Search This Blog

Thursday, July 21, 2022

NILIISHI DUNIA YA PEKE YANGU - 2

 







    Simulizi : Niliishi Dunia Ya Peke Yangu

    Sehemu Ya Pili (2)



    Nitaendelea kumuomba mwenyezi Mungu anisamehe kwani kilio nilicholia siku ile nilifikia hatua ya kukufuru.

    “Jamani huu ni mkosi, eeh Mungu hata hiki kidogo umekichukua unataka niishi kwenye dunia gani? Kwa nini huniui? Kwa nini unazuia mauti yangu? Nina faida gani ya kuendelea kuishi? Sina mama wala baba, sina bibi wala ndugu! Nitaishi dunia ipi jamani? Mungu hebu nioneshe dunia yangu, naamini kabisa hii si dunia ninayopaswa kuishi.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com

    Walijaribu kunibembeleza lakini hakuna hata mmoja aliyeweza kuninyamazisha. Maumivu niliyoyasikia hayakuwa tofauti na mtu aliyepasuliwa moyo kwa kisu butu, tena bila ya ganzi. “Wee Salha acha kumkufuru Mungu.”

    “Simkufuru, sijasema hata moja la uongo, hivi mimi naishi dunia gani ya mateso kiasi hiki? Kila kukicha nimekuwa miye, ina maana watu wa mateso wamekwisha mpaka niwe mimi peke yangu?” “Wee binti hebu mrudie Mungu wako, kifo ni kitu cha kawaida kwa wanadamu, muombee bibi yako apokelewe na kupumzishwa mahali pema peponi.” “Jamani naomba nikamuone bibi yangu.” “Hapana Salha, utamuona baadaye.” “Jamani naomba nimuone bibi yangu, maskini bibi nimekuacha ukiwa na siri nzito moyoni, kwa nini bibi usiniambie.” “Hebu mpelekeni akamuone bibi yake,” alisema mkuu wa polisi. Niliingizwa ndani na kumkuta bibi amelazwa kitandani akiwa amefunikwa shuka. Bado sikuamini kama bibi amekufa, nilimfunua na kumuona kama amelala. Nilianza kumtikisa taratibu huku nikimwita:

    “Bibi amka nimerudi,” lakini bibi hakuwa na jibu, alikuwa amelala.

    “Bibi jamani ni kweli wasemayo kuwa umekufa? Umeniacha na nani? Bibi unajua kabisa sina baba wala mama, kwa nini unaniacha peke yangu? Najuta kukuacha peke yako. Bibi amka usife, nionee huruma mimi bado mdogo, maisha siyajui... bibi.. bibiiiiiiiii,” nilipiga kelele huku nikimtikisa kwa nguvu aamke, kitu kilichofanya wanishike kwa nguvu kunitoa baada ya kumkumbatia bibi yangu kwa nguvu zote huku nikilia kwa sauti.

    Baada ya kutolewa nje, nilijikuta nikihema kwa shida na kujiona kama nakufa. Dunia niliiona ikizunguka, ghafla nilianguka chini na kupoteza fahamu. Niliposhtuka nilikuta wanakijiji wamejaa nyumbani wakipanga taratibu za mazishi, nilichukuliwa na akina mama wa kijijini ambao walinibembeleza kwani kila dakika nilimtaja bibi huku nikilia kwa sauti. Jioni bibi alizikwa kwa sheria ya dini ya Kiislam, sikwenda makaburini lakini nilielezwa kuwa siku ya pili ningepelekwa kuzuru kaburi la bibi. Nilijikuta nikijawa na mawazo yasiyo na mfano juu matukio ya kukatisha tamaa ya maisha yangu, nikawa najiuliza nitawezaje kuishi peke yangu. Nilishukuru jioni ile mama Solomoni alisema atanichukua na kuishi na mimi.

    Niliyaanza maisha mapya kwa mama Solomoni, japo akili yangu ilikuwa mbali sana kwa kutafuta njia ya mkato ya kuondoka duniani.

    Lakini mama Solomoni aliyekuwa akijua matatizo yangu kwa muda mrefu alikuwa karibu nami kwa kunifariji.

    Alinionesha mapenzi makubwa kuzidi hata watoto wake wa kuwazaa, nilitakiwa kupumzika kwa kipindi kile cha majonzi ya kifo cha bibi, alitumia muda mwingi kunisahaulisha kwa kunihadithia vitu ambavyo vilinifanya nicheke.

    Lakini hali ya kuzama katika dimbwi la mawazo ilikuwa ikinijia kila nilipokuwa peke yangu huku nikiwaza kwa nini nisijiue ili niepukane na tabu za dunia.

    Nakumbuka siku moja nikiwa peke yangu baada ya wenzangu wote kwenda shule, nilionesha uchangamfu na kuonekana nimekubaliana na hali halisi ya mambo yote yaliyotokea.

    Nilifanya kazi za nyumbani, wakati nikiosha vyombo wazo baya liliniingia kwani siku zote shetani hupenyeza ushawishi wake mbaya pale penye tatizo.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com

    Nilipata wazo la kujiua, niliviacha vyombo nje na kuingia ndani kutafuta fedha kwa ajili ya kununulia sumu ya panya ili ninywe na kuondokana na adha za dunia.

    Nilitafuta fedha sehemu zote hadi chumbani kwa mama Solomoni. Niliamini nikinywa sumu muda ule mpaka watakaporudi wangenikuta nimeshakuwa maiti.

    Lakini kila kona ya nyumba sikuona hata senti tano, nilikumbuka ugumu wa maisha ya kijijini, fedha zilikuwa ni vigumu kupatikana na mtu akiipata anatembea nayo kwenye pindo la khanga yake.

    Baada ya kutafuta kwa muda mrefu bila mafanikio, wakati nikitoka ndani nilipata wazo la kutumia njia nyingine ya kujiua kwa kujinyonga kwa kamba.

    Japo nilikuwa mwoga kutumia njia hiyo kwa kuamini kuwa kifo chake kina mateso makubwa hasa kwa mtu kutokwa na kinyesi, ulimi kuwa nje na macho kutoka kama ngumi.

    Nilichukua muda mrefu kuufikiria uamuzi huo mzito wa kujiua kwa kamba.

    Niliichukua kamba na kwenda hadi chumbani ambako nilichukua meza na kupanda juu na kuifunga kamba vizuri kwenye kenchi za miti.

    Ilinichukuwa muda mrefu kutengeneza kitanzi kutokana na uzoefu wangu mdogo wa kufanya jambo hilo.

    Baada ya kufanikiwa kutengeneza kitanzi nilikipimisha shingoni kwanza kabla ya kukivaa. Kisha nilishuka chini na kukiangalia huku roho yangu ikisita kuchua uamuzi huo.

    Kuna sauti iliniambia nijiue na nyingine ilinizuia na kuniambia kufanya kitendo hicho ni dhambi kubwa.

    Niliyakumbuka maneno ya bibi kuwa mtu akijiua maisha yake yote huwa ni motoni.

    Kutokana na mateso yale niliamini kabisa motoni ndiyo sehemu inayonifaa zaidi kuliko peponi.

    Nilijiuliza kama kweli Mungu anayaona mateso yangu ananipa msaada gani katika maisha yangu au ndiyo hivyo vitisho wa kuishi motoni milele.

    Nilijiuliza maisha ninayoishi kama yana tofauti na hayo ya motoni.

    Roho mbaya ilichukua nafasi kubwa katika nafsi yangu kwa kunitaka nitekeleze uamuzi ule wa kujinyonga.

    Nilipanda juu ya meza huku nikitetemeka na haja ndogo ikianza kunitoka, bado nilikuwa na ujasiri wa kutimiza kile nilichodhamiria, nilikishika kitanzi ili nikivae tayari kwa kujinyonga.

    Nilishtuliwa na sauti ya mama Solomoni aliyekuwa nje akiniita huku akija kwenye chumba nilichokuwemo. “Wee Salha uko wapi? Mbona umeacha vyombo nje vikichezewa na bata?”

    Nilibakia nikijiuliza nijinyonge haraka au niache kwa kuwa kuhofia kuwa ataniwahi, pia nilipata wazo la kujificha uvunguni kwa kuamini kuwa akinitafuta na kunikosa angetoka nami kuendelea na zoezi langu.

    Hilo nililiona ni wazo la kitoto kwani kama angeingia ndani na kukuta meza na kamba jinsi vilivyotengenezwa na kitanzi angejua kitu gani kilikuwa kikitaka kufanyika.

    Kabla sijapata jibu la maswali yangu, mlango wa chumbani ulifunguliwa na mama Solomoni aliingia. Alishtuka kuniona nikiwa juu ya meza nimeshikilia kamba.

    “Wee Salha unataka kufanya nini?”

    Sikumjibu niling?aa macho kama mwanga aliyekamatwa akiwanga mchana, alinifuata na kunibeba kutoka juu ya meza na kuniteremsha chini.

    “Salha mwanangu unataka kufanya nini?” Sikumjibu niliendelea kuporomosha mvua ya machozi.

    “Kwa nini umekuwa na mawazo mabaya kama hayo, kwa nini unampa nafasi shetani mwanangu?” Bado nilibakia kimya huku nikijilaumu kwa kuchelewa kuchukua uamuzi wa haraka.

    “Najua upo katika hali gani, lakini bado hutakiwi kumpa nafasi shetani, usimkumbatie kwani ni kiumbe kibaya sana ambaye huwa rafiki yako kabla ya kutenda, lakini ukishatenda hukuacha peke yako.” “Nisamehe mama,” nilijikuta nikijiona mkosefu mkubwa.

    “Siwezi kukuchukia hata siku moja, kuna jambo lolote baya tulilokutendea hapa nyumbani?” “Hakuna.”

    “Niambie mwanangu, kama kuna jambo lolote baya tuliokutendea au ndugu zako wamekufanya nini?” “Hakuna kitu mama.”

    “Sasa si tulishazungumza na kuelewana? Nini tena kimekukumba?”

    “Nilikuwa nataka kuosha vyombo, nilikashangaa wazo la kujiua likiniijia, ndipo nilipoingia ndani nitafute fedha, nikanunue sumu ya panya ninywe. Bahati nzuri sikuiona, nikapata wazo lingine la kujiua kwa kamba, ndipo nilipotafuta na kuifunga.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com

    “Naelewa kichwani mwako pepo mchafu wa kifo bado anakusumbua, unatakiwa maombi. Sijajua kwenye dini yenu mnafanya nini lakini kwenye dini yetu unaombewa na pepo mchafu wa kifo anakutoka.” “Niliwahi kusikia mtu mwenye matatizo anasomewa dua, yanaisha.”

    “Lakini mwanangu pale kanisani kwetu nimewaona hata waislamu wakija kuombewa bila kuhama dini zao.” “Basi nipeleke maana nina imani ninapoelekea ni kubaya zaidi, leo umeniwahi kesho nitafanya kitu kingine.” Tulikubaliana jioni ya siku ile nipelekwe kanisani nikaombewe, jioni ilipofika nilifika kanisani kuombewa. Watu walikuwa wengi sana walipita mbele kwa ajili ya kuombewa matatizo yao. Mchungaji alizungumza maneno mengi kabla ya kuanza kumpitia mmoja mmoja na kumshika

    kwenye paji la uso huku akikemea mapepo. Kila aliyeshikwa alianguka kwa nyuma na kudakwa na wasaidizi wake mchungaji au yule ambaye pepo alikuwa mgumu kutoka alimkemea kwa sauti ya juu mpaka lilipotoka na kutulia chini baada ya muda alisimama akiwa mzima. Katika watu waliotoka mbele, kama sikosei nilikuwa mtu wa kumi na aliponifikia alisema kwa sauti ya juu akiwa amenishika kwenye paji la uso: “Kwa jina la Yesu, pepo mchafu ondoka ndani ya mwili wa binti huyu, mwache huru, mwache huru, toka, toka, tokaaaa.” Baada ya kusema vile, nilijisikia kama nimepigwa shoti ya umeme na kuangukia kwa nyuma ambako kulikuwa na watu walionidaka. Nililazwa chini nikiwa sijifahamu. Baada ya muda nilinyanyuka na kuruhusiwa kwenda kukaa. Usiku mama Solomoni alinieleza: “Sasa mwanangu umekuwa kiumbe kipya.” “Nashukuru sana mama kwa msaada wako mkubwa.” “Najua ulikuwa katika wakati gani, siku zote mwanadamu aliyevamiwa na shetani huwa na kiza kizito mbele yake hata ayafanyayo huwa mabaya kwa vile hajui akifanyacho kutokana na kiza kilicho mbele yake.” “Ni kweli huwezi kuamini, sasa hivi moyo na mwili wangu umekuwa mwepesi, siwazi tena vitu vibaya zaidi ya kuyatamani maisha ambayo kwa kweli sasa ndiyo nayaona matamu.” Baada ya mazungumzo tulikwenda kulala kwa vile muda ulikuwa umekwenda sana. Asubuhi ya siku ya pili ilikuwa mpya kwangu kwani kila dakika niliyokuwa peke yangu, nilitubu makosa yangu kwa Mungu kwa kuamini nilichotaka kukifanya hakikuwa sahihi. Tokea siku hiyo, nilijikuta nami nampokea Yesu taratibu, japo si kwa asilimia kubwa kutokana na dini yangu ya kuzaliwa ya uislamu, kanisani sikwenda, lakini sala za nyumbani nilishiriki ikiwemo kusali kwa kupiga magoti. Siku zilikatika, afya yangu iliimarika siku hadi siku. Katika maisha yangu sitamsahau mama Solomoni kwa kunipa mapenzi ambayo yalinihamisha katika mawazo mabaya na kujiona nimezaliwa upya. Japo maisha yake yalikuwa ya kawaida, lakini upendo ulitawala ndani ya nyumba yake huku wanaye wakiniona kama ndugu yao wa kuzaliwa. Baada ya miezi saba kukatika nikiwa kwa mama Solomoni. Siku moja walikuja wageni ambao walikuwa ndugu wa mama Solomoni wanaokaa mjini. Katika kuwaandalia chakula na vinywaji, ndugu yake alinishangaa kwa heshima niliyoionesha muda wote toka walipofika mpaka muda ule. Nilimsikia yule mama akiuliza kwa kilugha: “Mama Solomoni, huyu mtoto mwenye heshima umemtoa wapi?” “Ni habari ndefu.” “Ya nini?” “Salha,” mama Solomoni aliniita. “Abee mama,” niliitikia kwa unyenyekevu. “Hebu kamalizie vile vyombo naona ndugu zako wanafanya mchezo.” “Hakuna tatizo.” Nilijibu huku nikitoka nje, wakati natoka nilimsikia akisema kwa kilugha kwa kuamini siijui kwa vile hakuwahi kunisikia nazungumza toka nitoke mjini. “Nimemtoa kijanja ili tuzungumze sipendi asikie kwani nitamtonesha kidonda ambacho naamini kimepona.” Sikutaka kusimama kwa kuamini japo nataka kuzungumziwa mimi, lakini yalikuwa hayanihusu. Nilipofika nje, kweli niliwakuta akina Rose wanapiga stori wamesahau kuosha vyombo. “Jamani mama kanituma niwasaidie kumaliza kuosha vyombo.” Nami sikutaka kuosha kwa haraka, niliosha taratibu ili kuvuta muda wa mazungumzo ya ndani. Hata baada ya kumaliza kuosha, sikuingia ndani kusubiri niitwe. Baada ya nusu saa nikiwa

    nimekaa chini ya mti, niliitwa ndani. “Da Salha unaitwa ndani na mama.” Bila kujibu nilinyanyuka na kuingia ndani na kumkuta mama amekaa karibu na mama mkubwa. Waliponiona naingia, wote waligeuza sura na kuniangalia Salha ameitiwa nini? Ili kujua, usikose

    Kwa vile nilikwishajua wanazungumzia nini, nilikwenda mpaka kwa mama na kuitika kwa unyenyekevu. “Abee mama.” “Mama yako mkubwa anakuita.” “Abee mama mkubwa,” nilimgeukia mama mkubwa. “Salha,” mama mkubwa aliniita. “Abee mama.” “Kwanza pole sana mwanangu kwa yote yaliyokukuta.” “Asante mama.” “Nimesikia yaliyokusibu lakini mtangulize Mungu kwa kila jambo.” “Sawa.” “Sasa ni hivi, kwanza nimevutiwa na tabia yako ambayo ilinitia wasiwasi na kuamini huenda ni kwa ajili ya kuwaona wageni, lakini nimeambiwa hii ni tabia yako ya asili. Sasa mwanangu nitaondoka na wewe kwenda mjini ambako utanisaidia kazi zangu ndogondogo huku nikikulipa fedha kidogo ambazo zitakusaidia kufanya mambo yako mengine bila kunitegemea.” “Mama amekubali?” Japo habari za kuhamia mjini zilikuwa nzuri, lakini sikutakiwa kuonesha nimefurahia sana, nilitakiwa kuonesha bado namhitaji mama Solomoni. “Kwa vile dada yupo peke yake nina imani utakuwa mtu wa kumtoa upweke, dada yako mkubwa muda mwingi anakuwa chuoni, kurudi kwake ni usiku hivyo muda wa mchana anahitaji msaada wa kazi ndogo ndogo.” “Sawa mama, kama wewe umeridhia mimi sina kipingamizi.” “Mama Solomoni na wanao wangekuwa kama huyu ungeringa.” “Mungu hamnyimi mja wake, kamnyima walezi kampa tabia nzuri ambayo itamfanya aishi sehemu yoyote.” Kwa vile walikuwa ndiyo wanajiandaa kurudi mjini nami nilielezwa nikaoge na kujiandaa kuhamia mjini. Nilikwenda kuoga na kujiandaa kusubiri kwenda mjini. Ilionesha maisha yao ni mazuri kwani walikuwa na gari la kutembelea lililowaleta kijijini. Baada ya maandalizi kukamilika niliagana na mama Solomoni ambaye kwangu ndiye aliyekuwa mzazi wangu na wanawake walikuwa ni ndugu zangu. Kwa kweli hata wao walihuzunika kutengana nami, kwani tulikuwa tumeshazoeana. Niingia kwenye gari na kuelekea mjini. Tulifika mjini majira ya saa moja jioni na kukaribishwa kwenye nyumba nzuri iliyokuwa na kila

    kitu ndani. Pamoja na ukubwa wa nyumba lakini familia ilikuwa ndogo, ilikuwa na watu wanne tu na mimi nilipoongezeka tukawa watano. Kabla ya mimi kufika, muda wote wa mchana mama Mather alikuwa peke yake mpaka jioni ambapo aliungana na familia yake. Nilijiuliza aliwezaje kuishi peke yake katika nyumba ile , maelezo niliyoyapata baadaye ni kwamba siku za nyuma alimchukua Rose mtoto wa mama Solomoni lakini alishindwana naye kutokana na muda mwingi kuwa kwenye „tivii? huku kazi za usafi hazifanyiki. Kwangu yote hayo sikuona kikwazo, kwani kufanya usafi yalikuwa maisha yangu tangu nilipobadilishwa kutoka mtoto wa familia na kuwa mfanyakazi, hata niliporudi kwa marehemu bibi bado niliendelea na kazi tena mara mbili zaidi, niliamini si tatizo. Maisha ya makazi mapya yalikuwa mazuri sana ambayo yalinifanya nisahau mateso yangu ya siku za nyuma. Kwani sehemu niliyokuwa sikuwa msichana wa kazi bali ni sehemu ya familia. Mchana nilifanya kazi na mama Mather na jioni Mather na Marry waliporudi nilipumzika na wao walifanya kazi za jioni. Kwa muda mfupi nilinawiri na kupendeza machoni mwa watu, siku za mapumziko tulifanya kazi kwa kushirikiana ambapo kulikuwa na tofauti kubwa na kwa mama Solomoni kule kazi nyingi nilifanya mimi japo hazikuwa kubwa. Makazi mapya walikuwa wacha Mungu, wote walikuwa wameokoka, pamoja na kuokoka lakini hawakunilazimisha kujiunga na dini yao, waliniacha na dini yangu hata vyakula ambavyo wao walikula lakini dini yangu ilivikataza waliviacha kwa ajili yangu ili isionekane wamenibagua. Kila siku mama Mather alikaa chini na kunieleza habari za kumcha Mungu kitu ambacho kilibadili akili yangu na kuamini dini ni njia ya kumjua Mungu na Mungu ni mmoja. Mwenyewe kwa hiyari yangu baada ya kujifikiria kwa muda mrefu kutokana na malezi mazuri niliyopata kutokwa kwa familia ya mama Mather niliamua kubadili dini na kuwa Mkristo ambaye nilimpokea Bwana Yesu kama mkombozi na mwokozi wa maisha yangu na kupewa jina la Ester. Nami nilihudhuria ibada kama kawaida, kutokana na tabia zangu za asili na nilivyompokea Bwana Yesu nilizidi kuwa kipenzi cha familia. Baada ya mwaka kukatika mama Mather aliniuliza kama nitakuwa tayari kujiendeleza kielimu. Nilikubali mara moja kwani jambo hilo lilikuwa akilini mwangu. Lazima niseme ukweli, naweza kusema niliweza kukufuru kwa kulaani tabia za mama za kukosa uaminifu pia kuzaliwa katika familia isiyo na mapenzi. Niliamini kabisa sehemu niliyotakiwa kuzaliwa ni ndani ya nyumba ya mama Mather. Siku nazo zilikatika nami nilijengeka kimwili na kuonekana mama wa familia hata kama ningeachiwa nyumba ningeweza kuiendesha bila matatizo. Katika nyumba ile baba mwenye nyumba, mzee Sifael alionesha mapenzi ya dhati kwangu hata kunipa zawadi za siri ambazo wenzangu na mama hawakuziona.

    Sehemu hii pia haikuweza kupatikana

    Wakati huo nilisikia sauti za nyayo kuonesha kuna zaidi ya mtu mmoja waliokuwa wakija chumbani kwangu. Dada Mather aliwahi kuchukua upande wa kitenge na kunifunga. Ajabu katika watu waliokuja alikuwepo na baba mzee Sifael. “Vipi Ester?” mzee Sifael alikuwa wa kwanza kuuliza. Kauli ile ilinishtua na kujiuliza, anachouliza mzee Sifael ni kweli hakijui au ndiyo kujifanya mwema mbele ya watu? Nilijikuta nikiangua kilio nilivyofikiria ninavyoonewa bila kosa na mfanya kosa ndiye anajifanya mwema mbele ya watu. “Ester umekuwaje mwanangu?” mama Mather aliniuliza akiwa amenikumbatia. Nilishindwa kusema kwa kukumbuka kauli ya mzee Sifael kuwa kama nitasema ukweli nitaweza kuivunja ndoa yake iliyodumu zaidi ya miaka 30. Nilijiuliza nitawaeleza kipi kinaniliza ambacho kilisababisha nivimbe macho, hivyo kuwa mekundu. Ghafla mama Mather alianza kukemea kilichonisibu bila kupata jibu nalilia nini. “Ewe baba wa mbingu na nchi kwa nini unampa mamlaka shetani kuichezea nyumba yangu? Naamini shetani hana mamlaka kwako naomba umtokomeze kwa jina la Yesu Kristo aliye hai. Ondoa pepo mchafu moyoni mwa Esther, CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.commuondolee mateso ya moyo. “Ni wewe uliyetueleza tukikutegemea hakuna kitakachoshindikana, hakuna zaidi chini na jua ila wewe Mungu wa kweli. Vunja nguvu za shetani ziteketeze kwa moto, zisionekane tena kwa jina la mwanao Yesu Kristo, shetani ameshindwa, toka... toka pepo mchafu... toka ndani ya moyo wa Ester toka ndani ya nyumba yetu...” mzee Sifael aliomba. Ilikuwa ajabu katika maombi yale, baba mwenye nyumba ndiye aliyekuwa akitoa sauti ya juu kuliko wote mpaka jasho likamtoka. Nilijiuliza yale maneno aliyokuwa akiyatoa mzee Sifael alikuwa akimwambia Mungu gani na alitaka shetani gani atoke moyoni mwangu na ndani ya nyumba. Niliamini basi shetani namba moja ni yeye aliyetakiwa kutoka ndani ya nyumba ya mama Mather aliyekuwa akimjua Mungu wa kweli na uzima. Baada ya maombi ambayo yalifanywa chumbani kwangu kwa wote kushirikiana kumfukuza pepo mchafu, huruma iliniingia nilipowaangalia mama na ndugu zangu Mather na Joyce ambao waliomba mpaka machozi yakawatoka. Moyoni nilisema sitasema kilichonitokea mpaka naondoka mule ndani kwa kuamini kabisa mimi nilikuwa mpitaji tu, nilikuta upendo ndani ya nyumba hiyo hivyo lazima niuache! Kauli yangu ya kweli ingekuwa sawa na moto kwenye kijiti kuutupa kwenye tenki la mafuta, niliamua kuzua uongo ambao nilijua itaonekana imani yangu ni finyu kwa kumpokea Yesu nusu na si kamili kwa kumtanguliza mbele kwa kila kitu. Baada ya maombi ya zaidi ya nusu saa mama Mather aliniita kwa sauti ya chini huku akijifuta jasho kwa upande wa kanga... “Ester.”

    “Abee mama,” niliitika kwa sauti ya chini. “Hebu nieleze nini tatizo?” “Jana nimeota ndoto mbaya sana, mama yangu yupo kwenye mateso mazito kutokana na baba kunifukuza nyumbani. Inaonesha toka nilipofukuzwa, mama yangu kuzimu analia tu, amedhoofu kwa kitendo cha baba kumgeuka baada ya kufa.” “Ooh! Kumbe ni hivyo, inabidi tufanye maombi kwa roho zote zilizo kuzimu.” Tulifanya maombi ya kumuombea mama yangu kisha nilikwenda kuoga na kufanya maombi ya pamoja kabla ya wote kuondoka kwenda kazini na shuleni. Mather kabla ya kuondoka alinifuata na kunieleza: “Mdogo wangu najua umekuwa huna kazi za kukufanya uwaze maisha mengine kwani kila siku ukiwa ndani hakukupanui mawazo. Nakuhakikishia kukutafutia kazi ya kukuweka busy hata ukirudi nyumbani uwe umechoka.” “Sawa dada nitashukuru.” “Basi mdogo wangu, Bwana akutangulie kwa kila jambo, unapenda jioni nikuletee nini?” “Chochote dada.” “Nitakuletea baga.” “Na nini?” “Soda ya kopo.” “Hapo umelenga.” “Dada Ester tutaonana jioni,” Joyce naye aliniaga. Mzee Sifael alionekana kuhitaji sana kuzungumza na mimi, nikajitahidi kumkwepa lakini hakuvumilia, aliniita na kunisogeza pembeni. Sikuweza kuonesha mabadiliko yoyote kwa vile nilikwishaapia moyoni mwangu kuwa sitasema kwa mtu yeyote kitendo cha kinyama alichonifanyia mzee huyo. Nilipofika pembeni nilijikuta nasahau maumivu yangu na kumuonea huruma mzee wa watu kwa jinsi alivyokuwa akikosa raha kama mgonjwa. Kabla ya kusema alichoniitia alinitazama, ghafla machozi yalimtoka, alitoa kitambaa mfukoni na kujifuta. Nilijiuliza anataka kuniambia nini, lakini sikujua. “Ester mama...” aliniita. “Abee baba,” nikaitika nikimwangalia machoni.

    Na hii haikupatikana

    (Into ya next part; ILIPOISHIA: Nilipozingatia kuwa mama Martha alikuwa akiniamini kama binti mwenye heshima, niliwaza nini kitatokea kama akisikia natembea na mumewe au ajue siku niliyopiga kelele

    nilibakwa na mumewe. Nilijiuliza nitaweka wapi uso wangu japo sikutakiwa kufunua kombe kabla mwanaharamu hajapita. SASA ENDELEA...)

    Nilijikuta nipo njiapanda kupata jibu la nini cha kufanya kwa kuamini kabisa muonja asali huwa haonji mara moja. Kitendo cha kunibaka nilijua hakikuwa cha bahati mbaya bali alikipanga kwa kuamini umaskini wangu ungenifanya nimkubalie na kuendeleza mchezo wake mchafu ambao mwisho wake ungekuwa mbaya kama bomu lililosubiri kulipuka. Lakini nilikumbuka kauli ya asubuhi ya mzee Sifael aliponiomba msamaha: “Najua nimekukosea sana, naijutia nafsi yangu kwa kitendo cha kishetani nilichokutendea. Nashukuru kwa kuokoa ndoa yangu, nakuahidi sitarudia tena na Mungu shahidi yangu, kama nitafanya hivyo tena basi uchukue uhai wangu. Ester nakuahidi kukupatia kitu chochote utakachokitaka ili kurudisha furaha yako.” Niliyarudia maneno yake akilini na kuanza kuyatafakari kabla ya kuchukua uamuzi mzito wa kuondoka pia kurudia dini yangu ya zamani. Wazo lingine liliurudisha moyo wangu kwa kuamini maneno yale yalionesha majuto na kuamini hatarudia tena. Lakini wasiwasi ulibakia kuwa, je, hajanipa ujauzito au kuniambukiza magonjwa ya zinaa? Nilijikuta nakubaliana na wazo jipya la kuachana na mpango wa kuondoka na kuamini Binadamu anayegundua kosa lake hawezi kulirudia. Nilipiga magoti pembeni ya kitanda kumuomba Mungu anipe ujasiri niweze kuyashinda majaribu yale. Baada ya maombi, nilipanda kitandani na usingizi haukuchelewa kunichukua mpaka nilipoamshwa na mama kwa ajili ya chakula cha mchana. Niliungana na mama kula chakula cha mchana, kila dakika aliniuliza hali yangu, ilionesha jinsi gani alivyokuwa na mapenzi ya kweli kwangu. Japo moyo wangu ulikuwa bado una kovu la kubakwa na mumewe lakini mapenzi yake yalinifariji. Niliamua kuliacha lile lipite kwa kuamini kitendo alichotenda mzee Sifael ni kosa kama la binadamu mwingine hivyo alitakiwa kusamehewa. Niliendelea na maisha yangu huku moyo wangu ukiwa umekufa ganzi, hata kuhudhuria kanisani kulipungua tofauti na mwanzo, watu wangu wa karibu wakawa wananiulizia lakini siri ilibakia moyoni mwangu. Siku nazo zilikatika ambapo nilianza kugundua mabadiliko mwilini mwangu. Hali ile ilinitisha sana, kwa vile nilikuwa nimeshakuwa na ufahamu nilikwenda duka la dawa na kuchukua kipimo cha ujauzito. Niliporudi nyumbani nilijifungia chumbani kwangu na kupima kwa njia ya haja ndogo. Baada ya kuweka haja ndogo kwenye kopo niliingiza kipimo, baada ya kukitoa jibu lilikuwa lilelile... nilikuwa nimenasa ujauzito. Nilipatwa na mshtuko wa ajabu, nikajiuliza itakuwaje kama nitaulizwa ujauzito ule wa nani? Sikuelewa ningejibu nini, pia ile heshima yangu ingepotea si kwa mama Martha pekee, hata wasichana wenzangu wa kanisani. Wazo la kutoa mimba sikulipa nafasi kabisa, niliapa toka nilipoponea kwenye tundu la sindano sitatoa ujauzito tena maishani mwangu. Niliamini baada ya kosa la kwanza ningekuwa makini maishani mwangu kwa kutoutoa mwili wangu kwa mwanaume kabla ya kuolewa. Lakini ilikuwa tofauti na mipango yangu, nilijikuta nimeshika ujauzito baada ya kubakwa na mtu niliyemuheshimu kama mzazi wangu. Nilijikuta nikiwa katika wakati mgumu sana, sikujua nifanye nini. Sikutaka kufanya pupa, niliweka vitu vyangu vizuri na kutoka sebuleni nikiwa

    sioneshi kitu chochote usoni kwangu. Kila nilipomuona mzee Sifael akipita, moyo ulikuwa ukinilipuka na kuona kuna umuhimu wa kumweleza siku ileile ajue atanisaidia nini japo niliamini kabisa atanishauri kutoa, kitu ambacho sikutaka kukisikia. Baada ya uzalendo kunishinda nilimwita mzee Sifael. “Samahani baba.” “Bila samahani mwanangu.” “Nilikuwa na mazungumzo na wewe.” “Hapa au pembeni?” “Nina imani pembeni ingefaa zaidi.” “Basi twende nje mwanangu tukazungumze,” mzee Sifael alisema huku akielekea nje, nami nilimfuata huku mama na kina Martha wakinitania. “Mmh! Mtu na baba yake mna siri gani? Au umeshapata mchumba nini?” Sikuwajibu, nilicheka tu huku nikimfuata baba nje, nilimkuta amesimama karibu na getini. “Mh! Mama ulikuwa unasemaje?” “Kuna tatizo limejitokeza.” “Tatizo gani tena mama?” mzee Sifael aliuliza kiungwana na kunifanya niwe na wakati mgumu wa kumweleza kwani niliona kama namuonea mtu aliyeamini baada la tukio lile baya Mungu amemuepushia mbali. “Hata nashindwa nianzie wapi unielewe.” “Sema tu mama nitakuelewa.” “Hivi karibuni niligundua mabadiliko mwilini mwangu na kunifanya leo niangalie afya yangu, muda si mrefu nimetoka kujipima na kujikuta nina ujauzito.” “Ooh! Ujauzito wa nani?” mzee Sifael alishtuka. “Wa kwako.” “Mimi?”

    “Kwani nani aliyenibaka?” “Hata kama nilikubaka lakini ujauzito si wangu,” mzee Sifael alijifanya kuruka futi mia. “Sikiliza baba toka nifike hapa sijawahi kukutana kimwili na mwanaume na wewe ndiye uliyeniingilia mara ya mwisho, kwa hiyo naomba uniambie utanisaidiaje kabla sijamwambia mama?” “Ha...ha...pana usifanye hivyo.” “Sasa niambie utanisaidiaje?” “Mmh! Mbona mtihani mzito.” “Sasa mimi nifanye nini?” “Ni kweli ujauzito ni wangu?” “Wewe unafikiri wa nani?” “Huna rafiki wa kiume?” “Sina.” “Siyo kitu, kesho tutafanya zoezi la kutoa hiyo mimba.” “Hapana suala la kutoa ujauzito wangu sahau.” “Una maana gani kusema hivyo?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com

    “Katika kitu ambacho sitakifanya maishani mwangu ni kutoa mimba.” “Sasa tutafanyaje? Njia nzuri ni kuitoa tu bila hivyo tutaharibu kila kitu.” “Tafuta njia yoyote ya kutatua tatizo hili, lakini mimba sitoi hata kwa mtutu.” “Lakini kwa nini Ester, huoni kama inaweza kuleta tafrani nzito ndani.” “Najua lakini katu sitatoa mimba,” nilisimamia msimamo wangu. “Kwa nini Ester hutaki kutoa mimba?” “Siwezi kupona mara mbili, mara ya kwanza nilichungulia kaburi, nikirudia nitakufa.” “Nitakupeleka kwa wataalamu.” “Hata kwa Mungu sikubali.” “Kwa hiyo tutafanyaje?” “Tafuta njia yoyote lakini si kutoa.” “Fanya hivi...hili suala njoo kesho kazini tuzungumze vizuri hapa si pazuri.” Kabla ya kuingia ndani mzee Sifael alinirudisha nyuma na kuniambia. “Sikiliza Ester ukiulizwa na mama yako mwambie umepata mchumba Muislam, sawa?” “Sawa.” Baada ya kukubaliana tuliingia ndani, walipotuona walisema kwa pamoja. “Mmh! Mtu na mtoto wake mna siri gani?” “Siyo lazima kuijua ndiyo maana tumezungumza wawili,” mzee Sifael aliwajibu. Sikujibu kitu, nilifika na kukaa pembeni ya mama. Muda wote niliokaa na mama sikuulizwa swali lolote mpaka muda ulipofika wa maombi ili kila mmoja aende chumbani kwake. Kama kawaida baba aliongoza maombi kuonesha kweli roho mtakatifu kamuingia kumbe alikuwa shetani mkubwa. Nilimuona muongo mkubwa aliyenifanya niichukue dini kwa kuamini mashetani kama wale ndiyo wachafuzi wa dini za watu huku wakionekana wapo mbele kumtukuza Bwana kwa midomo yao kumbe wachafu mioyoni. Tokea nilipobakwa na jinsi tabia ya mzee Sifael aliyokuwa akijionesha mbele za watu, moyo uliniuma na kufikia hata kuiona ibada yote aliyokuwa akiongoza ni ya kinafiki tofauti na mwanzo nilikuwa nikimwamini. Baada ya maombi ambayo kwa upande wangu niliyaona ya kinafiki tulikwenda kulala, usiku ulikuwa mrefu kwangu niliwaza hiyo kesho angeniambia kitu gani tofauti na utoaji wa ujauzito. Pamoja na kuwa na mawazo mengi usingizi ulinipitia na kushtuliwa alfajiri kwa ajili ya maombi ya asubuhi ya kumshukuru Mungu kutulaza salama pia kumuomba atuvushe siku salama. Baada ya maombi kabla ya kuondoka baba alimueleza mama: “Baadaye Ester aje kazini.” “Saa ngapi?” “Kuanzia saa tano.” “Nina imani amekusikia.” Baada ya kusema vile aliondoka na kuniacha na mama nikifanya usafi na kazi zote muhimu kabla ya kwenda kuonana na baba.

    Saa tatu na nusu mama aliniomba nijiandae kwenda kwa baba, baada ya matayarisho yote nilikwenda kazini kwa baba.

    Nilipofika hakutaka tuzungumzie pale, alinipeleka kwenye hoteli moja iliyokuwa tulivu na kuagiza vinywaji kabla ya mazungumzo. Siku hiyo alikuwa mpole kupindukia, nami nilikuwa kimya muda wote nimsikie anataka kuniambia nini.

    Kabla ya kusema nilishangaa kumuona mzee mzima akitokwa machozi na midomo ikimcheza kuonesha alikuwa na wakati mgumu mbele yangu kitu ambacho sikutaka kukipa nafasi kwa kuamini kosa langu lolote ni kifo changu.

    Niliendelea kujiapiza sitakubali hata kwa mtutu wa bunduki kutoa mimba kwa vile yaliyonikuta sitayasahau mpaka naingia kaburini. Baada ya kujifuta machozi aliniita jina langu kwa sauti ya chini. “E..e..ster.” “Abee baba.” “Kwanza samahani.” “Bila samahani baba.” “Najua nililolifanya kwa kweli halikukufurahisha.” “Ni kweli, lakini lilishapita.” “Bado mwanangu, lililopita lilikuwa dogo lakini hili ni kubwa sana.” “Sasa tutafanyaje na imeshatokea?” “Kwa nini hutaki tuitoe hiyo mimba?” “Baba nimekueleza hata kwa mtutu wa bunduki siitoi.” “Kwa nini Ester?” “Nilikueleza niliujaribu mchezo huu mpaka leo nazungumza na wewe ni Mungu tu, nilikuwa nimekwishapelekwa mochwari.” “Kwa sababu gani?”

    Sikutaka kumficha, nilimweleza maisha yangu ya uhusiano na mpenzi wangu wa kwanza mpaka aliponipa ujauzito na kisha kunishauri kama yeye kuutoa ujauzito na matokeo yake. Baada ya kunisikiliza alitulia kwa muda na kushusha pumzi nzito. Alitulia akiangalia juu akigongesha vidole kwenye meno kisha aliniita tena. “Ester.” “Abee.” “Inaonekana mlikwenda kwenye hospitali za uchochoroni.”

    “Nimekwambia hivi, hata kama zingekuwa hospitali za barabarani, sikubali yaliyonikuta nayajua, ungekuwa ni wewe ndiye yamekukuta usingethubutu kunishauri nitoe mimba.”

    “Sasa ukiulizwa mimba ya nani utasemaje?” “Ya kwako.” “Ha!” Alishtuka mpaka akasababisha vinywaji kumwagika. “Unashtuka nini, unataka niseme ya nani wakati baba wa mtoto ni wewe?”

    “Ester, chondechonde, utaharibu sifa yangu kuanzia ndani mpaka kanisani, si unajua kabisa mimi ni kiongozi wa kanisa?” “Huo uongozi wa kiroho au ushetani?” “Wa kiroho Ester, nilichokifanya hata mitume waliotangulia wapo waliofanya makosa kama mimi lakini walisamehewa.” “Hata mimi nilikusamehe, lakini bado roho mchafu yupo ndani yako kwa kutaka kukiua kiumbe kisicho na hatia. Umefanya dhambi ya kuzini, tena kwa kunibaka, dhambi hiyo hujatubu unataka kuua, wewe ni mtu wa aina gani?” nilimuuliza nikiwa nimemkazia macho. “Unafikiri ukisema hii mimba ni yangu nitaweka wapi sura yangu?” “Kwani uliponibaka ulitegemea nini?” “Nikwambie mara ngapi shetani alinipitia?” “Acha kunichekesha ina maana huyo shetani kazi yake kukupitia wewe tu kila siku?” “Sijawahi kufanya kitendo kama hiki ndiyo maana nina wasiwasi kuna mkono wa mtu, siwezi kumbaka binti yangu niliyemlea mwenyewe,” mzee Sifael alizungumza akiamini kabisa sijui historia ya uchafu wake wa nyuma.

    “Baba unajua unazungumza na mtu mzima, sasa kama nisingemuua mwanangu kutokana na akili za kitoto sasa hivi ningekuwa mama fulani hivyo usizungumze kama unazungumza na mtoto mdogo.” “Kwa nini?”

    “Hii tabia yako ya asili ya kubaka wasichana wanaokaa ndani mwako na kujificha kwenye kivuli cha ucha Mungu kama mzee wa kanisa naijua vizuri.”

    “Ester ni maneno gani hayo, mimi nimekuona mtoto kivipi?” “Unajua najua kila uchafu wako uliosababisha mama akimbie nyumbani, kwa hili ulilonifanyia si geni ni kawaida yako.” “Estaaa! Nani kakwambia uongo huo?” “Si kujua nani kaniambia, jua naelewa kila kitu juu ya uchafu chako.” Kauli yangu ilimfanya aone aibu na kuwa na kazi nzito mbele yangu, niliamini utapeli aliokuwa akiutumia kwa wasichana waliotangulia kwangu ulikuwa umejulikana.

    “Ester naomba msaada wako nipo tayari kukupa kiasi chochote cha fedha ili kuficha aibu hii.” “Naweza kukusaidia kwa njia yoyote tofauti na ya kutoa ujauzito huu.” “Basi niambie wewe unafikiria nifanye nini ili tuweze kuificha siri hii?” “Labda niondoke nyumbani.” “Wakikuuliza unakwenda wapi utajibu nini?” “Sitawaaga nitaondoka bila kuaga.” “Utakwenda wapi?” “Popote ambako ni mbali na hapa ili niweze kujifungua salama na kuanza maisha yangu mapya.” “Nikikupa milioni moja itatosha?” “Mmh! Nina imani itatosha,” nilikubali kwa kuamini fedha zile zilikuwa ni nyingi sana.

    “Basi kesho nitakupatia ili ukajiandae na safari yako.” “Sawa.” “Lakini kesho usiage kama unakuja kwangu.” “Kwa hilo shaka ondoa.” Tulikubaliana na siku ya pili nikapewa fedha ili nijiandae kuondoka, niliamini ile ndiyo ingekuwa njia mwafaka ya kuokoa ndoa ya mama Mather ambaye alikuwa bado ana vidonda ambavyo niliamini havitapona kutokana na uchafu wa mumewe ambao umejificha katika kivuli cha kumuabudu Mungu. Nilijiuliza kama wote wanaojiita wachunga kondoo wa Bwana kama wana tabia za mzee Sifael, hao kondoo zizini watabakia wangapi? Wasiwasi wangu ulikuwa kama kweli mzee Sifael ambaye ana heshima kubwa mbele ya waumini wa kanisa ambao humsalimia kwa kumshika mkono kwa unyenyekevu wakiamini mkono wake una chembe za baraka kutokana na ucha Mungu wake, kama alistahili heshima ile. Basi, mpaka Kristo atakaporudi zizi litakuwa tupu kwa kondoo wote kugeuzwa mishikaki na wachungaji uchwara wanaomcha Bwana kwa midomo yao lakini mioyo yao imeoza na inanuka huku harufu yake ikiwa haivumiliki. Nilifikiria jinsi mama Mather alivyompokea Bwana moyoni lakini mumewe ni shetani, machozi yalinitoka bila kizuizi. Kwa kweli siku ile niliporudi nyumbani sikupenda kuwa karibu na watu zaidi ya kujifungia ndani kujiuliza nimekubali kuondoka nitakwenda wapi? Na huko niendako nani atakuwa mwenyeji wangu. Siku za nyuma niliwajua wasichana wengi waliokimbilia mjini kutafuta kazi labda wangeweza kunisaidia. Niliamini kama ningekuwa sina ujauzito ningeweza kwenda mjini kwa tiketi ya kutafuta kazi, Lakini kwenda na ujauzito nilijiuliza nitaishi vipi na hata nikishikwa na uchungu nani CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.comatakayenisaidia. Lakini moyoni niliapa kwamba nikipata fedha nitaondoka tu, nilijua nikiendelea kuwepo pale huenda hali yangu ya ujauzito ingeonekana na kuwafanya wawe na maswali ambayo ningeshindwa kuyajibu. Nikiwa nimejilaza ndani, niliwaza niende mkoa gani ambao kidogo una unafuu wa maisha, wazo la haraka lilikuwa kwenda Dar es Salaam ambao nilielezwa na watu pamoja na changamoto kubwa lakini una unafuu kubwa ya maisha kama utajishughulisha. Nami niliamini kutokana na fedha nitakayokuwa nayo basi niwe mjasiriamali kama marehemu mama alivyokuwa akifanya katika kuyaendesha maisha yake. Niliamini kwa muda ambao ujauzito wangu unakuwa, nami nitakuwa tayari nimeishapata mwanga wa kufanya shughuli yoyote. Swali likabaki nitaondokaje na nguo zangu lazima nitaulizwa na nyumba haikuwa na mlango mwingine ambao ningeweza kuutumia kutoka ndani bila kuonekana.

    Sikujua nitafanyaje lakini nilipanga kuondoka siku ya pili yake pale nitakapokwenda kuchukua fedha. Sikutaka kurudi tena nyumbani kuogopa kupata wakati mgumu wa kutoroka. Lakini sikutaka kuumiza kichwa, nilipanga akirudi baba nimweleze na yeye atajua atanisaidia vipi. Kwa vile nilikaa ndani kwa muda mrefu, nilitoka na kukaa na mama ambaye muda mwingi alikuwa peke yake akisoma Biblia. Niliposogea karibu yake alinitazama, nilijikuta nikikwepesha macho yangu, hakuendelea kunitazama badala yake aliendelea kusoma Biblia yake. Hakusoma sana aliiweka pembeni na kunigeukia. “Ester,” aliniita. “Abee mama.” “Una tatizo gani mwanangu?” aliniuliza huku akinitazama usoni. “Mimi?” Swali lile lilinishtua kwa vile sikulitegemea. “Ester, kwani swali hili nimemuuliza nani?” “Mimi.” “Hebu nieleze una tatizo gani?” “Sina tatizo,” nilikataa kwa kuamini hajui lolote juu ya ujauzito wangu, labda kitu kingine. Itaendelea katika Gazeti la Risasi Jumamosi. “Ester mwanangu una tatizo, mimi ndiye mama yako japo sijakuzaa lakini sasa hivi ni zaidi ya mama yako naomba unieleze usinifiche kitu, una tatizo gani linalokusumbua?” “Mama mbona mimi nipo sawa,” nilijitetea. “Hapana, mi mtu mzima nina uzoefu wa kumjua vizuri mtu, si wewe Ester ambaye mwanzo alikuwa Salha ninayemjua, kuna mabadiliko makubwa sana hasa toka siku ile iliyoweweseka usiku.” “Mama nipo sawa ni wasiwasi wako tu.” “Si kweli, unaonesha kila siku ukiilazimisha furaha usoni mwako lakini kuna kitu kizito moyoni mwako. Hata ndugu zako wameishaniuliza una tatizo gani, lakini sikutaka kukuuliza haraka, nilijitahidi kuona labda utabadilika lakini tangu jana kuna kitu kingine kimetokea hata ule uchangamfu wako umepotea. “Umekuwa mwenye mawazo kila unapokuwa peke yako, unakuwa unahama kabisa kimawazo na kubakia mwili tu lakini wewe haupo sawa kabisa. Nakuomba mwanangu nieleze tatizo lako ni nini? Basi mweleze hata baba yako kama unaona huwezi kuniambia mimi.”

    “Ester mwanangu una tatizo, mimi ndiye mama yako, japo sijakuzaa lakini sasa hivi ni zaidi ya mama yako, naomba unieleze usinifiche kitu, una tatizo gani linalokusumbua?” “Mama mbona mimi nipo sawa,” nilijitetea. “Hapana, mi? mtu mzima nina uzoefu wa kumjua vizuri mtu, si wewe Ester niliyekuwa nakujua

    mwanzo, kuna mabadiliko makubwa sana hasa toka siku ile uliyoweweseka usiku.” “Mama nipo sawa ni wasiwasi wako tu.” “Si kweli, unaonesha kila siku unailazimisha furaha usoni kwako lakini kuna kitu kizito moyoni mwako. Hata ndugu zako wameshaniuliza kama una tatizo gani, lakini sikutaka kukuuliza haraka. Nilijitahidi kuona labda utabadilika lakini tokea jana kuna kitu kingine kimetokea, hata ule uchangamfu wa kulazimisha umepotea. “Umekuwa mtu mwenye mawazo, kila unapokuwa peke yako unakuwa unahama kabisa kimawazo na kubakia mwili pekee lakini wewe haupo kabisa. Nakuomba mwanangu nieleze tatizo linalokusumbua au hata umueleze baba yako kama unaona huwezi kuniambia mimi.” Mama aliniuliza kwa sauti iliyoonesha jinsi gani anaumia na matatizo yangu asiyoyajua. Maneno ya mama yalikuwa mazito moyoni mwangu kama kisu butu kilichoupasua moyo wangu bila ganzi. Nilihisi uchungu wa ajabu na kuanza kulia kilio ambacho niliamini kabisa kitazidi kumweka njia panda mama. Sikuweza kuvumilia, nilijikuta nikijitupia kifuani kwa mama na kuangua kilio cha sauti, nikiamini bado sitakiwi katika dunia ya watu bali najilazimisha tu kuishi. Nilijiuliza kwa nini kila siku niwe mimi tu, mama aliendelea kunibembeleza. “Ester mwanangu kuna kitu kizito kilitokea humu ndani, maono yangu ya kwenye njozi yananionesha lakini kwa nini hutaki kusema?” “Kitu gani mama?” nilishtuka kusikia vile na kujiuliza ni maono gani aliyoyaona ndotoni kwa kujitoa kifuani mwake. “Kuna kitu kinanionesha kuna tukio umefanyiwa na baba yako japo unaficha.” “Hapana mama sijafanyiwa kitu chochote na baba,” nilikataa kwa nguvu zote. “Lakini maono yangu yananionesha kuna aibu kubwa itaikumba nyumba hii bado sijajua ni kwa ajili ya ukimya wako au nini.” “Mama, baba hajanifanyia kitu chochote, kama angekuwa kanifanyia jambo kwa nini nisikwambie? Pia hata baba nisingekuwa naye karibu.” “Mmh! Sawa, lakini ndoto zangu huwa hazisemi uongo lazima itanipa jibu ndani ya miezi mitatu.” “Lakini mama labda ni ndoto za kumkumbuka mama yangu ndizo zilizonichanganya.” “Umeota mara ngapi?” “Ni siku ileile tu mama.” “Si kweli, ndoto ile ingetoka kama ungekuwa unanyanyaswa, lakini hapa unaishi kama wewe na kina Martha mmezaliwa tumbo moja. Kuna kitu unakificha lakini kumbuka mwanangu moto hata siku moja haufunikwi kwa shuka, lazima moshi utaonekana. “Kumbuka toka siku ile ulipoweweseka usiku umekuwa ukipungua kila siku, naishika Biblia hii ambayo naiamini, una jambo zito ambalo linahitaji msaada wa haraka kulitatua bila hivyo linaweza kupasuka kama bomu.” Niliamini mama alikuwa akihisi kitu ambacho alitaka nikitamke kwa mdomo wangu na si kingine, nikiri nimebakwa na baba ili auwashe moto. Lakini niliapa mpaka naondoka duniani nitaondoka na siri yangu moyoni. Niliamua kusema uongo ili aniache akitegemea kuna kitu nitamwambia. Lakini akishtuka atakuta sipo hivyo bado atabakia na swali lisilo na jibu. “Mama kuna kitu kinanisumbua wala hakihusiani na humu ndani, nimepata shida sana kusema lakini kwa vile umenitambua nakuahidi mama yangu kukueleza kila kitu, lakini si leo.” “Unataka kunieleza lini?” “Baada ya siku mbili.” “Kwa nini usinieleze leo?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com

    “Hapana mama mazungumzo yanahitaji nijiandae.” “Estaaa! Ujiandae vipi mwanangu?” “Najua utashangaa lakini kwa vile nimekueleza nitakwambia, nakuomba nipo chini ya miguu yako nikubalie.” “Sawa nimekukubalia, lakini nakuomba mtangulize Bwana Yesu kwa kila tatizo linalokuja mbele yako, hakika utaibuka mshindi.” “Sawa mama.” Baada ya kusema vile mama alinishika mkono kichwani na kunifanyia maombi mazito ili niondokewe na matatizo. Baada ya maombi ya zaidi ya dakika ishirini mama aliniacha. “Ester mwanangu kila unachokiona ni hila za shetani ambaye yupo kwa ajili ya kutuharibia wanadamu. Lakini siku zote mfanye Bwana ndiye kimbilio lako na siku zote shetani hushindwa.” “Amina, mama, siku zote nimekuwa nikifanya hivyo lakini bado matatizo yananifuata likitoka hili linakuja hili.”



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog