Search This Blog

Thursday, July 21, 2022

SINGIDANI - 5

 







    Simulizi : Singidani

    Sehemu Ya Tano (5)



    CHRIS alichanganyikiwa sana, alimwangalia baba yake akiwa haamini kabisa kama tayari alikuwa ameshajua kila kinachoendelea. Alihisi kichwa kumuuma sana.

    Alibaki amesimama palepale akimwangalia baba yake. Ndoa yake na Laura ilikuwa inayeyuka, jambo ambalo hakutaka kabisa litokee.

    “Una jipya la kuniambia?” Mzee Shila akauliza kwa hasira.

    “Baba tuliza hasira kwanza. Nahitaji kuzungumza na wewe.”

    “Sitaki mazungumzo na wewe, naomba uondoke haraka sana mbele ya macho yangu. Toka tafadhali,” akasema mzee Shila kwa hasira.

    Chris hakuwa na cha kufanya zaidi ya kuondoka. Baba yake alikuwa amekasirika katika kiwango cha mwisho kabisa. Aliingia garini kisha akapiga gia hadi nyumbani kwake Kijitonyama.

    Alifikia sebuleni na kujitupa kwenye sofa kubwa, akijaribu kutafakari. Macho yake tayari yalishaanza kulengwalengwa na machozi. Bila hiyari yake akajikuta akianza kulia.

    Hakuwa na msaada wowote kwa wakati ule. Alisimama ghafla na kuelekea kwenye jokofu kisha akatoa bia moja na kuifungua, akiwa palepale mbele ya jokofu lake, aliimimina kinywani mwake yote ikaishia humo!

    Aliposhusha chupa, ilikuwa tupu kabisa. Akachukua bia nyingine, akafanya vilevile kisha akachukua tena ya tatu, safari hii akatembea hadi kwenye sofa na kuketi.

    Akaendelea kunywa!

    Ni kama alikuwa amechanganyikiwa kabisa. Jambo lile lilimuumiza sana na aliona kama dunia yote ilikuwa ikimuangukia yeye.

    Amkose Laura?CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ni jambo ambalo hakutaka kabisa kuliruhusu litokee. Alihisi mwili wote ukitetemeka. Akiwa katika hali ile, akapata wazo la ghafla. Aliona usalama wake ulikuwa kwa mzee Ngeleja.

    Lilikuwa wazo alilolipitisha moja kwa moja. Haraka akachukua simu kisha akabonyeza jina la mzee Ngeleja na kumpigia! Simu haikuita muda mrefu, tayari mzee Ngeleja alikuwa hewani!

    “Shikamoo baba,” Chris akasalimia kwa heshima.

    “Marahaba mwanangu, vipi mnaendeleaje na maandalizi huko?”

    “Mambo yameharibika.”

    “Kuna nini? Hebu niambie mwanangu, acha kuniweka roho juu mimi na huu utu uzima.”

    “Baba amegundua kila kitu. Amejua mchezo wote. Amefahamu kuwa Laura siyo Mnyiramba. Hataki kusikia ndoa tena, amesema ataongozana na mimi hadi kijijini akanitafutie mke yeye mwenyewe!” Akasema Chris huku akilia.

    Kimya cha sekunde kadhaa kilipita. Mzee Ngeleja alibaki kimya huku sauti ya kilio cha Chris ikisikika kwenye simu. Baadaye mzee Ngeleja akaanza tena kuzungumza...

    “Mwanangu kwanza nataka kukuambia, ni afadhali jambo hilo limetokea!”

    “Afadhali? Kwa nini baba?”

    “Ingewasumbua sana baadaye!”

    “Kwa hiyo mzee uko tayari kuona ndoa yangu na Laura inayeyuka?”

    “Kwanza nataka kukutia moyo mwanangu. Hakuna ndoa inayoyeyuka hapo. Kwanza tayari ninyi ni wanandoa halali, maana mmefunga ya kimila. Hilo ondoa shaka kabisa.

    “Jingine ni kwamba, hilo ni jambo dogo sana ambalo lipo ndani ya uwezo wangu. Najua naweza kulishughulikia.”

    “Kivipi baba? Utafanyaje wakati wewe uko huko mbali?”

    “Kesho nakuja Dar, naomba uwe na amani. Kwa sasa jambo hili lifanye siri kabisa. Usimwambie hata Laura kama kuna kitu kama hicho kimetokea.”

    “Sawa baba.”

    “Ok! Siku njema, naomba uwe na amani.”

    “Ahsante.”

    Wakakata simu zao.

    Angalau sasa Chris alihisi amani moyoni mwake. Aliendea kunywa akiwa na matumaini ya ndoa yake kufungwa baada ya mzee Ngeleja kuahidi kumsaidia.

    ***

    Saa 10:00 alasiri, mzee Ngeleja akiwa ameongozana na mchungaji wa kanisa lililotarajiwa ndoa ya Laura na Chris kufungwa na mwenyeji wao Chris, walikuwa mbele ya geti la mzee Shila, Mbezi Beach.

    Kwa bahati nzuri, mzee Shila mwenyewe alikuwepo ndani. Chris aliwakaribisha na wote wakaingia hadi ndani. Sebuleni walimkuta mzee Shila amekaa na mkewe.

    Aliwakaribisha kwa hofu akiwa hajui ni akina nani na walichofuata nyumbani kwake. Kwa utulivu mkubwa, mzee Ngeleja aliketi, kisha mchungaji.

    “Karibuni jamani,” akasema mzee Shila akionesha wasiwasi kidogo.

    “Ahsante, nafurahi tumewakuta, tena wote kwa pamoja. Labda tujitambulishe, mimi naitwa mzee Ngeleja natokea Mwanza, ni baba mzazi wa Laura ambaye kwa wewe unamfahamu pia kwa jina la Njile, mchumba wake na Chris,” mzee Ngeleja akasema kisha akatulia kidogo.

    Mzee Shila akatoa macho, hakuweza kuzuia hasira yake.

    “Nimeongozana na mchungaji Samatta, huyu tumempitia mimi na Chris kanisani wakati tunakuja hapa nyumbani,” akasema kwa hekima sana mzee Ngeleja.

    “Karibuni sana.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ahsante. Kikubwa ni kuhusu vijana wetu, nimetoka Mwanza kwa ajili ya jambo hilo. Nahitaji tuweke haya mambo sawa!” Akasema mzee Ngeleja.

    “Mchungaji nakuheshimu sana, mzee mwenzangu nakuheshimu pia, lakini sijaona mtu wa kubadilisha maamuzi yangu. Nilichoamua nimeamua,” akasema mzee Shila.

    “Lakini mume wangu...” akadakia mama Chris.

    “Kaa kimya! Wakati wanaume wanazungumza unatakiwa kufunga bakuli lako!” akasema mzee Shila kwa ukali.





    MAMA Chris alitulia. Alimjua vizuri sana mumewe na tabia zake. Ni wazi kuwa kama angeendelea kubishana naye, jambo lolote baya lingeweza kutokea, kitu ambacho hakukitaka kabisa.

    Mchungaji alimwangalia mzee Shila ambaye uso wake ulijaa makunyanzi kutokana na hasira iliyokuwa imemkolea. Ilikuwa lazima afanye kitu kwa ajili ya kijana Chris ambaye alikuwa na jambo jema tu la kutaka kuoa.



    “Mzee Shila, nakubaliana na wewe, lakini nakuomba usitumie maneno makali. Hebu tuzungumze kwa utaratibu ili tuone cha kufanya,” akasema Mchungaji kwa sauti ya kusihi sana.



    “Kuna kipi cha kujadili hapa Mchungaji?” akauliza mzee Shila kwa sauti ya chini kidogo.

    “Sababu hasa za kukataa kijana wako asimuoe huyo binti, maana maandiko yamefafanua wazi kuwa, mwanamke ataacha familia yake na kuungana na mwanaume, nao watakuwa mwili mmoja. Jambo ambalo vijana wetu wapo tayari kwa hilo.



    “Sasa inawezekana kama mzazi ukawa na mawazo mazuri tu au sababu zinazosababisha uzuie, ni vyema basi ukasema mzee Shila,” akasema Mchungaji.



    “Kikubwa ni kwamba nataka mwanangu aoe nyumbani kwetu, ndicho nilichomwagiza na alifanya hivyo lakini kumbe alikuwa ananidanganya. Amenifanya maigizo mimi. Mpaka ndoa ya kimila imeshafanyika nikijua ni binti wa nyumbani lakini kumbe haikuwa hivyo,” akasema mzee Shila kwa hasira.

    Mchungaji akatulia.



    Akamwangalia Chris, kisha akamtupia swali: “Anayosema mzee ni ya kweli?”

    “Ndiyo Mchungaji.”

    “Kwa nini umefanya hivyo?”



    “Nakiri makosa Mchungaji. Unajua kubwa ni kwamba mimi nilikutana na Laura Singida, nikampenda sana. Nikajaribu kumchunguza, nikagundua kuwa ana mapenzi ya kweli kwangu, ndiyo maana nikafanya yote hayo.



    “Najua nimekosea lakini namuomba baba anisamehe, ila namhakikishia kwa asilimia kubwa, mwanamke ambaye nataka kuoana naye ana tabia njema, anafaa kuwa mke wangu, hilo namhakikishia baba,” akasema Chris kwa sauti ya upole.“Labda mimi niongezee hapo kidogo,” akasema mzee Ngeleja baada



    ya ukimya wa muda mrefu.

    Wote wakamgeukia.

    “Binti yangu alikuja nyumbani na kuzungumza na mama yake kuhusiana na suala hili. Mke wangu alikataa kabisa. Alikataa binti yake asiolewe na Chris kwa sababu ni msanii wa filamu.



    “Alisema wasanii wote ni wahuni, hawana tabia nzuri na hawezi kuwa mwaminifu kwenye ndoa. Mwanangu alishindwa kulala siku hiyo, maana alizungumza na mama usiku usiku akiwa ameingia tu kutokea chuoni Singida.



    “Baadaye alifikia uamuzi wa kuja ofisini kwangu kuzungumza nami kuhusu jambo hilo. Nilimsikiliza, hoja za mama yake sikuzidharau lakini kama mzazi nilitakiwa kufanya uchunguzi.

    “Nilichofanya, nilimwagiza Laura amwambie Chris aje Mwanza aonane na mimi. Kweli akaja. Nikazungumza naye na kumwuliza maswali. Niseme ukweli, kama mzazi ambaye nimemlea mwanangu kwa maadili, nilivutiwa na Chris.



    “Mawazo ya mama yake nikaona hayakuwa na uchunguzi. Nilikubaliana na Chris, akaondoka akiwa hajui kama kuna jambo lolote lililotokea. Nilipofika nyumbani nikazungumza na mwenzangu na nilimweleza yote hayo bila kumficha.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Alinielewa lakini baada ya mvutano wa muda mrefu sana. Hata hili lilipotokea huku Dar, Chris alinishirikisha na niliamua kuja ili nizungumze na mzee mwenzangu tuweke haya mambo sawa.



    “Nashauri, tuwaache hawa watoto waoane. Tuwape baraka zetu kama wazazi. Wanapendana kwa dhati na nakuhakikishia mzee mwenzangu, binti yangu nimemlea kwa malezi bora,” akasema mzee Ngeleja.

    Ukimya ukatanda!



    Mzee Shila akavuta pumzi ndefu sana, kisha akazishusha taratibu kabisa. Akamwangalia mwanaye... ni wazi kuwa kuna kitu alitaka kuzungumza...

    “Ni kweli ulikwenda Mwanza kuonana na huyu mzee?”

    “Ndiyo baba.”



    Maneno ya mzee Ngeleja yalimwingia sana. Alionekana dhahiri kutaka kukubaliana naye. Mzee Ngeleja alizungumza maneno ya msingi sana. Ghafla mzee Shila alisimama, akasogea alipokuwa amekaa mwanaye Chris.



    Akamwonyesha ishara kuwa asimame. Chris akasimama. Akamvutia kwake na kumkumbatia.

    “Mwanangu nimekubaliana na wewe, tuachane na yote yaliyopita...” akasema mzee Shila.

    Mama Chris akasimama, mzee Ngeleja akafuata, wote wakaunda duara dogo na kushikana mikono. Mchungaji akaanza maombi!

    Kikao kikaisha!

    ***

    Mazungumzo yaliyofuata yalikuwa ya kifamilia zaidi yaliyojaa upendo. Mzee Ngeleja alikaribishwa rasmi nyumbani na alipewa heshima zote. Alikaa hapo hadi jioni kabisa, wakizungumza mipango mbalimbali ya ndoa ya Laura na Chris.



    Usiku, Chris ndiye aliyempeleka mzee Ngeleja uwanja wa ndege kwa safari ya kurudi nyumbani kwake Mwanza. Ilikuwa furaha kubwa sana kwa Chris.

    ***

    Ilikuwa kama ndoto lakini ndivyo ilivyokuwa. Chris alikuwa na Laura mbele ya Kanisa la KKKT, Azania Front akifunga ndoa na mwanamke aliyempenda kutoka moyoni mwake.



    Kanisa lilikuwa limejaa, wazazi, ndugu, jamaa na wasanii wakubwa wa Bongo Movies kama Jaybee, Ramsey, Thaiyway na wengine wengi.



    Mchungaji Massawe alianza kwa kumwuliza Chris: “Christopher Joseph Shila, upo tayari kuoana na huyu Laura John Ngeleja awe mke wako, ushirikiane naye katika shida na raha, hadi kifo kiwatenganishe? Kama ndivyo, sema ndiyo Mungu anisaidie.”

    Chris hakujibu kitu!



    HISIA kali ilimshika Chris. Ni kama alikuwa kwenye ndoto ya kusisimua. Hakuamini kama ni yeye alikuwa mbele ya kanisa akiwa amevaa suti kali nyeusi na shati jeupe huku shingoni akiwa amevaa tai fupi nyekundu!

    Laura alitingisha! Alivaa gauni jeupe na shela iliyoburuzika hadi chini. Furaha ikamfanya asahau kuwa yupo kanisani na alitakiwa kujibu swali la Mchungaji ili kukamilisha uhalali wa ndoa yao.

    Kanisa zima lilikuwa kimya. Wengine walianza kuogopa, wakahisi huenda Chris aliamua kubadilisha mawazo. Kwamba aliamua kuachana na suala la ndoa na Laura.

    Haikuwa hivyo.

    Chris alimpenda sana Laura, alichanganywa na tukio lililokuwa mbele yake ambalo lilikuwa kama sinema ya kusisimua.

    “Christopher...” Mchungaji akaita.

    “Naam!”

    “Hujaona sehemu ya kusoma kijana wangu?” akauliza Mchungaji.

    “Nimeona.”

    “Sawa, nami nitakuuliza tena: “Christopher Joseph Shila, upo tayari kuoana na huyu Laura John Ngeleja awe mke wako, ushirikiane naye katika shida na raha, hadi kifo kiwatenganishe? Kama ndivyo, sema ndiyo Mungu anisaidie.”

    “Ndiyo Mungu anisaidie,” akajibu Chris.

    Ukumbi mzima ukalipuka kwa shangwe na nderemo. Matarumbeta nayo hayakuwa nyuma, yalisikika yakipulizwa na hivyo kuamsha shangwe ukumbini humo.

    Mchungaji akamgeukia Laura kisha akamwuliza: “Laura John Ngeleja, upo tayari kuoana na huyu Christopher Joseph Shila awe mume wako, ushirikiane naye katika shida na raha, hadi kifo kiwatenganishe? Kama ndivyo, sema ndiyo Mungu anisaidie.”

    “Ndiyo Mungu anisaidie,” akajibu Laura.

    Kelele zikazidi kuwa kubwa, kanisa zima lilishangilia. Ilikuwa furaha kwa wote. Zoezi lililofuata baada ya hapo ilikuwa ni kuvalishana pete.

    Ndoa ikawa imefungwa!

    Chris na Laura wakawa mume na mke rasmi.

    ***CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Sherehe ilikuwa katika Ukumbi wa Mlimani City. Hiyo ilikuwa ni baada ya maharusi na ndugu wengine kuzunguka sehemu mbalimbali za jiji na kupiga picha.

    Waandishi wa habari walikuwa mstari wa mbele kuhakikisha wanapata picha nzuri za kupamba magazeti yao. Chris kuoa ilikuwa habari kubwa sana kwa magazeti Pendwa Bongo.

    Waandishi na wapigapicha maarufu, Issa Mnally, Richard Bukos na Shakoor Jongo walikuwa wanashindana kutafuta picha bora zaidi ambayo ingependekezwa kutokea kwenye ukurasa wa mbele wa Gazeti la Ijumaa Wikienda siku ya Jumatatu.

    Achana na hao, wapigapicha wa magazeti mengine ya kila siku na michezo walipigana vikumbo kupata picha nzuri. Msanii wa Bongo Muvi kuoa halikuwa jambo dogo!

    Ndani ya Ukumbi wa Mlimani City, wasanii walikuwa wengi sana. Walialikwa watu maalum tu. Viongozi kadhaa wa kiserikali walikuwemo, wabunge, mawaziri, wakuu wa wilaya na madaktari.

    Ilikuwa sherehe yenye heshima kubwa sana. Chris alijisikia mwanaume kamili kati ya wanaume. Wapambe wao walikuwa ni wasanii wa filamu, Jaybee na mkewe Vanessa.

    MC wa shughuli hiyo alikuwa ni Chika, ambaye siku zote amekuwa akiongoza hafla mbalimbali za wasanii na watu wengine. Kwa Chris ilikuwa siku mpya ya kipekee ambayo ilikamilisha haja ya moyo wake.

    Wenye kunywa walikunywa sana. Chakula kililiwa hadi kikabaki. Fungakazi ilikuwa zawadi, watu walitoa zawadi nyingi sana, achilia mbali wazazi wa pande zote ambao waliwazidi wote.

    Alianza mzee Shila: “Umefanya kitu kikubwa sana mwanangu. Leo umenifanya nijisikie baba yako kamili. Nakupenda sana mwanangu. Kuhusu namna ya kuishi na mwenzako tumeshazungumza mengi, najua umeyashika.

    “Kuna kitu ambacho nataka kukisema mbele ya watu wote hapa. Kwa tendo hili, nasema kwamba nimebadili fikra zangu. Nilichukia sana mwanangu kutokuoa mapema, lakini sikutaka kusikia anaoa mjini.

    “Akilini mwangu niliamini wasanii wote ni wahuni, wana tabia mbaya na ni watu wasiofaa kwenye jamii. Kumbe nilikuwa nawaza tofauti. Nikadhani mke sahihi lazima atokee kijijini, kumbe siyo kweli.

    “Leo hii mwanangu amepata mke mwema, sahihi na mzuri ambaye atamsaidia kama vitabu vinavyosema. Ninawabariki wanangu, mkaishi kwa amani na upendo. Kuanzia sasa, sina kinyongo na kazi ya mwanangu Chris. Pamoja na kwamba nilikulazimisha kusomea udaktari, nashukuru unaifanya kazi hiyo vizuri.

    “Unasaidia kuokoa maisha ya Watanzania wengi kupitia taaluma yako. Wakati ukifanya yote hayo, bado pia unafanya sanaa kama sehemu ya kipato na fani uliyoichagua na kuipenda.

    Kuhusu zawadi, najua una gari la kutembelea, lakini mimi nimekununulia jingine, litakalofanana na hadhi yako ya ubaba, maana sasa umekuwa baba. Nimekununulia Toyota Range Rover, iko hapo nje. Funguo zake hizi hapa,” akasema mzee Shila na kwenda kumkabidhi.

    Shangwe zikaibuka upya!

    Chris alipokea funguo za gari, kisha akanyanyua mkono juu na kuwaonyesha wageni ukumbini. Ghafla akagonganisha macho na mtu ambaye hakutarajia kabisa kumuona!

    Chris alishtuka sana!



    MSHTUKO ulikuwa mkubwa kwa hakika, kumuona mtu yule ambaye pia hakumwalika na alikuwa na uhakika kuwa Laura naye hakumwalika, kulimchanganya sana.

    Akajitahidi kujikaza. Akaweka zile funguo za gari alizokabidhiwa na baba yake mfukoni. Baba yake akarudi kwenda kukaa sehemu yake. Chris alipomwangalia Laura akagundua kuwa, naye alikuwa amemuoana yule mtu.

    Alikuwa ni Julius.

    Jully, yule mwanafunzi aliyekuwa akisoma na Laura chuo Singida. Ni Jully ndiye aliyesaidia kuwaunganisha. Kwa maneno mengine kama si yeye, usiku ule pale club, kulikuwa na uwezekano mkubwa kwa Chris kumkosa kabisa Laura.

    Zoezi la zawadi likaendelea ambapo Mzee Ngeleja alitangaza kutoa ekari 50 za mashamba ya mpunga, yaliyopo Mbarali, Mbeya. Ilipofika zamu ya wageni waalikwa, Jully naye alikwenda.

    Alitoa bahasha ya kaki kwenye sehemu ya kuwekea zawadi kisha akamsogelea Chris na kumpatia karatasi ndogo.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hongera sana kaka, usijiulize ningekujaje hapa, ila naomba unitafute baada ya fungate, namba zangu zipo humu kwenye karatasi, kuna jambo lazima nikuambie.”

    “Poa.”

    Akatoka hapo na kwenda kwa Laura. Akamkumbatia na kumpongeza.

    ***

    Tayari mipango yote ya fungate ilikuwa imefanyika. Wazazi wa bwana na bibi harusi waliamua kuchangia fedha kwa ajili ya safari ya watoto wao.

    Ulikuwa muunganiko mzuri sana wa familia hizo mbili. Wazazi waliwataka watoto wao wachague kisiwa chochote duniani, waende wakastarehe kwa wiki mbili katika kufurahia ndoa yao mpya.

    Kitu cha kushangaza ni kwamba, wote kwa pamoja walikubaliana kwenda Zanzibar. Wazazi walishangaa.

    “Kwa nini Zanzibar?” Mzee Ngeleja aliuliza.

    “Kwanza ni hapahapa Tanzania, tunapenda kufanya utalii wa ndani baba. Lakini pia tuna mambo mengi sana ya kufanya kama wanandoa, hatutaki kwenda mbali wala kutumia muda mrefu kwa ajili ya fungate.

    “Wiki moja itatosha sana mjini Zanzibar kwa mapumziko ya fungate yetu, wiki nyingine tutakwenda Singida, halafu tutarudi Dar kuendelea na mambo mengine.”

    Hakuna aliyepinga, Mzee Ngeleja na Mzee Shila wakakubaliana kwa pamoja na watoto wao. Walilala The Atriums Hotel iliyopo Sinza–Afrika Sana ambapo asubuhi ya saa 4:00 waliondoka hadi uwanja wa ndege walipopanda ndege na kuelekea visiwani Zanzibar.

    ***

    Wakiwa wamejipumzisha kwenye bustani ndani ya Hoteli ya Karafuu mjini Unguja wakicheza michezo ya kimapenzi, Chris akamkumbuka Jully.

    “Mh! Lakini Jully anaonekana ana jambo muhimu la kuniambia, lakini sijajua ni nini. Ngoja nikachukue ile namba yake ya simu ndani,” akasema Chris.

    “Hapana dear, ngoja nikachukue. Umeweka wapi?”

    Chris akamwelekeza.

    Laura akanyanyuka na kwenda ndani, baadaye aliporejea alikuwa na karatasi yenye namba ya simu, akampa mumewe. Chris palepale akampigia Jully.

    “Kaka ulisema nikutafute baada ya fungate lakini naona kama nachelewa sana kujua, ndiyo maana nimekutafuta mapema,” akasema Chris mara baada ya Jully kupokea simu.

    “Usijali kaka, uko wapi?”

    “Zanzibar, tunaweza kuzungumza sasa?”

    “Siyo ya kwenye simu kaka, halafu napenda nikizungumza uwe na Laura.”

    “Njoo Zanzibar basi, kila kitu nitagharamia mimi.”

    “Kweli?”

    “Ndiyo, tena ikiwezekana leo. Sema nifanye mpango wa ndege ya jioni mara moja.”

    “Nakubaliana na wewe.”

    Ndivyo ilivyokuwa, mipango ikafanyika vyema, jioni yake Jully aliingia Zanzibar. Aliungana nao kwenye hoteli ileile waliyofikia. Jioni wakiwa wanapata chakula, Jully akaanzisha mazungumzo...

    “Kwanza hongereni kwa kufanikisha kufunga ndoa. Nataka kuwahakikishia kuwa, kila mmoja ni muhimu na maalum kwa mwenzake. Muishi kwa upendo, amani na kusikilizana.

    “Pia nimefurahi kwamba, mimi ni mtu pekee mliyeniamini na kunipa heshima ya kuwatembelea hadi kwenye fungate yenu, ahsanteni sana ndugu zangu,” akaanza kusema Jully.

    “Usijali kaka, tupo pamoja. Wewe ni mtu muhimu, maana bila wewe ilikuwa vigumu sana kumpata Laura.”

    “Ni kweli. Ila kuna jambo ambalo lazima niliseme kwa ukweli wa moyo wangu, maana nisipofanya hivyo nitabaki na mateso makubwa sana moyoni. Hiyo ndiyo sababu iliyonifanya nifunge safari kutoka Moshi hadi Dar kufuatilia kuhusu harusi yenu na hatimaye nikahudhuria.

    “Kuna jambo nimewafanyia, siyo zuri. Siyo la kiungwana hata kidogo, nataka kuwa mkweli kwenu, lakini nawaomba kabla sijaanza kusema, mkubali kunisamehe kwa nilichowafanyia kwanza,” akasema Jully, sasa akianza kutokwa machozi.

    Wote wakamshangaa.

    Jully akamgeukia Laura, akamwambia: “Laura tafadhali naomba unisamehe!”

    Laura hakumjibu, akamgeukia mumewe na kumwangalia kwa makini, akamwonesha ishara kuwa, akubali kumsamehe ili wamsikilize mpaka mwisho.

    Laura akatingisha kichwa.

    “Ahsante. Je, Chris nawe utanisamehe?” Akauliza Jully.



    “ENDELEA tu Jully, tupo hapa kwa ajili yako.”

    Moyoni Chris alikuwa na mzigo wa mawazo lakini ilikuwa lazima ajue ni kitu gani alichotaka kusema Jully.

    “Nashukuru sana. Sasa nipo radhi kuzungumza... mnakumbuka kuhusu ishu ya polisi Singida?” akauliza Jully.

    Wote wakaonekana kuvuta kumbukumbu vizuri, hakuna aliyekumbuka haraka kuhusu jambo hilo.

    “Sikia Jully, maadam umekubali kusema na umeshasema tukusamehe, sisi tupo tayari, huna sababu ya kutuchengesha tena. Sema ni nini?” akauliza Chris akiwa hajulikani kuwa alipandisha midadi tu au alikuwa amekasirika.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ni kweli. Kumbuka kuwa, ulifuatwa gesti uliyofikia Singida ukaambiwa kuwa unatembea na mke wa polisi, tena mkuu wa kituo, umeshakumbuka?” akauliza Jully.

    “Ni kweli, nimekumbuka.”

    “Mimi ndiyo nilihusika na mchezo wote ule,” akasema Jully kwa kujiamini.

    Muda huohuo Jully akapiga magoti chini huku akilia...

    “Nilifanya vile kwa tamaa tu. Nilitaka kutengeneza mchezo ili nipate fedha, lakini ikashindikana. Ni jambo linaloniumiza sana moyo wangu.

    Ningeweza kukaa na hili jambo moyoni, lakini linaniumiza na kunitesa. Pamoja na kwamba tamaa yangu ilikuwa kwenye fedha tu, kumbe ningeharibu jambo zuri la ndoa ambalo mmeshalitimiza.

    “Naombeni sana mnisamehe ili nafsi yangu iweze kutulia. Nina maumivu makali sana ndani ya mtima wangu. Msiponisamehe kwa kweli sitaweza kuishi nikiwa na amani moyoni mwangu. Naombeni tena kwa mara nyingine mnisamehe,” akasema Jully akiwa bado amepiga magoti chini.

    “Simama Jully,” akasema Chris lakini ghafla, Laura akadakia:

    “Jully naomba uondoke. Sikutegemea kama ungenifanyia ujinga wa namna hii? Yaani kukuamini kote kule kumbe wewe ndiye uliyetaka kunikwamisha? Ondoka tafadhali,” akasema Laura kwa hasira ya wazi kabisa.

    “No! No! No! Laura...usifanye hivyo, tunapaswa kushukuru kwa kuwa ameamua kuwa wazi kwetu, mwache, mwache tafadhali,” akasema Chris.

    “Baby huyu hafai. Kwa nini unamtetea? Vipi kama leo hii tusingekuwa tumeoana kwa ajili yake?” akasema Laura.

    “Hapana...huyu ni mtu mwema, angekuwa mbaya asingetafuta msamaha. Anayetafuta msamaha maana yake ameelewa alipokosea!” akasema Chris.

    Laura alionekana kuanza kuelewa. Akatulia na kumuacha Jully aendelee kuzungumza. Mwisho hakuna aliyeona sababu ya kutomsamehe.

    “Jully sisi tumekusamehe kutoka ndani, tunaamini ni shetani tu alikupitia. Kikubwa kwa sababu umekiri kosa na tunashukuru Mungu tumefanikiwa kufunga ndoa yetu. Hayo mengine yameshapita, tuache kama yalivyo, sasa tuangalie yanayofauata.

    “Baby tuna mambo mengi muhimu ya kufanya kwa ajili ya ndoa yetu,” akasema Chris akimvutia Laura kwake.

    Laura akaenda mzimamzima!

    Akajitupa kifuani mwa Chris na kutulia hapo, ni kama hawakumuona Jully aliyekuwa mbele yao. Mabusu yalitembea, wakabembelezana mpaka Laura alipotulia kabisa.

    “Usijali dear, yameshaisha sawa mama?”

    “Nimekuelewa mpenzi.”

    Jully alilipiwa chumba hotelini hapo, siku iliyofuata akasindikizwa hadi uwanja wa ndege, akaondoka kwenda Dar es Salaam, kabla ya kuunganisha katika ndege nyingine hadi Kilimanjaro.

    ***

    Chumba kilikuwa cha kuvutia sana, hali ya hewa ilikuwa tulivu sana chumbani. Manukato mepesi yalikuwa yamesambaa na kufanya harufu ya chumba hicho kuwa yenye kuvutia sana.

    Laura alionekana mwanamke mpya kabisa mbele ya Chris. Alimwangalia mke wake, akatabasamu. Alikuwa anang’aa. Akamvutia kwake, Laura akatabasamu!

    “Mke wangu mpenzi, nakupenda sana. Sitajuta kuwa na wewe daima.”

    “Ahsante mume wangu mpenzi, nami nakupenda pia. Wewe ndiye unayekamilisha ndoto zangu. nakupenda sana,” akasema Laura akionyesha kuzidiwa na hisia kali za mahaba.

    “Kuna kitu muhimu nataka kukuambia mpenzi,” akasema Chris.

    “Niambie baba, ni nini?”

    “Unakumbuka nilichokuambia wakati tunakutana Singida?”

    “Tuliongea mengi sana baba.”

    “Kubwa zaidi.”

    “Mh! Sikumbuki.”

    “Wewe ni Movie Star.”

    “Mh! Kweli dear?”

    “Excactilly! Tena tunatakiwa kuingia location haraka sana kuanza sinema yetu. Tunaanza mazoezi Singida wiki ijayo.”

    “Tayari unayo stori mpenzi?”

    “Haya maisha yetu tu, yanatosha kuwa stori. Ni kisa cha aina yake mpenzi. Nitaanza kuandika script kesho, keshokutwa twende Singida tukamalizie honeymoon, huko tutakuwa kambini kabisa.

    “Nataka nikufue kwa wiki mbili nzima, baada ya hapo tutakwenda Dar kuchukua wasanii wengine kisha tutarudi tena Singida kuanza kurekodi.”

    “Unalo jina la filamu tayari?”

    “Singidani.”

    Wote wakacheka.

    Laura akamrukia Chris. Bila kupoteza muda, Chris alimtupia kitandani, kisha akazima taa. Kazi ya kutafuta mtoto wa kwanza, ikaanza!

    ***CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Oke! Kaa tayari...action!” akasema Chris akimwangalia Laura wakati akimfanyisha mazoezi ya uigizaji.

    Alikuwa akimfundisha kucheza na hisia na kuvaa uhusika. Hapo walikuwa katika Hoteli ya Katala Beach ‘KBH’ iliyokuwa katika ufukwe wa Singidani mjini Singida.

    Kama mzaha, lakini kumbe Laura alikuwa na kipaji cha kuigiza kilichojificha. Walifurahia maisha hotelini hapo, kisha wakarudi Dar kupanga watu wa kuigiza katika Filamu ya Singidani.

    Ilikuwa sinema yenye wahusika wakubwa wanne; Dk. Chris, Ramsey, Rose Ndauka na Wema Sepetu. Mastaa hao na wasanii wengine walikaa kambini mwezi mzima wakirekodi.

    Laura sasa akawa staa wa filamu za Kibongo. Kazi ambayo ilimpa jina, heshima na mume bora.



    Mwisho.



0 comments:

Post a Comment

Blog