Search This Blog

Thursday, July 21, 2022

SINGIDANI - 1

 





    IMEANDIKWA NA : GLOBAL PUBLISHER



    *********************************************************************************



    Simulizi : Singidani

    Sehemu Ya Kwanza (1)



    CHRIS hakuweza kuvumilia zaidi, akatembea kwa haraka akitetemeka miguu. Alipowafikia akasimama na kuwaangalia kwa kuwakazia macho. Si Davis wala Pamela walioshtuka.

    Ni kama hawakuona chochote wala yeyote. Wakaendelea na shughuli zao. Muda huohuo, kwa ghafla sana, Chris akasikia kibao cha nguvu mgongoni mwake...

    “Nani?” akasema akipaza sauti.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Cut...” Director Mushi akasema akiwaamrisha wasitishe kuigiza.

    Chris akiwa amefura akageuza uso wake. Hamad! Alikutana na uso wa baba yake mzazi ukiwa umekunjamana!

    Mzee Joseph Shila.

    “Kweli unaweza kuzaa watoto lakini si wote watakuwa watoto bora. Daktari mzima, tena niliyepoteza mamilioni yangu kukusomesha nje ya nchi, unakaa na hawa wajinga wamevaa vichupi mnaigiza?

    “Hivi Christopher mwanangu utakua lini wewe? Lini utakuwa mtu mzima na kuelewa ninayokuambia? Pumbaaf, endelea na ujinga wako,” akasema mzee Shila kisha akaondoka zake.

    Chris akabaki ameduwaa.

    Mushi alibaki anashangaa tu asijue cha kufanya. Neno moja likamponyoka kwa haraka: “What is going on Chris?”

    Chris hakujibu.

    “Kwa nini tunaharibiana kazi? Hivi kweli scene moja inaweza kutuchukulia siku nzima? Jana ulisema unaumwa kichwa, leo umechelewa location ukasema ulikuwa kwenye upasuaji, baadaye tena sijui unamwita mtu aje kutuharibia kazi ili iweje?

    “Kama unaona hutaki kufanya hii sinema si uache kaka? Unadhani wewe ni staa sana siyo? Ni bora kufanya kazi na chipukizi wenye nidhamu kuliko kuhangaika na nyie mastaa mnaotusumbua vichwa kila siku,” akasema Mushi kwa hasira.

    Scene hiyo ilimsumbua sana kutokana na ugumu wake...tena siku hiyo walipatia kwa kiasi kikubwa sana kuvaa uhalisia katika kiwango cha juu. Kosa la mzee Shila lilimuumiza sana, maana liliwatoa wasanii katika mwendelezo mzuri wa kuvutia.

    “Samahani kaka, unanifikiria vibaya. Yule ni baba yangu.”

    “Baba yako?” akauliza Mushi kwa sauti ya upole.

    “Ndiyo...ni baba yangu.”

    “Imekuwaje?”

    “Ni habari ndefu.”

    “Samahani sana kaka.”

    “Usijali.”

    “Upo kwenye mood nzuri na tunaweza kuendelea?” akauliza Mushi.

    “Bila shaka.”

    “Kweli?”

    “Nitajitahidi...”

    “Sawa...usijali, tutaendelea palepale...kaeni tayari...kamera upo sawa? Boom please...light...Ok! Action...” akasema Mushi.

    “Pamela!!!” neno hilo likamtoka Chris huku machozi yakimiminika kwa kasi sana.

    Ilikuwa sauti iliyojaa huzuni na kitetemeshi cha hali ya juu. Kweli alivaa uhusika sawasawa. Ni kweli, tukio lile alitakiwa kutoa machozi, alipaswa kuonyesha huzuni kama alivyofanya.

    Hakuna aliyejua ila ukweli ni kwamba alifanikiwa zaidi kutokana na machungu ya kero za mzee wake na si kwa sababu ya tukio lililokuwa ndani ya scene ile.

    ***

    Mzigo mzito ulimjaa Chris kichwani. Mwanamke yule mrembo aliuteka mtima wake. Alikuwa mweusi, mrefu wa wastani mwenye umbo namba nane. Alisuka nywele zake katika mtindo wa rasta nene.

    Alivaa sketi fupi ya khaki, iliyofanya miguu yake ya bia ionekane vizuri zaidi. Chris akasahau mawazo yote, akatembea hadi kwenye mlango wa kuingilia chooni na kusimama hapo.

    Dakika mbili baadaye yule mrembo alitoka msalani na kumpita Chris pale alipokuwa amesimama. Yule msichana alimwangalia Chris ambaye alijitahidi kutabasamu lakini hakuonyesha kama alimuona! Akapita na hamsini zake. Chris akakasirika!

    Na umaarufu wote huo?

    Tanzania nzima ilimfahamu kutokana na umaarufu wake kwenye filamu za Kibongo. Mara zote amekuwa mstaarabu na kamwe huwa hatumii umaarufu wake kuwapata wasichana lakini safari hii alitamani sana kutumia silaha hiyo.

    Jambo la kusikitisha ni kwamba, silaha hiyo ni kama ilikuwa butu au haiwezi kabisa kutumika. Pengine ingeweza kutumika na ilikuwa na nguvu mujarabu lakini siyo kwa msichana yule!



    MARA kadhaa watu walikuwa wakimwangalia na kumnyooshea vidole wakisemezana ndani ya ukumbi huo. Wengine walimfuata na kumsalimia huku wengine wakitaka hata kupiga naye picha tu.

    Kwa msichana huyu ni tofauti. Hana muda naye kabisa. Pengine silaha ya kwanza haikuwa na nguvu au msichana yule si mpenzi wa filamu kwa hiyo hamfahamu.

    Labda! CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Bado alikuwa na silaha nyingine. Mavazi ya gharama aliyokuwa amevaa yalikuwa ni silaha kwa msichana yeyote wa mjini. Chris alikuwa amependeza sana. Alivaa kawaida tu, lakini alipendeza vilivyo.

    Silaha hiyo nayo imeshindikana!

    Chris akabaki akimsindikiza kwa macho mpaka alipoishilia. Akaanza kupiga hatua za taratibu kurudi alipokuwa amekaa awali. Lengo likiwa ni kuendelea na mawazo yake yaleyale!

    ***

    Macho ya Chris ni kama yalizingirwa na ukungu. Akaamua kuyapekecha kidogo ili kuuondoa ili aweze kuangalia vizuri. Kweli kabisa...alichokiona ni sahihi.

    Ni yule msichana alikuwa anacheza na kundi la vijana watano. Wale vijana walikuwa wamemzunguka, yeye akawa katikati yao. Kuna wakati, walianza kuingia katikati mmojammoja na kucheza na yule mrembo kwa zamu.

    Lilikuwa onesho la bure lililovutia ambalo lilisababisha wengine waache kucheza, wabaki kuwaangalia wao. Chris akafura!

    “Yaani wale watoto ndiyo wanaweza kushindana na mimi? Haiwezekani. Mimi ni mtoto wa mjini...” akawaza Chris akiinuka kusogea karibu na lile duara la vijana watano wakicheza na msichana yule mrembo!

    Yule anayeusumbua moyo wake.

    Mtikisiko wa moyo ulimvaa Chris. Hasira zikamkaba rohoni. Aliumizwa na msichana yule mrembo ambaye alikataa hata kumsalimia tu wakati tayari alikuwa ameshaufanya moyo wake mateka. Hasira zake sasa zilihamia kwa wale vijana.

    Chris akajikaza na kusimama kisha akasogea karibu na wale vijana. Akatoa macho. Hata yeye alijishangaa ni kwa nini alikuwa na hasira kiasi kile.

    Yule msichana hakuwahi kumfahamu kabla na hakuwa mpenzi wake. Kwa nini achanganyikiwe? Labda ni mapenzi, lakini kwa nini awakasirikie watu wengine ambao hawafahamu?

    Alikiri moyoni mwake kwamba alifanya makosa.

    “Nakosea sasa...nadhani huu umaarufu wangu unataka kunidanganya. Natakiwa kuwa mpole kwanza...” akawaza.

    Kitu alichogundua kwa haraka ni kwamba alitakiwa kupata liwazo kidogo. Ingekuwa rahisi zaidi kuliwazwa na msichana yule lakini kwa sababu anajifanya anamkataa, Chris alikuwa na kitulizo kingine.

    Alichepuka haraka hadi kwenye kaunta ndogo ya pembeni katika ukumbi ule. Akamvaa msichana aliyekuwa akihudumia.

    “Nataka toti tatu za Grant’s haraka tafadhali,” akasema Chris akiweka noti moja ya elfu kumi mezani.

    “Kaka Chris hata salamu?” yule mrembo akamwambia.

    Chris akageuza uso, akakutana na msichana mrembo, mweupe, mrefu, mwenye macho makubwa ya kung’ara. Alijilaumu sana.

    “Wakati mwingine unaweza kupoteza cast hivihivi...huyu msichana anafaa kuigiza,” akawaza akitabasamu.

    “Habari yako dada yangu?”

    “Salama, sasa mambo si hayo? Kwani ulivyonisalimia umekufa?”

    Chris akacheka.

    “Wewe utakuwa unatoka katika makabila mawili tu ya hapa Singida, kama siyo Mnyaturu utakuwa Mnyisanzu.”

    “Mh! Wewe umejuaje? Mimi Mnyaturu.”

    “Umeona sasa! Nilisema tu, nimefurahi kuwa mtabiri mzuri,” alisema Chris huku akiondoka zake.

    Anarudi kulekule! Msichana hana jipya kwake, anamtaka yule ya mwanzo. Kadiri muda unavyozidi kwenda anazidi kuwaza tofauti. Si kwamba alimtaka msichana yule kwa usiku mmoja tu; aliwaza ndoa kabisa.

    Ilikuwa mapema sana kwake kuanza kuwaza mambo makubwa kama yale lakini ndicho kilichokuwa kichwani mwake. Potelea mbali, hata kama akigombana na baba yake mzee Shila, bora aishi na yule mrembo!

    “Nimeshajua cha kufanya!” akajisemea Chris akipiga funda moja dogo, akachanganya na mate, akameza.



    SASA alipata wazo jipya. Wazo ambalo kwa hakika lingeweza kumsaidia kumpata yule msichana. Alianza kumfuatilia kijana mmoja ambaye alionekana kama wangeweza kuelewana kidogo. Aliachana na wote, akabaki akimwangalia huyo tu. Mara yule kijana akajitoa pale na kutembea akielekea chumba maalum cha kuvutia sigara. Chris na glasi yake, akamfuata yule kijana.

    “Oyaa mambo vipi?” Chris akamsalimia.

    “Aaaaah! Mkubwa, bora nimekuona nitapona. Inakuwaje mwana?”

    “Salama.”

    “Umeingia lini Singapore?”

    “Jioni ya leo...samahani huu ni mguu wako lakini kama hutajali kachukue kwanza kinywaji. Unakunywa nini?”

    “Ngumu bro.”

    “Ngumu?”

    “Ndiyo.”

    “Unamaanisha nini?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kitu cha konya ndo mzuka.”

    “Sawa, kachukue kubwa na pakiti nzima ya fegi,” akasema Chris akimkabidhi noti mbili za elfu kumikumi.

    Yule jamaa akaondoka na dakika mbili tu baadaye alirudi akiwa na chupa kubwa ya pombe kali aina ya konya na pakiti ya sigara. Akamrudishia chenji Chris ambaye alimshika mkono na kumtoa katika kile chumba cha kuvutia sigara.

    “Vipi?”

    “Njoo huku.”

    Waliishia kwenye sofa kubwa ndani ya ukumbi ule, pembeni na meza ya Pool Table ambapo bila kupoteza muda, Chris alianza kumwuliza kuhusu yule msichana.

    “Nimewaona muda mrefu mkicheza na yule dada. Vipi unamfahamu vizuri?” akauliza Chris.

    “Tunasoma naye.”

    “Kati yenu pale kuna mtu wake?”

    “Mtu wa wapi? Yule msichana ni mwanafunzi mwenzetu tu, hakuna mwenye kisu kikali pale kaka. Yule demu ni mkali chuo kizima.”

    “Mnasoma chuo gani?”

    “Uhasibu.”

    “Oke! Sikia nikuambie mdogo wangu, yule mtoto mimi nimempenda..siyo kwamba nakuambia kwakuwa sijui kutongoza laah! Nataka tu unisaidie kunikutanisha naye, maana naona kama ananata fulani hivi...mambo mengine nitajua mwenyewe.”

    “Usiogope mwanajeshi wangu, hilo limepita.”

    “Kweli?”

    “Wewe sema unataka aje sasa hivi?”

    “Ndiyo...”

    “Nakuja naye.”

    “Sawa.”

    “Njoo kwanza....” Chris akamwita yule kijana ambapo mara moja alirudi.

    “Hujaniambia jina lako bado.”

    “Naitwa Julius.”

    “Poa.”

    Julius akaondoka. Kama mchezo hivi, dakika moja baadaye, alifika alipokuwa amekaa Chris akiwa amemshika mkono yule msichana. Akamkalisha kwenye sofa kubwa, akamuweka katikati. Pembeni wakamzunguka na Chris.

    “Huyu ni kaka yangu...anaitwa Chris. Nimesoma na mdogo wake JK Nyerere Sekondari, Moshi. Tunaheshimiana sana lakini nimechukizwa na tabia yako ya dharau kwake,” Julius akamwambia yule msichana huku akimkazia macho.

    Chris akashtuka.

    “Mbona huyu dogo anataka kuharibu sasa?” akawaza.

    “Nimemfanyaje?” yule msichana akauliza.

    “Hujui? Najua unanata na una dharau lakini kwani wewe humfahamu Chris? Utakuja kupoteza bahati bure wewe mtoto wa kike...si kila mwanaume ni mhuni,” akasema Julius kwa hasira.

    Pamoja na kwamba kile alichokuwa akikifanya ilikuwa ni maigizo tu ili kumuunganisha na Chris lakini pia pombe aliyokunywa ilikuwa inafanya kazi yake sawasawa.

    “Samahani bro Jully.”

    “Siyo mimi, wa kumuomba msamaha ni huyu hapa...mimi nawaacha, naamini utafanya hivyo.”

    Yule msichana akatingisha kichwa kukubaliana naye. Julius akasimama na kurudi zake ‘Smoking Room’.

    Yule msichana alitulia kwa muda, Chris bila kupoteza muda, akamsogelea kidogo. Naye akaanza kumwangalia kwa macho yanayozungumza. Chris alikuwa akifikisha ujumbe wake moja kwa moja.



    ILA kilichotokea ukumbini mle alihisi ni kama alikuwa ndotoni. Ukweli haukuwa huo, hakuwa anaota. Kila kitu kilikuwa yakinifu kwa hakika kabisa.

    Akaufaidi uzuri wa yule msichana kwa karibu kabisa. Moyoni alikuwa na furaha akijua kuwa angalau alikuwa akielekea kutimiza lengo lake. Kukaa naye pale pekee kulimpa matumaini mapya.

    “Samahani kaka Chris,” akasema yule msichana kwa sauti iliyojaa utulivu na unyenyekevu.

    “Achana na samahani...unaitwa nani mrembo?”

    “Naitwa Laura.”

    “Nice name...sikia...sitaki kukupotezea muda wako. Kikubwa ni kwamba nahitaji kuzungumza na wewe. Si hapa club na ujue kabisa ni mambo ya kazi,” akasema Chris kwa uhakika kabisa.

    Laura akatulia kwa muda.

    Muda huu sasa, Laura alipata nafasi nzuri ya kumwangalia Chris kwa ukaribu. Aliyafumbua macho yake makubwa yaliyozungushwa na wanja hafifu mweusi na kuyatuliza usoni mwa Chris.

    Kuna kitu kipya aligundua; Chris alikuwa mwanaume mwenye wivu na aibu kidogo. Ukimya na uso wake uliojaa bashasha ulizidi kumpa matumaini kuwa amekutana na mwanaume makini.

    “Umesema kazi?” akauliza haraka kama aliyegutuliwa mawazoni.

    “Ndiyo.”

    “Mimi nasoma.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Najua lakini unaweza kufanya kazi nje ya masomo yako.”

    “Mh! Kazi gani?”

    “Sanaa.”

    “Unamaanisha filamu?”

    “Ndiyo! Wewe ni msanii mkali sana, hujapata nafasi tu. Unaweza kuwapindua wasanii wote wanaotamba Bongo Movies sasa hivi. Niamini mimi. Unaweza sana ni kiasi cha kupewa nafasi na kuelekezwa kidogo sana, utakuwa mkali.”

    “Unataka tuzungumze lini?”

    “Leo, maana kesho nasafiri kwenda Mkalama.”

    “Mkalama ni wapi?”

    “Yaani hujui wilaya ambayo ipo katika mkoa unaoishi?”

    “Mimi ni mwanafunzi tu hapa, natokea Mwanza. Kule ndiyo kwetu. Niambie kuhusu Ilemela, Sengerema, Kwimba, Ukerewe, Magu, Nyamagana na Misungwi nitakuambia lakini hapa najua hapahapa mjini tu labda sana Ikungi na Manyoni.”

    Chris akacheka.

    “Haya mama, nimekuelewa vizuri sana. Namaanisha usiku huu.”

    “Tukazungumzie wapi sasa?”

    “Hotelini.”

    Laura akafura!

    Macho ya Laura ni kama yalijitokeza yote yalipojificha. Yalizidi kuwa makubwa na kuchambua kope zake zilizotingishika kwa kasi kutokana na kufumba macho na kufumbua mara kwa mara.

    Sura ya Laura ilionekana wazi kabisa kuchukizwa na maneno aliyoyasikia kutoka kwa Chris. Alimwangalia kwa dharau kidogo, akimchambua kuanzia chini hadi juu.

    “Chris kumbe uko hivyo?” akauliza Laura kwa hamaki.

    “Nikoje?”

    “Sikia nikuambie, mimi siyo malaya kama unavyonichukulia. Nimekuja club kwa pesa yangu na nitaondoka mwenyewe baadaye kwa muda wangu lakini huwezi kunipata kirahisi hivyo kwa sababu sijui ya pesa zako au kwa vile unajulikana. Mimi siyo wa hivyo. Umekosea njia!”

    “Unanifikiria vibaya Laura. Mimi si mwanaume wa namna hiyo. Tafadhali usinipe sifa ambayo si yangu. Naomba unielewe, lengo langu ni kazi tu, hakuna kitu kingine.

    “Inawezekana hujajua thamani ya kipaji ulichonacho au hakuna aliyewahi kukuambia kuwa kuna kitu kama hicho ndani yako. Lakini pia inawezekana umeathiriwa na tabia ya wanaume wengi, wakitaka kumsaidia mwanamke lazima wawe wapenzi kwanza...that’s not me!”

    “Sasa kwa nini unataka iwe hotelini?” Laura akamwuliza akimkazia macho.

    “Vizuri sana. Kwanza ni kwa sababu ndipo nilipofikia lakini pia kuna utulivu mkubwa zaidi ya hapa.”

    “Lakini mbona hata hapa tunaweza kwenda kuzungumzia nje?”

    “Laura tafadhali heshimu mawazo yangu na unatakiwa kujua kuwa utakuwa salama kwa kila kitu. Tafadhali naomba ukubali.”

    “Sawa tutakwenda kuzungumza hotelini lakini kwa masharti!” akasema Laura sasa kwa utulivu.

    “Paaaaaa!” moyo wa Chris ukapiga kwa nguvu.



    SHINDI ulianza kunukia. Kukubaliwa tu na msichana yule kwenda naye hotelini kwa mazunguzo ilikuwa sehemu ya ushindi. Potelea mbali kuhusu masharti aliyosema angempa, yasingemshinda!

    “Kwanza masharti yapi?” akajiuliza Chris.

    “Hana cha kunishinda huyu,” akazidi kuwaza.

    Tabasamu changa lilichanua usoni mwa Chris wakati akizidi kufaidi uzuri wa macho ya msichana yule wa kuvutia; Laura! Kama kungekuwa na mashindano ya kumsaka mwanamke mwenye mvuto hasa wa kike, Laura lazima angeshinda.

    Nini hana?

    Angalia miguu yake. Hebu mtazamo anavyozungumza kwa mpangilio mzuri. Ona nyusi zake, angalia kiuno. Mwone hata mikono yake laini, mizuri inayoshawishi.

    Laura ni mwanamke wa haja. Hana upungufu wowote kwa kumwangalia. Chris alivuta pumzi ndefu sana, kisha akazishusha taratibu. Akanyanyua glasi yake yenye pombe kali na kuipeleka kinywani.

    Ilikuwa kali lakini hakujali. Aliifuta yote, aliposhusha glasi chini, ilikuwa tupu! Laura akawa anaangalia sinema ya bure. Akaachia tabasamu changa la kupendeza.

    “Sawa kaka Chris?” Laura akauliza.

    “Bila shaka Lau.”

    “Mbona hujauliza kuhusu masharti?”

    “Sina shaka kabisa na masharti yako, najua nitayamudu tu.”

    “Unajua ni nini?”

    “Kwanza utanirudisha chuo...” akasema Laura kwa sauti ya kudeka.

    “Hilo limepitishwa bila kupingwa....lingine?”

    “Hatutafanya chochote.”

    “Wewe! Chochote lazima tufanye, maana tunakwenda kuzungumza.”

    “Mi’ sitaki!”

    “Hutaki?”

    “Ndiyo sitaki.”

    “Sasa mbona umekubali kwenda hotelini?”

    “Nimekubali kwa ajili ya mazungumzo tu.”

    “Sasa kwani hayo mazungumzo siyo chochote?” akauliza Chris.

    Sura ya Laura iliyokuwa imekunjamana sasa ikarudi kawaida kabisa. Tabasamu likaonekana. Uzuri wake ukazidi kuchanua.

    “Tuondoke zetu basi!” akasema Chris.

    “Poa, twende.”

    Waliongozana hadi nje, wakashikana mikono kama vile walikuwa wakifahamiana kabla. Laura alijishangaa sana kumzoea Chris kwa muda mfupi kiasi hicho.

    Macho ya watu wote yalikuwa kwao. Tatizo ni umaarufu wa Chris. Moja kwa moja hadi kwenye taksi. Wakaingia.

    “Wapi brother?”

    “Aqua Vitae Resort.”

    “Buku tano tu.”

    “Endesha gari kaka.”

    Dereva ni kama alikuwa amechanganyikiwa. Haraka akawasha gari na kuliondoa kwa kasi kuelekea Aqua Resort.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ***

    Chumba kilikuwa kikubwa, kizuri chenye hewa safi iliyochanganyika na manukato hafifu yasiyokera pua. Chris alikuwa amekaa kitandani na Laura kwenye sofa kubwa! Taa chumbani mle ilikuwa ya rangi hivyo kumfanya Laura azidi kuonekana katika mwonekano wa kuvutia zaidi.

    Kitanda kilikuwa kikubwa, chenye mito mikubwa minne iliyopangwa vizuri kitandani. Mashuka meupe nayo yalizidi kukifanya chumba kionekane nadhifu zaidi.

    Ni saa nane za usiku!

    “Karibu sana Laura,” akasema Chris.

    “Ahsante sana.”

    “Kikubwa nilichotaka kukuambia ni kwamba wewe ni mrembo sana na unaweza kufanya vizuri kwenye sanaa kama ukiwezeshwa na kupewa mwongozo mzuri. Nakuambia ukweli, kuna uwezekano mkubwa sana wa kumfunika hata Wema au Johari.

    “Niamini mimi, uwezo wako ni mkubwa sana Laura. Kubali nikusaidie tafadhali. Isitoshe nina sinema yangu mpya ambayo naiandaa, kuna sehemu ndani yake inahitaji sana msichana kama wewe. Nakuhakikikishia wewe ni staa na maisha yako yanaweza kubadilika ukitumia kipaji chako ipasavyo,” akasema Chris kwa sauti ya taratibu sana.

    Shoti ya umeme wa mapenzi ilimwingia moyoni. Ilikuwa nafasi kubwa na muhimu sana kwake. Hakutakiwa kufanya ajizi katika nafasi ile ya pekee. Msichana mrembo kama Laura kuingia chumbani kwake halafu aondoke hivihivi?

    “Kaka Chris, kweli mimi naweza kuwa msanii? Naweza kuwazidi hata mastaa?”

    “Kabisa...niamini mimi. Ni marekebisho madogomadogo tu.”

    Chris aliwaza kwa muda, alitakiwa kuwa na mbinu za kisasa ili aweze kumpata Laura. Lakini alijihakikishia moyoni kwamba alimpenda kwa dhati ya moyo wake. Kumpata kwa usiku ule tu halikuwa jambo muhimu kwake, alimtaka kwa maisha yake yote!

    “Lakini nikimkosa usiku huu, sitaeleweka. Anaweza kuniona sijakamilika,” akazidi kuwaza Chris.



    CHRIS aliinuka kitandani lakini akiwa tayari ameshainuka, akajishangaa maana hakujua aliinuka ili kufanya nini! Hakutaka kuonekana kama alikuwa hajui cha kufanya.

    Akamwangalia Laura kwa jicho lililojaa ubembe, kisha akamsogelea na kukaa kwenye sofa kubwa lililotosha kukaliwa na watu wawili tu, akapiga magoti chini yake.

    Bado hakujua alichotaka kumwambia. Bahati nzuri, Chris alikuwa na utajiri wa maneno kwa hiyo haikumpa shida sana. Laura akashangazwa na namna Chris alivyopiga magoti mbele yake.

    “Sikia nikuambie Laura. Mimi ni mwanaume wa tofauti sana. Mara zote nimekuwa mkweli na ninayeheshimu hisia zangu. Kila kinachotoka kinywani mwangu, huwa yakinifu kabisa,” akasema Chris, kisha akatulia kidogo.

    Ni kama alikuwa akifikiria jambo. Kichwani Laura akaanza kuona hisia za mapenzi kutoka kwa Chris kwenda kwake. Pamoja na kwamba alikuwa ameonja kidogo kilevi, hakuwa tayari kumpa Chris mwili wake kwa sababu tu ni staa wa filamu.

    Alifika pale hotelini kwa heshima tu. Alimwamini ghafla sana. Hakutegemea kama angetongozwa na hata kama angetongozwa, hakuwa tayari kujiachia kwa siku hiyohiyo!

    “Ameanza....nilijua tu. Wanaume bwana!” akawaza Laura.

    “Lakini hapati kitu hapa,” akawaza tena.

    Chris akaendelea: “Shika haya maneno yangu Laura. Nayaona maisha yako miaka miwili ijayo, jinsi utakavyokuwa staa na maisha yako yatakavyobadilika.

    “Acha nikutengeneze. Najua ninaweza kukufanya ukawa juu kuliko unavyowaza. Unacho kipaji kikubwa sana Laura.”

    Chris alikuwa akizungumza kwa hisia kali sana. Hata hivyo si kweli kwamba, Laura alikuwa na kipaji cha kuigiza – alikuwa mrembo! Hiyo ilikuwa gia tu ya kumwingiza kwenye kumi na nane zake.

    Laura aliachia tabasamu pana. Moyoni Chris akaugulia maumivu ya shoti ya mapenzi. Alizidi kuchanganyikiwa. Kila dakika, kila sekunde, uzuri wa Laura uliongezeka.

    Pamoja na kuelezwa yote hayo, Laura hakuzungumza chochote. Alibaki kimya tu akimwangalia Chris. Macho yao kuna wakati yaligongana na wote hawakuweza kuhimili kuangaliana japo kwa sekunde tano tu mfululizo.

    Tayari kuna kitu kilianza kuingia moyoni mwa Laura lakini hakukiamini sana. Eti ameanza kumpenda Chris!

    “Siyo kweli. Hizi si hisia zangu. Ni pombe tu,” akawaza.

    Ghafla Chris akasimama. Alifanya kitendo hicho kwa haraka sana kama aliyeamrishwa. Alirudi nyuma kidogo hadi alipofikia kitandani. Akachukua taulo kubwa pale kitandani kisha akalitupa begani mwake.

    “Samahani...” akasema Chris.

    “Ndiyo!”

    “Naingia bafuni kidogo.”

    “Sawa.”

    Chris akapiga hatua nyingine fupi, akaufikia mlango wa kuingia bafuni. Akashika kitasa na kukinyonga kidogo. Mlango ukafunguka. Mara moja akaingia, halafu akaufunga.

    Punde tu maji yalianza kusikika yakichuruzika. Chris alikuwa anaoga. Alipomaliza, alijikausha vizuri kisha akajifunga taulo yake kiunoni. Akabeba zile nguo zake na kutoka mle bafuni.

    Kwa Laura lilikuwa tukio la ajabu sana. Chris aliingia chumbani na taulo tu. Ajabu kubwa ni Chris kutoka na taulo lakini lingine ni mshangao wa mwili wa Chris.

    Kutoka moyoni, Laura alikiri kuvutiwa na mwonekano wa Chris. Taulo lilimfanya mwili wake uonekane kwa ukamilifu wake. Kifua cha mazoezi kilionekana dhahiri, huku tumbo lake likiwa limefunikwa na bustani nzuri ya kupendeza!

    Siku zote Laura amekuwa akichanganywa zaidi na miili ya wanaume wa namna hiyo. Shoti ya umeme wa mapenzi ikahamia kwa Laura. Bado alikiri kuwa hajampenda Chris lakini angalau kwa usiku ule angemfaa sana!

    “Oooooh! Kumbe yupo hivi? Hebu angalia jamani. Chris ananipa mateso sasa,” akawaza Laura alipomwangalia Chris tumbo lake.

    “Samahani kwa mara nyingine, sikujali kutoka na taulo kwa sababu najua hakuna tatizo. Wewe ni rafiki yangu. Au nimekosea?” Chris akasema.

    “Uko sawa.”

    Chris akafungua begi lake kisha akatoa bukta na tisheti, akarudi tena bafuni. Huko alivaa kisha akarudi tena chumbani. Mawazo yalimjaa Chris. Ni kweli alimtaka sana yule mrembo usiku ule lakini aliogopa angeweza kumkosa kama angemwambia mambo ya mapenzi mapema.

    Wazo lake kichwani alijua amepata mke, siyo demu wa kuzugia! Mwisho aliamua kuzishinda hisia zake ili aweze kutengeneza kitu chenye manufaa mengine makubwa zaidi mbele yake.

    Angejua!!!CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Laura yeye aliumizwa sana na mwili wa Chris. Alitamani sana asikie akimwambia angehitaji kuwa naye usiku ule. Ni kwa usiku ule tu! Laura hakuwa na chembe ya mapenzi ya kudumu na Chris.

    Hakuna aliyejua kilichokuwa moyoni mwa mwenzake.



    ILIKUWA hisia kali za mapenzi lakini kila mmoja alikuwa na hofu ya kumweleza mwenzake kwa hofu ya kuonekana malaya. Chris aliugulia akiwa bado amemkumbatia kwa nguvu akiendelea kuhisi joto zuri la kusisimua la Laura.

    Laura aliumia sana, hisia za mapenzi ziliwaka kama moto wa kifuu. Alitaka kusema chochote lakini yeye ni mwanamke; ingewezekanaje? Lilikuwa jambo gumu sana kwake.

    Ghafla, kwa msukumo wa hisia ambazo hazikuwa na majibu. Laura alijitoa kifuani mwa Chris. Akasimama hatua mbili kutoka kwa Chris.

    “Usiku mwema dada Laura!” Chris akasema kwa sauti ya chini.

    “Dada!” neno hilo likajirudia kichwani mwa Laura.

    Kuitwa dada pekee kulitosha kabisa kumfanya agundue kuwa, Chris hakuwa akimtaka. Bado moyoni mwake alisimamia jambo moja kubwa; hampendi Chris hata kidogo ila hisia za mapenzi za usiku ule pekee ndizo zilizokuwa zikimpelekesha puta!

    Akamwangalia Chris kwa makini, kisha akamwambia: “Hunitoi?”

    Lilikuwa swali la mtego sana. Kwa usiku ule, saa tisa kasoro za usiku ilikuwa vigumu kwa mtoto wa kike kutoka mwenyewe katika hoteli ile kubwa. Kutoka kwenye chumba walichokuwepo hadi kufika getini ilikuwa ni mwendo wa dakika tatu, kutokana ukubwa wa hoteli ile.

    “Nitakusindikiza usijali. Siyo kukusindikiza tu, nitahakikisha unafika salama.”

    “Unamaana unataka kunipeleka?”

    “Sina maana hiyo, nitamwita dereva akupeleke.”

    Wakatoka nje, Chris akafunga mlango na kuanza kutembea wakiwa wameshikana mikono. Wakiwa katikati ya safari yao kuelekea getini, Chris akatoa simu yake na kumpigia dereva wake aitwaye Maulanga. Akamwambia afike haraka sana Aqua Hotel usiku ule.

    Kwa kuwa bado alikuwa Skyway Club, ilikuwa rahisi sana, dakika kumi tu zilitosha kumfikisha Maulanga Aqua Hotel. Chris akamwambia Mulanga ahakikishe anamfikisha Laura anapoishi.

    “Mambo ya pesa hayo tufanye kesho lakini hakikisha anafika salama ndugu yangu.”

    “Sawa kaka.”

    Laura akamsogelea tena Chris ambaye alimvutia kwake. Akamkumbatia na kumbusu. Wakaagana. Akaingia kwenye gari na baada ya muda mfupi sana, Maulanga aliingiza gia namba moja.

    Gari likayoyoma!

    ***

    Kwa mbali Chris alijilaumu na kujiona mjinga kwa kumkosa Laura. Taratibu kila kilichotokea chumbani akiwa na mrembo yule, kikaanza kujirudia kichwani mwake.

    Kulikuwa na kila dalili za Laura kumwelewa somo lake lakini akajisahau na kuamua kuachana na jambo hilo.

    Chris aliumia sana. Hata hivyo alijipa moyo akiamini kwamba, lengo lake hasa halikuwa kumtumia kwa usiku mmoja, bali awe mke wa maisha yake yote.

    Jambo hilo ndilo lililompa moyo na kuamini kuwa, bado Laura angekuwa wake! Uchovu wa pombe, mawazo ya mapenzi na baridi kali ya Singida usiku huo, vilimfanya Chris asichukue muda mrefu kupata usingizi!

    Akapotelea usingizini.

    ***

    Aliamka akiwa mchovu sana, bado mning’inio wa ulevi uliendelea kumsumbua. Alijimwagia maji kisha akatoka na kwenda mgahawani kupata kifungua kinywa, akarudi tena chumbani kwake.

    Kwa kuwa alipanga kusafiri kwenda kijijini Mkalama siku iliyofuata, aliamua kuhama hoteli na kwenda Kibaoni, jirani na Stendi Kuu ya Mabasi ya Mikoani Singida, Misuna.

    Maulanga ndiye aliyemsaidia kupata hoteli nzuri iliyokuwa barabara kuu ya Dodoma – Mwanza. Akampigia Laura na kumwelekeza. Akaahidi kufika hapo saa kumi jioni.

    ***

    Laura hakuwa mwongo, alifika pale hotelini kama walivyokubaliana na Chris ingawa alichelewa kwa saa nzima mbele. Alimpigia Chris aliyemwelekeza hadi chumbani kwake.

    Akaingia.

    Mazungumzo ya hapa na pale yakaendelea, huku jambo kubwa lililotawala likiwa ni kumsaidia Laura ili aweze kuwa msanii mkubwa wa filamu za Kibongo.

    Mwisho Chris hakuweza kuvumilia. Mazoea ya muda mrefu yalimfanya amweleze ukweli Laura kuhusu maisha yake yote na lengo la safari yake kuelekea kijijini Mkalama.

    “Tafadhali usinifananishe na wahuni, moyo wangu umetuama kwako. Hapa natakiwa kuoa, baba amenipa miezi mitatu tu ya kukamilisha jambo hilo. Najua siwezi kukutana na mwanamke wa hadhi yangu kijijini.

    “Nimekupenda wewe na naamini hisia zangu. Ndiyo maana hata jana sikutaka kufanya chochote na wewe kwa sababu najua ninachohitaji kwako ni kikubwa zaidi ya tendo la usiku mmoja tu.

    “Tafadhali naomba unisaidie kwa hilo. Nipe nafasi moyoni mwako. Nakupenda sana Laura,” Chris akasema kwa hisia kali sana.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    HUMBA kilikuwa kikubwa chenye kila kitu. Giza jepesi la jioni lilianza kuchukua nafasi chumbani mle. Taratibu jua liliendelea kuzama na kufanya ukimya wa jioni uanze kuingia taratibu.

    Ndani ya chumba hiki, watu wawili walikuwa wamezama katika mazungumzo muhimu sana. Dk. Chris anajaribu kueleza namna anavyougulia mapenzini kwa msichana mrembo Laura.

    Kwa hakika Chris aliamua kujitutumua. Alijihisi mpweke na hakutaka kabisa kumkosa. Tayari alishakatisha safari yake ya kijijini kwao ambako alitakiwa aende kutafuka mke huko.

    Laura alimtosha kabisa.

    Laura ni kama hakusikia vizuri kauli ya Chris. Kama alisikia basi alikuwa hajaamini maneno ya kijana huyo ambaye anasumbua katika ulimwengu wa filamu za Kibongo.

    “Chris una hakika na unachokizungumza?” Laura aliuliza kwa sauti laini, tamu ambayo ilikuwa burudani tosha kwa Chris.

    Jibu lilikuwa rahisi sana: “Nina zaidi ya hakika Laura. Nipe nafasi. Nitaumia sana nikikukosa. Moyo wangu umeniambia unakupenda wewe tu. Tafadhali usiniumize wala kuniadhibu.”

    “Siamini maneno yako Chris.”

    “Kwa nini mama?”

    “Sikuamini tu. Nyie wanaume maneno mengi sana, hasa ninyi wasanii. Mh! Hapo utasema maneno yote lakini ukinipata tu, mapenzi yanaishia hapo. Kwa kweli nimeondoa kabisa imani na wanaume.”

    “Kuna tofuati kubwa sana kati ya wanaume na Chris. Mimi ni tofauti na wengine wote unaowajua au uliowahi kukutana nao. Mimi ni kweli ni mwanaume, lakini ni Chris. Nipe nafasi tafadhali.”

    Kama ni filamu basi Chris alikuwa kwenye kipande cha mapenzi na aliweza kuvaa uhusika wake kisawasawa. Unaweza kudhani hivyo, lakini safari hii Chris hakuwa mbele ya kamera.

    Alikuwa akizungumza kutoka ndani na kueleza hisia za kweli za moyoni mwake. Laura alimteka kwa hakika.

    “Hata kama nikikubali Chris, kumbuka baba yako ameshasema anataka mke wako atoke kijijini. Angalia... kwanza mimi siishi kijijini, pia siyo Mnyiramba kama baba yako anavyotaka. Mimi ni Msukuma. Itakuwaje?”

    “Najua cha kufanya Laura. Ninalo wazo.”

    “Wazo gani?” Laura akauliza harakaharaka.

    “Lipo lakini nataka kujua kwanza kutoka kwako. Wewe unanipenda?” Chris akamwuliza Laura.

    “Ndiyo... kwa nini nimchukie binadamu mwenzangu? Nawapenda watu wote.”

    “Tafadhali Laura, usiniumize hisia zangu. Usiutese moyo wangu tafadhali. Nazungumzia mapenzi hapa. Tunajadiliana kuhusu maisha mama. Tafadhali chukulia kwa uzito huohuo Laura.”

    “Nakupenda Chris,” Laura akasema mara moja tu, akanyamaza.

    “Kweli?”

    “Ndiyo... lakini bado kuna mambo nahitaji kuzungumza kidogo na wewe. Kuna vitu nataka kujua zaidi kuhusu wewe. Nadhani tukutane Club jioni, tuzungumze zaidi.”

    Chris alisimama alipokuwa amekaa, akapiga hatua fupi nne, akamfikia Laura. Akamnyooshea mikono yake miwili kama ambaye alitaka kupokewa. Laura akaipokea.

    Taratibu Chris akamwinua Laura, akasogea mzimamzima. Akamlaza kifuani mwake. Miili yao ikakutana. Wote kwa pamoja wakapata msisimko mkali sana.

    “Nakupenda sana Laura,” Chris akatokwa na maneno hayo huku akimwaga machozi.

    “Nakupenda pia Chris, sikutegemea kama ningekupenda kwa kiwango hiki. Ngoja niwe mkweli... sikukupenda hata kidogo lakini sasa naona ni kwa namna gani ningepoteza mtu muhimu sana maishani mwangu.

    “Nimekupa kila kitu mpenzi wangu. Nakupa moyo wangu. Chukua mwili wangu. Nichukue baba. Nichukue mpenzi. Mimi ni wako kwa kila kitu. Nifanye upendavyo!”

    Chris akasisimka!CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Sheria yake ilikuwa ileile. Ndani ya nafsi yake, huba zito lilimlemea. Kamwe hakutaka kuonekana mhuni. Pamoja na maneno yale ya Laura kuashiria kwamba alikuwa tayari kwa lolote, moyoni Chris alikataa!

    “Ahsante dear. Nami nimekukabidhi kila kitu mpenzi wangu. Nakupenda sana.”

    “Nitoe baba niondoke, jioni tukutane Club sawa?”

    “Sawa mama.”

    Wakatoka nje wakiwa wameshikana mikono. Laura akaingia kwenye taksi na kuondoka zake. Ahadi ilikuwa kukutana Club usiku.

    ***



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog