Search This Blog

Friday, November 18, 2022

KAZI ZA NDANI NCHINI OMAN ZILIVYONIKUTANISHA NA KIFO - 2

 






Simulizi : Kazi Za Ndani Nchini Oman Zilivyonikutanisha Na Kifo
Sehemu Ya Pili (2)




PAMOJA na kukarahishwa na maswali yaliyokuwa katika dhana halisi ya kibaguzi, lakini nilivyoingia tu ndani ya lile jumba, akili yangu ikahamia kwenye mandhari ya mule ndani. Niwe mkweli, tangu nizaliwe hadi leo hii, sijawahi kuona sebule nzuri kama lile la jumba la kifahari la tajiri Abdallah Mustapha lililopo Suwaiq nje kidogo ya Jiji la Muscut nchini Oman.

Macho yangu yalikuwa hayatulii, niligeuza shingo huku na kule, nikivutiwa na fenicha ghali zilizokuwa mule ndani. Nilikuwa mtulivu wakati Marimu akifanya mazungumzo na yule msichana wa Kiarabu utaratibu wa mkataba wangu.

“Shika hii,” yule msichana wa Kiarabu alinipa karatasi.

“ Agripina Soma vizuri huo mkataba wako wa kazi mama, kisha tia saini hapo chini, ” Mariamu ambaye alikuwa kama wakala wangu alishadadia baada ya kuwa nimepokea karatasi ile.

Nilipitia ule mkataba ulioandikwa kwa Lugha ya Kingereza. Pamoja na kwamba sijui lolote kuhusu mambo ya sheria, hasa sheria za mikataba ya ajira. Nilihisi tu, mkataba ule ulikuwa na mapungufu fulani ambayo nashindwa kuyabainisha hapa moja kwa moja.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Nilipo gota kwenye nukta ya mwisho ya mkataba ule, sikuamini nilipoona nitalipwa kiasi cha Riyal 100 ambayo kwa pesa za kwetu ilikuwa ni karibu shilingi laki sita na ushee.

Yanii kufanya usafi, kuosha vyombo, kufua na kupika, hivyo tu. Nalipwa laki sita na ushee!!!

Niliona ni pesa nyingi nilizo takiwa kulipwa ukilinganisha na kazi nitakazokuwa nikifanya. Niliamini wakati wa kupunguza umasikini kwenye familia yangu ndiyo huo.

Sikutaka kuchelewa. Nilimwaga saini kwenye ile karatasi na nikawa nimeingia mkataba wa miaka miwili Kwa makubaliano ya kuongezewa mkataba endapo mwajiri wangu atakubaliana na utendaji wangu wa kazi.

Muda mfupi badaye, nilielekezwa mazingira ya jumba lile sanjari na kutambulishwa kwa wafanya kazi wenzangu wawili mmoja mwanamke aliyeitwa Fatuma emeke kutoka Liberia na yule mvulana wa Kisomali, ambaye nilitambulishwa kwa jina la Hussein Jabal, baada ya mambo hayo kukamilika Mariamu aliniaga:

“Mimi naondoka.”

“Sawa...Lakini kuna ajambo nilitaka kukuuliza Mariamu.”

“...kuhusu?”

“Kuhusu uvumi wa wasichana wa kazi kufanyiwa ushenzi wakiwa huku ikiwemo kubakwa.”

“Kubakwa!!!” Mariamu alishangaa.

“Ndio, kubakwa”

“Kubakwa ni sehemu ndogo sana ya changamoto zilizopo huku, kwanza ni jambo la kawaida tu, kikubwa unachotakiwa kufanya ni kuwa tayari kuipokea hali hiyo pale itakapokutokea.” Mariamu aliongea kauli hiyo kiwepesi sana.



“Niwe tayari kubakwa pale hali hiyo itakapo tokea?”niliuliza nikiwa nimemkazia jicho.

“Siyo uwe tayari kubakwa...”

“Bali?”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

“Uwe tayari kufanya mapenzi kwa hiyari.”

“Sijaja huku kufanya mapenzi na mtu wa aina yeyote. Lakini pia, sikuja huku ili ninyanyasike kwa namna yeyote ile Mariamu, hukunieleza mambo hayo kabla ya kupanda ndege, kwa nini unanigeuka?” nilisema kwa sauti kavu lakini yenye viashiria vya hofu kubwa.



“Ngoja nikupe siri moja...” Mariamu alisema. Kabla hajamaliza mara Zakia alitokea na kunitaka nianze majukumu yangu.

Mariamu aliniaga, akanipa miadi ya kuonana wakati mwingine. Nikabakia nikiwa na mashaka na wasiwasi moyoni.

Mashaka yalikuwa makubwa sana. Sikuwa na imani tena na Mariamu. Kama nilivyosema awali, mwanamke huyo nilimwona ni mtu aliyejaa hila usoni mwake, tangu siku ya kwanza aliponipokea uwanja wa ndege wa Muscat.

Siku hiyo, nilianza kazi kwa nidhamu na umakini. Mwenyeji wangu akiwa ni Fatuma Emeke msichana mweusi na mzuri wa umbo kutoka nchini Liberia.

Siku kadhaa nikiwa ndani ya ile nyumba ya kihafahari, kama mfanya kazi wa ndani (house girl) nilibaini jambo jipya.



Yule mwanamke wa kiarabu. Zakia Al Majidi mke wa Abdallah Mustapha alikuwa ni mke wa pili wa tajiri huyo ambaye alikuwa na watoto wawili wa kiume kutoka kwa mke wake waliokuwa wakiishi na mama yao katika mji wa Al Jibrih mashariki mwa Jiji la Muscut nchini Oman.

Niliendelea kufanya kazi nikiwa ni mtu mwenye mori na ari. Sikuwahi kukutana na matukio kama yalivyokuwa yakivumishwa nikiwa Tanzania. Ama nilivyokuwa nikihisi. Hapakuwa na mtu aliyewahi kunisumbua kimapenzi aidha kuninyanyasa kwa namna yoyote ile ingawa majivuno na ubaguzi wa rangi wa Bi Zakia, sikuwa napendezwa nao.

Nilimaliza mwezi mmoja salama, nililipwa mshahara wa kwanza vizuri bila tatizo lolote. Siku napokea pesa kama malipo ya kazi zangu lilikuwa ni jambo la furaha mno kwenye maisha yangu. Niliamini huo ndiyo muda wa kukamilisha ndoto zangu za kupunguza hali ya maisha duni kwenye familia yangu.

Hapa kuna jambo moja nimesahau kulieleza: Nimesahau kueleza kwamba, moja ya sheria ambazo ziliwekwa na Bi Zakia pale nyumbani kwake, dhidi ya wafanyakazi wa ndani ilikuwa ni kutotumia simu za mkononi. Hadi leo sijui yule Mwarabu kwa nini alituwekea sheria ya kijinga vile.

Nakumbuka Kila mwisho wa wiki, nilikuwa nikifunga safari hadi Muscut. Huko nilipiga simu nyumbani, nikawasiliana na na familia yangu. Lakini pia, nilikuwa nikiwatumia pesa kwa njia kama ‘mape-xpress’ ‘western union’ ‘telegram’ na kadhalika.

Katika kipindi chote cha maisha yangu ndani ya nyumba ya tajiri Abdallah Mustafa, mtu wa karibu kwangu alikuwa ni yule mvulana Hussein Jabal, raia wa Somalia. Ukiachilia mbali Fatuma ambaye alikuwa ni mfanyakazi mwenzangu wa wa kike tuliyeshirikiana kwenye kazi zote za ndani. Ukaribu wangu na mvulana huyu ulitokana na uwezo wake wa kuzungumza Kiswahili.

Mbali na hilo, Hussein alikuwa ni mtu mcheshi na msikivu, Kila siku baada ya kazi, tulikaa kwenye bustani ya majani na kuzungumza mambo mengi, nilipata kuelewa mambo mengi kuhusu mtu yule. Hata yeye alijua mambo kadhaa kuhusu maisha yangu.

Ukaribu wangu na Hussein ulinifanya nimzoe. Kumzoea kukazaa hali ya kumuwaza kila wakati. Hali ile ya kumuwaza kila wakati, kukatengeneza hali nyingine ya kummisi hususani pale awapo mbali na mimi.

Taswira ya sura ya Hussein Jabal ilianza kuniganda kichwani mwangu. Sikutaka kujiongopea kabisa kwamba moyo wangu hauvutiwi na uso wenye pua ndefu, macho makubwa sanjari na meno yaliyojipanga vizuri mithili ya punje za muhindi.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Sikutaka kabisa kujifariji kuwa nafsi yangu haikuvutika na umbo kakamavu la yule mvulana.

Lakini hata hivyo, akili yangu haikuwa tayari kuukubali ukweli uliotoka moyoni mwangu, ukweli wenye viashiria vyote vya mapenzi kwa mvulana yule.

Nilijikumbusha na kujionya juu ya msukumo huo. Sauti moja kichwani iliniambia jiepushe na mapenzi, yatakuletea matatizo mapenzi, fuata kilichokuleta Agripina. Sauti hiyo ilikuwa ikigonga kichwa changu kama kengele, lakini pamoja na hilo, bado moyo wangu ulikumbwa na wazimu dhidi ya mvulana yule. Taa nyekundu ilikwisha waka moyoni.



Nilijikumbusha na kujionya juu ya msukumo huo. Sauti moja kichwani iliniambia jiepushe na mapenzi, yatakuletea matatizo mapenzi, fuata kilichokuleta Agripina. Sauti hiyo ilikuwa ikigonga kichwa change kama kengele, lakini pamoja na hilo, bado moyo wangu ulikumbwa na wazimu dhidi ya mvulana yule. Taa nyekundu ilikwisha waka moyoni.

Bila kutarajia nikajikuta mimi na mvulana yule tunaanzisha mahusiano ya kimapenzi. Mapenzi ambayo yalikuja kuleta madhila makubwa mno kwenye maisha yangu hadi leo hii ninapo simulia mkasa huu.

mahusiano yetu yalianza kama mzaha. Awali nilichukulia kama nimepitiwa na jinamizi la mahaba na tamaa za mwili kwa bahati mbaya. Niliamini mwisho wa penzi lile ni kupotea kama lilivyokuja, akini kadri siku zilivyokuwa zikiyoyoma ndivyo mapenzi yangu na mtu yule yalivyozidi kustawi na kukua kwa kasi.

Hussein Jabal alikuwa ndiyo mvulana wa kwanza kuujua mwili wangu. Nakumbuka siku ya kwanza kugaragara nae kitandani, ilikuwa ndiyo mara yangu ya kwanza kuingia kwenye sayari ya mahaba kunako sita kwa sita. Huwa siwezi kuisahau siku hiyo.

“Asante Agripina,” Hussein alisema akiwa amelala chali. Kichwa changu kikiwa juu ya kifua chake. Tukiwa kama tulivyozaliwa.

“...kwa?”

“Kwa penzi tamu...na...Kwakuwa mwanaume wa kwanza kufungua bikira yako.”

“Usijali Hussein ila jambo moja....”nilisema huku nikigeuza shingo yangu na kumwangalia machoni. Tukawa tunatizamana.

“Usiniache tafadhali.”

“Siwezi kukuacha Agripina, nataka siku moja tukaishi Mogadishu, huko kwetu Somalia.”

“Kweli?”

“Kabisa.”

Huo ulikuwa ni mwanzo wa mimi kuingia kwenye mambo ya kiutu uzima. Uhusiano kati yangu na mvulana yule ulikuwa ni siri ya watu watatu. Kwa maana ya mimi mwenyewe, Hussein pamoja Fatuma Emeke, ambaye alikuwa ni mfanyakazi mwenzangu kutoka Liberia.

Usiri wa penzi langu na mvulana yule, raia wa Somalia ulitokana na jambo moja kuu. Tuliogopa Sheria kali ya nchi ya Oman iliyokuwa ikisimamia misingi ya ‘sharia’

Ilikuwa hairuhusu vijana ambao hawajaoana kuwa kwenye uhusiano wa kimapanzi. Adhabu yake ilikuwa ni kuchapwa viboko hadhalani au kufukuzwa nchini humo kwa wageni.

Tuliendelea kufanya kazi kwa bwana Abdallah Mustapha kwa nidhamu kubwa huku mahusiano yangu na Hussein yakiendelea kwa kasi lakini yakiwa kwa siri kubwa.

Kila siku usiku nilikuwa nikiondoka chumbani kwangu na kwenda chumbani kwa Hussein. Huko nilifanya nae mapenzi usiku kucha na alfajiri kabla ya adhana, nilirejea chumbani mwangu.

Hayo ndiyo yalikuwa maisha yangu huko Suwaiq nchini Omani kabla ya siku moja kutokea tukio moja lililobadili dira ya maisha yangu!

http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

****



“Ta, ta, ta...” sauti ndogo ya mshale wa saa ya ukutani ilisikika. Ilikuwa yapata saa sita na nusu usiku, nilikuwa nimelala chali huku macho yangu yakitizama kwenye dari.

Hakuna kilichosikika zaidi ya sauti ndogo ya saaa ya mshale sanjari na mkoromo mdogo uliokuwa ukitoka kwa Fatuma aliyekuwa kwenye usingizi wa pono.

Nilijinyanyua kitandani na kuketi kitako, macho yangu yalihamia kwenye kipimo cha kupima ujauzito, bado moyo wangu ulishindwa kukubaliana na ukweli kwamba nilikuwa mjamzito. Niliogopa. Muda wa kuwa na mtoto haukuwa sahihi.

Nilivuta pumzi kwa ndani na kuzitoa kwa mkupuo. Kwa mujibu wa saa ile ya ukutani ilikuwa yapata saa sita kasoro, usiku.

Nilavaa nguo, nikatoka nje. Nikatembea kwa kunyata kukifuata kibanda alichokuwa akilala Hussein, ndani ya nyumba ile ya tajiri Abdallah Mustapha.

Kulikuwa na ukimya eneo lote la nyumba ile ya kifahari. Nilisogea hadi mlangoni mwa chumba cha Hussein na kusukuma mlango.

Alaa!

Mlango ulikuwa umefungwa kwa ndani.

Haikuwa kawaida kwa Hussein kufunga mlango hasa kwa kipindi ambacho tunakuwa tumekubaliana kuwa nitakwenda chumbani kwakwe.

Nikasukuma tena. Mlango haukufunguka.

Kuna nini? Nilijiuliza kimoyomoyo.

Nikayatembeza macho kulia na kushoto nikichukua tahadhali ya kubambwa.

Nikarudi tena mlango, sasa nikataka niugonge kidogo kumwamsha Hussein nilihisi huenda alipitiwa na usingizi na alijisahau akafunga mlango.

Lakini kabla sijatekeleza hilo, ghafla nikasikia sauti kutokea mule ndani.

Ilikuwa ni sauti ya kilio cha mwanamke, nikamakinika na hali hiyo. Nikatega sikio.

Toba!

Nikaendelea kugundua kuwa ilikuwa ni sauti ya kimahaba ya mwanamke aliyekuwa ndani ya chumba cha Hussein Jabal.

Ndani ya chumba kulikuwa na watu waliokuwa wakifanya mapenzi.

Hussein ananisaliti!....

Ndiyo wazo la kwanza kupita kichwani mwangu.

Mwili ukanitetemeka. Donge zito likanikaba kooni, nikahisi uchungu wa ndani kwa ndani. Wivu ukanivaa.

Nikaugonga mlango kwa nguvu. Sikujibiwa zaidi ya kuendelea kusikia sauti ya mwanamke aliyekuwa akilia. Kilio cha raha.

Kitendo hicho kikazidisha wahaka ndani ya nafsi yangu. Kichwa changu kikawa na maswali lukuki.

Ndani ya lile jumba la kifahari, tulikuwa wanawake watatu. Fatuma Emeke, Zakia ambaye ni mke wa Abdallah Mustapha pamoja na mimi.

Kivyovyote vile Hussein ndiye alikuwa akifanya mapenzi na mwanamke mule ndani. Swali kuu ni Je mwanamke huyo ni nani?

Ni Fatuma au ni Zakia? Fatuma nilimwacha chumbani akikoroma. maana yake ni kwamba siyo Fatuma. Ni nani? Zakia.

Nilipo muwaza tu mwanamke huyo, hapo hapo taswira ya tabia zake zikanijia akilini.

Mbali ya wivu dhidi ya mumewe, Alikuwa ni mwanamke mwenye dharau na majivuno, mtu mweusi kwakwe alikuwa ni kikatuni kisicho na maana yoyote.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Alikuwa ni mbaguzi asiye na mfano. Hakupenda kuchangia meza moja ya chakula na watumishi wake wa ndani. Siku zote alimini mtu mweusi yupo duniani kwa ajili ya kumtumikia mtu mweupe.

Kwa mantiki hiyo anawezaje kuwa ndiye mtu aliye ndani wakifanya mapenzi na Hussein Jabal mvulana asiye na mbele wala nyuma kutoka huko Mogadishu nchini Somalia.

Sasa kama ni hivyo mwanaume huyo anafanya mapenzi na nani?

Nilijihoji huku nikijawa na wivu mwingi kifuani kwangu, donge zito lilinikaba kooni kila nilivyozisikia kelele za kilio cha mahaba kutoka mule ndani.

“Yanii huyu bwana anipe mimba halafu kama haitoshi ananisaliti!! Nilifadhaika san.

kwa nguvu zangu zote niliusukuma mlango na kuingia ndani.

Sikuamini macho yangu....





ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog