dogo, nikisema nami nikujibu kwa hisia kama ambavyo wee unahisi, basi itakuwa tunadanganyana tu mdogo wangu, tufanye vitu kwa uhakika."



    "Sawa, lakini ujue mimi unanitia shaka, hata hivyo mimi siamini kama wewe hujui lolote kuhusu Zainab, ikiwa wewe mwenyewe ni mdau mkubwa sana wa mambo hayo." Aliongea Sungura huku akicheka na kumfanya Simba atabasamu



    "Dogo ujue Zainab ni shemeji yangu, hivyo heshima ilitawala kila sekunde, asingeweza kufanya kitu chochote ambacho kingeweza kuharibu sifa yake mbele yangu na kila sehemu aliokaa yeye, mie nilipita kama upepo." Sungura akacheka na kuongeza



    "Na ulipokuwepo wewe nae alikuona kama mkwe vile."



    "Kumbe kusoma kuzuri eenh? Umeanza kujua sasa," cheko zikatawala tu kwa wale ndugu huku wakiendelea kurekebisha mambo ya chakula cha mchana.



    Chakula chao kilipokuwa tayari, Sungura alikitayarisha na kusogeza kwenye mkeka wao pale ndani na kumkaribisha ndugu yake wakaanza kula huku wakipiga soga.



    Simba ni mchezaji mzuri sana wa mpira wa miguu wakati Sungura yeye hupenda zaidi mchezo wa Basketball ama mpira wa kikapu. Hivyo walipomaliza tu kula, walipumzika kwa muda mchache na Simba akaanza yeye kuondoka kwenda mazoezini ambapo si mbali sana.



    Siku ya Leo Sungura hakuwa na mpango wa kwenda mazoezini, alikuwa na hamu kubwa sana ya kuonana tena na Zainab, hivyo alipanga ule muda wa kwenda mazoezini, yeye autumie kwa kuonana na Zainab.



    Alijiandaa na kupendeza, akajipiga pamba nzuri alizonunua Iringa na kujitazama mwenyewe ili kujihakiki kama amependeza. Aliporidhika, akatoka na kufunga milango kisha akaelekea nyumbani kwa kina Zainab.



    Walikutana njiani, hatua kadhaa kutoka kwa kina Sungura, Zainab akisema ameagizwa maeneo ya pale jirani nao. Basi ikawa haina budi kukubali tu, lakini Sungura akamwambia anaomba pindi atakapokuwa akirudi kutoka huko, apite kwao atakuwa anamsubiri.







    Zainab akataka kujua kuna nini? Sungura akamwambia kuna mengi anataka kuzungumza nae, kwa mara ya pili wakakubaliana kukutana mara tu atakapotoka huko alipo agizwa atafika moja kwa moja kwa kina Sungura.



    Haraka haraka Sungura akarejea kwao na kujiandaa kwa ugeni ule wa dharula, akachukua pesa kutoka kwenye hifadhi ya kaka yake na kwenda kuchukua vinywaji kidogo yakiwa ni maandalizi ya kumpokea mgeni wake.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Muda ulizidi kukimbia, wakati walipokutana ilikuwa ni saa 10 na sasa ilitimu saa 11 na nusu, Sungura akaanza kuingiwa na hofu ya Zainab kutokuja. Akajilaza kwenye mkeka akiwa ameacha mlango wazi.



    Sijui tuseme bahati ilikuwa ni mzuri ama ni mbaya, usingizi ukampitia japo ulikuwa ni wa mang'amung'amu, lakini ulimchukua. Hadi sauti nyororo ya kike iliokuwa ikibisha hodi ndio ilimshtua kwenye usingizi ule wa jioni.



    Japo alikuwa hajamuona aliebisha hodi, lakini aliamini kabisa kwamba huyo atakuwa ni Zainab kutokana na kuitambua vema sauti ile. Na kweli alikuwa ni Zainab aliefika pale ikiwa ni saa 12 inakaribia na nusu jioni.



    Alikuwa amebadilika, mwanzo wakati walipokutana alikuwa ameziachia nywele zake zikiwa zimechanwa tu, lakini muda huu sasa zilikuwa zimesukwa vema na kumfanya azidi kupendeza na sura yake kuonesha uzuri wake wa asili.



    Zainab alikuwa ni binti ambae analinda mno asili yake, hakuwa akitumia vipodozi vyovyote vyenye kemikali, bali alitumia zaidi vitu vya asili ambavyo vilimpendezesha zaidi na kumpa mvuto wa kipekee.



    Alikuwa ni mnene kiasi, umbo lake likiwa limeendana na urefu wake wa kadri ambao ulishindwa kumuweka kwenye kundi la wanawake warefu wala wafupi bali akiwa saiz ya kati, nywele zake ni ndefu zinazofika begani pindi zikifumuliwa.



    Alimkaribisha kwenye kiti lakini Zainab akagoma nae akaungana na Sungura kuketi chini kwenye mkeka uleule aliokuwa amekaa yeye. Sungura akamuuliza ni vipi amechelewa kiasi kile? Zainab akamuomba msamaha kwa kutokumuambia ukweli wa kile kilichompeleka kule.



    Kitu kilicho mfanya kuchelewa ni kusuka, kule alikwenda kusuka na muda ule pale ndio wamemaliza. Sungura akamuelewa na kumsifu kwamba amependeza. Kwa sura ya aibu Zainab akashukuru.



    Ndio ikapatikana fursa sasa ya kuanza kuulizana yaliyojiri kwa kipindi kile walichokuwa mbalimbali.



    "Zainab nimekuwa nawe mbali kwa muda mrefu sana,"



    "Ni kweli Sungura, tena ukiwa kimya kabisa kana kwamba hujaniacha mie huku."



    "Acha tu mpenzi wangu, tayari kipindi kile cha likizo nilinunua simu, lakini hata sikujua ni vipi nitakupata, kila nikimuomba kaka Simba akutafute..." Akanyamaza ghafla Sungura.



    "Ikawaje sasa?" Aliuliza Zainab kwa shauku



    "Alikuwa akikataa."



    "Ulimuuliza ni kwa nini hataki?"



    "Ndio, lakini hakunipa sababu yoyote ya msingi."



    "Na angeanzaje kwanza? Jinsi ninavyo muheshimu, hata sijui kama ningesimama iwapo yeye angenisimamisha, kifupi ninamuogopa mno, kwanza hata hapa roho si yangu, nimejilazimisha mno kuingia humu ndani," kauli ya Zainab ikamchekesha Sungura.



    "Kwa kipi hasa cha kumuogopa kaka yangu?" Alimuuliza huku akimshika kidevu kukutanisha macho yao.



    "Kwako wewe yule ni kaka ila kwangu mie yule ni kama mkwe," akatoa kicheko kikubwa.



    Sungura akatikisa kichwa kusikitika kuona Simba anachukua sifa ya kuwa mzazi na hali ni ndugu. Akamuuliza juu ya mahusiano yao kipindi cha miaka yao miwili ya kuwa mbalimbali.



    "Sungura mimi siwezi kukusaliti wewe japo ulinipotezea na kukaa kimya, niliamini kuwa utarudi tu ndio maana niliamua kuendelea kuheshimu uhusiano wetu, sijui upande wako."



    "Sioni mwingine chini ya jua hili la Mungu, wewe nachukulia kama wa kwanza na wa mwisho."



    "Kweli Sungura ama unasema ili kuniridhisha tu mie?"



    "Ninachokisema ndio ninachokimaanisha mpenzi wangu," alisisitiza Sungura na kumfanya Zainab atabasamu kisha akaomba ruhusa ya kuondoka kurejea kwao.



    Wakapanga kukutana tena siku ifuatayo. Kwa mara ya kwanza Sungura akachukua namba ya simu ya Zainab na kubeep kwake. Akmbusu mpenzi wake na kisha wakatoka akimshindikiza. Kwa mbali njiani waliweza kumuona Simba akiwa na wenzie wakirejea kutoka mazoezini.



    Zainab akamtaka Sungura wajifiche, Sungura akagoma hadi Zainab alipomvuta pembeni ya nyumba moja na kumshikilia. Safari ikaendelea mbele baada tu ya Simba na wenzie kupita na mwishowa safari ya wale wapenzi wawili ikaishia ndani kabisa ya nyumba ya kina Zainab.



    Pale nyumbani na mtaani kiujumla, Sungura alitambulika kama kijana mpole sana aliefiwa na wazazi wake. Upole wake na kukubali kwake kutumwa na kila mtu pale mtaani ukamfanya apendwe sana na watu wa rika zote eneo lile. Hakukaa sana akaaga na kuondoka kurejea kwao.



    Usiku mzima Sungura aliutumia kuzungumza na Zainab, hadi Simba akamfukuza chumbani na kumtaka aende akazungumze na mpenzi wake huko nje ama akate simu. kwa kuwa ilikuwa ni usiku sana, ikamlazimu akubali kukata simu.



    Akamuaga mpenzi wake kwa shingo upande na kukata simu, sasa akapata nafasi ya kuutafuta usingizi. Haikuchukua muda mrefu usingizi ukampitia.



    Maisha yaliendelea na mapenzi yao yakikua kwa kasi sana, Zainab akawa hakatiki kwa Sungura na Sungura nae simu yake ikawa haiishiwi salio. Kila wakati alikuwa na Zainab isipokuwa usiku na asipokuwa nae machoni, basi simu ilihusika kwa kiwango kikubwa mno.



    Kila saa walilolitumia wakiwa pamoja, lilikuwa ni saa la furaha, mapenzi yaliwatawala. Sasa hakukuwa tena na mtu aliekuwa na swali wala hakukuwa na nafasi ya kuuliza uhusiao wao ulivyo, kila mmoja aliweza kuona kwa macho yake mwenyewe.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Mapenzi makubwa waliokuwa nayo vijana wale wawili, yaliwafanya wazazi wa Zainab washindwe kuongea lolote, walishindwa kukubali uhusiano ule uwepo wala hawakuweza kuuzuia kuendelea, wakabaki kimya tu wakitazama hatma yao.



    Kipindi hicho chote, Sungura alikuwa akisubiri matokeo yake ya mtihani aliokuwa amefanya wa kidato cha 6 ili kama atafaulu, aende akajiunge na Chuo kikuu kwa ajili ya masomo ya Juu na iwapo atafeli ajue ni nini cha kufanya.



    Zainab hakuwa akijua lolote juu ya jambo hilo hadi alipomuuliza mpenzi wake juu ya mipango yake na mustaqbali wa maisha yake. Ndio Sungura akamueleza mchakato mzima wa elimu yake na kuegemea zaidi kwenda chuo kuliko kufeli.



    Hadi Zainab akamuuliza ina maana yeye hawezi kufeli?



    "Hata mimi ninaweza kufeli japo siamini kama itatokea kwa mimi kufeli."















    "Huamini kama kuna kufeli mpenzi wangu?" Aliuliza Zainab huku akiwa anamtazama.



    "Sio hivyo, lakini pia ndio hivyo, hebu tazama pia hata historia yangu."



    "Naona ndio tangu Elimu ya Msingi kwenda Sekondari na kisha kwenda Advance, kote ulipita vizuri,"



    "Naam upo sahihi, lakini unajua ni kwa nini tunafeli kwenye masomo na katika maisha pia?"



    "Ndio, kama kwa shule ninajua, tunafeli kielimu kwa sababu matokeo yanatoka mabaya."



    "Si kweli mpenzi wangu! Matokeo hayatoki mabaya, bali matokeo yanatoka kama vile sisi tulivyotaka yatoke." Aliguna Zainab na kusema



    "Sijakuelewa Sungura." Huku akimtazama kwa umakini mkubwa kama vile yupo darasani.



    "Ni hivi sisi tunafeli sio kwa sababu hatuna akili ama hatuelewi, hapana."



    "Sasa tunafeli kwa sababu gani?" Swali hilo Sungura tayari alikuwa na jibu, kwani alilitegemea.



    "Tunafeli kwa sababu hatujajiandaa na kile tunacho kutana nacho, na kwa kawaida unaposhindwa kujiandaa, unakuwa umejiandaa kushindwa," alimjibu huku akimuwekea kidpole mdomoni.



    "Duh! Sasa nimekuelewa, hivyo hata mie kidato changu cha 4 nilishindwa kujiandaa?"



    "Yap! Na ndio maana ulifeli, lakini bado hujachelewa wangu, muda wa kusoma ni huu sasa."



    "Unasema? Kusoma tena?” huku akijinyooshea kidole cha shahada kifuani mwake “Mimi huyu? Zai… Aah wapi!" Zainab alitikisa kichwa kukataa.



    Sungura akatabasamu na kumueleza umuhimu wa kwenda shule, akamueleza faida ya elimu na fursa kibao zinazo jitokeza mara kwa mara na hudakwa na watu wenye elimu zao, hivyo kuwaacha wale wasio kuwa na elimu kama yeye wakirandaranda tu mitaani.



    “Si lazima uwe na degree ama Diploma Mpenzi wangu, elimu hata kiasi tu inaweza kukuongoza kuliko kutokuwa nayo kabisa,”



    "Hata bado hujanishawishi, mbona wapo wengi sana wenye elimu na hawana kazi kama mie hapa?"



    "Lakini leo hii Zain wewe usie na elimu na mtu mwenye elimu mkipewa mitaji sawa mpenzi wangu na kuanza kufanya kitu, lazima yule mwenye elimu atakuzidi tu, kwani yeye anakua na kitu cha ziada ambacho wewe unakuwa hauna."



    "Mpenzi wangu wala hujaniambia kitu hapo, wapo wafanya biashara wakubwa sana wala hawajasoma hata kidogo na wana endelea kufanya biashara sana tu."



    "Hebu watazame vizuri hao wafanyabiashara unaosema wewe, utakuta wamezungukwa na wasomi nyuma yao, wameajiri wasomi na wanaopambana kweli watoto wao wasome."



    Mada ilikuwa moto sana lakini Sungura akashindwa kabisa kumshawishi Zainab ambae aliamini kusoma ni kupoteza muda tu, pamoja na mifano yote aliompa, lakini haikumtosha kuamini kuwa elimu ni muhimu kwa karne hii ya sasa, karne ya Sayansi na Teknolojia.



    Akamuacha tu kama alivyo na wakaagana kwa mara nyingine ikiwa ni usiku kisha Zainab akaingia ndani na Sungura aliporidhika kwamba Zainab kaingia ndani, nae ndio taratibu akageuza kurejea nyumbani kwao.



    Lakini bado hakuwa ameridhika japo alimuona mwenyewe akiingia ndani, akampigia simu na kumuuliza kama yupo salama, Zainab akamjibu ndio, kisha wakaagana kwa miadi ya kuchat baadae wakimaliza kazi zao.



    Usiku ule ambao walipanga kuchat haukuwa na kero yoyote kwa Simba, mawasiliano yalikuwepo usiku ule, lakini waliwasiliana kwa njia ya ujumbe mfupi wa maneno. Walichat kwa muda mrefu mno.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Hakuna aliemuaga mpenzi wake, bali wote walipitiwa na usingizi. Kila aliekuwa anapitiwa na usingizi, akishtuka na kukuta Msg toka kwa mpenzi wake, anaijibu na kulala, hadi alfajiri walipolala zaidi.



    Zainab ndio alianza kuamka na kumpigia simu Sungura lakini hakupokea kwani tangu usiku uliopita alipokua akichata nae, alikata sauti ili isiwe kero kwa kaka yake, hivyo hadi asubuhi ile simu ilikuwa ikiita kimyakimya ndio maana haikupokelewa na ukizingatia mtu mwenyewe kalala.



    Baada ya kumaliza kazi zake ndogondogo, Zainab sasa ndio akapata muda mzuri wa kukaa na kutafakari maneno ya mpenzi wake. Aliyapa maana sasa, ndio akaona umuhimu wake, akajifikiria sana, kwanini Sungura amshauri kurudi shule? Je kweli kuna fursa kwenye elimu?



    Akili yake yenyewe ikaanza kukinzana kuwa atapoteza muda, lakini hapohapo akajiuliza muda unapotea kwa kwenda shule ama kwa kukaa tu nyumbani bila kazi? Miaka miwili sasa imekatika mimi nimekaa tu nyumbani, hapana, amesema kweliSungura.



    Sasa hakuwa tayari tena kufikiria mara mbili, akanyanyuka na kumfuata mama yake aliekuwa akianika nguo na kumuuliza kama baba yake yupo, mama akamjibu ndio kisha akaendelea na shughuli zake bila kutaka kujua anamuulizia wa nini.



    Moja kwa moja hadi ulipo mlango wa chumba cha wazazi wake na kuugonga. Baba akatoka na kumkuta mwana amesimama mlangoni kama ana jambo vile anataka kuliwasilisha.



    "Mama vipi hujambo?"



    "Sijambo baba, shikamoo!"



    "Marahaba mwanangu, vipi kuna usalama kweli?"



    "Ndio baba, sijui una muda kidogo tuongee?"



    "Haina shida Zainab, unasemaje?" Huku wakiongozana, hadi kwenye masofa na kuketi wakiwa wametazamana baba na mwana, baba ndio akaanza kuvunja ukimya.



    "Haya nakusikiliza mwanangu."



    "Baba nimekaa na kutafakari kwa umakini, nimeamua ni heri nirudi shule, nataka kurudi kusoma sasa."



    "Zainab..." Baba aliita kwa mshangao akiwa katoa macho haamini kile anachokisikia.



    "Abee baba!"



    "Mbona sikuelewi? siku zote umekuwa ukikataa kusoma, nimekuwa nikikaa nawe mara kwa mara kukubembeleza usome kwa takriban miaka miwili sasa, imekuwaje leo?"



    "Amini baba muda tu ndio ulikuwa haujafika, sasa ndio wakati muafaka wa jambo hilo." Aliongea Zainab huku akichezea vidole, alishindwa kusema ukweli kuwa ameshawishiwa na mapenzi yake makubwa kwa Sungura.



    "Hebu muite mama yako," Baba aliamuru na Zainab akanyanyuka na baada ya dakika chache baadae akarudi akiwa ameongozana na mama yake.



    Mbele alitangulia Zainab na mama yake akimfuatia kwa karibu sana. Walipoketi tu chini, Mama Zainab akamuuliza mumewe kuna nini kwani ameitika wito. Mzee Mapunda akamwambia amsikilize mwanae, leo kaja na jambo jipya kabisa.



    Mama akamgeukia mwanae na kumuuliza kulikoni. Zainab akamueleza mama yake dhumuni la kutaka kusoma, mama nae akashangaa na kumuuliza



    "Mwanangu, mwaka jana wote sisi si tulikuwa tukikubembeleza usome ukakataa? Mwaka huu pia umekataa, sasa ni kipi kilichokushawishi leo hadi umetaka kusoma? Ama kuja kwa huyo Sungura ndio kumesababisha?" Aliongea ukweli uliomgusa Zainab ila akakana





    "Hapana mama ujue hakuna kitu kizuri kama elimu na hakuna muda mzuri kuliko huu tulionao sasa, kipindi kile mnaniambia sikuwa tayari kujiendeleza wazazi wangu."



    "Ok! Kwa hiyo kwa sasa upo tayari kwa masomo?" Aliuliza baba.



    "Ndio baba, nipo tayari."



    "Makubwa!" Aliguna mama yake na kupiga makofi ya mshangao huku akijiegemeza kwenye sofa.



    "Lakini kwa muda huu utaweza kweli kukimbizana na wenzio? Maana tayari ni mwezi na kidogo tangu kidato cha 5 waanze masomo," alisema Mzee Mapunda huku akitazama kalenda ya ukutani.



    "Baba mimi nataka kusoma lakini si shule."



    "Sasa unataka kusoma nini?" Aliuliza mama yake kwa mshangao huku akimtazama na kunyanyuka kwenye mgongo wa lile sofa alilokuwa ameegamia.



    "Nataka kwenda Chuo, napenda kuchukua masomo ya Uhusiano wa Jamii."



    "Ok! Una maanisha Public Relations?" Mzee alichangia.



    "Ndio baba." Mama akaona kama vile wanamchelewesha tu, alikuwa haelewi lolote linalo zungumzwa pale. Akanyanyuka na kuaga kwamba anaenda kumalizia kufua huko nje.



    Mzee Mapunda akamwambia mwanae atafute chuo atakacho kisha amjulishe ili yeye afanye taratibu zote, Zainab akamshukuru baba yake na kisha mzee akamuuliza kama kuna jingine. Zainab akamjibu kuwa hakuna kingine, yeye amemaliza ya kwake.



    Basi Mzee Mapunda akanyanyuka na kurejea chumbani kwake akimuacha mwanae akiwa na furaha tele, huku nyuma nae Zainab akanyanyuka na kuelekea chumbani mwake kwa nia ya kwenda kuchukua simu na kumpigia mpenzi wake ili kumueleza kile kilichojiri.



    Lakini alipoingia ndani alikuta kuna miito mi3 ambayo haikupokelewa, yaani missed calls, alipozifungua akauta si za mtu mwingine bali ni zote ni za mtu mmoja ambae hakuwa tofauti na Sungura.



    Zainab akampigia sasa na hakuchelewa kuipokea, na kutokana na sauti ya Zainab kuwa na bashasha iliopitiliza, Sungura akahisi tu hapa kuna kitu. Wakasalimiana na Zainab akamwambia Sungura anataka waonane siku ileile. Sungura akataka kujua kuna nini.



    Zainab akamtoa shaka kwa kumwambia wala asiwe na shaka, atajua tu wakikutana. Hali ya sintofahamu ikamtawala Sungura, akawa na wasiwasi, hata nae akajua kuwa Sungura amepata hofu. Akamhakikishia kuwa si habari mbaya ni nzuri tu na tena yeye ndio atafurahi mno.



    Wakapanga wakutane kwenye uwanja wa shule wa Basketball itakapotimu saa 10 jioni. Sungura ndio alianza kuwasili na kuanza kupasha moto viungo ili kuchangamsha misuli, hadi wanamaliza hatua ile ya kwanza, bado alikuwa hajamuona Zainab.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Amani ikaanza kumtoweka taratibu, akaisogelea simu yake na kuichukua. Alipoiwasha zikaingia msg 2 moja ikiwa ni ya jamaa yake ambayo wala haikumsumbua sana kuisoma na kuifuta.



    Ujumbe mwingine wa simu ulikuwa umetoka kwa Zainab aliekuwa akimjulisha kuwa atachelewa kufika lakini hatoacha kuja, amsubiri pale atafika kabla hawaja maliza mazoezi. Akajibu poa na kuirudisha simu alipokuwa kaiweka na kurejea dimbani.



    Roho yake sasa ikawa shwari, amani ikamrudia tena, akarejea uwanjani na kuwashawishi wenzie wajigawe na kuanza kufanya mazoezi ya kuchezea mpira. Kila dakika kadhaa zilizokwenda, Sungura alikuwa akimtazama Zainab kama kafika.



    Lakini hakumuona, kumbe Zainab kafika kitambo nakukaa kwenye kundi la mashabiki ambao walikuwa wamejitenga kidogo. Aliweza lakini kumuona mpenzi wake akiwajibika ipasavyo.



    Robo ya pili ndio Zainab akajitokeza na kuwa karibu na uwanja sehemu ambayo hata Sungura angeweza kumuona kwa urahisi. Ilikamilika robo ya pili na kabla ya robo ya 3 kuanza, Sungura akaomba kuppumzika.



    Lengo lilikuwa ni kupata nafasi ya kuzungumza na mpenzi wake, akatoka uwanjani na kuvaa nguo zake za kawaida baada ya kuvua zile za mazoezi na kuungana na mpenzi wake kuwatazama wengine wakicheza.



    Shauku aliokuwa nayo ya kutaka kujua ilikuwa ni kubwa, hivyo alipoketi tu chini, akamuuliza kulikoni. Zainab akamwambia kwamba amekubali kurudi shule. Sungura hakuamini, akamuuliza kama ni kweli ama ndio wapo kwenye utani tu.



    Akamhakikishia kuwa akisemacho ni kweli, akafurahi sana na kumbusu shingoni mbele ya watu wala hakuhofia chochote. Zainab akamwambia kwamba bado ana mtihani mmoja wa kujua chuo kipi kinachomfaa japo tayari somo kaisha lichagua.



    Sungura akamuuliza ni somo gani alitakalo, akamjulisha, hapo ndio Sungura akamwambia kazi ile amuachie yeye, ndani ya masaa yasio zidi 24 atakuwa amempatia chuo kizuri ambacho ana hakika hata yeye atakipenda.



    Swali lililofuatia ni kwamba wazazi wake wamemchukuliaje mara tu baada ya kuwaambia kuwa anataka kurudi kusoma ukizingatia wao waliisha mbembeleza sana kipindi cha nyuma na alikataa?



    "Tena ilikuwa kazi, kama vile mama alishtuka!"



    "Kwamba?"



    "Wewe ndio sababu ya mimi kurudi shule."



    "Kivipi yaani?"



    "Alisema labda kwa kuwa wewe umerudi ndio maana mimi nimekubali kusoma, nafikiri aliamini nimetamani kurudi kusoma kwa vile wewe umerudi na elimu, kumbe..."



    "Kumbe nini sasa?" Aliuliza huku akicheka.



    "Ujue Sungura wao wamekuwa wakinishawishi kwa miaka miwili kuhusu suala la kusoma na sikukubaliana nao, lakini wewe umenishawishi kwa masaa yasiozidi mawili na nimekubali."



    "Hapo ndio utaona tofauti ya ubabe wa wazazi na nguvu ya penzi."



    "Hakuna lolote."



    "Lakini hata mimi pia nilikata tamaa jana usiku, nikajua wewe hutaki kabisa shule."



    "Na ndio ukweli ulikuwa hivyo, basi tu maneno yako makali."



    ""Pole sana mpenzi wangu, nyanyuka twende zetu nyumbani, muda umetutupa mkono."



    "He! Kumbe tumebaki wawili tu peke yetu? Twende mpenzi wangu!" Zainab alimjibu huku akitazama huku na kule, Sungura akanyanyuka na kumpa mikono yake yote Zainab atumie kama nguzo ya kunyanyukia, wakaanza kuondoka.



    Njiani Sungura akamjulisha mpenziwe Zainab kuwa kuna watu wanakuja wiki ijayo kucheza nao mechi ya kirafiki, akamuomba asiache kufika kwenye mechi. Zainab akakataa katakata, lakini Sungura alijaribu sana kumbembeleza.



    Zainab akamwambia ule mchezo yeye haupendi, ni heri ingekuwa ni mpira wa miguu angekwenda. Sungura akamwambia atajitahidi kumfundisha akiisha ujua, ataupenda. bado hakukubali, ikabidi Sungura ajidai kapoa kama vile ameumia kwa ombi lake kukataliwa.



    Ili ombi lake likubaliwe, Zainab akamwambia Sungura ampigie magoti. Hiyo haikuwa ngumu, akaanza kupiga magoti, Zainab akamdaka na kumzuia akimwambia kwamba anamtania tu, kwani ule mchezo nae anaupenda sana.



    Akamuahidi ni lazima atakuwepo kwenye mechi tangu mwanzo hadi mwisho wala asijali.





    "Kumbe mpenzi wangu unanipenda eeh?" Aliuliza Zainab



    "Leo umenipata, ila jua kabisa ipo siku yako nawe," Zainab alicheka hadi akashika magoti. Wakawa tayari wamefika njia panda ya kila mmoja kuelekea kwao, wakaagana kila mmoja akikatisha kuelekea nyumbani.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Siku hiyo usiku waliongea kidogo tu na hatimae wakaamua kuchat. Hawakuchukua muda mrefu Zainab akaomba kupumzika kwani alikuwa amechoka sana, wakaagana na kila mmoja akakitafuta kitanda.



    Lakini Sungura alipopanda kitandani, hakulala, bali alichukua simu yake na kuanza kutafuta chuo kupitia mtandao. Chuo ambacho aliona kitamfaa mpenzi wake, alipenda achague kile ambacho kitakuwa ni kizuri zaidi, tena alipenda kisiwe mbali na alipo yeye.



    Alipata vyuo vitatu ambavyo aliviona vinafaa, kimoja kilikua Dodoma, kingine kilikuwa Iringa na cha mwisho alikipata huko Dar Es Salaam. Uchaguzi wa mwisho wa kuamua ni kipi kinachomfaa zaidi, akauacha kwenye nafsi ya Zainab.







    ITAENDELEA 

0 comments:

Post a Comment

Blog