Search This Blog

Thursday, November 24, 2022

FACEBOOK IMEHARIBU MAISHA YANGU - 3

 

     

     



     Simulizi : Facebook Imeharibu Maisha Yangu

    Sehemu Ya Tatu (3)

     

     



    "Bibi yangu aliniambia maneno ya mdomo huumba halisi,na nina uhakika ninachokiongea kwa mdomo wangu Mungu ataniumbia"



    Aliendelea kuongea huku machozi yakifumba macho yake na kitambaa alichokuwa anatumia kujifuta kilikuwa kimelowana tayari kwa wingi wa machozi alikuwa kama yatima vile, Resh alikuwa akifungasha baadhi ya mizigo yake tayari kwa kurejea shuleni tena,tangu tukio la Adam kupotea hakuna aliyetegemea hata siku moja Resh atawaza kurudi tena shuleni kwani waziwazi akili yake ilionekana kuathirika kwa kiasi kikubwa kwa kumpoteza Adam katika mazingira yasiyoeleweka.





    "Baba kesho narejea shule si unajua tayari shule imefunguliwa?" Reshmail alimkurupua mzazi wake huyo kutoka alipokaa kwa mshangao



    "Umesema nini malkia wangu!" alihoji Manyama huku akiwa wima



    "Narejea shule kesho" kwa msisitizo na tabasamu alijibu Reshmail.



    Mzee Manyama hakuamini kwani alikuwa akiwaza ni namna gani atamshawishi mwanae aweze tena kurejea shuleni baada ya matatizo yote yaliyojitokeza kwa mchumba wake Adam ambaye hadi wakati huo bado mwili wake ulikuwa haujapatikana wala taarifa yoyote zaidi ya nguo zikiwa na matundu ya risasi na damu.



    "asante sana mwanangu nakupenda sana" mzee Manyama aliongea kwa furaha huku akimkumbatia mwanae.



    Tangu kupotea kwa Adam aliyehisiwa kuwa tayari amekufa kulipokelewa kwa hisia tofauti na wananchi huku asilimia kubwa ikiegemea upande wa imani potofu za kishirikina wakihusisha tukio hilo na utajiri alionao Mh. Manyama na uchaguzi uliokuwa mbele yake.



    **** *******



    "Wamemtoa mwanangu kafara ili waongeze utajiri,nilimwambia Adam aoe msukuma mwenzake ona sasa,watoto wa siku hizi wabishi wanajifanya wanajua sana na elimu yao inawadanganya"



    mama yake Adam alikuwa analaani vikali mbele ya mume wake wakiwa ndani ya nyumba yao maeneo ya Igoma kwa 'one-way'



    "Usiseme hivyo mama Adam kumbuka sisi ni wakristu,tumwachie Mungu yeye ndio atajua nini cha kufanya"



    Babaye Adam alimtuliza mkewe huku akimgongagonga mgongoni kwa kutumia kiganja cha mkono wake wa kuume.



    Mawasiliano baina ya familia hizi mbili ya Adam jijini Mwanza na ya Reshmail jijini Dar-es-salaam yalikuwa yamekatika licha ya baba yake Adam (mzee Michael) kutangaza kuwa kutoka moyoni mwake amesamehe yote yaliyotokea na anaamini ni mipango ya Mungu.



    Lakini kinyongo kilionekana dhahiri kwa matendo,upendo wa zamani haukuwepo tena jambo hilo lilimfadhaisha sana mzee Manyama kiasi cha kukondeana na kukosa umakini katika utendaji wake wa kazi jambo lililoishusha sana heshima yake kama mbunge aliyekuwa anaheshimika sana kuanzia bungeni hadi jimboni kwake,



    Wapinzani walitumia fursa hiyo kumchafua hasahasa na kweli uchafu huo ukakubalika kwa wananchi kwa ujumla Manyama hakuwa na lake tena pale,wananchi walimpuuzia sana tofauti na zamani na hata hiyo miaka miwili iliyobaki wananchi waliiona kama ni mingi sana kuwa na kiongozi wa aina yake.



    Kuliko fedheha yote hiyo Mh. Manyama kwa hiari yake mwenyewe alipitisha kura ya maoni ya wananchi kuhusu imani waliyonayo kwake kama mbunge wao.



    Asilimia 70 ya waliopiga kura walidai hawana imani naye huku asilimia kumi na nne tu ndio wakidai bado wana imani naye na kura zilizobaki zikiharibika,rasmi Manyama akawa ametolewa bungeni na katika uchaguzi mdogo uliofanyika akachaguliwa mbunge kutoka chama cha upinzani na maisha yakaendelea huku Mh.Manyama akiendelea na biashara zake mikoani.



    * **



    Adam akiwa pale bustanini alivamiwa ghafla na wanaume wawili wa shoka wakiwa na bunduki,ishara ya kidole mdomoni ilimfanya atulie tuli kisha wakamwonyesha ishara kwamba awafuate alifanya kama walivyotaka hadi kwenye gari iliyokuwa imepaki pembeni kidogo ya nyumba yao Adam alishangazwa sana na ukimya uliokuwepo hakuwepo mlinzi wala mama mkwe wake.



    Safari yao ilikwenda mpaka Iringa gari iliyokuwa na vioo vyeusi 'tinted' ilimzuia Adam kujua ni wapi alipo,gari ilizimishwa ndani ya jumba kubwa sana ambapo alipelekwa kwenye chumba kikubwa tu,hofu kubwa ilimtawala hakujua kwa nini yuko pale,hakupigwa wala kupewa bughudha yoyote,hali hiyo ilzidi kumshangaza



    "au ndio wachuna ngozi" alijiuliza Adam kwa hofu tele.



    Hayo ndio masharti ambayo mama Reshmail alitoa kwa vijana aliowapa tenda hiyo ya kumtorosha Adam pale nyumbani. Shida yake haikuwa kumtesa Adam bali kumweka mbali na mwana (Reshmail) ambaye alikuwa amempagawisha ipasavyo katika mapenzi ya jinsia moja.



    Suala la pesa halikuwa tatizo hata kidogo alichohitaji ni kutimiziwa alichotaka. Mkataba wa miaka mitano ndio alioingia na watu hawa kukaa na Adam bila kumruhusu kutoka nje ya jingo.



    Bi Gaudencia aliamini kwamba kwa kutokomea Adam mbele ya uso wa Reshmail ilikuwa fursa nzuri ya kurudisha tena uhusiano wake na Reshmail ambao ulikuwa unaelekea kufa lakini kinyume chake alikuwa ameibua chuki kubwa baina yake na mwanae ?heri wote tukose kama ni hivyo? alijiapiza mama Reshmail baada ya kuona dalili za kumshawishi Reshmail hazipo tena



    Alikuwa ni Reshmail mwingine kabisa mkasa uliomkumba ulimbadilisha sana na kuitanua akili yake sana,Eveline naye alisikitishwa na yaliyomkumba shoga yake akajitahhdi sana kuwa karibu naye kumpa moyo huku akijiepusha sana kufanya vitendo ambavyo vitamkumbusha Resh jinsi alivyoweza kukutana na Adam.



    Ni katika kujiepusha na kumkera rafiki yake huyo kipenzi Eveline akajikuta amefuta picha za uchi na filamu za ngono katika kompyuta yake akawa si mtu wa kutoroka shule,hakuwa tena mtu wa wanaume na hatimaye akawa Eveline wa kuigwa na wanafunzi wenzake jambo hilo liliwaduwaza sana wanafunzi pale shuleni lakini ndio hivyo Eve alikuwa amekubali mabadiliko katika maisha yake.



    Juhudi zao katika masomo ziliendelea kuwaweka katika nafasi nzuri ya kufanya vizuri mtihani wao wa mwisho. Hawakuyazungumzia tena yaliyopita tena walijadili mapya na yanayowanufaisha



    "Eveline wewe ni kama dada yangu nakupenda sana"



    "Nakupenda pia Reshmail umebadili maisha yangu moja kwa moja nina maisha mazuri sasa" alijibu Eva kwa upole huku akimwangalia Reshmail aliyekuwa anaishusha chandarua yake aweze kulala. Ni kweli walitokea kupendana wawili hawa.



    "Hivi Resh una mpango bado wa kusomea uhasibu mi lazima niwe mhasibu"



    "Mh! unavyojiaminisha utadhani tumefaulu tayari" alijibu Resh.



    "He! mi najua sisi kufaulu kwetu sio swali ni jibu,swali ni je tunaenda chuo gani na kusomea nini." alijiaminisha Eveline.



    "ok! nilidhani nitasomea uhasibu lakini kwa heshima ya Adam nitasomea sheria" alijibu Reshmail kwa furaha.



    "Mh! na upole wako huo na mambo ya kutoa hukumu wapi na wapi? mwenzio naangalia ankara" alisema Eva.



    "Wala hata siendi kuhukumiana naenda kwa heshima tu" alisisitiza Reshmail.



    "Mh! haya mheshimiwa hakimu napenda kujitetea kama ifuatavyo"



    Eve alitania akifuatiwa na kicheko kikubwa kutoka kwa Reshmail.





    Maisha yaliendelea vyema sana tu japo yalikuwa maisha ya mashaka Adam aliruhusiwa kuongea na kuuliza kila kitu kasoro swali moja tu "Kwa nini niko hapa?",ndio hakuruhusiwa kuliuliza hata kwa mbali,watu wote pale hawakuwa na ubaya nae hata kidogo,hawakumtesa,hakugombezwa wala hakufanya kazi,alipewa huduma zote za msingi,aliweza kutoka nje na kwenda bustanini lakini nje ya geti hakuruhusiwa.



    Tayari aliyazoea maisha haya lakini kumbukumbu ya jinsi alivyochukuliwa ndani ya jumba la wakweze bila kupata msaada wowote ule "Nani atakuwa nyuma ya haya yote mlinzi alikuwa wapi? Mama Resh je?" alijiuliza sana bila kupata wa kumpa jibu.



    "Hivi unaitwa dada nani vile?" Adam alimuuliza dada mmoja ambaye kila baada ya siku tatu alikuja kufanya usafi katika chumba chake.



    "Naitwa Beatrice Cosmas niite Bite" alijibu huku anafuta vioo kwa dirisha la chumba cha Adam.



    "Una jina zuri wewe mh!"Alisanifu Adam.



    "Asante wewe ni Adam eeh!" aliongezea yule binti huku akiwa ameacha shughuli yake aliyokuwa anafanya.



    "Ndio mimi ni Adam! samahani nikuulize maswali machache"



    "Uliza tu lakini sitakujibu sasa hivi"



    "Kwa nini?"



    "We uliza yote ndo nitakwambia kwa nini"



    "Hivi hapa ni wapi? kwa nani? na kwa nini nipo hapa?"



    "Ndio hayo matatu tu?...sawa nitakujibu kwa sharti dogo sana yaani"



    "Sharti gani hilo mi nipo tayari"alitoa uhakika Adam bila hata kulijua sharti lenyewe.



    "Sikia Adam sina haja ya kuzunguka zunguka nina mwaka wa pili hapa kitu kinaitwa mwanaume katika mwili wangu ni kama ndoto sasa ni wewe wa kutii kiu yangu na mimi nitajibu maswali yako" alijieleza Bite,jambo ambalio lilikuwa zito na la kumshangaza Adam.



    "Mh! au ndo mtego tena kutoka kwa Reshmail? dah! ikiwa hivyo nitaaibika kweli mimi"Alijiwazia Adam kwa mashaka makubwa kabla ya kujibu.



    "Basi utakuja kunijibu baadaye!" alisema Adam.



    "Haya usiku na wewe jiandae" alijibu na kuaga Bite.



    Hayawi hayawi mara yakawa usiku wa saa tatu,Bite tayari ndani ya chumba cha Adam ndani ya khanga moja peke yake.



    "Haya nipe nikupe hakuna longolongo hapa" alizungumza Bite.



    "Subiri taratibu basi,sikiliza" alianza kujitetea Adam wakati Bite anajisogeza kitandani,Adam alikuwa amechelewa tayari joto la Bite lilipenya katika mwili wake na kumchanganya hadi kujikuta akifanya kinyume na alivyotarajia kwamba atafanikiwa kutegua mtego wa Bite badala yake alikuwa ameshafanya mapenzi na Bite.



    Kwa Bite ulikuwa ushindi mkubwa sana kwani tangu aletwe hapo kuwa msaidizi wa kazi za ndani ya vyumba hakuwahi kutoka nje ya jengo hilo,sio kwamba alikuwa amefungwa hapana kila kitu kilikuwepo ndani kila siku pia alikuwa ameridhika kuwa hapo.



    "Hapa ni Iringa,nimejibu swali lako la kwanza tuendelee tena nikujibu swali la pili na tatu" alisema Bite kwa shauku kubwa sana.



    "Hapana Bite imetosha kwa leo sijisikii vizuri,siku nyingine basi sawa!" alidanganya Adam na Bite hakuwa mbishi akambusu Adam shavuni akajiondokea zake.



    Ilimchukua takribani siku tano Bite kugundua kwamba tayari ameshika ujauzito jambo ambalo halikuruhusiwa katika jumba hilo na alipewa onyo kali wakati anaingia hapo. Kwa usalama wake na Adam alifikiria suala la kutoroka lakini haya yote aliyafanya baada ya kuongea na Adam na kumweleza hali halisi.



    Ni katika wasaa huo alimweleza Adam chanzo ambacho kinaweza kuwa kimemsababishia yeye kuwepo pale



    "Umemchukulia kigogo mpenzi wake,umemendea mtoto wa kizito au umemkataa kimapenzi mtu maarafu" hizo ndizo zilikuwa baadhi ya sababu alizoorodheshewa na Bite,lakini kwake yeye aliona hakuna hata moja inayomuhusu kwani wazazi wote wawili wa Reshmail walimpenda sana hakuwa tayari kuweka hisia kwamba pengine moyoni wanamchukia.



    "Usijali lakini hutakaa milele humu,huwa unafika



    Muda aliyekuweka humu akiridhika unatoka.



    "Nitamlea mtoto,napenda watoto hata kama usipokuwa mpenzi au mume wangu nitampenda sana na nitamwita....."



    "Christian akiwa mvulana au Christina akiwa msichana" alidakia Adam ambaye kwa mbali alianza kumtamani Bite kimapenzi.



    * * *



    Biashara za baba yake zilikuwa zinaendelea vizuri na skendo lake lilikuwa linafifia taratibu. Hadi anamaliza kidato cha sita Reshmail mapenzi kwa wazazi wake yalikuwa palepale na japo hakutaka kumwongelea Adam jena alikuwa na picha yake waliyopiga pamoja siku moja kabla ya tukio lile la kushangaza na kuumiza.



    Reshmail kwa ruhusa ya wazazi wa Eveline alienda nae mpaka kwao ambapo walikaa wote kwa siku tano kisha akarejea tena Arusha.



    Urembo wa Reshmail ulipagawisha kila mwanaume na hata baba yake ilifikia kipindi akakiri kwamba kweli pale alizaa mtoto mmoja wa kipekee na kweli alikuwa wa kipekee. Mama Resh bado alikuwa na matamanio lakini kwa sasa alimwogopa sana Reshmail tofauti na miaka mingi iliyopita.



    "Baba na mama wiki ijayo nataka kwenda Mwanza kwa wazazi wa Adam" Resh alitoa hoja yake wakiwa mezani wanakula.



    "Wapi? Mwanza! hawatakuelewa mwanangu utakuwa kwa maksudi kabisa unafufua shari iliyopoa tayari"



    Kwa busara tele na upole mzee Manyama alimweleza mwanae ambaye pia aliyapokea kwa nidhamu ya hali ya juu na kichwa chake kuyakubali kuwa yana maana kubwa ndani yake.



    "Nimekuelewa baba sitaenda tena" alijibu kwa unyenyekevu sana Reshmail.





    Matokeo ya kidato cha sita yalipotoka hayakuwa ya kushangaza sana kwa upande wake kwani alikuwa amevuna alichokipanda. Reshmail alikuwa amepata daraja la kwanza na ndivyo alivyotarajia,furaha yake iliongezeka baada ya kumwona katika orodha Eveline Maige rafiki yake kipenzi naye akiwa amepata daraja la kwanza huku wakitofautiana pointi kadhaa.



    Akiwa anajiandaa kumpigia simu tayari simu yake iliwakawaka na kuandika "pacha" jina ambalo alikuwa amemwandika Eve katika simu yake,badala ya kuongea wote kwa pamoja wakaanza kucheka,walicheka sana hadi simu ilipokatika. Zilikuwa ni furaha kutoka moyoni,kwa nini wasifurahi wakati ndoto zao zilikuwa zinatimia?



    Tanzania Commission of Universities (T.C.U) ilipotoa uchaguzi wa kwenda vyuoni Reshmail kama alivyopenda alichaguliwa chuo kikuu cha mtakatifu Augustine Mwanza kwa masomo ya sheria huku Eveline Maige akipelekwa Mzumbe chuo kikuu kwenda kuchukua masomo ya uhasibu shahada ya juu.



    "Ndugu hakimu naomba kujitetea!" Eve alimtania Resh utani wao wa shuleni siku walipokuwa wanaagana.



    Walikuwa wametenganishwa hatimaye lakini mawasiliano yao yalidumu



    Kama alivyojiwekea kiapo chake cha kutopenda hovyohovyo ni hivyohivyo alivyoingia pale chuoni,hakuringia uzuri wake lakini hakutaka pia usumbufu unaopitiliza kutoka kwa wanaume yaani kwa kifupi alikuwa na msimamo mkali sana,ni rafiki yake (Eve) pamoja na wazazi wake ambao wangeweza kubashiri sababu hasa inayomfanya binti huyu awe hivi na si mtu mwingine pale chuoni.



    Maringo yake yalifichwa na werevu wake darasani,kwani ilikuwa ni warembo wachache sana wa aina yake waliofanya vizuri kimasomo,jambo hilo lililowavutia waalimu wengi sana na wanafunzi ambao wanapenda maendeleo kimasomo. Reshmail hakuwa mtu wa mambo mengi hakunywa pombe wala kwenda kumbi za starehe usiku starehe yake ilikuwa ni kusoma na michezo.



    Mnamo mwezi wa pili michezo ya FAWASCO ilipoanza michezo hiyo inayohusisha vitivo vyote pale chuoni,kwa maksudi alichaguliwa kuwa mhamasishaji kwa wasichana wajibu alioufanya vizuri ipasavyo na kikubwa zaidi akawa pia mdhamini mkubwa sana. Moyo wake wa kujitolea uliwavutia sana wanadarasa wenzake ambao baadhi walimpenda huku wengine wakidai ana maringo, msimamo wa Reshmail ulibaki palepale.



    Mwaka wa pili pale chuoni ndio ulikuwa mbaya kwake. Darasa walilolitumia mwaka wa pili wanafunzi wa kitivo cha sheria,lililojulikana kama Mombasa Raha kwa mbele lilikuwa na picha kubwa sana ya Adam ambayo ilikuwa pembeni ya ubao wa kufundishia hiyo ikimaanisha kwamba kila atakapoingia darasani lazima aione,"ADAM THE GREAT" yaliandikwa maandishi haya chini ya picha kubwa ya Adam.



    Amani,ikatoweka kabisa moyoni mwake kumbukumbu mbaya za kumpoteza mpenzi wake Adam zikaanza kumrejea kwa kasi sana.Reshmail akaanza kujihisi yeye ndiye chanzo cha yote hayo,tofauti na waalimu wake hakuna mwanafunzi aliyemfahamu Adam zaidi ya kujua tu historia ya yaliyomkuta na wengi kuichukulia kama simulizi tu ya kusadikika. Reshmail alianza kuwa mtoro darasani na hata alipoingia badala ya kumwangalia na kumsikiliza mwalimu,mawazo yake yote yalivutwa na picha ya Adam yenye tabasamu pana mara zote aliamini inamuangalia yeye na kumlaumu kwa kumkatisha masomo yake kwa penzi la mtandaoni.



    "Adam stop blaming me!!(Adam usinilaumu)" alipiga kelele kwa nguvu Reshmail bila kujitambua.



    Mwalimu alimshangaa na hakuelewa kilikuwa kimemsibu nini "Is she dreaming? (Anaota?)" aliuliza mwalimu Sijjo aliyekuwa anawafundisha somo la mawasiliano (Communication skills),darasa zima likacheka kwa fujo sana,lakini Reshmail alikuwa analia huku akitetemeka sana,kwa ghadhabu akasimama na kutoka nje.



    Japo ulikuwa ni mwezi mmoja tu tangu waanze masomo ya mwaka wa pili lakini

    tabu na mateso aliyokuwa ameyapata yalitosha kumshawishi kuwa huenda amesoma hapo kwa miaka kumi.Wazazi wake hawakuwa na la kufanya,Eveline alibaki kumwonea huruma shoga yake huyu alijaribu mara kwa mara kumpigia simu lakini haikuwa tiba ya tatizo la Reshmail.



    Ni kweli Reshmail asingeweza kujilazimisha kuwa na furaha kwani ni yeye aliyemshawishi Adam awe nae kimapenzi na ni yeye huyuhuyu alimshawishi Adam aende kwao kwa ajili ya kujitambulisha na safari hiyo ikawa ya mwisho ya Adam.



    "Nikiwaambia waalimu wangu watanielewaje,na hata wakinielewa itakuwaje wanafunzi wenzangu wakijua siri hii? watajenga picha gani tena kuhusu mimi, mh! niepushe na hali hi bwana,kama uliweza kuniondolea mawazo haya hadi nikamaliza kidato cha sita vyema hebu baba na sasa ondoa tena na hili jaribu zito mbele yangu na jina lako lisifiwe."



    aliweka ombi fupi Reshmail katika mawazo yake hayo. Lilikuwa ni jambo gumu sana kwa Reshmail alikonda sana na punde si punde maneno ya wakosaji yakaanza tena "Mh! kumbe ndio maana anakataa wanaume kumbe anaishi kwa matumaini maskini,dada mrembo kama huyu" yalisikika maneno hayo katika vijiwe vya wanafunzi pale chuoni.



    Ilikuwa ni kero kubwa kila alipokatiza vidole vilimwelekea yeye umaarufu wake wa awali kwamba ni mrembo ukaongezeka maradufu karibia chuo kizima lakini wakati huu ilikuwa ni sifa mbaya kwamba ana virusi vya UKIMWI hata yeye aliyasikia maneno hayo yalikuwa yakivuma kwa kasi,hakuwa na uwezo wa kuzuia tetesi hizo



    "Wangejua kwamba mi ni bikra na wanayoyasema yote ni uongo,hata wasingenyanyua midomo yao michafu kuropoka upuuzi huo,lakini bila Adam watajuaje?" alijiuliza Reshmail akiwa chumbani mwake katika hosteli ya Ngulelo aliyokuwa amepanga chumba alichoishi peke yake. Marafiki zake taratibu wakaanza kumtenga wakiamini ameathirika,hilo halikumuumiza kichwa kwani alilitegemea sana hasa hasa dhana ya unyanyapaa kwa waathirika iliyokuwa inatawala chuoni hapo.



    ***



    Bite alifanikiwa kutoroka katika ngome ile kubwa aliyokuwa amehifadhiwa Adam. Kwa jinsi alivyokuwa amezoeleka pale haikumchukua muda mrefu kumshawishi mlinzi amfungulie geti atoke kidogo na ndio ikawa jumla hakwenda mbali sana na mkoa wa Iringa bali aliweka kambi yake maeneo ya Uyole Mbeya mkoa uliopo jirani na Iringa ambapo kipesa kidogo alichoondoka nacho pale ndani alifungua kibanda chake sokoni na kupanga nyumba eneo jirani la Igawilo akianzia maisha ya kulala chini hadi aliponunua godoro.



    Biashara ya kuuza nyanya na mbogamboga ilimkimu sana maisha yake kwani wazo wala tegemeo lake halikuwa kununua gari,au kujenga nyumba hapana lengo lake lilikuwa uhai pekee,na shilngi elfu moja alizozipata zilikuwa zinamtosha kabisa.



    Alikuwa mchangamfu na mstaarabu sana,wateja walivutika kwake kwa kasi kufaidi ukarimu wake katika biashara.Tumbo lake lilianza kukua taratibu,kina mama sokoni wakaanza kuhisi tayari Bite kapata mjanja Mbeya amemjaza mimba,lakini miezi yake ya kujifungua ndiyo ilifungua akili za waliokuwa na maswali na kugundua kwamba ile mimba alikuja nayo pale na sio kwamba aliipatia pale. Salama bin salmin Bite alijifungua mtoto wa kiume miezi tisa ilipowadia.



    "Mh! baba yake atafurahi tena alimpa jina pale tu nilipomwambia nimeshika mimba" Bite kwa furaha tele aliwaambia kina mama wa pale sokoni,akiwemo jirani yake mama wawili,ni hao ndio walikuwa ndugu zake.



    "Hongera Bite,sijui ndio unakuwa mama nani vile" Bite alihojiwa na mama wawili



    "Mwanangu anaitwa Christian" alijibu Bite huku akibusu kichanga chake hicho ambacho kilikuwa kinarusharusha miguu na mikono yake huku na huko.



    Christian alizaliwa akiwa na afya tele na hakusumbuliwa na magonjwa wakati wa ukuaji wake mwaka wa kwanza,ilikuwa furaha kubwa kwa mama yake.



    **************



    Miaka ilizidi kukatika wazo la Bi. Gaudencia kumtoa Adam katika jumba lile lilikuwepo kichwani mwake kwani udhaifu alioupata Reshmail pamoja na kashfa mbaya anazozipata pale chuoni zilimsononesha sana lakini ataanzia wapi kuificha aibu yake pale ambapo Adam,akasababisha uovu wa mama huyu uwekwe hadharani.



    Ni jambo hilo lililomuumiza kichwa mama huyu.



    "Reshmail na baba yake watanielewaje kwa mabaya niliyowafanyia,nimeishusha heshima ya mume wangu aliyekuwa na heshima kubwa bungeni" alizidi kuwaza



    Huku Iringa maeneo ya Ruaha Adam alikuwa anauanza mwaka wa tatu,akiishi kama nyumbani kwake,lakini hakuridhika hata kidogo maisha hayo ya ufungwa.



    Miaka mitatu ilikuwa mingi sana "Mama na baba yangu wanahisi niko wapi? vipi kuhusu mpenzi wangu Reshmail,hapana imetosha nahitaji kutoka hapa,lakini lazima nijiulize nitatoka vipi hapa katika ngome hii" alijisisitiza Adam japo ulinzi madhubuti ulioongezwa kutokana na kutoroka kwa Bite katika mazingira ya kutatanisha pale ngomeni



    ***



    Mwaka wa pili uliisha hivyohivyo kimateso makali yaliyojawa na kumbukumbu mbaya na isingekuwa kuhamishwa kwa darasa la sheria mwaka wa pili kwenda katika maghorofa ya Mwanjonde chuoni hapo basi Reshmail angefeli vibaya masomo yake kutokana na msongo wa mawazo.



    Akiwa mwaka wa tatu afya yake ilirejea tele kwani hakuwa akiiona tena picha kubwa ya Adam machoni pake hali hiyo ya afya kurejea ilizusha msemo mpya tena,tofauti na mwanzo walivyosema ana Ukimwi,sasa walisema "Akikonda ana virusi,akinenepa ameanza kutumia dozi"



    Yote hayo alituhumiwa Reshmail lakini kamwe hakuwahi kuthubutu kunyanyua mdomo wake kujibu vijembe hivyo yeye alikuwa mkimya huku akipambana na masomo hadi alipoumaliza mwaka wake wa nne vyema.



     

    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog