Search This Blog

Thursday, July 21, 2022

PENZI BILA MAUMIVU - 5







      Simulizi : Penzi Bila Maumivu

      Sehemu Ya Tano (5)



      Miongoni mwa wanachuo walioonyesha msimamo wao mkubwa kwa Mungu alikuwa Peter, kila siku chuoni hapo alikuwa akiamka asubuhi sana, anasali mpaka muda wa kwenda kunywa chai kisha kuingia darasani.

      Mbali na kusoma, maisha yake yalitawaliwa na maombi tu, kila wakati alipokuwa, alikuwa akichezesha lipsi zake kumaanisha kwamba alikuwa akiomba kitu kilichomfanya kuamini kwamba alisogea karibu na Mungu.

      Hakufikiria kitu chochote kile, kila kitu kilichopita alikichukulia kuwa kama historia ambayo kamwe isingeweza kujirudia maishani mwake, aliamua kwa asilimia mia moja kuyakabidhi maisha yake mikononi mwa Mungu.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      Mchungaji ambaye alitamani sana siku aje kuwa kama yeye ni Reginald Bonke ambaye alipokuwa akiombea wagonjwa, waliponywa na hata wale waliokuwa na ulemavu wowote ule mwilini mwao walipokea uponyaji.

      “Nitafanya nini ili niwe kama Bonke?” aliuliza Peter.

      “Unatakiwa kuomba sana,” alijibu profesa wa chuo hicho, mchungaji Kennan Willton.

      “Hilo tu?”

      “Hapana! Maombi yako yasiwe hivihivi, ni lazima ufunge pia, jitahidi kuwa karibu na Mungu na ninakuahidi kwamba utakwenda kuona miujiza yake mingi,” alisema mchungaji Willton.

      “Sawa, nitafanya hivyo!”

      Hakutaka kuishia kimaneno tu bali alichokifanya ni kuanza kufanya kile alichokuwa ameambiwa, alianza kuomba sana, kila wakati akawa mtu wa kuomba, hakutaka kupata muda mwingi wa kula, hata muda wa mapumziko haukuwa ukitosha, alichokuwa akikifanya ni kuomba tu.

      Wakati mwingine akawa akifunga kwani maombi ya mfungo yalikuwa na nguvu mno, siku ambayo alifunga, alijifungia chumbani kwake siku nzima akiomba tu. Maisha yake yakaanza kubadilika kwa kiasi kikubwa mno, kila siku akawa mtu wa kumuabudu Mungu tu.

      Alikaa chuooni hapo mwaka mzima, hatimaye akarudi nchini Tanzania. Alikuwa na nguvu mno, alipokuwa akiingia kanisani, kwa kumwangalia tu, watu walikuwa wakiogopa, uwepo wa Mungu ulionekana mwilini mwake kiasi kwamba kila mtu aliyekuwa akizungumza naye alizungumza naye kwa kutokujiamini kabisa.

      Kanisa hilo lilipoandaa mkutano, Peter akaanza kuwaombea watu waliokuwa wakifika uwanjani hapo. Miujiza mikubwa ikatokea kiasi kwamba watu hawakuamini kile walichokuwa wakikiona, mtoto yule wa mchungaji ambaye aliondoka nchini Tanzania kwenda kusoma nchini Canada, leo hii alikuwa na upako mkubwa mno mpaka wa kuponya wagonjwa, watu hawakuamini.

      Jina lake likaanza kukua, kila alipoambiwa kwa kupewa sifa aliweka wazi kwamba si yeye aliyekuwa akifanya hivyo bali ni Mungu aliye juu. Hakuwa mbali na Lydia, alichokifanya ni kutangaza ndoa na baada ya mwezi mmoja, Peter akamuoa msichana huyo kanisani na hata aliporudi Canada kuendelea na masomo, alikuwa na pete yake kidoleni.

      “Mchungaji.....”

      “Hapana! Mimi si mchungaji, mimi ni Mwinjilisti.”

      “Sawa Muinjilisti, Mungu amekupa nguvu kubwa sana ambazo kila mtu anatamani kuwa nazo, siri ya kuwa hivyo ni nini?”

      “Kumuomba Mungu kila wakati, hiyo ndiyo siri yenyewe,” alisema Peter.

      Chuo kizima akawa gumzo bado aliendelea kumuomba Mungu kila siku. Baada ya kumaliza mwaka huo, akarudi nyumbani na watu wengi akiwemo baba yake kumshauri kufungua kanisa lakini Peter hakutaka kukubaliana nao.

      “Haiwezekani, hakuna Mwinjilisti mwenye kanisa, wenye kanisa ni wachungaji,” alisema Peter.

      Hayo ndiyo yakawa maisha yake, kila siku alikuwa na kazi ya kuwaombea watu kitu kilichowafanya wengi kumshangaa kutokana na nguvu alizokuwa nazo.

      Alijijengea heshima, watu wengi waliokuwa na wagonjwa wao wakampeleka kwa Peter ambaye alifanya miujiza mingi na watu kubaki midomo wazi kwa kutokuamini kile walichokuwa wakikiona.

      “Au jamaa anapanga nao?”

      “Hakuna bwana! Unamjua Chungua?”

      “Ndiyo! Si yule mlemavu wa mtaa wa pili?”

      “Ushamuona sasa hivi?”

      “Hapana! Mara ya mwisho kumuona ni wiki iliyopita.”

      “Sasa nnikwambie kitu! Jamaa alimuombea Chungua, ule ulemavu umeondoka,” alisema jamaa huyo.

      “Acha masihara!”

      “Ndiyo hivyo!”

      Kila kitu alichokuwa kikifanya alisema kwamba utukufu ulitakiwa kubaki kwa Mungu, hakujipa utukufu kwa kuamini kwamba si yeye aliyekuwa akifanya hivyo, kuponya watu na kutenda miujiza.

      Kutokana na kile kilichokuwa kikiendelea, Peter akajikuta akiwa mtu maarufu nchini Tanzania, kanisa lao lilizidi kupata watu, watu wakamjua zaidi Peter kuliko hata mchungaji wa kanisa hilo.

      *****

      Watu zaidi ya Elfu sitini walikata tiketi kwa ajili ya kuangalia tamasha kubwa lililotarajiwa kufanyika ndani ya Jiji la Berlin katika Uwanja wa mpira wa Timu ya Hertha Berlin, Olympio, tamasha la mwanamuziki aliyekuwa akivuma kwa kasi kipindi hicho, Tatiana ambaye alikuwa akifanya ziara yake kuzunguka sehemu mbalimbali duniani.

      Ziara hiyo kwenda nchini Ujerumani ikatangazwa sana, kila mtu akapania kumuona msichana huyo jukwaani, watu hawakulala vizuri, wengi walikuwa na hamu ya kumuona msichana huyo aliyekuwa na uzuri wa ajabu mno.

      Wakati watu wakimsubiri kwa hamu kubwa, hapo ndipo kulipoanza kuvuma uvumi kuhusiana na suala zima la ubaguzi wa rangi. Kukaokotwa makaratasi kadhaa yaliyoyokuwa yakimdhihaki Tatiana kutokana na ngozi yake, tena makaratasi yote hayo yalikuwa yakitupwa mitaani, watu walipoyaokota na kuyasoma, waliompenda, walichukia mno.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      Hilo lilikuwa moja ya jambo lililoumiza vichwa vya wengi, wakataka kufahamu ni nani aliyetuma makaratasi hayo jijini Berlin lakini hakukuwa na mtu aliyefahamu lolote lile, yaani hata wao walipigwa na upofu mkubwa wa kutokujua chanzo cha karatasi zile mitaani.

      Tatiana akashikwa na hofu, historia ya nyuma juu ya nchi hiyo kuwa ya kibaguzi mno ikajirudia kichwani mwake na kuanza kuogopa mno. Washauri wake walimwambia asiende nchini Ujerumani lakini Tatiana hakutaka kujali kelele za kibaguzi, alichokuwa akikitaka ni kwenda nchini humo tu.

      Alikaa na mpenzi wake, Buffet na kujadiliana naye kwa muda mrefu juu ya wao kwenda nchini Ujerumani, walikubaliana kwa moyo mmoja kwamba walitakiwa kwenda kwani tayari watu walitoa kiasi kikubwa cha fedha ili kumuona, hivyo kuahirisha ziara kilikuwa kitu ambacho kingepunguza mvuto wake kwa mashabiki wake.

      “We have nothing to do, we have to get there,” (Hatuna cha kufanya, twende huko) alisema Buffet.

      Hawakuwa na jinsi, ili Tatiana asiweze kupoteza mashabiki wake walitakiwa kwenda huko, hawakutakiwa kuhofia kitu chochote kile, ilikuwa ni lazima wafanye kila liwezekanalo ili ile heshima aliyokuwa nayo iwe kama kawaida.

      Makaratasi yaliendelea kusambazwa, kukaonekana kuwa na kamchezo fulani kalichokuwa kakichezwa na kikundi fulani cha watu, japokuwa serikali ya nchini Ujerumani ilijitahidi sana kufanya kila linalowezekana ili kuwagundua watu hao lakini hawakufanikiwa kabisa.

      Maandalizi makubwa kuliko sehemu zingine yakaanza kufanyika, baada ya kukaa siku mbili, wakaanza safari ya kuelekea nchini Ujerumani tayari kwa kufanya shoo moja babu kubwa ambayo aliamini kwamba ingewaacha watu midomo wazi.

      ******

      “Ich liebe immer noch Partner , deine Liebe zu mir tut.“ (Bado ninakupenda mpenzi, penzi lako kwangu halitokufa)

      “Sind Sie sicher?“ (Una uhakika?)

      “Warum liebst du sie?” (Ndiyo! Kwani huyo malaya umempendea nini?)

      “Nur seine Popularität,“ (Umaarufu wake tu.)

      “Verließ ihn , Popularität nicht etwas haben, gerade jetzt, dass ich ufuike schnell , nicht möglich ist, treffen Sie angekommen?“

      (Achana naye, umaarufu hauna kitu sasa hivi, naomba ufuike haraka, si inawezekana kuonana ukifika?)

      “Vollständig , dies sehr seltsam.“(Sijajua kabisa, huyu malaya kaniganda sana.)

      “Struggling Partner! Aber ich werde es nicht mehr reagiert Tonhöhe sein, werden Sie im Hotel ein beliebter präsentieren.“

      (Jitahidi mpenzi! Hata mimi nitakuwa uwanjani hapo kukupokea, nitakuwepo katika hoteli mtakayokuwepo kipenzi.)

      Buffet alikuwa bize akichati simuni, muda wote aliokuwa akichati, uso wake ulijawa na tabasamu pana, alifurahia kile alichokuwa akiandikiwa, moyo wake ukajisikia amani kubwa.

      Pembeni yake alikuwepo mpenzi wake, Tatiana aliyeonekana kuchoka mno, alipokuwa amelala, akachukua nafasi hiyo kuchati na msichana wake aliyekuwa nchini Ujerumani, msichana ambaye alimpenda kwa moyo wa dhati kuliko alivyompenda Tatiana.

      Msichana huyu aliitywa Nikola, alikuwa Mjerumani halisi ambaye alikuwa mtoto pekee wa tajiri mkubwa nchini Ujerumani, bwana Kurt. Wawili hawa walionana zamani mno, walipendana kwa kuwa walisoma shule moja na mpaka Buffet alipokuwa akifika nchini Ujerumani, mtu wake wa kwanza kuonana naye alikuwa msichana Nikola.

      Mapenzi yao hayakufa, waligombana mara kwa mara na kurudiana, waliishi pamoja na baadae kugombana tena, ndivyo walivyoishi na hata katika kipindi ambachjo msichana Nikola aliposikia kwamba Buffet kapata msichana aitwaye Tatiana, moyo wake ulimuuma mno.

      Hakuwa na cha kufanya, kila alipokuwa akiona picha walizopiga Tatiana na Buffet, moyo wake ulimuuma mno ila hakuwa na cha kufanya, akabaki na maumivu makali ya moyo.

      Siku ziliendelea kukatika, alipoanza kusikia kwamba mwanamuziki huyo alikuwa njiani kufanya shoo nchini Ujerumani, kitu cha kwanza kabisa akaanza kuwasiliana na Buffet kwa lengo la kurudiana tena kama uilivyokuwa kawaida yao.

      Buffet hakuwa na kipingamizi, japokuwa alikuwa na Tatiana aliyemfanya kuwa maarufu pia lakini kwa Nikola hakupindua, akajikuta moyo wake ukianza kumpenda tena msichana huyo na kumuona Tatiana kama takataka.

      Alichokifanya Nikola ni kuandaa watu wake kwa ajili ya kumchafua Tatiana, tena huku akiwalipa kiasi kikubwa cha fedha, hakutaka Wajerumani wampende kwa kuwa alikuwa mtu mweusi, hivyo akachapisha karatasi nyingi kwa ajili ya kuzisambaza tu ili jina la Tatiana liharibike.

      Akafanikiwa na hakugundulika kabisa. Baada ya siku kadhaa, Buffet akaanza kuelekea nchini Ujerumani huku akiwa na mpenzi wake, Tatiana pembeni. Ndani ya ndege, muda mwingi alikuwa akiwasiliana na Nikola na kupanga kile kilichotakiwa kufanyika lakini mwisho wa siku wawili hao waweze kuwa tena kama ilivyokuwa zamani.

      Wakakubaliana, mioyo yao ikarudi mapenzini kwa mara nyingine tena, Buffet, hakutaka kuwa na Tatiana tena, moyo wake ukaanza kumrudia Nikola ambaye aliona wivu sana kumuona Buffet akiwa na msichana huyo, alitaka kufanya kila liwezekanalo, hata kuua aue lakini mwisho wa siku aweze kuwa na Buffet.

      Tatiana hakulifahamu hilo.



      “I want to sleep my love...” (Ninataka kulala mpenzi wangu) alisema Tatiana kwa sauti ya chini iliyoonyesha ni kwa jinsi gani alikuwa amechoka.

      “Don’t you wan’t to eat?” (Hautaki kula?)

      “I’m tired, I cant’t do anything else, let me sleep.” (Nimechoka, siwezi kufanya kitu kingine chochote, acha nilale)

      Safari ndefu kutoka nchini Marekani mpaka Ujerumani ilimchosha mno Tatiana, hakuwa na hamu ya kula, kitu alichokuwa akikifikiria ni kulala tu. Kwa Buffet, alikuwa amechoka lakini kwake ilionekana hiyo kuwa nafasi kubwa na ya kipekee aliyokuwa akiililia sana.

      Hakutaka kulala, tayari alikwishawasiliana na Nikola na kuambiwa kwamba alikuwa hotelini humohumo chumba namba 72 hivyo walitakiwa kuonana. Hakutaka kupoteza muda, kwa kuwa tayari alizungumza naye kwa kirefu, akatoka chumbani humo, kwa mwendo wa kunyata na kisha kuanza kuelekea nje huku akiwa na kisingizio kichwani mwake kwamba alifuata chakula.

      Kwa mwendo wa harakaharaka akaanza kutembea kuelekea kulipokuwa na chumba cha Nikola, alipofika, hakugonga hodi, kwa kuwa mlango uliachwa wazi, akaufungua na kuingia ndani.

      Nikola alikuwa kitandani, hakuwa na nguo yoyote mwilini mwake, alipomuona mpenzi wake wa kitambo akiingia chumbani, akanyanyuka na kuanza kumsogelea, wote wawili wakakumbatiana kimahaba na kuangushana mpaka kitandani.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      “Nimekukumbuka mpenzi,” alisema Nikola huku machozi yakianza kuusanyika machoni mwake.

      “Nimekukumbuka pia, umekuwa mzuri sana mpenzi wangu,” alisema Buffet huku akionekana kuchanganyikiwa kwa furaha.

      Hakutaka kumkumbuka Tatiana mahali hapo, mtu ambaye alimfikiria sana, aliyempagawisha kuliko wote alikuwa Nikola tu. Umbo lake lilikuwa zuri, sura yake ya kitoto ikampagawisha zaidi mpaka kuhisi kwamba chumbani humo alikuwa na msichana mpya ambaye hakuwahi kuonana naye kabla.

      “Nikupe nini?” aliuliza Nikola.

      “Mapenzi yako motomoto,” alijibu Buffet na kisha kuanza kubusiana.

      Usiku huo wakakumbushia enzi, kipindi chote hicho Tatiana alikuwa amelala chumbani na hakushtuka kuona uchafu aliokuwa akiufanya mpenzi wake katika chumba kingine na msichana mwingine.

      Buffet alitumia masaa mawili kuwa chumbani humo na kisha kutoka na kuelekea mghahawani kuchukua juisi na kisha kurudi chumbani ambapo bado alimkuta Tatiana akiwa usingizini.

      Hakutaka kukaa kimya, akaanza kuchati na Nikola huku akimwambia namna alivyompagawisha kitandani na kumfanya kukumbuka mbali. Hakutaka tena kuwa na msichana kama Tatiana, kwa kuwa alikuwa amekwisharudiana na Nikola, akatafuta njia ya kuachana na msichana huyo.

      Mpaka inafika asubuhi, Buffet alikuwa akichati na Nikola tu simuni, penzi lao likafufuka upya na kila mtu akawa na hamu ya kutaka kuchati na mwenzake zaidi. Hakukuwa na mtu aliyeweza kuwatenganisha tena,

      Siku hiyo ilikuwa ni ya kuzunguka huku na kule, kulitembelea Jiji la Berlin ambalo lilikuwa na vivutio vingi. Kila alipopita, watu walitaka kupiga naye picha, kumuona mwanamuziki huyo ilikuwa ni bahati kubwa, hivyo kumuacha akipita lilikuwa suala gumu.

      “Mbona una mawazo mpenzi?” aliuliza Tatiana, kila alipokuwa akimwangalia Buffet, alishindwa kuelewa kuna tatizo gani.

      “Sina mawazo.”

      “Sasa tatizo nini?”

      “Nahisi kuumwa.”

      “Jamani! Basi changamka mpenzi, huoni picha zinavyopigwa mfululizo, changamka basi,” alisema Tatiana.

      Mawazo ya Buffet hayakuwa hapo kabisa, alikuwa akimfikiria msichana Nikola tu. Kichwa chake kilivurugika kwa msichana huyo, hakutaka kusikia kitu chochote kile, alichokuwa akikifikiria ni kuwa na msichana huyo tu.

      Hakujua ni kwa namna gani angeweza kuachana na Tatiana na mwisho wa siku kurudi kwa mwanamke ambaye aliutesa mno moyo wake. Alijaribu kufikiria mengi, yale aliyotakiwa kufanya lakini mwisho wa siku hakujua afanye nini.

      “Ushamwambia?” aliuliza Nikola simuni.

      “Kumwambia nini?”

      “Kwamba haumtaki!”

      “Naogopa sana Nikola.”

      “Unaogopa nini?”

      “Sijui naogopa nini, ila naogopa kufanya hivyo,” alisema Buffet.

      “Kwa hiyo nikusaidie?”

      “Utanisaidieaje?”

      “Kesho, muda atakaotoka uwanjani, naomba usipande naye gari moja,” aliandika Nikola.

      “Huwa hatupandi pamoja hasa anapokuwa kikazi.”

      “Sawa. Kesho shoo yake ikiisha, usipande naye gari moja.”

      “Kwa nini?”

      Nikola hakutaka kujibu swalihilo, hakutuma tena meseji na hata Buffet alipojaribu kumpigia, msichana huyo hakuwa akipatikana kitu kilichomuacha kwenye wakati mgumu wa kufahamu juu ya meseji ile ya mwisho aliyokuwa amemwandikia.

      *****

      Watu walijazana ndani ya Uwanja wa Olympio, kila mtu aliyekuwa uwanjani hapo alikuwa na shauku ya kuangalia tamasha kubwa lililotangazwa sana katika vyombo vya habari duniani juu ya mwanamuziki aliyekuwa na nyota ya kupendwa sana, Tatiana ambaye alitarajiwa kufanya onyesho katika uwanja huo.

      Watu wengi waliokuwa ndani ya uwanja huo walikuwa na fulana zilizokuwa na picha ya Tatiana ambaye alitarajiwa kushusha shoo kubwa ambayo haikuwahi kutokea tangu nchi ya Ujerumani kuanznishwa.

      Uwanja ulijaza, watu walijaa kila sehemu na hakukuwa na nafasi kabisa, watu wote walijazana uwanjani hapo kwa ajili ya kumwangalia mwanamuziki aliyekuwa akishika nyoyo za kila mtu kipindi hicho, Tatiana.

      Ilipofika saa moja usiku baada ya maandalizi kukamilika, Tatiana akapanda jukwaani hapo na kuanza kutumbuiza. Uwanjani ilikuwa mshikemshike, hata wale walinzi waliokuwa uwanjani hapo, walionekana kutokufaa kutokana na wingi wa watu waliokuwa wakitaka kupanda jukwaani japo kumshika msichana huyo.

      Wengine wakashindwa kuvumilia, wakaanza kulia huku wakishangilia, msichana mweusi aliyekuwa akibaguliwa nchini Ujerumani, matokeo yake akaanza kuwaliza Wazungu kitu ambacho hakikuwahi kufanywa na mwanamuziki mweusi yeyote yule.

      Wakati Tatiana akiendelea kutumbuiza, Buffet alikuwa nje ya uwanja huo, hakutaka hata kuwepo ndani kwani moyo wake ulikuwa ukimfikiria Nikola tu. Hapo nje hakuwa peke yake, kwa kuwa kulikuwa na mghahawa mkubwa, akaelekea hapo ambapo akaonana na Nikola na kuanza kuzungumza naye huku kwa mbali akiisikia sauti ya mpenzi wake ikitumbuiza.

      “Unaogopa nini?” aliuliza Nikola.

      “Namheshimu tu.”

      “Kwa hiyo huwezi kumuacha?”

      “Sijajua, ila unataka ufanye nini?”

      “Nimuue!”

      “Umuue Tatiana?”

      “Ndiyo!”

      “Haiwezekani! Naomba usifanye hivyo!”

      “Haina jinsi Buffet.”

      Nikola hakutaka kukaa sana mahali hapo, alichokuwa amekisema ndicho alichotaka kuona kikitokea. Alimchukia Tatiana na ilikuwa ni lazima amuue, alitaka kusababisha ajali kama ile iliyomuua mwanamuziki wa Kimarekani, Aaliyah.

      Buffet alibaki akiwa na mawazo tele, japokuwa alihisi kwamba moyo wake ulikuwana mapenzi ya dhati kwa msichana Nikola lakini kuna kipindi alifikiria kwamba alikuwa na chembechembe za mapenzi kwa msichana huyo mrembo, Tatiana.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      Nikola alipoondoka, naye akarudi uwanjani mpaka tamasha lilipoisha saa sita usiku na kisha kuelekea sehemu ya kuegeshea magari kwa ajili ya kuondoka. Muda wote huo, Buffet hakuwa na furaha, alionekana kuwa na hofu kubwa huku kwa kumwangalia tu ungegundua kwamba kulikuwa na kitu alichokuwa akikijua ambacho kilimsumbua moyoni mwake.

      Mara baada ya kusaini vitabu vya mashabiki wake, Tatiana akaingia garini huku akiwa na furaha tele, aliwapungua mikono, vioo vikapandishwa na kuanza kuodoka mahali hapo huku akiwa na msafara wa magari matano.

      Moyoni alifarijika mno, hakuamini kama alimaliza vizuri kufanya shoo ile iliyokuwa imehudhuriwa na watu wengi. Msafara wa magari hayo ukaanza safarui kuelekea hotelini, kila mmoja alikuwa kimya garini, walipofika kwenye makutano ya Barabara ya Welsing na Bulsberg, hapohapo ukasikika mlio mmoja mkubwa, gari alilopanda Tatiana ambalo lilikuwa katikati ya magari hayo yaliyosimama kwenye mataa, likaanza kubimbilika, watu walioshuhudia tukio lile, wakashika vichwa vyao, vilio vikasikika, kila mtu akabaki ameduwaa, gari alilokuwa amepanda Tatiana, lilikuwa nyang’anyang’a.

      “Tatiana.....” alijikuta akiita Buffet, hapohapo akateremka kutoka garini na kuanza kukimbia kule lilipokuwa gari lile alilokuwa Tatiana.



      Ilikuwa ni ajali mbaya mno, gari lile alilokuwa Tatiana lilirushwa kutoka lilipokuwa na kubimbirika kwenda upande mwingine, kila mtu aliyeiona ajali ile, alihuzunika kwani kwa muonekano tu, hakukuwa na mtu yeyote aliyehisi kama kuna mtu alikuwa mzima ndani ya lile gari.

      Damu zilitapakaa sehemu yote hiyo, ajali ile ambayo ilionekana ni ya kizembe ikaanza kulaumiwa na kila mtu. Ilikuwaje gari ligongwe wakati lipo katika mataa tayari kwa kuvuka? Dereva aliyeligonga gari lile alikuwa na utaalamu gani wa kuhama kutoka barabara nyingine na kuhamia barabara ile na kuligonga? Kila swali lililoulizwa, hakukuwa na mtu mwenye jibu sahihi.

      “Tatiana....” aliita Buffet, alikuwa amefika katika gari lile, alijaribu kuchungulia ndani, damu zilianza kuchurizika kutokea ndani ya gari lile kitu kilichomshtua sana Buffet.

      Watu wengine waliokuwa katika magari mengine ambao walikuwa kwenye msafara ule wakateremka na kuelekea kule kulipokuwa na gari lile kisha kuanza kusaidia kufungua milango kwa ajili ya kuwatoa majeruhi wale.

      “Mlango haufunguki,” alisema jamaa mmoja.

      “Vunja kioo,” alisema jamaa mwingine.

      Hakukuwa na cha kufanya zaidi ya kuvunja vioo vya gari lile kisha kuwatoa majeruhi. Vazi alilokuwa amelivaa Tatiana, kwa kuliangalia tu, usingeweza kugundua kama lilikuwa jeupe kwani lilitapakaa damu kila sehemu.

      Walichokifanya ni kuwatoa majeruhi hao na kisha kuwaingiza kwenye magari mengine na kuanza kuwapeleka katika Hospitali ya Helios Klinikum Berlin-Buch iliyokuwa umbali wa kilometa moja kutoka hapo walipokuwa.

      Ndani ya gari, Buffet alikuwa pembeni ya Tatiana, alikuwa akilia tu kwani kile kilichokuwa kimetokea, kilimuumiza moyo wake. Hakujua afanye nini, alibaki akilia tu kwani kila kitu kilichokuwa kimetokea, alikifahamu na hata mtu aliyepanga ajali ile alimfahamu sana, alikuwa mpenzi wake, Nikola.

      Japokuwa Tatiana alikuwa hoi na hakuweza hata kutingisha kiungo chochote kile, lakini bado Buffet alikuwa na mapenzi ya dhati kwa msichana Nikola ingawa kile kilichokuwa kimetokea hakukipenda kabisa.

      Hawakuchukua muda mrefu wakafika katika hospitali hiyo ambapo manesi waliokuwa nje wakaleta machela na kisha miili ya majeruhi wale kuchukuliwa na kuanza kupelekwa ndani. Buffet hakunyamaza, aliendelea kulia huku akimtaka Tatiana aamke kitandani pale lakini hakuweza kufanya hivyo, aliumizwa vibaya na alikuwa amepoteza fahamu.

      “Subirini hapa,” alisema nesi mmoja, walikuwa nje ya mlango ulioandikwa Theatre (chumba cha upasuaji).

      “Nataka niwe naye karibu dokta.”

      “Hapana! Subirini hapa.”

      Hawakuwa na jinsi, kwa sababu waliambiwa wasubiri, wakafanya hivyo. Wakakaa kwenye kiti, Buffet alikuwa akibubujikwa na machozi tu, kile kilichokuwa kimetokea kilimuumiza moyo wake, hakutaka kumkumbuka tena Nikola japokuwa alimpenda sana msichana huyo.

      Hapo ndipo alipoanza kujuta kwamba ni bora angemkataa msichana huyo mapema na kuwa na Nikola ili kile kilichokuwa kimetokea kisingetokea, ila huo haukuwa muda wa majuto, ulikuwa ni muda wa kufikiria nini kilitakiwa kufanyika baada ya hapo.

      Walikaa pale kwa zaidi ya masaa matatu, hakukuwa na mtu yeyote aliyezungumza nao zaidi ya madaktari kuingia na kutoka kwa kupishana tu. Kila mmoja alionekana kuwa bize kwani kile kilichokuwa kimetokea kiliwatia presha hata wao wenyewe.

      Vyombo vya habari havikuwa mbali, mara baada ya kusikia kwamba kulikuwa na ajali mbaya iliyokuwa imetokea, kwa haraka wakaanza kuelekea katika hospitali hiyo ili kupata uhakika juu ya kile kilichokuwa kimetokea.

      Watu wakazidi kuogopa, walijua fika kwamba ajali ile ilikuwa ni ya kupanga kutokana na jinsi ilivyokuwa imetokea, ila mpaka katika kipindi hicho, hawakujua ni nani alikuwa nyuma ya kile kilichokuwa kimetokea.

      Watu wakaanza kukusanyika katika hospitali hiyo, walionekana kuchanganyikiwa mno, matukio kadhaa ya nyuma yaliyomtokea mwanamuziki Tatiana, na lile lililokuwa limetokea, yaliwahuzunisha sana kwani hawakuamini kama kungekuwa na mtu aliyekuwa akitafutwa na kifo namna ile.

      Masaa matano yalipita, hawakupokea taarifa zozote kutoka ndani ya kile chumba zaidi ya madaktari kupishana kwa zamu tu. Wengine wakashindwa kuvumilia zaidi, wakainuka na kuondoka kwa ahadi kwamba wangerudi hospitalini hapo baadaye.

      Ingawa wote waliondoka lakini Buffet hakutaka kuondoka, alikuwa hospitalini pale, alikalia kiti huku akiwa amejiinamia chini, machozi hayakukauka, kila alipokuwa akimkumbuka Tatiana, aliendelea kulia.

      “Samahani!” aliisikia sauti ya mtu mmoja, alipouinua uso wake, alikuwa daktari.

      “Ndiyo dokta!”

      “Pole kwa kilichotokea!”

      “Asante sana. Niambie nini kinaendelea ndani.”

      “Tumejitahidi sana.....”

      “Lakini amefariki?”

      “Hapana! Bado anapumua, ila kwa kutumia msaada wa mashine,” alijibu dokta yule.

      “Atapona?”

      “Tuna uhakika huo.”

      Majibu ya daktari yule yalimridhisha lakini hakutaka kuyaamini kwa asilimia mia moja kwamba Tatiana ataweza kupona kwani kwa jinsi alivyokuwa amemuona, aliumizwa vibaya mno kichwani.

      Hakuwa na jinsi, kwa sababu yeye ndiye aliyesema kwamba mpenzi wake angepona, hakuwa na jinsi zaidi ya kusubiri na kuona kile ambacho kingeendelea. Ilipofika saa kumi na moja alfajiri, Buffet hakuweza kuendelea kukaa hospitalini hapo, alichokifanya ni kurudi hotelini kupumzika kwani usiku mzima hakuwa amelala.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      Alipofika hotelini, akaingia chumbani kwake na kujilaza. Wala hazikupita dakika nyingi, akaona simu yake ikiita, alipokiangalia kioo cha simu ile na kuona jina la Nikola, akajikuta akiiweka simu ile pembeni.

      Mapenzi mapenzi tu, kichwa chake kikaanza kumfikiria Nikola pia, hakuweza kuuzia moyo wake kuacha kumfikiria msichana huyo kwani bado aliuteka mno moyo wake, akajikuta akiiangalia simu yake na kisha kuichukua. Kwa kuwa simu ilikuwa imekwishakata, akaamua kupiga yeye.

      “Unasemaje?” aliuliza Buffet hata kabla ya salamu.

      “Nini kinafuata?” ilisikika sauti ya Nikola ikiuliza swali.

      “Kuhusu nini?”

      “Kwani tulipanga nini? Au bado unampenda?” aliuliza Nikola kwa sauti ya kiburi.

      “Hapana! Ulichokifanya sijakipenda, ni bora ungeacha niachane naye kwa usalama,” alisema Buffet.

      “Nimekupa masaa mangapi ufanye hivyo? Mbona hukufanya maamuzi?”

      “Hata kama Nikola, vitu vingine si vya kufanya harakaharaka.”

      “Sasa ninataka uniambie, nini kinafuata!”

      “Nikola, naomba muda.”

      “Muda zaidi! Wa nini?”

      “Kwanza apone.”

      “Haiwezekani Buffet! Yaani hapo haiwezekani kabisa. Hebu niambie kwanza nijue, unanipenda?”

      “Nakupenda lakini.....”

      “Lakini nini?”

      “Ngoja ap...” alisema Buffet lakin hata kabla hajamaliza sentensi yake, Nikola akakata simu.

      Buffet akachanganyikiwa, kitendo cha kukatiwa simu kikamfanya kufikiri kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa kuwasiliana na msichana huyo. Hakutaka kumuacha, hakutaka kuona akiondoka zake, alikuwa akimuhitaji mno hivyo alichokifanya ni kumpigia simu, mbaya zaidi, simu ilikuwa ikiita pasipo kupokelewa kitu kilichozidi kumchanganya na kumuumiza moyo wake.

      “Pokea simu Nikola,” alisema Buffet huku akiwa na presha kubwa, simu haikupokelewa, iliendelea kuita na hata alipojaribu baadae, haikuwa hewani, ilizimwa jambo lililomchanganya sana Buffet.

      Watu hawakuamini kile kilichokuwa kimetokea, kila mtu aliyesikia kuhusu ajali aliyokuwa ameipata Tatiana, alisikitika mno kwani kulionekana kuwa na mpango kabambe wa watu fulani waliotaka kumuua msichana huyo.

      Maandamano yakaanza kufanyika shemu mbalimbali duniani, watu wakaingia barabarani na kushika mabango na kulaani juu ya kile kilichokuwa kikiendelea kwamba wahusika walitakiwa kuacha kwani kile alichokuwa akikifanya Tatiana kilikuwa ni kipaji chake na hakutakiwa kushambuliwa.

      Maandamano yale yakawasukuma viongozi mbalimbali wa serikali ya Tanzania na Marekani, wakawasiliana na hapo ndipo walipoanza kufanya upelelezi wa chini kwa chini kwa kutumia shirika la upelelezi la CIA kwa nchini Marekani na Interpool kwa ajili ya kuhakikisha mtu aliyefanya hilo anajulikana haraka iwezekanavyo.

      Kitu cha kwanza kabisa, wapelelezi kutoka nchini Marekani wakasafiri mpaka nchini Tanzania, huko, walikuwa wakienda kufuatilia kile walichokuwa wakihitaji kukifahamu juu ya Tatiana kwani walikuwa na wasiwasi kwamba inawezekana chimbuko la mambo hayo yote lilianzia nchini Tanzania.

      Walipofika huko, kitu cha kwanza kilikuwa ni kuonana na wazazi wake, wakazungumza nao kisha kuwauliza maswali kadhaa kuhusu Tatiana. Mzee Sangiwa na mkewe walikuwa kwenye maumivu makali na hapo walikuwa wakijiandaa kwa ajili ya kuelekea nchini Ujerumani.

      “Taarifa zinasema kwamba Tatiana alikuwa kipofu tangu alipozaliwa, kweli?” aliuliza mpelelezi mmoja, kutokana na kuwa wa kimataifa, hata lugha ya Kiswahili haikuwasumbua, walikuwa wakizungumza zaidi ya lugha saba, tena kwa ufasaha.

      “Ndiyo!”

      “Unamfahamu mtu wa kwanza kuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi?” aliuliza Kim.

      “Ndiyo! Alikuwa mchungaji Peter Lazaro.”

      “Sawa. Hakuna tatizo,” alisema Kim na kisha yeye na wenzake kuondoka mahali hapo pasipo kuuliza huyo Peter alikuwa nani na aliishi wapi.

      Walikuwa na kila kitu mikononi mwao, walichokuwa wakikihitaji ni mahali watu hao walipokuwa. Walifuatilia kwa kipindi kichache na wakagundua kwamba Peter ndiye alikuwa mpenzi wa kwanza wa Tatiana.

      Umakini wao wa kutafuta wahusika, pia walifanikiwa kuingia katika simu ya Tatiana na kuangalia mawasiliano yake kwa ujumla, tangu siku ya kwanza alipoanza kutumia simu mpaka siku hiyo.

      Mbali na hiyo, pia walipitia mawasiliano yake na barua pepe, kulikuwa na watu wengi waliokuwa na wasiwasi nao, ila kubwa zaidi Peter. Wakaondoka Shinyanga na kuelekea Mwanza ambapo huko wakakutana na mwinjilisti Peter na kuanza kuzungumza naye.

      “Unamfahamu Tatiana?”

      “Ndiyo! Nyie ni wakina nani?”

      “Usijali, sisi ni watu tunaofanya naye muziki.”

      “Sawa!”

      “Unafahamu nini kuhusu yeye?”

      “Ni mwanamuziki.”

      “Alikwishawahi kuwa mpenzi wako?”

      “Ndiyo! Ila aliniacha.”

      “Kwa nini?”

      “Sijajua, ila nahisi kwa sababu alimpata mwanaume mwingine,” alisema Peter.

      “Ulijisikiaje ulipoachwa, ulikasirika?”

      “Ndiyo lakini kila kitu kimepita.”

      “Ulisoma wapi ulipofikia elimu ya chuo?”

      “Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.”

      “Mwaka gani?”

      Yalikuwa ni maswali mfululizo, watu wale waliokuwa mbele yake walionekana kuwa makini mno, wakati akiulizwa maswali na Kim, mpelelezi mwingine alikuwa bize na simu yake. Mwingine alikuwa wakimwangalia kwa umakini machoni.

      Pembeni yao, kama umbali wa hatua thelathini walilisimamisha gari lao lililokuwa na vioo vilivyowekwa tinted nzito. Ndani ya gari lile, kulikuwa na watu ambao kazi yao ilikuwa ni kucheza na sura tu.

      Walikuwa na kamera zenye uwezo mkubwa, walikuwa wakiurekodi uso wa Peter huku wakiwa na picha kadhaa zilizokuwa zikionyesha sura zilizokuwa na muonekano tofautitofauti hali iliyowafanya kugundua mwanaume huyo alikuwa akifikiria vipi.

      “Anaonekanaje?”

      “Sura yake inafanana na hii hapa,” alisema mpelelezi mmoja garini huku akiionyesha sura fulani kwenye kompyuta.

      “Na picha hiyo inasemaje?”

      “Mtu mwenye huzuni, aliyeumizwa, nahisi kuna kitu,” alisema jamaa huyo.

      “Kingine?”

      “Wakati mwingine sura yake inafanana na hii hapa.”

      “Inasemaje?”

      “Mtu mwenye hasira.”

      Wapelelezi walitumia zaidi sura kusoma hisia za mtu alizokuwa nazo moyoni mwake, waliamini kwamba kama mtu angeweza ishara fulani usoni mwake, ilimaanisha kitu fulani, hivyo ndivyo ilivyokuwa.

      Katika aina ya sura alizokuwa akiziweka Peter zilionyesha ni jinsi gani aliumia alipokuwa ameulizwa kuhusu Tatiana na ni kwa jinsi gani alikuwa na hasira. Wapelelezi wale aliokuwa akizungumza nao hawakutaka kukaa sana mahali hapo, wakaaga na kuondoka.

      Hawakusihia hapo, bado walitaka kufahamu mengi kuhusu muinjilisti Peter hivyo walichokifanya ni kuanza kuangalia fedha zilizokuwa kwenye akaunti yake. Zilikuwa fedha ndogo sana ambazo waliamini asingeweza kufanya harakati za kummaliza Tatiana kwa kumlipua na bomu au hata kusababisha ajali.

      “Turudini Marekani,” hilo ndilo walilolifanya, wakarudi zao nchini humo pasipo kugundua kwamba mtu huyo ndiye aliyehusika katika kumchoma kisu Tatiana, ila kwa kuwa walikwenda kwa ajili ya kupeleleza juu ya ajali hiyo, hawakutaka kujali sana.

      Wapelelezi wengine waliendelea na zoezi lao nchini Marekani kuona ni nani hasa alikuwa nyuma ya kila kitu. Walichokuwa wakikifanya ni kuchukua simu ya Tatiana na kuangalia mawasiliano yake aliyokuwa akifanya na watu wengine tangu mwaka huo uingie, hawakuwafanikiwa kuona kitu chochote kile, walijaribu hata kuangalia mtiririko wa meseji, kote huko hawakugundua kitu.

      Hawakuishia hapo, walichohisi ni kwamba inawezekana akawa anawasiliana na mtu kupitia barua pepe lakini napo huko hawakuambulia kitu chochote ambacho kingeweza kuwasaidia, wakaendelea kuvisumbua vichwa vyao.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      “Tufanye nini?” aliuliza mmoja wa wapelelezi.

      “Na vipi kuhusu mpenzi wake?”

      “Nani? Buffet?”

      “Ndiyo!”

      “Mmh! Sidhani!”

      “Tujaribu.”

      Hawakuwa na jinsi, walikuwa kwenye wakati mgumu kuliko nyakati zote, walitaka kuhakikisha kwamba kila kitu walichotakiwa kukifanya walikifanya. Wakaanza kurudi tena katika chumba cha mitambo, kulikuwa na wafanyakazi wengi lakini kila mmoja alikuwa bize na mambo yake.

      Wakaanza kupiga hatua kumfuata kijana mmoja ambaye alionekana kuwa na miaka ishirini lakini alikuwa balaa katika suala zima la kompyuta na network. Huyo ndiye aliyekuwa akihakikisha kila kitu kinafanyika kama kinavyotakiwa.

      Walipomwambia jukumu alilotaka kulifanya kwa kipindi hicho, hakuwa na jinsi, akaiwasha kompyuta yake na kisha kuanza kufanya utaalamu wake, mara akaingia katika barua pepe ya Buffet na kuanza kuangalia kila kitu.

      Walipekua na kupekua, walitazama barua pepe zilizoingia, zilizotoka na zile zilizohifadhiwa, hawakuishia hapo, waliangalia mpaka katika mafolda yake lakini kote huko hawakuambulia kitu cha kuweza kuwasaidia.

      “Twende simuni, namba yake hii hapa,” alisema mpelelezi mmoja na kisha kuanza kuangalia humo simuni.

      Mtu wa kwanza kabisa kuona akiwasiliana naye, yaani simu yake kumpigia na hata kupigiwa alijulikana kwa jina la Nikola, walijaribu kuangalia mahali msichana huyo alipokuwa akiishi, wakajua ni Ujerumani ndani ya Jiji Munich, ila katika kipindi hicho alikuwa ndani ya Jiji la Berlin, hivyo ndivyo kompyuta yao ilivyoonyesha.

      “Hebu fuatilia na meseji zote zilizokuwa zikienda kwa huyu binti, kisha ingia na kusikiliza mawasiliano yao kwa njia ya sauti,” alisema mpelelezi mmoja na kisha kuanza kufanya kama alivyoambiwa.

      Walichokiona, kikawapa uhakika kwamba binti huyo alikuwa nyumba ya kila kitu. Kwanza wakaanza kuziona meseji zilizoonyesha kwamba alikuwa akilitaka penzi kutoka kwa mwanaume huyo, hawakuishia hapo, walizikuta mpaka meseji zilizokuwa zikisisitiza Buffet afanye jambo fulani la kumuacha Tatiana lakini hakutaka kukubali kulifanya kwa haraka mno.

      Waliendelea mpaka meseji zilipokwisha, hivyo wakaona kulikuwa na umuhimu wa kusikiliza mazungumzo yao. Wakafanya hivyo, watu hao hawakuwa wamezungumza sana zaidi ya kutumiana meseji, simu ya mwisho kabisa kuzungumza ilikuwa ni siku ya tukio la ajali lilipotokea ambapo Buffet alikuwa akilalamika juu ya kile kilichokuwa kimetokea.

      “Unasemaje?”

      “Nini kinafuata?”

      “Kuhusu nini?”

      “Kwani tulipanga nini? Au bado unampenda?”

      “Hapana! Ulichokifanya sijakipenda, ni bora ungeacha niachane naye kwa usalama.”

      “Nimekupa masaa mangapi ufanye hivyo? Mbona hukufanya?”

      “Hata kama Nikola, vitu vingine si vya kufanya harakaharaka.”

      “Sasa ninataka uniambie, nini kinafuata!”

      “Nikola, naomba muda.”

      “Muda zaidi! Wa nini?”

      “Kwanza apone.”

      “Haiwezekani Buffet! Yaani hapo haiwezekani kabisa. Hebu niambie kwanza nijue, unanipenda?”

      “Nakupenda lakini.....”

      “Lakini nini?”

      “Ngoja ap...”

      Waliyasikiliza mazungumzo hayo, hawakutaka kujifikiria, hawakutaka kujiuliza, wakajua moja kwa moja kwamba msichana huyo na Buffet ndiye waliyekuwa wamesababisha ajali hiyo! Mjadala ukafungwa.

      “Ni lazima tuwasiliane na polisi wa Ujerumani kuwakamata watu hawa wakati upelelezi zaidi ukiendelea,” alisema mpelelezi mmoja na hapohapo kuwaambia wapelelezi wengi akiwemo kiongozi wao juu ya mchakato mzima walivyokuwa wameuendesha na mwisho wa siku kuwakamata watu waliokuwa wakiwahitaji.



      Buffet hakutaka kutoa simu sikioni, alikuwa akisikilizia ili mpenzi wake aipokee na hatimaye kuzungumza naye. Nikola hakupokea simu ile kitu kilichomfanya kujisikia vibaya mno kwani kitu pekee alichokuwa akikitaka ni kuzungumza naye tu.

      Alichokifanya ni kutoka chumbani kwake kwa lengo la kwenda chumbani kwa msichana huyo ili aongee naye, alipofika mlangoni, akajaribu kuufungua mlango, ukawa umefungwa kwa ndani, akaanza kugonga hodi.

      “Nani?” ilisikika sauti ya Nikola kutoka ndani.

      “Buffet.”

      “Nikusaidie nini?”

      “Naomba nizungumze nawe mara moja.”

      “Uzungumze nami kuhusu nini?”

      “Naomba ufungue mpenzi.”

      Hakukaa sana mlangoni, mlango ukafunguliwa na Nikola kusimama mlangoni. Alionekana kukasirika, uso alikunja ndita, kwa jinsi alivyoonekana, hakuonekana kuwa na furaha hata mara moja jambo lililomfanya Buffet kukosa raha.

      “Naomba unisamehe!”

      “Nikusamehe umefanya nini?” aliuliza Nikola.

      “Naomba unisamehe! Nipo tayari kumuacha akiwa kitandani ili niwe nawe,” alisema Buffet huku akimaanisha alichokisema.

      Mpaka kufikia kutoa kauli hiyo, Buffet akakaribishwa ndani na kukalishwa kitandani. Kila alipokuwa akimwangalia Nikola, alikuwa msichana mrembo, mwenye sifa za kuwa mwanamke mzuri duniani.

      Japokuwa Tatiana alikuwa mrembo kuliko Nikola lakini kwake msichana huyo alionekana kuwa kila kitu. Buffet alibaki akimeza mate ya tamaa mara baada ya kuuona upaja wa Nikola ambao ulifichwafichwa na nguo ya kulalia ambayo kwa chini ilikuwa na mauamaua fulani.

      “Unamaanisha unachokisema?” aliuliza Nikola, Buffet akayatoa macho yake upajani mwa Nikola na kumwangalia usoni.

      “Ndiyo! Ila naomba unipe nafasi moja tu, kisha baada ya hapo, tutaelekea Munich kuanza maisha yetu,” alisema Buffet.

      “Nafasi gani?”

      “Nataka nirudi hospitalini nikamuage Tatiana, japo kwa kumbusu tu,” alisema Buffet.

      “Nikupe dakika ngapi mpaka kurudi?” aliuliza Nikola.

      “Saa moja.”

      “Sawa. Unaweza kwenda, ukipitiliza, tusijuane,” alisema Nikola.

      “Hakuna tatizo.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      Hilo ndilo aliloliomba na kuruhusiwa, alichokifanya ni kuondoka hotelini hapo na kurudi hospitalini. Japokuwa alikuwa ameumia sana lakini hakuwa na la kufanya, ili kuwa na msichana Nikola ilitakiwa amuache Tatiana.

      Alijua fika kwamba Tatiana alikuwa msichana mrembo hasa zaidi ya Nikola lakini hakujua kwa nini alimpenda sana Nikola, hakuwa na jinsi, kila kitu alichokuwa akikfanya mahali hapo ni kumfurahisha Nikola na mwisho wa siku kuwa naye tu.

      Hakuangalia dunia ingesema nini, hakuangalia watu wangemuonaje, kitu pekee alichokuwa akikihitaji mahali hapo ni kuwa na Nikola tu, hivyo alitakiwa kufanya kile alichokuwa akikihitaji msichana huyo wa Kijerumani.

      Hospitalini kulikuwa na idadi kubwa ya watu, wote hao walifika hospitalini hapo kwa ajili ya kumuona mwanamuziki huyo. Kulikuwa na usumbufu mkubwa kwani kila mtu aliyeambiwa aondoke, hakuondoka, alitaka kumuona Tatiana tu.

      Kama ni fujo, zilikwishatokea mahali hapo, watu waligoma kabisa, ila kwa kuwa ilikuwa ni hospitalini, polisi hawakufanya kitu zaidi ya kukubaliana na watu hao tu, kusimama nje ya hospitali hiyo, ila kuingia ndani, hakuna aliyeruhisiwa.

      Mara baada ya kufika hapo, Buffet akaanza kuufuata mlango, polisi wote walimfahamu, hawakumzuia, wakampa ruhusa ya kuingia ndani ya jengo hilo. Wakati akipiga hatua kuelekea katika chumba alicholazwa Tatiana, machozi yalikuwa yakimbubujika tu, hakuamini kama hiyo ndiyo ingekuwa siku ya mwisho kumuona msichana huyo.

      Alipofika, akaambiwa asubiri nje kwani ndiyo kwanza mgonjwa alikuwa akiandaliwa mara baada ya kutolewa kutoka katika chumba cha upasuaji, hilo halikuwa tatizo, alichokifanya ni kusubiri huku muda wote macho yake yakiwa kwenye saa yake tu, alikumbuka vilivyo kwamba alipewa saa moja tu.

      Baada ya dakika ishirini, daktari akamruhusu kuingia ndani, akaanza kupiga hatua kuelekea katika kitanda alicholala Tatiana, alipomuona tu, jinsi uzuri aliokuwa nao, alijikuta akimpenda zaidi msichana huyo.

      Mawazo juu ya Nikola yakapotea kwa muda, mapenzi yake akahisi yakianza kurudi tena, alimwangalia namna alivyokuwa kimya kitandani pale, moyo wake ulimuuma mno, binti mrembo, alikuwa akipumulia mashine ya oksijeni huku akiwa na bandeji kubwa kichwani mwake.

      “Tatiana! Amka mpenzi!” alisema Buffet kwa sauti ya chini huku akimwangalia Tatiana kitandani pale na kisha kumbusu shavuni.

      Moyo wake uliumia mno ila hakuwa na cha kufanya, kwa muonekano wa harakaharaka kitandani pale, Tatiana alionekana kutokuwa na dalili za kuamka leo wala kesho. Huku akibubujikwa na machoz mashavuni mwake, ghafla akahisi simu yake ikianza kutetemeka mfukoni mwake, alichokifanya, ni kuitoa simu ile na kuangalia mpigaji, alikuwa Nikola.

      “Muda unayoyoma,” ilisikika sauti ya msichana huyo simuni.

      “Nakuja, nakuja mpenzi,” alisema Buffet.

      Mapenzi makubwa aliyokuwa nayo kwa Nikola, akajikuta akiondoka chumbani hapo ili aweze kumuwahi hotelini. Ni kweli alimpenda Tatiana lakini mapenzi ya Nikola yaliusisimua moyo wake mno.

      Alipofika hotelini, akaungana na Nikola na hatimaye kuanza safari siku hiyohiyo kuelekea jijini Munich. Kuwa na msichana huyo kulimpa faraja moyoni mwake, hakutaka tena kukumbuka kuhusu Tatiana aliyekuwa hospitalini huku amepoteza fahamu kutokana na ajali mbaya ya gari iliyotokea.

      Walitumia masaa mawili kwa usafiri wa treni mpaka kuingia jijini Munich ambapo hapo walitegemea kuanza maisha yao mapya. Maisha yalikuwa ni ya furaha tele, Buffet hakutaka kukumbuka chochote kile kuhusu Tatiana, kwake, alimchukulia kama msichana wa kupita ambaye kwa kipindi hicho aliamua kuishi na Nikola tu.

      Maisha yao yakafana jijini Munich, msichana Tatiana akasahaulika kichwani mwake, hakuwepo moyoni, aliyekuwa akimfikiria kwa wakati huo alikuwa Nikola tu ambaye alikuwa kwenye mapenzi ya dhati huku wakianza kuweka mikakati ya kuanza kuishi pamoja kama mume na mke, kwa kifupi ni kwamba walitaka kufunga ndoa, mpaka mwezi mmoja unakatika, walikuwa kama pete na kidole.

      *****

      Tatiana alikuwa kwenye hali mbaya, pale kitandani hakupata nafuu hata mara moja, siku zilikatika na bado hali yake ilizidi kuwa mbaya kiasi kwamba madaktari wakaogopa mno kwa kuona muda wowote ule mwanamuziki huyo angeweza kufariki dunia.

      Dunia nzima ilikuwa kimya, ilikuwa ikisikilizia kile kilichokuwa kikiendelea kule Ujerumani, wengi walishauri kwamba ingekuwa vizuri kama Tatiana angechukuliwa na kupelekwa katika moja ya hospitali nchini Marekani lakini madaktari hawakutaka kutoa ruhusa hiyo kutokana na hali yake mbaya aliyokuwa nayo.

      Siku zikakatika, madaktari wakashangaa, hawakuelewa mpenzi wake na Tatiana alikuwa mahali gani kwani tayari wiki nzima ilikuwa imepita lakini mwanaume huyo hakurudi tena hospitalini. Jambo hilo lilizua maswali mengi yasiyokuwa na majibu.

      Taarifa juu ya kutokuwepo kwa Buffet hospitalini zikaanza kutolewa, watu walishangaa, hawakujua alipokuwa mwanaume huyo na sababu gani iliyomfanya kumkimbia msichana huyo mrembo katika kipindi alichokuwa hoi hospitalini.

      Watu wakahofia kwamba inawezekana Buffet akawa ametekwa na kuuawa na mwili wake kutupwa sehemu lakini mawazo hayo yakafutika kwani polisi nao walikuwa makini kufuatilia lakini hawakuambulia chochote kile.

      “Where is this buddy?” (Mshikaji yupo wapi?) aliuliza jamaa mmoja, alikuwa ameshika Gazeti la New York Times la nchini Marekani, lilitoa taarifa kuhusiana na kutoweka kwa Buffet hospitalini.

      “I don’t know, maybe he has been kidnapped,” (Sijui, labwa atakuwa ametekwa)

      “Impossible.” (Haiwezekani)

      “Why not?” (Kwa nini isiwezekane?)

      “I don’t know, but it is impossible,” (Sijui lakini haiwezekani)

      Maswali yaliendelea kumiminika juu ya mahali alipokuwa Buffet, hakukuwa na mtu aliyejua ukweli wowote kwamba mwanaume huyo aliamua kumtoroka Tatiana kwa sababu alikutana na msichana wake wa zamani.

      Kilichofanyika ni kupigiwa simu na watu wake wa karibu, simu haikupatikana na hata kazini kwake hakuwepo. Watu walisikitika mno kwani kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele bado hali ya Tatiana ilikuwa tete nchini Ujerumani.

      Wiki ya pili ilipoingia tangu Tatiana afikishwe hapo hospitalini, wazazi wake wakafika kwa ajili ya kumjulia hali. Watu wengine walizuiliwa kuingia katika chumba alicholazwa msichana huyo ila wao wakaruhusiwa kwa kibali maalumu na kuingia.

      Walichokiona mbele yao, kiliwasikitisha mno, Tatiana alikuwa kimya kitandani, alikuwa akipumulia mashine ya oksijeni, alikuwa hoi na hakukuwa na dalili zozote kama kuna siku angeweza kuinuka kitandani pale.

      Wazazi wake wakajikuta wakibubujikwa na machozi, walimsogela na kisha kuanza kumwangalia, mioyo yao iliwauma mno, hakukuwa na picha mbaya ambayo waliiona katika maisha yao kama ile iliyomuonyesha Tatiana kitandani huku akiwa hajitambui kabisa.

      “Hii ni laana,” alisema mzee Sangiwa huku akionekana kuwa na majonzi mno.

      “Laana?”

      “Ndiyo! Haya yote ni kwa sababu ya Peter,” alisema mzee Sangiwa.

      “Usiseme hivyo mume wangu!”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      “Huu ndiyo ukweli. Tangu amuache Peter, amekuwa kwenye misukosuko mikubwa, huyu ni Peter, mke wangu, kuna kila sababu ya kumuomba msamaha Peter,” alisema mzee Sangiwa huku akiyafuta machozi yaliyokuwa yakimbubujika mashavuni.

      Hicho ndicho alichohisi mzee Sangiwa, kila alipokuwa akimwangalia Tatiana kitandani pale alisikia sauti moyoni mwake ikimwambia kwamba kile kilichokuwa kikiendelea kutokea katika maisha ya binti yake kilikuwa ni laana.

      Walilia na kulia lakini machozi yao hayakubadilisha kitu chochote kile, bado msichana yule aliendelea kulala kitandani pale huku akiwa hajitambui kabisa.

      Siku zikakatika na wiki ya tatu kuingia, mzee Sangiwa hakutaka kukaa nchini Ujerumani, alichokifanya ni kufanya kila liwezekanalo arudi Tanzania ili atakapokwenda huko arudi na Peter ambaye aliamini kwamba ni laana yake ndiyo iliyomuweka msichana huyo kitandani kwa muda mrefu.

      “Hapana! Hautakiwi kwenda, huwezi kuniacha peke yangu, ni bora aje yeye,” alisema mkewe.

      “Sasa atakuja vipi?”

      “Tuwasiliane na balozi wetu nchini hapa, anaweza kutusaidia,” alishauri mama Tatiana.

      Hicho ndicho walichokifanya, wakawasiliana na balozi na kumwambia kilichokuwa kikiendelea hospitalini, walipewa pole na balozi huyo kuahidi kufika hospitalini hapo siku inayofuatia, hivyo hawakumwambia kile walichotaka kumwambia.

      Siku iliyofuata, majira ya saa nne asubuhi balozi huyo alikuwa hospitalini hapo, akawapa pole kwa kile kilichokuwa kikitokea na kuwaahidi kwamba kila kitu kingekuwa salama, hivyo alihitaji muda wa kulishughulikia suala la msichana huyo hospitalini hapo.

      “Ila kuna jingine,” alisema mzee Sangiwa.

      “Lipi hilo?”

      “Kuna mtu tunataka aje huku kumuona Tatiana.”

      “Nani?”

      “Peter!”

      “Ndiye nani?”

      Hawakuwa na jinsi, kutokana na kile kilichokuwa kikiendelea, wakaamua kumhadithia kila kitu kilichokuwa kimetokea kipindi cha nyuma. Ilikuwa stori yenye kuhuzunisha mno, balozi yule na familia yake walipoisikia, walibaki wakihuzunika tu kwani mambo yaliyokuwa yametokea, hata naye ikaanza kumuingia akilini kwamba inawezekana ile kuwa laana kutokana na kile kilichokuwa kimetokea.

      “Nitahakikisha kijana huyo anafika nchini Ujerumani, msijali, nitashughulikia,” alisema balozi yule.





      Watu walizidi kuponywa magonjwa yao, huduma aliyokuwa akiifanya Peter ilionyesha ni kiasi gani muinjilisti huyo alivyokuwa na upako mkubwa. Wachawi walibadilisha maisha yao na kumuabudu Mungu, waliokuwa wazinzi, wakaacha njia zao na kumfuata Mungu.

      Kila kitu kilichokuwa kikiendelea katika mikutano mbalimbali ya Injili ilionyesha ni kwa jinsi gani Mungu alikuwa akitenda miujiza kutokana na huduma aliyokuwa nayo muinjilizisti Peter.

      Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake ya kila siku, aliendelea kumtumikia Mungu, aliyabadilisha maisha yake na katika kipindi hicho, mke wake, Lydia alikuwa mjauzito.

      Huo ulikuwa mkutano wake wa pili ndani ya mwaka mmoja, Uwanja wa Nyamagana mkoani Mwanza ulijaza watu wengi waliohitaji ukombozi katika maisha yao. Kila siku Peter alikuwa mtu wa kukaa chumbani mwake na kuanza kuomba, hiyo ndiyo ilikuwa siri kubwa ya yale yaliyokuwa yakifanyika, hakujinyakulia utukufu, kila kitu alimuachia Mungu kwa kuamini kwamba yeye ndiye aliyekuwa akifanya yote hayo.

      Baada ya siku kadhaa, akapokea wageni kutoka serikalini, walifika nyumbani hapo na kuzungumza naye kwamba alikuwa akihitajika haraka iwezekanavyo nchini Ujerumani. Aliposikia hivyo tu, alijua kwamba hiyo itakuwa ishu ya Tatiana, hakujua ni kitu gani kilichoendelea, ila alichokifanya ni kwenda huko.

      Hakutaka kwenda peke yake, aliongozana na mkewe mpaka nchini Ujerumani ndani ya Jiji la Berlin, hapo, wakaunganisha mpaka hotelini ambapo gharama zote zilikuwa kwa balozi huyo. Hotelini hapo, Peter alikuwa na mawazo mno, alimkumbuka Tatiana, aliyakumbuka yote aliyofanyiwa lakini katika yote hayo, hakuonyesha chuki, yalikuwa yamepita na aliyaacha yawe hivyo.

      “Usifikirie sana mume wangu kuhusu Tatiana!” alisema mkewe.

      “Najua, ni muda mrefu sana, msichana huyu amekuwa kwenye matatizo mengi sana, nahisi Mungu anataka kufanya kitu kwa ajili ya maisha yake,” alisema Peter huku akiifungua Biblia na kuanza kupitia vitabu kadhaa.

      “Hata mimi nakubaliana nawe, cha msingi tukamuone tu, nahisi kuna mengi Mungu atataka kufanya kwa ajili ya maisha yake,” alisema mke wake.

      Siku hiyo walizungumza mengi na kisha kulala. Siku iliyofuata, wakafuatwa na gari kutoka ubalozini ambapo wakachukuliwa na kupelekwa katika hospitali hiyo ambapo baada ya kufika, moja kwa moja wakapelekwa katika chumba alicholazwa Tatiana.

      Japokuwa kulikuwa na watu wengi waliotaka kumuona msichana huyo lakini wao waliruhiswa kutokana na kibali maalumu walichokuwa nacho. Walipofika chumbani humo, macho yao yakatua kwa wazazi wa Tatiana na balozi aliyekuwa na familia yake.

      Wakasalimiana. Peter akaanza kupiga hatua kukifuata kitanda alicholazwa Tatiana. Alipofika, akaanza kumwangalia msichana huyo, hapohapo kumbukumbu za maisha yake ya nyuma aliyopitia na msichana huyo yakaanza kujirudia kama mkanda wa filamu, ghafla machozi yakaanza kujikusanya mashavuni mwake.

      “Tatiana....amka,” alisema Peter huku akimwangalia. Watu wote walikuwa kimya.

      “Peter,” aliita mzee Sangiwa.

      “Ndiyo!”

      “Hii ni laana Peter, yote yametokea baada ya kukuacha wewe,” alisema mzee Sangiwa.

      “Hakuna, nahisi Mungu anataka kuzungumza nami kuhusu yeye. Hebu subiri,” alisema Peter.

      Akayarudisha macho yake kwa Tatiana, akamshika mkono na kuyafumba macho yake. Wote wakabaki kimya, walimwangalia Peter, hawakujua alifanya nini, ila alibaki kimya kabisa. Ghafla, machozi yakaanza kububujika mashavuni mwake, moyo wake ukaumizwa mno.

      Akamwachia mkono Tatiana na kisha kuelekea pembeni, aliisikia sauti ikimwambia kitu, ilimhuzunisha sana, alibaki akilia peke yake kiasi kwamba watu wengine wakaanza kuogopa.

      “Mchungaji, tuambie kuna nini,” alisema mzee Sangiwa.

      “Tatiana atapona,” alisema Peter.

      “Asante Mungu!”

      “Ila...”

      “Kuna kuna nini?”

      “Hatoweza kuona tena,” alisema Peter huku akiyafuta machozi yake, mama Tatiana, bi Frida akaanza kulia kwa sauti kubwa, kile alichoambiwa kwamba binti yake asingeweza kuona tena, kiliuchoma moyo wake.

      ****

      Ilikuwa ni taarifa mbaya lakini walitakiwa kukubaliana nayo, mtu ambaye walimuamini sana, Peter aliwaambia kwamba msichana Tatiana hatoweza kuona tena katika maisha yake yote, ila pale kitandani, angepona kama kawaida.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      Machozi hayakukauka machoni mwa bi Frida, kila alipokuwa akiyakumbuka maneno ya Peter, yaliuumiza mno moyo wake, akawa hana la kufanya. Kila mmoja ndani ya chumba kile alibaki akimwangalia Tatiana aliyekuwa akiteseka kitandani, mioyo yao iliumia sana lakini hawakuwa na jinsi.

      Baada ya kuwa kipofu tangu alipozaliwa, akafanikiwa kupata umaarufu, fedha lakini mwisho wa siku, ajali aliyoipata ilibadilisha maisha yake yote. Kila walipokuwa wakifikiria hilo, mioyo yao ilizidi kuhuzunika.

      “Tatiana....” alisema Peter, kila mmoja akatega sikio kusikia alitaka kuzungumza nini.

      “Amefanyaje?”

      “Hii si laana yangu,”alisema Peter.

      “Kama si laana ni nini?” aliuliza mzee Sangiwa.

      Peter akabaki kimya, akatoka kule pembeni alipokuwa amesimama na kumsogelea Tatiana kitandani pale, tayari machozi yaliyokuwa yakimtoka yalilowanisha shati lake, alipofika karibu na kitanda cha Tatiana, akasimama na kumwangalia msichana huyo usoni.

      “Mungu anataka tujifunze kuhusu Tatiana,” alisema Petr huku akimwangalia msichana huyo.

      “Tujifunze nini?”

      “Tatiana alikuwa mnyenyekevu, Mungu alimpa sauti nzuri, alikuwa na lengo la kuisikia sauti ya msichana huyu ikimuimbia kila siku. Alipopata umaarufu, akajisahau, akajitoa katika suala la kumtumia Mungu na kuanza kumtumikia shetani kwa nyimbo zile za kidunia.

      “Mungu amefanya haya ili tujifunze kwamba unapopata nafasi, Mungu anapoacha neema yake juu yako, kamwe usiichezee. Tatiana alipewa nafasi, akaichezea na ndiyo maana Mungu amemrudisha kule alipokuwa,” alisema Peter huku machozi yaliendelea kumbubujika.

      Vilio vikazidi kusikika ndani ya chumba kile, maneno aliyoongea Peter yalimuumiza kila mmoja, hawakuamini kama kila kitu kilichokuwa kimetokea kilikuwa ni mipango ya Mungu kumrudisha kule alipokuwa kutokana na kuiacha njia yake na kwenda njia nyingine.

      Hali yake iliendelea kuwa mbaya kitandani pale, mpenzi wake, Buffet alikuwa amemtoroka na hakukuwa na mtu yeyote aliyejua mahali alipokuwa. Mateso yote hayo aliyapitia peke yake kitandani.

      Siku ziliendelea kukatika, Peter na mkewe wakarudi nchini Tanzania ambapo mara kwa mara walifanya maombezi kwa ajili ya Tatiana, Mungu amponye na kuwa kama zamani.

      “Koh koh koh!” kilisikika kikohozi kutoka kwa Tatiana.

      Wazazi wake ambao walikuwa pembeni, wakasogea kule alipokuwa, hawakuamini kama binti yao alikuwa amerudiwa na fahamu baada ya kipindi kirefu kupita. Wakamsogelea pale alipokuwa na kisha kumshika mkono.

      “Who are you?” (Wewe ni nani?) aliuliza Tatiana kwa sauti ya chini, alihisi mbele yake kulikuwa na watu.

      “Tatiana binti yangu!”

      “Mama!”

      “Nipo hapa binti yangu,” alisema mama yake huku sauti yake ikisikika kama mtu aliyekuwa na majonzi mno.

      “Nini kimetokea mama! Mbona sioni chochote, madaktari wamenifumba macho?’ aliuliza Tatiana, hakuwa akiona kitu chochote kile zaidi ya giza.

      Bi Frida hakujibu kitu chochote kile, alibaki akilia tu kwani swali alilouliza binti yake lilimhuzunisha mno. Akashindwa kuvumilia kubaki chumbani mule, akatoka na kuelekea nje. Mzee Sangiwa akabaki chumbani mule, alikuwa akibubujikwa na machozi lakini hakutoa sauti yoyote ya kilio kwa kuhofia kwamba angemfanya Tatiana kuwa kwenye wakati mgumu.

      “Tatiana binti yangu!” aliita mzee Sangiwa huku akimshika mkono binti yake.

      “Baba! Kumbe upo hapa! Naomba uniambie, mbona sioni,” aliuliza Tatiana.

      “Sikiliza mwanangu!”

      “Baba niambie kuna nini,” alisema Tatiana lakini hata kabla hajapewa jibu, ghafla mlango ukafunguliwa na daktari mmoja aliyeongozana na nesi kuingia ndani.

      Kitu cha kwanza kabisa wakamtaka mzee Sangiwa atoke chumbani mule kwani walitaka kumfanyia vipimo Tatiana huku nao wenyewe wakimshukuru Mungu kwa muujiza alioufanya kwamba mara baada ya kupita kipindi kirefu, hatimaye msichana huyo alikuwa amefumbua macho.

      Walichokifanya ni kumchoma Tatiana sindano ya usingizi, walitaka wachukue kila kipo wakati yupo usingizini, hawakutaka afahamu kitu chochote kile. Baada ya kumfanyia vipimo hasa kumpeleka katika chumba maalumu, wakampa muda wa kupumzika kisha kuwaita wazazi wake kwa ajili ya kuzungumza nao huku wakiwa na mkalimani ambaye aliifahamu vilivyo lugha ya Kiswahili.

      “Kuna kitu tunataka kuwaambia,” alisema Dk. Berg.

      “Kitu gani?”

      “Kuhusu binti yenu.”

      “Tunajua, ni kwamba hatoona tena.”

      “Mmejuaje?”

      “Tuliambiwa. Ila mnaweza kutuambia tatizo limekuwaje kiutaalamu.”

      “Kuna msuli mmoja mkubwa ambao huwa unawezesha kuyafanya macho haya yawe na nguvu ya kuona, msuli ule unaonyesha kwamba ulirekebishwa baada ya kulegea kwa kipindi kirefu, alipopata ajali, msuli ule umelegea sana kiasi kwamba sisi kama madaktari, kuurudisha kwenye hali yake ya kawaida ni ngumu sana, na kama tukiulazimisha, unaweza kukatika kitu kinachopweza kupelekea kifo chake kwani damu zitatoka na kuelekea ubongoni,” alisema Dk. Berg huku akiwapa karatasi gumu (X-ray) kwa ajili ya kuangalia kile kilichokuwa kimetokea baada ya kupiga picha.

      Taarifa za kuzinduka kwa Tatiana kukaanza kutangazwa kila kona, wazazi wake hawakujua taarifa hizo ziliwafikiaje watu wengine lakini ndani ya masaa matano tu, tayari dunia nzima ilijua kile kilichokuwa kimetokea.

      Watu walitangaza kupitia katika mitandao ya kijamii kama Facebook, Twitter, Instagram na mingine mingi huku vituo vya televisheni na redio vikitumia nafasi hiyohiyo kuwapa watu taarifa juu ya kile kilichokuwa kimetokea likiwemo suala la kutoweza kuona tena.

      “Mungu wangu! Hatoweza kuona tena?” aliuliza mwanamke mmoja, alikuwa ameshika simu na alikuwa akisoma habari mbalimbali kwenye Mtandao wa Kituo cha Televisheni cha BBC.

      “Nani?”

      “Tatiana!”

      “Nani kakudanganya?”

      “Wameandika hapa. Angalia mwenyewe.”

      Zilikuwa taarifa zilizomhuzunisha kila mtu aliyeziona, msichana mrembo ambaye alivuma kwa kipindi kichache na kupata mafanikio makubwa, hatimaye hakuwa na uwezo wa kuona tena, kila aliyezisoma taarifa zile alihuzunika na hata wengine kulia kabisa.

      Tatiana alipopewa taarifa kwamba asingeweza kuona tena, akabaki akilia tu, hakuamini kile alichokuwa ameambiwa lakini kila alipojaribu kufumbua macho yake, yalifumbuka lakini hakukuwa na kitu chochote alichokiona mbele yake zaidi ya giza tu.

      “Mama! Sitoona tena?” alimuuliza mama yake huku machozi yakimbubujika mashavuni.

      “Tatiana....”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      “Mamama niambie...sitoona tena?’ aliuliza tena huku machozi yakiendelea kububujika mashavuni mwake, kile kilichoendelea, hakikumuumiza yeye tu bali hata wazazi wake na watu wengine.

      *****

      Makachero wa CIA wakishirikiana na wale wa Ujerumani wakaanza kazi ya kumtafuta Buffet na Nikola ambao waliamini kwamba walikuwa jijini Berlin kama ambavyo mawasiliano yao ya mwisho yalivyoonyesha.

      Kazi haikuwa ndogo hata mara moja, ilikuwa kubwa na nzito, walijitahidi kuwatafuta jijini hapo tena kwa kugawanyika kimakundi lakini hawakufanikiwa kuwaona kitu kilichowafanya kuhisi kwamba inawezekana watu hao wakawa wameondoka zao nchini humo.

      Hawakukata tamaa, waliamini kwamba kuna siku wangeweza kuwaona watu hao hivyo wakaendelea zaidi kuwatafuta katika kila kona lakini matokeo yakaendelea kuwa yaleyale kwamba watu hao hawakupatikana kabisa.

      “Lakini huyu msichana si anajulikana?”

      “Ndiyo! Tena hiyo ndiyo njia nyepesi, cha msingi tuwasiliane na wazazi wake.”

      Hicho ndicho kilichofanyika, kwa haraka sana wakaanza kuwasiliana na wazazi wa Nikola walioishi ndani ya Jiji la Munich, walitaka kufahamu mahali alipokuwa msichana huyo kwa kipindi hicho.

      Walichokifanya ni kuanza kufuatilia vitu vyake vingi vilivyokuwa vikiendelea. Walichogundua ni kwamba msichana huyo alikuwa akisubiri majibu yake kutoka katika Chuo cha Ludwin Maximilians kilichokuwa hapohapo jijini Munich ili aweze kujiunga nacho kwa masomo ya biashara.

      Mtu ambaye alikwenda nyumbani kwao alikuwa mpelelezi lakini yule aliyejifanya raia wa kawaida, alikwenda kama mhudumu wa posta, kazi yake ilikuwa ni kupeleka vifurushi katika makazi ya watu.

      “Nimekuja kumuona Nikola,” alisema jamaa huyo, alionekana kijana mpole mno, kwa kumwangalia, usingedhani kwamba alikuwa mpelelezi.

      “Hayupo! Alitoka.”

      “Sawa. Kulikuwa na mzigo wake hapa!”

      “Kutoka wapi?”

      “Chuo cha Ludwig Maximilians.”

      “Hebu tuuone.”

      “Hapana! Mpaka awepo ndipo atakabidhiwa kwani anahitajika kusaini pia, akifika, mwambie atupigie simu,” alisema jamaa huyo, hakutaka kuendelea kusubiri, alichokifanya ni kuondoka nyumbani hapo.

      Nikola alipopewa taarifa kuhusu mtu aliyeleta mzigo wake nyumbani kwao, alishtuka sana, alikuwa na hamu kubwa ya kujiunga na chuo hicho kikubwa jijini Munich, alichokifanya ni kutoka hotelini alipokuwa akiponda starehe na Buffet na kisha kuelekea nyumbani haraka sana.

      Simu ikapigwa na hivyo mtu huyohuyo kufika nyumbani hapo huku akiwa na mwenzake, walipomuona msichana Nikola, hawakutaka kufanya kitu chochote kile zaidi ya kumuweka chini ya ulinzi hali iliyomchanganya sana msichana huyo kwani hakujua kosa lake hasa lilikuwa nini.

      “Kuna nini jamani?” aliuliza Nikola huku akionekana kuchanganyikiwa.

      “Wewe twende! Utayajua yote tukifika kituoni.”

      “Naomba niwasiliane na mwanasheria wangu!”

      “Hii si sehemu yake, utawasiliana naye ukiwa kituoni.

      Wakamchukua na kuondoka naye nyumbani hapo. Wazazi wake walishangaa, hawakujua ni kitu gani kilichokuwa kimetokea mpaka binti yao kuchukuliwa na watu waliojitambulisha kwamba ni wapelelezi kutoka CIA.

      Kulionekana kuwa na tatizo kubwa, mpaka mtu kukamatwa na CIA kutoka nchini Marekani, halikuonekana kuwa jambo dogo. Wazazi hao hawakutaka kubaki mahali hapo, walichokifanya nao kuingia ndani ya gari na kuanza kuwafuatilia ili kuona kama kweli walitoka polisi au la.

      “Buffet yupo wapi?”

      “Ninataka kuzungumza na mwanasheria wangu kwanza,” alisema Nikola huku macho yake yakianza kukusanya machozi.

      “Utazungumza naye tu. Tunamtaka Buffet.”

      “Sijui yupo wapi.”

      “Sawa.”

      Walichokifanya ni kuchukua simu yake na kisha kuangalia majina, hasa kwa simu zilizoingia na kutoka, wala hawakuchukua muda wakaliona jina la Buffet ambapo wakaichukua ile namba na kuanza kuangalia kwenye kompyuta yao kwa staili ya kuitraki ili wafahamu mahali alipokuwa mwanaume huyo.

      Simu ikaanza kuonekana, ikaanza kusoma mahali alipokuwa, alikuwa katika Hoteli ya Lion King iliyokuwa pembezoni mwa Jiji la Munich, wakaanza kuelekea huko. Walitaka kuwa na watu hao wote ili watakapokwenda kituoni kusiwe na tatizo lolote lile, au kumtafuta mtu mwingine.

      Walipofika hotelini hapo, wakateremka na kisha kuelekea mapokezini, baada ya kuonyesha vitambulisho vyao, wakaambiwa chumba alichokuwa Buffet na kuelekea huko. Hawakuwa na kazi kubwa, walifanikiwa kazi kwa asilimia mia moja, wakamchukua Buffet ambaye alikuwa akishangaa tu, wakampeleka mpaka garini ambapo huko akakutana na mpenzi wake ambaye alikuwa akilia tu.

      “Nikola! Kuna nini?”

      “Sijui! Wamenichukua tu na kuniambia niwaambie ulipo.”

      “Kwa hiyo ukawaambia?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      “Hapana! Wamechukua simu yangu na kuanza kutraki namba yako,” alisema Nikola huku akiyafuta machozi yake.

      Safari hiyo iliishia kituo cha polisi ambapo wakawekwa ndani na kuambiwa wasubiri. Wote kwa pamoja walikuwa wakishangaa, watu wakiowafuata na kuwakamata hawakuwa polisi wa Ujerumani, walikuwa ni Wamarekani ambapo baadae wakavaa makoti yao makubwa yaliyosomeka CIA mgongoni.

      “Kuna nini? Mbona mmetuleta hapa?” aliuliza Buffet huku akionekana kuwa na hasira, alikuwa ameshasahau kuhusu Tatiana.

      “Mnamfahamu huyu?” aliuliza jamaa mmoja miongoni mwa watu wanne waliokuwepo ndani ya chumba kile, alikuwa ameitoa picha ya Tatiana na kuiweka mezani. Buffet alipoiona sura ile, moyo wake ukapiga paaaa.

      “Mnamfahamu?”

      “Ndiyo! Ni Tatiana!”

      Hicho ndicho walichotaka kukijua kwanza kama watu wale walikuwa wakimfahamu msichana huyo au la. Hapo ndipo walipoanza kuwaambia kile kilichokuwa kimetokea, ilikuwa ni stori ndefu iliyohusu ufuatiliaji wao mpaka mwisho wa siku kuwadaka.

      Waliwaambia kuhusu mawasiliano yao kwa njia ya meseji na sauti ambapo mpango mzima wa kummaliza Tatiana ulikuwa umepangwa, waliposikia hivyo na meseji hizo na sauti zao kuonyeshwa, kila mmoja akainamisha kichwa chake na kuanza kulia kwani tayari waliona kwamba walikuwa hatarini.

      Hawakuchukuliwa na kuhukumiwa nchini Ujerumani, wakapelekwa nchini Marekani ambapo huko kesi ikaanza kuunguruma. Kila mtu aliyesikia juu ya kile kilichoendelea alisikitika, utetezi mkubwa wa Buffet ni kwamba alishawishika kiurahisi kwa kuwa alimpenda kweli Nikola na alikwenda kwa Tatiana kwa sababu alihitaji kuwa maarufu kupitia msichana huyo tu.

      Kesi hiyo iliunguruma kwa muda wa miezi sita, kipindi chote hicho, ilikuwa ikiahirishwaahirishwa mara kwa mara lakini mwisho wa siku, huku ikatolewa na wote kwa pamoja kufungwa kifungo cha miaka kumi jela kwani kile kilichotokea lilikuwa moja ya tukio lililopewa jina la kukusudia kuua.

      “Nisamehe Tatiana! “ alijisemea Buffet wakati akichukuliwa na kupelekwa katika gari la magereza, uso wake aliuinamisha, waandishi wa habari walikuwa wakipiga picha tu kwa ajili ya magazeti yao ya siku inayofautia.

      ****

      Kwa mara ya pili, Tatiana alikuwa kipofu, hata alipopona kabisa, hakutaka kukaa nchini Marekani, alichokifanya ni kurudi nchini Tanzania tena kijijini Chibe, kule alipozaliwa ili kama kufa, basi alitaka kufa ndani ya nchi yake, tena katika kijiji alichozaliwa.

      Kila Mtanzania alihuzunika, wengi walikuwa wakimlaumu Buffet na msichana wake Nikola kwa kile walichokifanya kwa msichana yule. Nyota kali ya mafanikio iliyokuwa ikiwaka, ilizimika ghafla.

      Kila siku Tatiana alikuwa mtu wa kulia tu, aliyakumbuka maisha yake ya zamani, alitamani kurudi kule alipokuwa, aombe msamaha kwa kila kitu kilichotokea ili arekebishe maisha yake lakini hilo halikuweza kujirudia tena.

      Mapenzi yalimchanganya, mapenzi hayohayo yalimfanya kuwa kipofu kwa mara nyingine tena. Peter hakutaka kumtenga Tatiana, akaamua kurudi kijijini kule kama ilivyokuwa zamani. Kipindi kile, alirudi akiwa na mapenzi ya dhati, alilia sana lakini katika kipindi hiki alirudia akiwa mtu tofauti kabisa, alimchukulia Tatiana kama msichana wa kawaida, kila kitu kilichopita kama mapenzi na ubaya aliotendewa, akaamua kuusahau, hakutaka kuupa tena nafasi.

      Kila Tatiana alipokuwa akiisikia sauti ya Peter, alibaki akilia tu. Katika maisha yake yote hakuwahi kumuona mwanaume huyo, hakujua alifananaje, alipotabasamu uso wake ulikuwaje. Alikuwa kipofu ambaye mara kwa mara alikuwa akishinda chumbani kwake.

      Kupitia fedha zake, akafungua biashara nyingi, akaendelea kuingiza fedha na kuwa mwanamke tajiri kuliko wote Afrika Mashariki. Alichokifanya ni kugawa asilimia ishirini ya utajiri wake kwa Peter kama msamaha kwa kila kitu kibaya alichomfanyia kwani aliamini kwamba mwanaume huyo alikuwa akimpenda kwa mapenzi ya dhati.

      “Naomba unisamehe kwa kila kitu Peter, ni shetani tu aliyenifanya nikuumize,” alisema Tatiana huku akilia, machozi yalimbubujika mashavuni mwake.

      “Usijali Tatiana! Mungu ni mwema, labda kutokuwa nawe kulikuwa na sababu, labda ningekuwa nawe hata hatua hii niliyofikia ya kumtumikia yeye nisingeifikia,” alisema Peter kwa sauti ya chini.

      “Peter! Moyo wangu unakupenda mno, nahisi mapenzi mazito kwangu juu yako, ninakupenda, una mke, ila kamwe sitoweza kuwa nawe tena, japokuwa ninakupenda, kamwe moyo wangu hautokuwa na maumivu juu ya upendo wako kwa mke wako,” alisema Tatiana kwa sauti ya chini iliyoonyesha kuwa alikuwa na maumivu makali ya moyo.

      Baada ya safari ndefu katika maisha yake, Tatiana hakuwa na jinsi, alitakiwa kukubaliana na ukweli uliokuwepo kwamba kila kitu kilibadilika na hatimaye akawa kipofu kama alivyokuwa kipindi cha nyuma.

      Japokuwa alikuwa na utajiri mkubwa maishani mwake lakini hakuweza kubadilisha kitu chochote kile. Kila mwaka, masupastaa wengi walikuwa wakifika kijijini hapo kumjulia hali, walimfariji na kumtia nguvu ili kuendelea kupambana katika maisha yake.

      Baada ya miaka miwili, akaamua kuandika kitabu cha maisha yake, alielezea kila kitu, tangu siku ya kwanza alipopata ufahamu mpaka siku ile ambayo maisha yalibadilika na kuwa kipofu tena. Hakuficha kitu, alieleza mapenzi mazito aliyokuwa nayo kwa Peter mpaka siku aliyokuja kumsaliti na kuwa kipofu kwa mara nyingine tena.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

      Kilikuwa moja ya vitabu vilivyohuzunisha mno, kila aliyekisoma, alibubujikwa na machozi na kumuonea huruma Tatiana. Kitabu hicho kiliandikwa kwa lugha saba na kulisambazwa duniani kote. Kiliteka hisia za watu wengi, kilinunulika mno, aliuza zaidi ya kopi milioni ishirini, utajiri wake ukaongezeka, ila kwake, utajiri mkubwa bila kuona chochote kile, ilikuwa kama mateso mazito yasiyoweza kubebeka.



      MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog