Search This Blog

Thursday, July 21, 2022

NISAMEHE LATIFA - 4

  







    Simulizi : Nisamehe Latifa

    Sehemu Ya Nne (4)



    Mateso yakawa mateso, Ibrahim akawa mtu wa kuhuzunika kila siku, hakuona raha ya ndoa tena, kuna kipindi alikuwa akilala peke yake chumbani, Nusrat hakuwa nyumbani, alikuwa klabu akiponda raha na wanaume wake wa Kiarabu.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Yalikuwa ni maumivu yasiyoelezeka moyoni mwake, rafiki yake mkubwa kitandani akawa mto, kila alipolia, machozi yake yalidondokea kwenye mto, kila alipohitaji faraja ya kukumbatiwa, aliukumbatia mto.

    Kila kitu kikabadilika, kuna kipindi alitamani kumuacha Nusrat lakini wakati mwingine alipokuwa akifikiria kwamba msichana huyo alishughulika na vitu vingi katika maisha yake likiwepo suala la kazi, alishindwa kufanya hivyo.

    Nusrat aliporudi nyumbani, hakuwa mzungumzaji sana, kila alipofika, alilala popote pale kwani pombe zilimjaa kichwani mwake. Hakuwa na muda wa kuongea na mume wake, alimuona kuwa takataka kwa kuwa alijua kwamba maisha yake yalimtegemea yeye.

    Siku zikakatika, Ibrahim alipoona amechoka, ameshindwa kuvumilia, hapo ndipo alipoanza kumtafuta yule mzee ambaye alikuwa akizungumza naye kipindi cha nyuma, mzee ombaomba aliyekuwa akikaa karibu na eneo la Mnazi Mmoja kwa ajili ya kuzungumza naye.

    Alipofika huko, mzee yule hakuwepo kitu kilichompa wakati mgumu, akaanza kumtafuta kwa kuulizia. Haikuwa kazi nyepesi, kila alipoulizia, hakukuwa na mtu aliyejua mahali alipokuwa, hakukata tamaa, alizunguka na kuzunguka na mwisho wa siku kufanikiwa kukutana na mtu ambaye alimuelekeza alipokuwa.

    “Yule mzee alizidiwa hapa, alipelekwa hospitalini, baada ya hapo hakurudi tena. Ila yupo Magomeni Mapipa, ukifika pale, ulizia kwa mzee Majeed, mzee mwenye ndevu nyingi kama Osama, huwa anaishi nje ya nyumba ya huyo mzee, kibarazani,” alisema kijana muuza maji ambaye alimfahamu fika mzee huyo.

    Ibrahim hakutaka kuchelewa, kwa kuwa alikwishapewa maelekezo ya kutosha, hapohapo akaanza kuelekea huko. Njiani alikuwa na mawazo mno, kile kilichokuwa kimetokea, kilimuumiza mno hivyo akatamani kumuona mzee yule ili amshauri juu ya kile kilichokuwa kikiendelea.

    Hakuchukua muda mrefu akafika Magomeni Mapipa ambapo baada ya kuulizia kwa mzee Majeed, akaelekezwa na kuelekea huko. Mazingira aliyomkuta nayo mzee yule yalimuumia mno, hakuamini kile alichokuwa akikiona kwamba mzee masikini, aliyekuwa ombaomba alikuwa kibarazani amelala, pale alipokuwa, jua kali la saa saba liliwaka na kumuunguza lakini hakujali, hakuwa na sehemu nyingine zaidi ya hiyo. Ibrahim akahisi kulia.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Japokuwa hakuwa na fedha za kutosha lakini hakutaka kumuona mzee yule akiendelea kuishi katika maisha yale, maisha yaliyojaa umasikini mkubwa ambayo kila alipokuwa akiyafikiria, alijikuta akibubujikwa na machozi tu.

    Akampangia chumba katika Mtaa wa Tandale na kumtaka kukaa huko, mara kwa mara alikuwa akielekea huko na kumsaidia kiasi fulani cha fedha ambacho aliamini kabisa kingeweza kumsaidia.

    Siku zikaendelea kukatika, baada ya mwezi mmoja, aliporudi ndani ya nyumba ile aliambiwa kwamba mzee yule alikuwa amepelekwa hospitalini, kidonda kile alichokuwa nacho kiliongezeka na kilizidi kuoza japokuwa alikuwa akitumia dawa.

    Ibrahim akachanganyikiwa, hakutaka kubaki mahali hapo, kwa kuwa aliifahamu Hospitali ya Mwananyamala sehemu ilipokuwa, akaanza kwenda huko. Njiani, mawazo yake yalikuwa kwa mzee huyo tu, moyoni mwake alihisi kulikuwa na kitu kilichomsukuma kumsaidia mzee yule, hakujua alikuwa na nani na alikuwa na nini, msukumo moyoni mwake ulimwambia ni lazima amsaidie mzee huyo.

    Alipofika hospitalini hapo, akaingia mpaka ndani na kupewa maelekezo juu ya mahali alipolazwa mzee huyo, akaelekea huko. Alipofika nje ya chumba kile alicholazwa, akaruhiswa na kuingia ndani.

    Mzee yule alikuwa kwenye maumivu makali mno ya mguu wake, kidonda kile kilipelekea mguu ule kuanza kuoza. Ibrahim alipomwangalia, alishindwa kuyazuia machozi yake, yakaanza kububujika mashavuni mwake.

    “Wewe ni ndugu yake?” aliuliza daktari.

    “Ndiyo! Kuna nini?”

    “Hebu nifuate.”

    Akaanza kuondoka na daktari yule kuelekea katika ofisi yake ambayo haikuwa mbali na chumba kile. Walipofika, wakaingia ndani na moja kwa moja kutakiwa kukaa kitini.

    “Ndugu yako tumemkuta ana tatizo kubwa mguuni mwake,” alisema daktari yule.

    “Tatizo gani?”

    “Ana kansa ya mguu. Tuliangalia, tukagundua kwamba alichomwa na kitu chenye kutu hivyo kumletea tetenasi. Ugonjwa huu umekuwa ukiua watu wengi sana, kwake, umesababisha mguu kuoza, tukiuacha hivihivi, ni lazima ataoza zaidi kitu kinachoweza kusababisha kifo chake,” alisema daktari yule.

    “Ooppss..! Kwa hiyo nini kifanyike?”

    “Akatwe mguu! Hicho ndicho kinachotakiwa kufanyika ili kuokoa maisha yake,” alisema daktari yule. Ibrahim akashtuka.

    *****

    Alihitaji kuwa bilionea, ndivyo alivyokuwa kwa kipindi hicho, maisha yake yalibadilika, Latifa yule wa kipindi cha nyuma hakuwa huyu wa sasa, alikuwa na kila kitu alichokihitaji katika maisha yake.

    Jina lake lilikuwa kubwa, alisikika katika kila masikio ya mtu duniani, dawa yake ilileta mapinduzi makubwa na ilisifika kila kona. Latifa alikuwa ni zaidi ya wanamuziki, alikuwa ni zaidi ya wacheza soka na alikuwa ni zaidi ya waigizaji filamu, kila alipopita, aliheshimiwa, watu wengine waliposikia kwamba alitarajia kupita barabara fulani, walikusanyika, yaani wengine walitaka kumuona tu.

    Ndugu zao waliokuwa hoi vitandani kwa sababu ya magonjwa ya kansa, walipona na kuwa wazima kabisa, walimshukuru Latifa na hakukuwa na malipo mengine ambayo wangeweza kufanya zaidi ya kumheshimu na kumpenda maisha yao yote.

    Latifa hakuishia nchini Marekani, chini ya kivuli cha Umoja wa Mataifa katika Shirika cha Afya Duniani, WHO, akaanza kuzunguka nchi mbalimbali duniani. Hiyo ilimpa heshima, ilimuongezea umaarufu na kila alipokuwa akienda, watu walikusanyika na kutaka kupiga naye picha.

    Latifa akawazidi umaarufu hata watu wengine, alipotua nchini Uingereza, kwa heshima kubwa, akaalikwa mpaka bungeni ambapo huko akapewa nafasi ya kuzungumza, kila neno lililotoka mdomoni mwake, lilikuwa lenye kuleta matumaini makubwa kwamba alikuwa kwenye mikakati ya kutengeneza dawa za magonjwa mengi sugu likiwemo UKIMWI.

    Hakuishia barani Ulaya, alizidi kuzunguka katika nchi nyingine, alifika mpaka Urusi ambapo huko akapokewa na watu wengi wakiwemo madaktari wakubwa, walioheshimika, madaktari waliokuwa na nyadhifa za kupokelewa na viongozi wakubwa katika nchi nyingine, ila kutokana na kile alichokifanya, wote walikuwa uwanjani kumpokea.

    “Ni binti mdogo mno,” kila aliyemuona Latifa alizungumzia juu ya muonekano aliokuwa nao Latifa.

    “Nini kinafuata?”

    “Nitataka niende na Afrika pia, japokuwa hakuna magonjwa mengi ya kansa, ila natakiwa kwenda kuwaona hata haohao wagonjwa wachache, nitaanzia na Monrovia nchini Liberia,” alisema Latifa.

    Taarifa zikatolewa, nao Waafrika ambao kila siku walijiona kutengwa, wakajiandaa kumpokea mtu wao, msichana aliyekuwa maarufu mno duniani kutokana na dawa ya magonjwa ya kansa aliyekuwa ameitengeneza, Latifa.



    Waliberia walijipanga katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Daniel Oduber Quiros, kila mmoja alikuwa na hamu ya kumuona Dk. Latifa ambaye alitarajiwa kuingia katika uwanja huo muda mchache ujao.

    Idadi kubwa ya watu waliokuwa mahali hapo walikuwa na fulana zilizokuwa na picha za msichana huyo huku zikiwa zimeandikwa neno Hero likiwa na maana ya shujaa. Si wote waliokuwa na fulana hizo bali wengine walikuwa na mabango yaliyoandikwa maneno mengi ya kumsifia msichana huyo kutokana na ukombozi aliokuwa ameuleta duniani.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Miongoni mwa watu waliokuwa uwanjani hapo alikuwemo Waziri wa Afya nchini humo, bwana Fredrick Taylor aliyetangulizana na mkewe. Waandishi wa habari kutoka katika vyombo mbalimbali vya habari nchini humo walikuwepo uwanjani hapo huku wakiwa na vitendea kazi vyao, kikundi cha ngoma za kienyeji kilikuwa tayari huku watoto wawili waliokuwa na maua wakiwa wamewekwa tayari.

    Aliyekuwa akisubiriwa hakuwa rais kutoka nchi fulani, alikuwa Latifa, msichana mwenye asili ya Kihindi ambaye mama yake alifukuzwa nyumbani na kutamani kujiua huku baadaye akisaidiwa na kijana toka Mtaa wa Tandale ambaye ndiye aliyemlea Latifa mpaka muda huo.

    Baada ya saa moja, ndege binafsi ikaanza kuonekana angani, taarifa zikatolewa kwamba ndege ile iliyotarajiwa kutua ndiyo ambayo ilimbeba Latifa, wapiga picha na watu wengine wakaanza kujiandaa.

    Iliposimama, ngazi ikashushwa, ikawa sawasawa na zuria jekundu. Walioanza kuteremka walikuwa watu kadhaa ambao alitangulizana nao na mwisho wa siku kuteremka Latifa mwenyewe.

    Alichokiona, akashindwa kuyazuia machozi yake kububujika mashavuni mwake. Msichana yeye, aliyeteswa na mapenzi, msichana ambaye mama yake alikufa kwa Ugonjwa wa UKIMWI baada ya kufanya sana ngono na walevi wa gongo, leo hii alikuwa akipokelewa kishujaa.

    “I can’t believe this,” (Siamini hili) alisema huku akionekana kushtuka.

    Zaidi ya watu elfu tano walikuwa wamekusanyika ndani ya uwanja huo, walipomuona tu, wakashindwa kuvumilia, wakaanza kupiga makofi na vigelegele vya shangwe. Msichana maarufu kuliko wote duniani alikuwa akiteremka katika ngazi za ndege, alipofika chini, akaanza kusalimiana na bwana Taylor kisha kukabidhiwa maua na watoto wale, kikundi kile cha ngoma za asili kiliendelea kupiga ngoma zile kisha baada ya hapo akachukua nafasi hiyo kupiga picha na baadhi ya watu waliokusanyika uwanjani hapo kisha kupanda ndani ya gari na kuondoka.

    Siku iliyofuata ilikuwa ni siku maalumu kwa Latifa kupelekwa katika hospitali ya taifa ya nchi hiyo, huko, akapata nafasi ya kuonana na wagonjwa mbalimbali waliokuwa hoi vitandani. Hakuwaacha, alizungumza nao mengi, aliwafariji na pia kuwatia nguvu kwamba wangepona magonjwa yao.

    “Siamini kukuona,” alisema mgonjwa mmoja.

    “Kwa nini?”

    “Nilisikia mengi kuhusu wewe, nilisikia kuhusu maisha yako, yalinigusa sana, mwisho wa siku nikafikiri kwamba ni mwanamke mtu mzima, kumbe binti mdogo!” alisema mgonjwa huyo huku akimshangaa Latifa.

    “Kwani hukuwahi kuniona kabla kwenye televisheni?”

    “Sikuwahi! Nimekuwa nikiugua uti wa mgongo kwa mwaka wa tano sasa, siwezi kusimama, siwezi hata kukaa, maisha yangu yote kwa kipindi hicho ni kulala kitandani tu,” alisema mgonjwa huyo maneno yaliyomuumiza mno Latifa.

    “Pole sana!”

    “Ahsante! Karibu sana katika nchi hii yenye utajiri wa almasi zilizojaa damu,” alisema mgonjwa yule.

    “Nashukuru! Ila hautakiwi kuziita almasi zilizojaa damu. Vita vilikwisha, kila kitu kimebaki na kuwa historia, sahau yaliyopita,” alisema Latifa huku akifahamu fika kwamba nchini hiyo ilikuwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe miaka kadhaa iliyopita.

    Hakuishia hapo, siku hiyo alitaka kuzunguka kote, kila aliyemuona, hakuamini kama siku hiyo alikutana na msichana mwenye jina kubwa, msichana aliyeuwa bilionea mkubwa duniani.

    *****

    Dunia nzima ilijua uwepo wa Latifa barani Afika, kila mtu alikuwa na hamu ya kumuona msichana huyo mrembo aliyegundua dawa ya magonjwa ya kansa ambayo kwa kipindi hicho ndiyo iliyokuwa ikizungumza katika kila kona.

    Watu wengi walitamani kutembelewa na msichana huyo ambaye kwa kipindi hicho alikuwa amemaliza ziara yake ya kutembelea nchini Liberia na alikuwa akijiandaa na safari nyingine ya kuelekea nchini , Kongo, Ivory Coast na sehemu nyingine barani Afrika.

    Kila alipopita, Latifa aliacha gumzo kubwa, watu walimzunguka kwa lengo la kuzungumza naye. Kila alipokanyaga, vituo mbalimbali vya televisheni vilimuita na kufanya naye mahojiano, alialikwa katika shule mbalimbali kwa ajili ya kuzungumza na wanafunzi huku wakati mwingine akitembelea kambi za wakimbizi kwa lengo la kuwajulia hali na kuwakumbusha kwamba pamoja na kila kitu kilichokuwa kikitokea, bado alikuwa pamoja naye.

    Alipanga kwenda nchini Tanzania, alitamani kuwaona watu aliozoea kuwaona miaka ya nyuma, alitamani kuyaona mazingira ya Tanzania ambayo aliyaacha kipindi cha nyuma. Aliikumbuka nchi hiyo, umasikini mkubwa uliokuwa umeigubika, watu waliokuwa wakifanya kazi usiku na mchana, kila alipowakumbuka, aliuona upendo mkubwa ukiendelea kuongezeka kwa Watanzania wenzake.

    “Nitafika Tanzania, nitataka kutembelea sehemu zote nilizowahi kutembelea,” alisema Latifa huku akiwa kwenye Hoteli ya La Revancha iliyokuwa katikati ya Jiji la Dar nchini Senegal.

    Pamoja na kutamani kufika nchini Tanzania, bado aliendelea kumkumbuka Ibrahim ambaye kwake alionekana kuwa miongoni mwa watu katili ambao hawakutakiwa kuishi katika dunia hii. Alikumbuka vilivyo kile kilichotokea kipindi cha nyuma, namna alivyotukanwa na kudharauliwa mbele ya macho ya watu, hakika aliuahidi moyo wake kwamba asingeweza kumsamehe Ibrahim.

    “Siwezi kumsamehe! Mungu, naomba unisamehe ila kwa Ibrahim, siwezi kumsamehe,” alisema Latifa huku akionekana kuwa na hasira mno.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ilikuwa ni saa 4:00 usiku, alikuwa amejiandaa kulala tayari kwa kuanza safari ya kuelekea nchini Kongo kisha kwenda Tanzania ambapo angeanzia mkoani Kigoma na kutembelea Hospitali ya Maweni kabla ya kwenda katika kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu.

    “Ngriii...ngriiii...ngriiii....” ilisikika simu ya mezani ikiita chumbani humo. Kwa hali ya kichovu Latifa akainuka kutoka kitandani na kuifuata simu hiyo, alipoifikia, akaunyanyua mkono wa simu ile na kuupeleka sikiona.

    “Hallo!” aliita.

    “Hallo! Samahani, kuna mgeni wako hapa.”

    “Mgeni wangu?”

    “Ndiyo!”

    “Anaitwa nani?”

    “Anaitwa Dominick!”

    “Mmmh! Sawa! Nakuja.”

    Latifa alibaki akishangaa tu, jina la mgeni aliyekuwa akimhitaji lilimtia wasiwasi kwani hakujua alikuwa nani na alihitaji nini kutoka kwake. Hakutaka kujali sana, kwa kuwa alifahamu kwamba alikuwa mtu wa watu, akaamua kuvaa na kushuka mpaka mapokezini ambapo huko akaonyeshewa mwanaume aliyekuwa akimhitaji.

    Kwa kumwangalia, alionekana kuwa mwanaume mpole, mtanashati ambaye alivalia shati jeupe, surali nyeusi na tai nyekundu, uso wake ulipendezeshwa na miwani ya macho iliyomfanya kuonekana msomi mwenye masta.

    “How are you!” (Habari yako!) alisalimia Latifa.

    “Usijali, mimi ni Mbongo mwenzanko,” alisema Dominick huku akiachia tabasamu pana usoni mwake, tabasamu lililomfanya kupendeza vilivyo.

    “Hahah! Samahani! Kumbe ni Mtanzania mwenzangu! Nasikia ulikuwa ukinihitaji,” alisema Latifa.

    “Yeah! Kuna mengi nataka kuzungumza nawe,” alisema Dominick.

    “Yapi hayo?” aliuliza Latifa huku akishtuka.

    “Usishtuke, si mapenzi, tunaweza kukaa sehemu?”

    “Hakuna tatizo!”

    Latifa alijisikia huru, kuwa na Mtanzania mwenzake kulimfanya kujisikia amani moyoni. Walichokifanya ni kusogea pembeni mpaka katika mgahawa uliokuwa hotelini hapo na kisha kutulia.

    Kabla ya kuzungumza chochote kile, wakabaki wakiangaliana kwa sekunde kadhaa, macho ya Dominick yalionyesha dhahiri kile kilichokuwa kikiendelea moyoni mwake, alionekana kuwa katika dimbwi zito la mahaba.

    “Samahani kwa kukusumbua,” alisema Dominick.

    “Bila samahani!”

    “Kwa jina ninaitwa Domick Simon, nimezaliwa Tanzania ila nilikuja hapa kwa ajili ya masomo yangu ya udaktari katika Chuo cha Touba kilichokuwa katika Mji wa Touba, Mashariki mwa nchi hii. Siku chache zilizopita nilisikia kwamba ungekuja hapa Senegal kwa ajili ya kutembelea wagonjwa katika ziara yako hii iliyo chini ya WHO,” alisema Dominick, Latifa alikuwa kimya akimsikiliza.

    “Ndiyo!”

    “Nilihitaji kujifunza mengi kutoka kwako, ninahitaji nisafiri nawe sehemu mbalimbali, nadhani kupitia wewe, naweza kupata vitu ambavyo vinaweza kunisaidia sana,” alisema Dominick huku akionekana kuhitaji msaada wa dhati.

    “Mmmh!”

    “Nini tena?”

    “Hakuna tatizo, ila nina sharti moja,” alisema Latifa.

    “Usijali Latifa, nitajigharamia kila kitu,” aliingilia Dominick.

    “Simaanishi gharama.”

    “Unamaanisha nini?”

    “Sitaki mwisho wa siku useme kwamba unanipenda, sihitaji mapenzi kwa sasa, ninahitaji kuwa peke yangu,” alisema Latifa huku akimwangalia Dominick usoni.

    “Hahaha! Yaani nikuepende wewe? Acha utani Latifa! Hilo sharti si gumu, nimekubaliana nalo,” alisema Dominick.

    “Hakuna tatizo! Safari inaanza kesho asubuhi kuelekea Kongo,” alisema Latifa.

    “Hakuna tatizo.”



    Dickson Simon Magembe, alikuwa mmoja wa wanafunzi waliofanya vizuri sana nchini Tanzania katika mtihani wa kidato cha sita mwaka mmoja uliopita. Uwezo wake mkubwa wa darasani uliomfanya kuongoza Tanzania nzima ukaipelekea serikali ya nchi hiyo kumdhamini kwenda kusoma nchini Marekani katika Jimbo la Los Angeles.

    Kwa kuwa alilelewa katika familia iliyopenda kusaidia watu mbalimbali waliokuwa kwenye matatizo, alichokifanya ni kuiambia serikali kwamba hakutaka kwenda kusoma nchini Marekani bali alitaka kupelekwa nchini Senegal ili atakapofika huko, apate muda wa kuwatembelea watu mbalimbali waliokuwa kwenye kambi za wakimbizi ili aweze kuwasaidia.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Serikali haikukataa, ilichokifanya ni kumsikiliza na hatimaye kumdhamini kwenda nchini humo ambapo mara baada ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Touba, mara chache alikuwa akipata nafasi ya kwenda katika kambi za wakimbizi na kuzungumza nao, alifanya kila kitu kwa kutengeneza makala kwa njia ya video kwa ajili ya maisha yake ya baadaye.

    Aliwazoea wakimbizi, kila alipowaona namna walivyopata tabu, alijikuta akibubujikwa na machozi mashavuni mwake. Picha mbaya za watu waliojeruhiwa vibaya, watu waliokuwa wakiteseka kwa magonjwa mabaya yakiwemo ya zinaa mara baada ya kubakwa na wanajeshi, yalimuumiza mno.

    Aliishi huko kwa miaka miwili na ndipo alipoanza kusikia kuhusu Latifa. Alivutiwa naye, msaada alioutoa wa kuisaidia dunia nzima kutokana na magonjwa ya kansa akavutiwa nayo, alichokifanya ni kuanza kumfuatilia msichana huyo.

    Latifa alipoanza ziara ya kutembelea nchi mbalimbali Afrika hapo ndipo akaona lingekuwa jambo la maana sana kama angeonana na msichana huyo na kuzungumza naye, kweli alifanikiwa.

    Alipomwangalia Latifa, alikuwa msichana mrembo, mwenye mvuto, msichana mwenye macho mazuri, yaliyong’aa mithili ya goroli, lipsi pana, nywele ndefu zilizofika mpaka mgongoni. Moyo wake ukampenda lakini huo haukuwa muda wa mapenzi na alijiahidi kwamba asingeweza kuwa na msichana huyo katika maisha yake yote zaidi ya kufanya naye kazi tu.

    Alipopewa sharti la kutokuzungumzia mapenzi, kwake halikuwa tatizo, hakuhisi kama moyo wake ulikuwa kwenye mapenzi na msichana huyo mrembo, alichokifanya ni kukubaliana naye.

    Siku iliyofuata ndipo safari ya kuelekea nchini Kongo ilipoanza, walichukua ndege, wakakaa pamoja huku wakizungumza mengi. Japokuwa Latifa tayari alikuwa bilionea lakini hakutaka kujali, alikuwa na nidhamu na fedha zake na hakutaka kutumia kiasi kikubwa cha fedha pasipo kuwa na sababu.

    “U mwanamke mrembo sana, umechukua wapi urembo huo?” aliuliza Dominick.

    “Umeanza!”

    “Nimeanza nini sasa?”

    “Nilikwambia nini jana?”

    “Daah! Kwani kuna kosa kama nikimsifia Mungu?”

    “Hapana! Mambo ya uzuri achana nayo kwanza. Kumbuka, hapa kazi tu,” alisema Latifa, alionekana kubadilika.

    “Ooh! Ok! Nilishasahau, hakuna tatizo,” alisema Dominick, akavuta Jarida la Boniventure na kuanza kulisoma.

    Ndege iliendelea kukata mawingu, baada ya masaa kumi ikaanza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa N’Djili uliokuwa katika jiji kubwa la Kinshasa nchini Kongo. Ndege iliposimama, abiria wote wakaanza kuteremka.

    Kama ilivyokuwa katika nchi nyingine, watu zaidi ya elfu tano walikuwa wamekusanyika uwanjani hapo tayari kwa kumpokea msichana Latifa. Kila alipofika, aliacha alama kubwa ya umaarufu wake.

    Alipendwa kwa kuwa alionekana kuwa msichana mwenye huruma nyingi kuliko wote. Alipofika nje ya jengo la uwanja huo, huku akiwa na Dominick, waandishi wa habari wakaanza kumsogelea na kuanza kumpiga picha mfululizo.

    “Mmh! Kumbe maisha ya mastaa yapo hivi!” alisema Dominick, alimwambia Latifa kwa sauti ya chini karibu na sikio.

    “Yapo vipi?”

    “Hayana raha, kila kona karaha,” alisema Dominick.

    Walipofika nje kabisa, tayari mlango wa gari moja likafika uwanjani hapo, lilikuwa lina bendera ya nchi hiyo, lilikuwa la kifahari sana. Mwanaume mmoja aliyevalia suti akawafuata na kuwaambia kwamba walitakiwa kwenda kuingia ndani ya gari lile.

    “Ni gari la serikali?” aliuliza Latifa.

    “Ndiyo!”

    “La nani?”

    “Waziri Mkuu!”

    “Mmmh! Mwenyewe yupo wapi?”

    “Wewe twende, tutaongea mbele ya safari,” alisema mwanaume huyo, walipolifikia gari lile wakaingia ndani na kuanza kuondoka, furaha ambayo watu walikuwa nayo kipindi hicho wakaanza kulikimbiza huku wakishangalia.

    “Karibu sana Latifa,” alimkaribisha mwanaume huyo aliyezungumza Kiswahili vizuri kabisa.

    “Ahsante sana. Aya, nijibu sasa,” alisema Latifa.

    “Nchi hii ipo kwenye matatizo sana,” alisema mwanaume yule.

    “Matatizo gani?”

    “Watu wanataka waziri mkuu ajiuzulu.”

    “Kisa?”

    “Machafuko yaliyotokea, yaani watu wana hasira naye, anaishi kwa kujifichaficha tu, kama angeonekana hata pale uwanjani, wangeweza kumuua,” alisema mwanaume yule.

    “Nimekuelewa.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Safari iliendelea mbele, walizungumza mambo mengi huku kila mmoja akimuuliza mwenzake maswali. Kila swali ambalo Latifa aliliuliza lililonekana kuwa muhimu, Dominick aliliandika kwenye notebook yake.

    Hawakuchukua muda mrefu wakaingia katika jumba moja kubwa la kifahari, kwa kuliangalia kwa nje tu isingekupa wakati mgumu wa kugundua kwamba mmiliki wa jumba hilo alikuwa mmoja wa watu wenye fedha nyingi.

    Gari liliposimamishwa ndani ya eneo la jumba hilo, wote watatu wakateremka. Latifa akabaki akiliangalia jumba lile la kifahari, lilikuwa moja ya majumba makubwa aliyowahi kuingia, kulikuwa na bustani nzuri ya maua, masanamu yaliyonakshiwa kwa unga wa dhahabu, kulikuwa na mbuga ndogo ya wanyama iliyokuwa imezungushiwa fensi huku ndani yake kukiwa na wanyama wachache, kulikuwa na bwawa kubwa la kuogelea, kwa kuliangalia tu, ungegundua kwamba mtu aliyekuwa akiishi ndani ya jumba hilo alikuwa mtu mwenye pesa nyingi.

    Wakaingizwa ndani, kulikuwa na makochi makubwa yaliyozungushiwa vyumba vilivyokuwa na rangi ya dhahabu, kadiri Latifa na Dominick walivyokuwa wakiliangalia, bado akili yao iliwaambia kwamba mtu aliyekuwa akilimiliki jumba hilo hakuwa mtu wa mchezo kwenye mambo ya fedha.

    Mara mwanaume mmoja akatokea mahali hapo, alikuwa mfupi, mwenye kitambi kikubwa, sura mbaya huku kichwani akiwa amenyoa mtindo wa kijana ujulikanao kama kiduku.

    Alikuwa na umri mkubwa, kama miaka sitini lakini kwa kumwangalia, muonekano wake ulikuwa wa ujana zaidi. Alivalia fulana iliyokuwa na picha ya muimbaji wa Marekani, Jay Z, mikononi alivalia saa ya dhahabu. Miguuni, alivalia raba zilizokuwa na chata kubwa ya Nike, kwa muonekano wa harakaharaka usingeweza kugundua kama mwanaume huyo alikuwa mtu mzima.

    “Karibuni sana,” aliwakaribisha huku naye akijiweka kochini.

    Huyo alikuwa waziri mkuu nchini Kongo, alikuwa miongoni mwa viongozi waliochukiwa mno, machafuko yaliyokuwa yakitokea nchini humo mara kwa mara, yeye ndiye aliyekuwa akisuka mipango huku lengo lake kubwa likiwa ni kuchukua dhahabu na kuwauzia Wazungu.

    Wakongo hawakumpenda, waliandamana hadharani kupinga uwepo wake nchini humo, walimchukia sana lakini hawakujua walitakiwa kufanya nini kwani kila uchaguzi mkuu ulipofika, alishinda kwa kishindo kikubwa, ila kwa kuiba kura nyingi.

    “U msichana mzuri sana Latifa,” alisema bwana Nelson Savimbi huku uso wake akiupendezesha na tabasamu pana lakini uso haukubadilika, bado ulikuwa mbaya.

    “Nashukuru sana.”

    Walizungumza mambo mengi, Latifa aliyeonekana kuwa mchangamfu zaidi alimwambia kile kilichokuwa kimemleta nchini Kongo hivyo kuhitaji muda wa siku mbili kwa ajili ya ziara ya kutembelea hospitali za nchini humo na baadhi ya kambi za wakimbizi.

    Hilo halikuwa tatizo haa kidogo, alichokifanya bwana Savimbi ni kumruhusu na hivyo kuwasiliana na wahusika na kuwaambia juu ya uwepo wa Latifa nchini humo. Baada ya kuzungumza kwa kipindi kirefu hapo ndipo walipoondoka na kuelekea katika hoteli kubwa ya nyota tano, The Bufalloes iliyokuwa katikati ya Jiji la Kinshasa.

    “Nakutakia usiku mwema Latifa,” alisema Dominick.

    “Ahsante! Nawe pia,” alisema Latifa na kuingia chumbani kwake.



    Usiku hakulala vizuri, kichwa chke kilikuwa kikifikiria juu ya safari yake kubwa ya mafanikio aliyokuwa nayo, ilikuwa safari ndefu ambayo kwa kipindi hicho alijivunia mno kuwa hapo alipokuwa.

    Hakuacha kuwakumbuka wanaume waliouumiza moyo wake, wanaume aliotokea kuwachukia kuliko wote katika dunia hii. Hakumpenda Ibrahim hata mara moja, alimchukia Liban, mwanaume wa Kihindi ambaye aliamua kumuacha kwa kuwa tu aliwasikiliza ndugu zake.

    Hakutaka kujificha, alikiri kwamba kati ya watu aliokuwa akiwachukia mno basi watu hao walikuwa mstari wa juu kabisa. Usiku huo hakuacha kukumbuka kuhusu mama yake, aliambiwa kwamba mama yake aliitwa Nahra, mwanamke mrembo aliyekuwa mlevi ambaye alifukuzwa na wazazi wake mara baada ya kupewa mimba na mtu mweusi kisha kumfukuza.

    Chuki yake ikaongezeka, watu aliokuwa akiwachukia wakaongezeka, pia alimchukia baba yake ambaye hakuwa akimfahamu, sababu kubwa ya kumchukia ni jinsi alivyomfukuza mama yake kisha kuingia kwenye ulevi mkubwa uliompa Ugonjwa wa UKIMWI na mwisho wa siku kufariki.

    Mbali na baba yake, aliwachukia babu na bibi yake kwa upande wa mama kwa kitendo chao cha kumfukuza mama yake kisa tu alizaa na baba yake. Moyo wake ulimuuma mno ila wakati mwingine alibaki akimshukuru Mungu kwa kuamini kwamba isingekuwa hivyo, inawezekana leo hii asingekuwa hapo alipokuwa.

    Siku iliyofuata, akajiandaa tayari kwa kuanza safari ya kuelekea katika hospitali mbalimbali, alipomaliza kujiandaa, akatoka nje ambapo akakutana na Dominick akiwa tayari nje, alipomuona, tabasamu pana likajengeka usoni mwake.

    Hotelini hapo kulikuwa na ulinzi mkubwa, polisi walikuwa wakizunguka huku na kule kuhakikisha kwamba ulinzi unakuwa mkubwa na wa kutosha. Japokuwa Latifa hakupendwa kulindwa na silaha lakini hakuwa na jinsi, alikubaliana na kila kitu.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wakaondoka na kuelekea katika Hospitali ya Mobutu. Idadi kubwa ya watu ilikuwa hospitalini hapo, waandishi wa habari kutoka katika vyombo mbalimbali vya habari walikuwa mahali hapo kwa ajili ya Latifa tu.

    Gari lile lililombeba yeye na Dominick liliposimama, wakatoka nje, waandishi wakawasogelea na kuanza kuwapiga picha. Latifa aliachia tabasamu pana, akashindwa kuvumilia, akajikuta akibubujikwa na machozi ya furaha, akaanza kuwapungia mikono watu hao.

    Alichokikuta ndani ya hospitali hiyo kilimliza, hospitali ilikuwa chafu, huduma mbovu, wagonjwa walirundikana kila chumba, hakukuwa na mpangilio wowote ule. Kila aliyezungumza naye, walimwambia wazi kwamba huduma ilikuwa mbovu hivyo waliiomba serikali iweze kuwasaidia kudumia huduma na si kula hela na kuuza madini kiholela.

    “Nitawasaidia kufikisha kilio chenu,” alisema Latifa.

    Ziara ya siku mbili ikafanyika kwa mafaniko makubwa, walipomaliza wakaanza safari ya kuelekea nchini Tanzania katika Mkoa wa Kigoma. Walipofika huko, wakachukuliwa na kupelekwa katika Hoteli ya Hiltop na kuchukua vyumba humo. Kama ilivyokuwa sehemu nyingine, hata huko pia watu wengi walitamani kumuona msichana huyo mdogo mwenye mafanikio na hatimaye kuwa bilionea mkubwa akiwa na umri mdogo tu.

    Waandishi wa habari na watu wengine walikusanyika katika Hoteli ya Hiltop kwa ajili ya kumuona Latifa ambaye wala hakuwa na hiyana, akaonana na watu hao kwa kukaa nao sehemu fulani kisha kuanza kuzungumza nao, walikuwa kama hamsini hivi.

    “Unajisikiaje kuwa Latifa?” aliuliza mwanamke mmoja.

    “Najisikia kawaida, ila najiona kuwa na thamani, hiki ndicho nilichokitaka, nitambulike mimi ni nani na nina mchango gani katika jamii,” alijibu Latifa huku akiachia tabasamu.

    “Na huyo ni nani? Shemeji yetu?” aliuliza mwandishi mmoja.

    “Nani? Huyu? Huyu ni rafiki yangu, anaitwa Dominick, nilikuwa naye tangu Senegal,” alijibu Latifa huku akichia tabasamu pana.

    “Mnapendeza kuwa pamoja, kama wapendanao,” alisema mwandishi mwingine, akawasogelea na kuwapiga picha.

    Maneno yale kama yakawa yameibua kitu fulani moyoni mwa Latifa, akauhisi moyo wake ukiingiwa na kitu cha tofauti kabisa, kitu alichokuwa nacho kipindi cha nyuma mara baada ya kuisoma barua aliyoandikiwa na Ibrahim.

    Alipomwangalia Dominick, mvulana huyu aliachia tabasamu pana, kitu ambacho hata yeye mwenye hakujua kilikuwa nini, akaona kuwa mwanaume mzuri mno, akahisi kuanza kumpenda.

    Maswali yaliendelea zaidi, Latifa aliwajibu wote lakini kichwa chake kiliingia katika fikra nyingine kabisa, alikuwa akimfikiria huyo Dominick aliyekuwa bize akiandika. Mara baada ya kumaliza mahojiano, wakaimama na kuelekea ndani.

    “Dominick...” aliita Latifa, mwanaume huyo akamsogelea na kusimama karibu yake, walikuwa koridoni katika ghorofa ya tano hotelini.

    “Naaam..” aliitikia Dominick huku akimwangalia Latifa, walikuwa karibukaribu mno.

    “Au basi...” alisema Latifa, akageuka na kuingia chumbani.

    Kichwa chake kikaanza kusumbuka, yule Dominick ambaye alimwambia wazi kwamba hakutaka siku amwambie kwamba alikuwa akimpenda, leo hii alijikuta akianza kumfikiria, mapenzi yakaanza kuchomoza moyoni mwake.

    Usiku hakulala, alibaki akimfikiria mwanaume huyo tu. Kitandani, ni mawazojuu ya Dominick ndiyo yalikuwa yakimsumbua kila wakati. Hakujua afanye nini, hakujua kama lingekuwa jambo la kawaida kumwambia mwanaume huyo kwamba alimpenda.

    “Dominick...These feelings have to stop right now, I can’t bear them,” (Dominick...hisia hizi zinatakiwa kutoka sasa, siwezi kuzibeba) alisema Latifa huku akibimbirikabimbirika kitandani pale.

    Alibaki na mawazo mpaka ilipofika saa nane usiku ndipo alipopatwa na usingizi. Alipoamka asubuhi, akajiandaa na kutoka nje ambapo baada ya kumuona Dominick, akajikuta akishtuka na moyo wake ukidunda kwa nguvu.

    “Umeamka salama?” aliuliza Dominick huku akitoa tabasamu lilimvuruga kabisa Latifa.

    “Nimeamka salama, wewe?”

    “Hata mimi nipo poa.”

    Siku hiyo safari ilikuwa ni kwenda katika Hospitali ya Mkoa ya Maweni na hospitali nyingine hapo Kigoma, kote huko, watu walikuwa wakijazana na kumwangalia Latifa, kila aliyemuona hakutaka kuamini kama msichana yule alikuwa Mtanzania kama walivyokuwa.

    Wagonjwa wakafarijika, maneno aliyokuwa akiyazungumza msichana huyo yakawatia nguvu na kujiona wakiingiwa na nguvu za kusonga mbele. Baada ya siku nzima ya kuwatembelea wagonjwa, siku iliyofuata ilikuwa ni zamu ya kwenda katika kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu.

    Huko, Latifa alijikuta akibubujikwa na machozi, hakuamini kama kulikuwa na watu waliokuwa wakipitia mateso makubwa kama alivyokuwa watu hao. Wengi walikuwa wagonjwa, madaktari walikuwepo kwa ajili ya kuwahudumia lakini kutokana na idadi ya wakimbizi kuwa wengi, hata wale madaktari walionekana kuwa wachache.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Siku hiyo napo akashinda hukohuko, baada ya kumaliza kila kitu, wakarudi Kigoma Mjini ambapo wakachukua ndege na kuanza safari ya kwenda Dar es Salaa, sehemu ambayo alizaliwa Latifa, sehemu kulipokuwa na watu wengi aliokuwa akiwachukia.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog