Search This Blog

Friday, July 15, 2022

VIGANJA MASHAVUNI MWANGU - 3

 







    Simulizi : Viganja Mashavuni Mwangu

    Sehemu Ya Tatu (3)

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Sikujua alikuwa na mawazo tele, aliwachukua watoto wale na kuishi nao huku kila mmoja akijua kwamba walikuwa wameuawa ufukweni. Hawakuwa watoto wasumbufu, hawakuwa watoto wa kulia na kwa sababu walikuwa wamemzoea sana, muda wote walionekana kuwa na furaha mno.

    Moyo wake ulimuuma mno, alijua ni kwa jinsi gani CAssian na mkewe, Naseku walikuwa wakiumia, walilia na hivyo alichokifanya ni kutamani kuwasiliana nao kwa lengo la kuwakabidhi watoto wao.

    Hakutaka kuchelewa, haraka sana akachukua simu na kumpigia Cassian, simu haikuita sana, ikapokelewa na sauti ya mwanaume huyo kuanza kusikika upande wa pili.

    “Sikujua!” aliita Cassian, kwa jinsi alivyosikika, msichana huyo akajua kwamba aliwekwa loud speaker, ila hakutaka kujali.

    Hakutaka kupindisha maneno, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumuomba msamaha kwa kila kitu alichokuwa amekifanya, alijua kwamba aliwaumiza na kuwafanya kulia lakini aliyafanya yote hayo kwa kuwa nyuma kulikuwa na mtu aliyemlazimisha kufanya hivyo.

    Hakutaka kuficha, alimwambia Cassian kwamba mtu aliyekuwa amemtuma alikuwa Evelyne ambaye alilipa kiasi kikubwa cha pesa kuhakikisha watoto hao wanauawa haraka iwezekanavyo kwa kuwa tu siku za nyuma aliumizwa hivyo na yeye alitaka kuwaumiza.

    Cassian aliposikia maneno hayo, mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda kwa kasi, hakuamini alichokisikia, ilikuwa msichana huyo aendelee kuwafuatilia na wakati walikuwa wamekwishamalizana tangu kitambo? Moyo wake ukawaka kwa hasira, hakutaka kuona akibabaishwa na msichana huyo hivyo ilikuwa ni lazima kupambana naye.

    “Watoto wangu wapo wapi?” aliuliza Cassian huku akitetemeka, pembeni alikuwepo mke wake aliyekuwa akisikia kila kitu, machozi yalikuwa yakimtoka kwa furaha kwani aliamini kwamba angewapata watoto wake.

    “Ninao!”

    “Unao hapo? Niambie upo wapi nikufuate,” alisema Cassian.

    “Naogopa!”

    “Unaogopa nini?”

    “Utanikamata!”

    “Sikujua! Umenisaidia, uliagizwa kuwaua watoto wangu, hukufanya hivyo, kwa maana hiyo umenisaidia, siwezi kukumata. Nakuahidi hata kuja huko nakuja na mke wangu tu. Usiogope, niambie upo wapi,” alisema CAssian.

    Alimaanisha, alichokuwa akikihitaji kilikuwa ni watoto wake tu, japokuwa Sikujua alikuwa akiogopa lakini hakuwa na jinsi, akawaambia mahali alipokuwa na mwanaume huyo kwenda huko kuwachukua watoto wake.

    Njiani, hakukuwa na aliyeamini, hawakujua ni kwa namna gani walitakiwa kumshukuru Sikujua ambaye alitumwa kuwaua lakini hakutaka kufanya hivyo kwa kuwa tu moyo wake ulijikuta ukishikwa na upendo wa ajabu, huruma ambayo haikuwahi kumpata kabla.

    “Mke wangu! Usilie, ngoja tukawachukue watoto wetu,” alisema Cassian huku akiendesha gari kuelekea Magomeni.

    Hawakuchukua muda mrefu wakafika huko, kwa maelekezo ya msichana huyo, wakatokea nyumbani kwake alipokuwa akiishi na kuingia ndani. Hawakuamini, waliwakuta watoto wao wakiwa kwenye kochi sebuleni huku kukiwa na chupa ya maziwa pembeni.

    Haraka sana Naseku akawasogelea, akawabeba kisha kuwakumbatia. Huzuni aliyokuwa nayo moyoni, kilio alichokuwa amelia kwa siku tatu mfululizo kikapotea, furaha ya ajabu ikamuingia moyoni mwake.

    Cassian akamsogelea mke wake na kumkumbatia. Wakati hayo yote yakiendelea, Sikujua alikuwa pembeni, alionekana kuwa na hofu nzito moyoni mwake, aliteteka, hakujiamini, aliona kama mwanaume huyo angemfanyia jambo lolote lile baya.

    “Hutakiwi kuogopa Sikujua,” alisema Cassian huku akimwangalia msichana huyo.

    Walimshukuru msichana huyo kwa wema wake, hawakuwa na cha kumlipa kwani kwa kuwaokoa watoto wao walimaanisha kwamba hiyo ilikuwa ni zaidi ya pesa, kilikuwa kitu kikubwa ambacho hata kama wangemlipa milioni mia moja bado isingelingana na kile alichowafanyia.

    “Unataka tukufanyie nini?” aliuliza Cassian huku akimwangalia Sikujua.

    Msichana huyo hakuhitaji kiasi chochote cha pesa, kitu pekee alichokihitaji ni kuwa huru tu. Hiyo haikutosha, Cassian akamuahidi kwamba angemlipa kiasi cha shilingi milioni hamsini, angemfungulia biashara kwanii kwa jinsi maisha aliyokuwa akiishi hapo nyumbani kwake, hayakuwa mazuri hata kidogo.

    “Halafu mimi niache nidili na huyu msichana,” alisema Cassian kisha kuondoka nyumbani hapo huku Sikujua akiwa na amani tele moyoni mwake.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Huo ndiyo ukawa mwanzo, kupatikana kwa watoto hao ilikuwa siri kubwa, aliamini kwamba kama wasingewaficha basi hali ya Sikujua kule alipokuwa ingekuwa mbaya, inawezekana wenzake ambao walikubaliana wawamalize wakajua kwamba walidanganywa na hivyo kumuua yeye.

    Akamuhakikishia ulinzi na hivyo kuendelea na maisha yao kama kawaida. CAssian alipanga kumtafuta Evelyne, alitaka kummaliza kwa kile alichokiona kwamba kingemfanya kuwa na amani moyoni mwake, akamwambia mke wake alichotaka kukifanya kwamba amtafute msichana huyo na kumuua lakini mkewe akamsihi kwamba hakutakiwa kufanya hivyo.

    “Ila alitaka kuwaua watoto wetu!” alisema Cassian.

    “Bado si sababu!”

    “Kwa hiyo tumuache?”

    “Ikiwezekana!”

    “Ila atarudi tena na kuwaua endapo atajua kwamba wapo hai!” alisema Cassian.

    “Tuongeze ulinzi, uwe mkubwa zaidi na tusimwamini mtu,” alisema Naseku.

    Mkewe akaubadilisha moyo wake, maneno mazito yakamuingia na kumwambia kwamba hakutakiwa kulipa ubaya kwa ubaya bali alitakiwa kulipa ubaya kwa wema, akaamua kuachana na msichana huyo na kufanya mambo yake.

    Familia ikawa ya furaha tena, siku zikakatika, kila mtu aliyafurahia maisha yake. Kuwa na watoto hao ndani ya nyumba ilikuwa siri kubwa, cha ajabu kabisa hata polisi hawakujua kama watoto hao walipatikana.

    Ulinzi ukawa mkubwa, hakukuwa na mtu aliyeruhusiwa kuingia ndani ya nyumba hiyo kiholelaholela, Cassian na mkewe wakaishi kama jinsi ambavyo mabilionea walivyokuwa wakiishi. Siku zikakatika, miezi ikakatika mpaka watoto hao, Walter na Walker walipofikisha umri wa miaka miwili.

    Walikuwa wameungana kama ilivyokuwa. Japokuwa walikuwa hivyo lakini hawakutaka kabisa kwenda kuwatenganisha, waliungana sehemu mbaya, walichangia sehemu ya ubongo, kwa kuwaangalia, walionekana kuwa na furaha tele, hawakuonekana kuumizwa na hali waliyokuwa nayo.

    Japokuwa walikuwa wameungana lakini watoto hao walikuwa wazuri wa sura, hata wazazi wao walipokuwa wakiwaangalia, walionekana kuwapenda, walivutia na walikuwa na uhakika kwamba wangemvutia msichana yeyote ambaye angewaangalia.

    Walipofikisha umri wa miaka mitatu wakaanza kusoma katika shule ya chekechea ya Amazon Day Care iliyokuwa Mikocheni B, shule iliyokuwa ikisomwa na watoto wa mawaziri na matajiri mbalimbali Tanzania. Mbali na watoto wa matajiri, pia kulikuwa na watoto wa mabalozi wa nchi mbalimbali.

    Siku ya kwanza kufika shuleni hapo kila mtu alikuwa akiwashangaa, walimu hawakuamini kama wangeweza kuwaona watoto walioungana kama hao, walizoea kuwaona katika televisheni na sehemu nyingine lakini hawakuamini kama ingetokea siku wangewaona kwa macho yao.

    Waliwashangaa lakini wakati mwingine waliamini kwamba Mungu alikuwa wa ajabu sana kwani pamoja na kuungana huko watoto hao walikuwa wazuri mno, sura zao zilionyesha kabisa kwamba huko mbeleni wasichana wangechanganyikiwa nao sana.

    “Jamani hawa watoto wazuri sijawahi kuona,” alisema mwalimu Getrude huku akiwaangalia watoto hao, alitamani hata wangekuwa watoto wao.

    “Kweli kabisa. Ningepata watoto wenye sura nzuri kama hawa, nadhani ningewaambia wazazi wa watoto wa kike mtaani kwangu wawe makini na mageti yao,” alisema mwalimu Susan na wote kuanza kucheka.

    Walimu walikuwa wakiuzungumzia uzuri wa watoto hao, walikuwa na uzuri wa ajabu mno. Shuleni hapo walikuwa wachangamfu mno, japokuwa kwa siku za kwanza watoto wengine walikuwa wakiwaogopa lakini mwisho wa siku wakawazoea na kucheza nao kiasi kwamba kila mmoja alifurahia uwepo wa watoto hao shuleni hapo.

    “Jamani! Nina wasiwasi, wale Jackline na Rosemary, nahisi baadaye huko kutakuja kutokea jambo,” alisema mwalimu Susan ofisini.

    “Wale watoto wa mabalozi?”

    “Ndiyo! Yaani naona wamezidisha ukaribu na watoto hawa. Wakiendelea kuwa karibu hivi kila siku, miaka na miaka, kuna jambo linaweza kutokea,” alisema mwalimu huyo na wengine kuanza kucheka.

    Jackline alikuwa mtoto wa Balozi wa Marekani, Bwana Godluck Puff huku Rosemary akiwa mtoto wa Balozi wa Uingereza, Bwana Emmanuel Sinclair. Wawili hao walianza kusoma kutika shule hiyo, walikuwa watoto wa Kizungu waliokuwa wazuri mno.

    Walikuwa watoto wakimya sana, hawakuwa wazungumzaji lakini tangu Walter na Walker wahamie shuleni hapo, watoto hao wakaanza kuonyesha uchangamfu wa ajabu kiasi kwamba hata walimu walikuwa wakiwashangaa.

    Walikuwa wakicheza pamoja, kula pamoja na kufanya vitu vingine pamoja. Katika kipindi ambacho watoto hao walipokuwa wakifuatwa na wazazi wao kurudi nyumbani ilikuwa ni kilio, hawakutaka kuachana, hawakutaka kuona wakitenganishwa, kila siku walitamani kuwa pamoja.

    Kutokana na ukaribu wa watoto wao, Cassian na mkewe wakajikuta wakiwa karibu na wazazi wa watoto hao wa kike, kwa kuwa walitambua kwamba walizoeana, wakaanza kuwapeleka nyumbani kwao na kuanza kucheza pamoja na wakati mwingine kutoka nao pamoja kitu kilichowafanya watoto hao kuwa na furaha tele.

    Ilikuwa ni kama wamegawana, Jackline akawa karibu sana na Walter huku Rosemary akiwa karibu sana na Walker, kwa kifupi walikuwa na urafiki wa ajabu, urafiki uliomshangaza kila mtu aliyekuwa akiwaangalia. Walikuwa watoto hivyo kila mmoja kuhisi kwamba ni utoto tu lakini cha ajabu kila walivyozidi kukua, ukaribu ukaongezeka zaidi

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Watoto wao ndiyo walikuwa furaha yao, kila walipokuwa wakiwaangalia, mioyo yao ilijisikia faraja na kuona kwamba Mungu aliwabariki kwa kuwapa watoto hao waliokuwa na sura nzuri kupita kawaida.

    Kila siku ilikuwa ni lazima kwa Naseku kuwapeleka watoto wake shuleni kwa gari lake, hakutaka kumwamini mtu na kitendo hicho kilionekana kuwa sahihi kwa kuwa kilimfanya kuwa karibu na watoto wake.

    Walter na Walker waliendelea kukua, walikuwa watoto wenye furaha tele kiasi kwamba mpaka watu wengine walikuwa wakishangaa kwani walijua kwamba wangekuwa kwenye huzuni tele kutokana na hali ya kuungana lakini ndiyo kwanza kila siku walikuwa watoto wa kucheka tu.

    Siku zikaendelea kukatika, watoto Catherine na Jackline waliendelea kuwa pamoja nayo, kwenye kila hatua waliyokuwa wakikua, walikuwa pamoja huku ukaribu wao ukiongezeka kila siku.

    Baada ya miaka minne, wakaanza kusoma darasa la kwanza katika shule hiyohiyo. Ilikuwa ni furaha kwao, walisoma kwa bidii, walipendwa kila kona, kwa darasani, hawakuwa na akili nyingi lakini kila siku walionekana kupenda sana kusoma.

    Watu waliwapenda kwa kuwa walikuwa na sura nzuri. Katika kipindi hichohicho cha darasa la kwanza ndipo walimu wakagundua kwamba mapacha hao walikuwa na vipaji vikubwa mno.

    Walter alikuwa na uwezo mkubwa wa kuimba, kila alipokuwa akiambiwa aimbe wimbo wowote ule, sauti yake iliwashangaza watu wengine, wakabaki wakishangaa, hawakuamini kama duniani kulikuwa na mtoto aliyekuwa na sauti kali ya kuimba kama ilivyokuwa kwa Walter.

    Kwa Walker, hakuwa muimbaji, yeye alikuwa na uwezo wa kuchora. Tangu alipokuwa chekechea, hakukuwa na kitu alichokipenda kama kuchora, alijua kuchora sana zaidi ya watoto wengine.

    Vipaji vyao havikujificha, kwa kuwa vilikuwa vimeonekana, walichokifanya Cassian na mkewe ni kuwaendeleza katika vipaji hivyohivyo walivyokuwa navyo. Kwa Walter, akatafutiwa mwalimu wa kwaya kwa ajili ya kumfundisha namna ya kuimba na kupangilia sauti yake.

    Uwezo wake ulikuwa mkubwa mno, kila alipokuwa, maisha yake yalikuwa ni kuimba tu. Kanisani alikuwa gumzo, japokuwa alikuwa na miaka saba lakini kila mmoja alipenda kusikia namna alivyokuwa akiimba, aliwafurahisha watu wengi kiasi kwamba kanisani hapo akawa muimbaji kiongozi, kwenye kila ibada ya kusifu na kuabudu, alikuwa akichaguliwa yeye.

    Wakati Walter akiwa muimbaji, Walker hakuwa na uwezo wowote wa kuimba, yeye alikuwa mchoraji, alikuwa na uwezo mkubwa wa kuchora kiasi kwamba mpaka watu wengine walikuwa wakishangaa.

    Walter alikuwa mzungumzaji, alipenda sana kuongea, alikuwa na uwezo wa kuongea maneno mengi kwa wakati mmoja lakini Walker alikuwa mkimya, hakuwa mzungumzaji, mpole ambaye muda wote alionekana kuwa siriazi kupita kawaida.

    “Who do you want to be?” (unataka kuwa nani?) aliuliza Cassian huku akiwaangalia watoto wake.

    “A Pop star like Michael Jackson,” (niwe staa wa Pop kama Michael Jackson) alijibu Walter harakaharaka.

    “What about you?” (vipi kuhusu wewe?) aliuliza Cassian huku akimwangalia Walker.

    “I want to be a greatest picture artist ever in the world,” (nataka kuwa mchoraji bora kuliko wote waliowahi kutokea katika dunia hii) alisema Walker huku akimwangalia baba yake.

    Waliishi katika ndoto, kila siku ilikuwa ni lazima kufanya mazoezi kwa kile walichokuwa wakitaka kuwa. Bado vipaji walivyokuwa navyo viliwashangaza watu wengi, hawakuamini kama kungekuwa na watoto waliokuwa na uwezo mkubwa kwa vile walivyokuwa nacho kama wao.

    Kwenye mashindano mbalimbali shuleni, walipewa zawadi nyingi, waandishi wa habari waliposikia kuhusu wao, wakaanza kuwatafuta kwa lengo la kuzungumza nao na kuandika mengi kuhusu watoto hao.

    Kuwapata halikuwa jambo jepesi, kila walipokwenda shuleni hapo, walikataliwa kuonana nao kwani ulinzi wao ulikuwa mkubwa kutokanma na heshima kubwa aliyokuwanayo baba yao.

    Waandishi hao hawakukoma, kila kona walipokuwa waliendelea kusikia sifa za watoto hao, walikuwa wakiwashangaza kila mtu aliyekuwa akisikia kuhusu wao, juu ya vipaji vikubwa walivyokuwa navyo.

    Kwa mwaka mzima walikuwa wakiwatafuta lakini hawakuweza kuwaona. Walipofikisha umri wa miaka kumi, baba yao akawafungulia chaneli katika Mtandao wa Youtube kwa ajili ya kuionyesha dunia kwamba kulikuwa na watoto waliokuwa na vipaji vya hatari ambao walikuwa wameungana.

    Kwa kutumia pesa zake, akaanza kuitangaza chaneli hiyo, watu wengi wakaiona na kuangalia vipaji vya watoto hao. Kila mmoja aliyekuwa akiangalia alishangaa, hakuamini kama katika dunia hii kungekuwa na watoto waliokuwa na uwezo kama Walter na Walker.

    Wakaanza kupata umaarufu wakiwa wadogo kabisa. Katika kila kona ya dunia walikuwa wakizungumziwa wao tu. Watu wengi wakataka kufahamu mahali walipokuwa, walitaka kujionea kwa macho yao uwezo mkubwa waliokuwa nao watoto hao.

    Waandishi kutoka BBC, CNN na vituo vingine vya habari vya kimataifa vikasafiri mpaka nchini Tanzania kwa lengo la kuonana na watoto hao. Halikuwa jambo jepesa kuwapata, walikuwa watoto wa ndani tu na hata walipokuwa shuleni, ilikuwa vigumu mno kuwaona.

    Waandishi hao wakatumia majina ya vituo vyao, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumtafuta Cassian, hakuwa mwepesi kuonana na watu hasa alipokuwa ofisini kwake, waandishi hao walihangaika kwa muda wa wiki nzima ndipo wakakutana naye na kuanza kufanya naye mahojiano.

    Walimwambia wazi jinsi walivyokuwa wakishangazwa na vipaji walivyokuwanavyo watoto hao, kila mtu alishangaa, haikuwa Afrika tu bali dunia nzima ilikuwa ikistaajabu kwa kile kilichokuwa kikiendelea.

    Moyo wa Cassian ukajisikia faraja, watoto wake wakawa maarufu, hilo ndilo alilitaka kwa kipindi kirefu, alijua kwamba walikuwa wameungana, alijua kwamba kama wangeendelea kuishi hivyo tu ilikuwa ni lazima kukata tamaa na kujiona kwamba hakukuwa na tumaini jingine na wakati mwingine hata kumlaumu Mungu na ndiyo maana alikuwa akipambana kuhakikisha kwamba wanakuwa na furaha hata kama wanakuwa kwenye hali ya kuungana.

    “Wana miaka mingapi?” aliuliza mwandishi wa BBC.

    “Miaka kumi ila mwaka huu katikati watakuwa na miaka kumi na moja,” alisema Cassian.

    “Na una watoto hawa tu?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ndiyo! Ila mama yao ni mjauzito. Natumaini kupata mtoto mwingine mwaka huu,” alijibu Cassian.

    Alikuwa akiulizwa maswali mengi kuhusu Walker na Walter, baada ya kumalizana naye wakataka kuwaona watoto hao na kufanya nao mahojiano kitu ambacho hakikuwa na tatizo lolote lile.

    Wakaondoka na kuelekea nyumbani huko, walitakiwa kuwasubiri mpaka watakaporudi kutoka shuleni. Hilo halikuwa tatizo, walisafiri kutoka nchini Marekani, Uingereza mpaka Tanzania kwa ajili ya watoto hao tu, hivyo wakawasubiri, na baada ya saa mbili, watoto hao wakafika nyumbani na kuanza kuwahoji baadhi ya maswali huku wakiwaonyeshea jinsi vipaji vyao vilivyokuwa hatari.

    Dunia ikazidi kuwatambua, waliendelea kujulikana kila kona. Wazungu hawakutaka watoto hao wakae Tanzania, walichokifanya ni kuandaa matamasha na hivyo kuwaomab wazazi hao ruhusa ya watoto hao kushiriki katika matamasha mbalimbali yaliyokuwa yakifanyika humo.

    Pesa zikazidi kuongezeka katika akaunti ya Cassian, akawaongezea pesa watoto wake, nao, wakaanza kupata utajiri mkubwa, kwenye kila tamasha walilokuwa wakihudhuria, watu walikuwa wakilipia sana kwa ajili ya kuona miujiza waliyokuwa nao watoto hao.

    Mbali na kupokea pesa za waandaaji wa matamasha, pia wamiliki wa YouTube wakaanza kuwalipa pesa nyingi kwani chaneli yao ilikuwa ikitazamwa na watu wengi, mpaka kufika idadi ya watu bilioni moja, idadi ambayo ilikuwa ikiwafukuzia Justin Bielber kwa video yake ya wimbo wa Sorry na Adele kwa wimbo wake wa Helo.

    They have received cheque of twenty milion dollars from YouTube,” (wamepokea cheki ya dola milioni ishirini kutoka Youtube) alisema jamaa mmoja aliyekuwa akiangalia kwenye mtandao kuhusu watoto hao.

    “Sure?” (kweli?)

    “Yeah! Check this out,” (ndiyo! Angalia hii)

    Kwa kuwa walikuwa wakiishi sana katika nchini za huko, baba yake, Cassian akaamua kuwaanzisha masomo katika shule ya St. Monica iliyokuwa Washington nchini Marekani, shule ambayo ilikuwa ikikuza sana vipaji vya watoto waliokuwa mahali hapo.

    Hapo, kulikuwa na waimbaji wengi lakini kitu cha ajabu kabisa kila mmoja alikuwa akimshangaa Walter, alikuwa akiimba kiasi kwamba wengine wakampa jina la malaika, waliamini kwamba sauti yake ilikuwa nzuri hata ya hao malaika waliokuwa na kazi kubwa ya kumsifu na kumwabudu Mungu.

    Kwa Walker kila mtu alikuwa akishangaa, alikuwa mchoraji mkubwa, alijua kuchora picha za kila aina, kila mtu aliyekuwa akiziangalia picha zake alikuwa akipigwa na butwaa, alikuwa hatari katika uchoraji wake.

    Waliishi nchini Marekani, wazazi wao walikuwa wakienda kuwaangalia mara kwa mara. Na baada ya miezi kadhaa baba yao akawaambia kwamba mama yao alijifungua salama mtoto wa kike na kuamua kumpa jina la Ester.

    “Is this the one?” (ndiye huyu?) aliuliza Walter huku akiangalia picha ya Ester.

    “Yes! She is!” (Ndiyo! Ndiye yeye)

    “We look alike,” (tumefanana sana) alisema Walker huku naye akiiangalia picha hiyo.

    Miaka saba baadaye, walikuwa watu maarufu kuliko wote nchini Marekani. Majina yao yaliongoza kutafutwa katika tovuti ya Google kitu kilichomaanisha kwamba kwenye kila kona watu walikuwa wakitaka kufahamu mambo mengi kuhusu hao.

    Katika kipindi hicho ndipo wakakumbuka kitu. Kipindi walichokuwa wadogo kulikuwa na wasichana wawili waliokuwa marafiki zao sana nchini Tanzania, wasichana hao walikuwa Catherine na Jackline.

    Hawakujua mahali walipokuwa, waliondoka nchini Tanzania zamani sana na hawakujua kama wasichana hao walikuwa hai au walikufa.

    Walichokikumbuka ni kwamba mmoja alikuwa mtoto wa balozi wa Uingereza nchini Tanzania na mwingine mtoto wa balozi wa Marekani nchini Tanzania hivyo kuanza kuwatafuta katika mitandao ya kijamii.

    “I’ve got her,” (nimempata) alisema Walker huku akiiangalia kompyuta yake, alikuwa amempata rafiki yake wa utotoni, Rosemary.

    “How about Jackline? Did you find her?” (vipi kuhusu Jackline? Umempata?) aliuliza Walter huku akiwa na hamu ya kujua mahali alipokuwa msichana huyo.

    “Give me one sec,” (nipe sekunde moja)

    Haraka sana Walker akaanza kuangalia kwenye tovuti ile, alikuwa akimtafuta msichana huyo kwa kumsaidia ndugu yake huyo. Alichukua dakika zaidi ya tano kuangalia kila kona, kila alipoona jina lililofanana na la rafiki wa ndugu yake, alikuwa akiliangalia kuona kama alikuwa yeye au la.

    “I’ve found her!” (nimempata) alisema Walker huku akimwangalia ndugu yake, japokuwa alikuwa akimwambia habari nzuri, uso wake ulionyesha kuwa na shaka kupita kawaida.

    “Let me see,” (acha nione) alisema Walter na kisha kuanza kuangalia, alitaka kujua sababu iliyomfanya ndugu yake kuwa katika hali hiyo.

    Haraka sana akaichukua iPad aliyokuwa nayo ndugu yake na kuanza kuangalia. Kile alichokiona hakuonekana kuamini, aliliona jina la msichana huyo, picha yake lakini habari ambayo ilimshangaza ni kwamba msichana huyo alikuwa amepata ajali mbaya ya gari alipokuwa akielekea chuoni Oxford nchini Uingereza.

    Walter hakuamini alichokuwa akikiangalia, akahisi kama kitu chenye ncha kali kikiwa kimeuchoma moyo wake, baada ya sekunde kadhaa, machozi yakaanza kumtiririka mashavuni mwake.

    Hakutaka kukubali, hakutaka kuona rafiki yake huyo akiteseka kitandani na wakati yeye alikuwa hai. Alichokifanya ni kumwambia Walker kwamba ilikuwa ni lazima kusafiri na kuelekea nchini Uingereza kwa ajili ya kumuona msichana ambaye alihisi kumpenda kwa penzi la dhati moyoni mwake.

    Wakawasiliana na wazazi wao na kuwaambia kwamba ilikuwa ni lazima kusafiri kuelekea nchini Uingereza kwa ajili ya kumuona msichana huyo aliyekuwa hoi kitandani.

    “Hamuwezi kwenda peke yenu! Nisubirini!” alisema Cassian kwenye simu.

    “Utachelewa baba!” alisema Walter.

    “Siwezi kuchelewa, nakuja baada ya siku mbili.”

    “Sawa.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Moyo wa Walter ukakosa amani, muda mwingi alikuwa akimfikiria msichana huyo. Alimpenda kutoka moyoni mwake, alijua kwamba kilikuwa kimepita kipindi kirefu sana lakini bado moyo wake ulikuwa kwa msichana huyo aliyekuwa hajitambui kitandani.

    Aliona baba yake akichelewa kuja, alichokuwa akikihitaji ni kumuona msichana huyo tu. Baada ya siku alizoahidi baba yake kutimia, wakaondoka nchini Marekani na kwenda Uingereza ambapo huko wakapelekwa moja kwa mja mpaka katika Hospitali ya Queen Elizabeth kwa lengo la kumuona msichana huyo.

    Walipofika hospitalini, umati mkubwa wa watu ulikuwa ukiwashangaa, wengine wakawasogelea kwa lengo la kupiga nao picha. Walikuwa maarufu, walipendwa na kila mmoja alitamani sana kuwa nao karibu kwani vipaji walivyokuwa navyo vilimshangaza kila mmoja.

    Hawakuwa na haja ya kujitambulisha walikuwa wakina nani bali walikuwa na haja ya kuuliza mahali alipolazwa msichana huyo. Kwa kuwa ulikuwa muda wa kuona wagonjwa, walipoambiwa mahali alipokuwa, haraka sana wakaondoka na kuelekea huko.

    Wakafungua mlango na kuingia ndani. Msichana Jackline alikuwa kitandani, alikuwa kimya, pembeni yake walikuwa wazazi wake, kwa jinsi walivyoonekana tu walikuwa wamekata tamaa, hawakuamini kama binti yao angeweza kuzinduka na kusimama tena.

    Kila walipomwangalia, waliona kabisa huo ndiyo ungekuwa mwisho wake kitandani pale. Walter aliumia mno, alimwangalia Jackline huku akihisi akichomwa na kitu chenye ncha kali, hapohapo machozi yakaanza kumtoka. Mbali na wazazi wa Jackline waliokuwa chumbani humo, pia pembeni yao kulikuwa na kijana mwingine, huyu aliitwa Edmund, kijana aliyekuwa mpenzi wa Jackline aliyekuwa kitandani.



    Walikuwa na umri mdogo lakini walionekana kuwa na mapenzi ya dhati, kila siku walikuwa pamoja huku mtoto Catherine akijitahidi kumuonyeshea Walter kwamba kweli alikuwa akimuhitaji kama rafiki katika maisha yake.

    Siku ziliendelea kukatika, wakaendelea kukua zaidi na zaidi, ukaribu ule ukaongezeka kiasi kwamba Catherine akawa haoni wala hasikii kwa Walter, kila siku ilikuwa ni lazima awe mtu wa kwanza kuzungumza naye shuleni wakati anaingia na awe mtu wa mwisho kuzungumza naye wakati akiondoka.

    Ilikuwa hivyo, wazazi waliendelea kuwashangaa, haikuwa rahisi kuona watoto waliokuwa wakipendana kiasi hicho, walishindwa kuwatenganisha na kwa jinsi walivyokuwa wakiwaona walivyopendana, walihisi kabisa hapo baadaye kungekuwa na ugumu mkubwa kuwatenganisha.

    Siku zikaendelea kukatika, baada ya miaka mitano, baba yake, Bwana Gordon Smith akamaliza muda wake wa kuwa balozi wa Uingereza nchini Tanzania hivyo kurudi na familia yake nchini huko.

    Hilo likawa pigo kubwa kwa Catherine, siku za kwanza zilikuwa ni ngumu sana kwake, alikuwa akilia kila wakati, alikosa furaha na muda mwingi alikuwa mtu wa huzuni tele. Wazazi wake wakajaribu kumletea marafiki wengi wa kukaa naye lakini hakubadilika, bado kichwa chake na moyo wake ulimfikiria mtu mmoja tu, Walter aliyekuwa nchini Tanzania.

    Baada ya miaka mingine mitano kukatika, Catherine akafanya vizuri katika masomo yake na hivyo kuchaguliwa kusoma katika Chuo Kikuu cha Oford kilichokuwa hapohapo Uingereza.

    Bado hakuacha kumfikiria Walter, alimkumbuka mwanaume huyo, alipata marafiki wengi lakini kwa Walter ilikuwa ni tofauti kabisa, alikuwa rafiki aliyejali na kumsikiliza, aliufurahisha moyo wake na muda mwingi alitamani kumuona tena mbele yake, alitamani kumwambia kwamba katika maisha yake yote hakika asingepata rafiki wa kweli kama alivyokuwa yeye.

    Wakati kichwa chake kikimfikiria sana ndipo akaamua kumtafuta katika mtandao. Hakupata kazi kumpata kwani mapacha hao walikuwa maarufu mno nchini humo kutokana na vipaji walivyokuwanavyo.

    Moyo wake ukaridhika, alifurahi kumuona Walter, mwanaume aliyekuwa akimpenda kupita kiasi. Alitamani kusafiri kuelekea nchini Tanzania kwa ajili ya kuonana naye lakini masomo yalikuwa yakimbana na kuwa na ratiba ndefu mno.

    Siku zikakatika, mwanaume huyo aliendelea kuishi moyoni mwake. Kila siku ilikuwa ni lazima kuingia katika chaneli yao iliokuwa YouTube na kuanza kumwangalia jinsi alivyokuwa akiimba, sauti yake nzuri ilimtetemesha, hakuhisi kama kungekuwa na mtu aliyekuwa na sauti nzuri kama ilivyokuwa kwa mwanaume huyo.

    Wakati kichwa chake kikimfikiria Walter ndipo mwanaume mwingine akaanza kujisogeza. Huyu aliitwa Edmund, mwanaume aliyekuwa akisomea masuala ya IT hapo Oxford.

    Siku ya kwanza Edmund alipomuona Catherine moyo wake ulitetemeka mno, hakudiriki kuyatoa macho yake kwa msichana huyo, alikuwa mzuri wa sura, alikuwa mrembo mno kiasi kwamba kila alipokuwa akimwangalia, hakuisha hamu kabisa.

    Akaanza kujipendekeza, kitu cha kwanza alichokuwa akikihitaji ni kuwa rafiki yake, wazungumze kama marafiki lakini mwisho wa siku amwambie ukweli kwamba alikuwa akimpenda kupita kawaida.

    Kwa msichana kama Catherine halikuwa jambo jepesi hata kidogo, alikuwa msichana mgumu kuzoeleka lakini kwa Edmund naye hakuwa mwanaume aliyekuwa na moyo mwepesi wa kukata tamaa.

    Aliendelea kumfuatilia msichana huyo huku kila alipokuwa akimuona, alimfuata na kupiga naye stori. Catherine hakuwa akipenda ukaribu na mwanaume huyo lakini kwa kuwa alianza kumng’ang’ania sana mwisho wa siku akajikuta akiwa karibu naye.

    Kichwa chake kilifikiria urafiki zaidi lakini kichwa cha Edmund kilifikiria mapenzi zaidi. Walikuwa karibu kiasi kwamba mpaka watu wengine wakahisi kwamba wawili hao walikuwa wapenzi.

    Edmund hakutaka kukaa kimya, alijua kwamba kama wangezoeana zaidi basi suala la kaka na dada lingeingilia kati kitu kilichomfanya kuanza kumchombeza msichana huyo kwa maneno ya hapa na pale.

    Siku za kwanza ilikuwa ngumu kwa msichana huyo kuelewa lakini baada ya Edmund kung’ang’ania zaidi, mwisho wa siku akampata msichana huyo na kuanza kuwa wapenzi.

    “Edmund!” aliita msichana huyo.

    “Unasemaje mpenzi!”

    “Naomba nikuombe kitu!”

    “Kitu gani?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kuna mwanaume ninampenda. Tena zaidi ya ninavyokupenda wewe. Kama utataka tuendelee kuishi pamoja, sawa, ila tukubaliane kwamba kama mwanaume huyo akija tena maishani mwangu, naomba tu tuachane kwa amani,” alisema Catherine huku akimwangalia Edmun.

    Edmund akakaa kimya kwa muda, akamwangalia Catherine, maneno aliyozungumza msichana huyo yalikuwa ni yenye kuumiza mno, hakuamini mtu kama Catherine angemwambia maneno hayo kwamba wawe wapenzi wa muda na kama mwanaume aliyekuwa akimpenda angerudi maishani mwake basi huyo ndiyo ungekuwa mwisho wao.

    Hilo halikumuingia akilini hata kidogo lakini aliamini kwamba kama angemkatalia Catherine basi huo ndiyo ungekuwa mwisho wao hivyo alichokifanya ni kumkubalia ili aone huyo mwanaume alikuwa nani ambaye alitaka kulikatisha penzi lake kutoka kwa msichana huyo.

    “Haina shida!”

    “Una uhakika umekubali kutoka moyoni?”

    “Ndiyo mpenzi!”

    “Kabisa?”

    “Kabisa.”

    Catherine akamkumbatia mwanaume huyo, machozi ya furaha yalikuwa yakimtoka kwani hakuamini kama Edmund angekubaliana naye katika hilo.

    Siku zikaendelea kukatika, moyo wa mwanaume huyo ulimkereketa, alitamani sana kumfahamu mwanaume huyo, alikuwa wapi, aliishi wapi na alikuwa akifanya ni kipindi hicho.

    Alijaribu kumdadisi sana Catherine ili amwambie kuhusu mwanaume huyo lakini Catherine alikuwa mgumu kufanya hivyo, alichoambulia ni kujua jina lake tu kwamba aliitwa Walter.

    “Jina tu linatosha,” alisema Edmund huku akionekana kuwa na hasira kali mno.

    Edmund hakujiskia raha hata kidogo, kila alipokuwa akikaa, jina la Walter ndilo lililokuwa likimjia kichwani mwake. Akatokea kumchukia mwanaume huyo hata kabla hajamtia machoni mwake, alijua kwamba huyo ndiye alikuwa mtu pekee ambaye angelikatisha penzi lake kutoka kwa msichana huyo mrembo.

    Hakuwa tayari kuona hilo likitokea, hakuwa tayari kuona akimkosa Catherine kwa kuwa kulikuwa na mwanaume aliyeitwa Walter katika dunia hii.

    Hakuwahi kufikiria kama mwanaume huyo alikuwa Mtanzania, alichohisi ni kwamba alikuwa Muingereza hivyo kuanza kufuatilia chini kwa chini huku wakati mwingine akiuliza kama kulikuwa na mwanaume aliyekuwa na jina hilo.

    Baada ya miezi minne kupita huku akiendelea kuwa katika penzi na Catherine ndipo akapewa taarifa kwamba mpenzi wake huyo alikuwa amepata ajali ya gari baada ya kugongwa na hivyo kukimbizwa katika Hospitali ya Queen Elizabeth.

    Alichanganyikiwa, kama kichaa akaondoka nyumbani kwao na kuelekea katika hospitali hiyo. Alipofika, akauzuiliwa kwa kuwa msichana huyo alikuwa katika chumba cha upasuaji akipewa matibabu.

    “Ilikuwaje?” aliuliza Edmund huku macho yake yakiwa mekundu mno na machozi kumtiririka mashavuni mwake.

    “Alipata ajali ya gari!”

    “Aligongwa au?”

    “Alikuwa ndani ya gari lake, likagongwa na mgongaji kukimbia,” alijibu kijana aliyeishuhudia ajali hiyo ambaye ndiye alishughulika na watu wengine kumkimbiza msichana huyo katika hospitali hiyo.

    Moyo wake ukachoma sana lakini hakuwa na jinsi. Siku hiyo hakuweza kumuona msichana huyo na hata wazazi wa msichana huyo walipofika, walimsifu Edmund kwa moyo wake kujitolea kuwa mtu wa kwanza kufika hospitalini hapo.

    Siku iliyofuata ndipo wakaruhusiwa kumuona msichana huyo. Alikuwa ameumia vibaya kichwani mwake huku akiwa amefungwa bandeji kubwa kichwani na kwa maelezo ya madaktari waliwaambia kwamba fuvu la kichwa chake lilikuwa limepata ufa ambapo kwa kitaalamu lilijulikana kama skull fracture.

    “Atapona?” aliuliza Bwana Gordon.

    “Ndiyo! Kwa kawaida fuvu la kichwa likipata ufa, maumivu huwa kwa siku saba mpaka kumi, baada ya hapo mgonjwa atakuwa kwenye hali ya kawaida na ili fuvu lirudi katika hali ya kawaida, itamchukua miezi zaidi ya ishirini na nne, ila akiwa chini ya uangaliazi,” alisema Dk. Wayne.

    Hizo zilikuwa ni kama siku za mateso kwa msichana huyo, alikuwa kimya kitandani na hata baada ya kuyafumbua macho yake hakuweza kuzungumza lolote lile, alikuwa kimya huku akiwaangalia watu waliokuwa katika chumba chake.

    Siku ziliendelea kukatika, msichana huyo aliendelea kupatiwa matibabu hospitalini pale na baada ya siku tatu, Walter na Walker wakafika hospitalini hapo. Siku hiyo ilikuwa kizaazaa, kila mtu aliyekuwa akiwaona, alitaka kupiga nao picha, walikuwa maarufu, watu waliokuwa na vipaji ambavyo havikuwa vya kawaida kabisa.

    Kwa kuwa muda wa kuona wagonjwa ulikuwa umefika, wakaruhusiwa kwenda moja kwa moja katika chumba kile. Edmund aliwaona lakini hakuwajua, alikuwa bize na masomo na hakuweza kufuatilia mambo ya habari au yale yaliyokuwa yakiendelea katika mitandao ya kijamii.

    Aliwashangaa wanaume hao lakini wazazi wa Catherine walikuwa wakiwakumbuka vizuri, walikuwa marafiki wa binti yake. Kidogo Walter alipomuona Catherine kitandani pale moyo wake ukafurahi, wakamsogelea na kisha kumshika mkono.

    Edmund alikuwa kimya akifuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Catherine aliposhikwa mkono, akayafumbua macho yake, tabasamu pana likamjia usoni mwake.

    “Walter! Atlast you have come to see me,” (Walter! Hatimaye umekuja kuniona) alisema msichana huyo huku tabasamu pana likiendelea kuonekana usoni mwake. Edmund aliposikia jina la Walter tu, akashtuka, mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda kwa nguvu, hakuamini kama mmoja wa mapacha wale walioungana alikuwa Walter ambaye Catherine alisema wangeachana kama tu mwanaume huyo angerudi maishani mwake.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kupatikana kwa Walter kulimaanisha kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa uhusiano wake na msichana Catherine aliyekuwa kitandani. Moyo wa Edmund uliuma na kuchoma sana, kila alipokuwa akimwangalia mwanaume huyo ambaye aliungana na pacha mwenzake kulimaanisha kuwa huo ndiyo ungekuwa mwisho, yaani alitakiwa kusahau kila kitu kilichokuwa kimetokea.

    Hakutaka kukubali, kwa wakati huo alikuwa tayari kupoteza kila kitu isipokuwa kumpoteza Catherine ambaye kila alipokuwa akimwangalia, kila siku uzuri wake uliongezeka maradufu.

    Japokuwa alikuwa kitandani lakini kitendo cha kumuona Walter akiwa amefika mahali hapo, Catherine akaonekana kuwa na furaha mno, furaha ambayo Edmund mwenyewe alikiri moyoni kwamba hakuwahi kumuona msichana huyo akiwa kwenye furaha kama siku hiyo.

    “Nilikukumbuka sana,” alisema Catherine huku akimwangalia Walter machoni.

    “Nilikukumbuka pia. Sikutaka nione ukiendelea kuwa kwenye matatizo halafu mimi nipo. Nitahakikisha nakulinda maisha yangu yote,” alisema Walter.

    Wazazi wa pande zote tatu walibaki wakiwaangalia watu hao, kadiri muda ulivyozidi kwenda mbele ndivyo ambavyo Edmund alivyozidi kuumia. Hakukuwa na mtu aliyefahamu kile walichokuwa wameongea zaidi ya wao wawili tu.

    Alivumilia tu kukaa na hata alipokuwa akitambulishwa, alijibaraguza kwa kuonekana kuwa na tabasamu pana na wakati moyo wake ulikuwa ukiwaka moto kwa wivu.

    Hakutaka kubaki mahali hapo, akaondoka na kurudi nyumbani. Ndani ya gari, alikuwa akilia kama mtoto, hakuamini kilichokuwa kikiendelea. Uwepo wa Walter ulimaanisha kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa maisha yake.

    Alipofika nyumbani, akajifungia chumbani na kuanza kulia. Alipenda mpaka kufikia hatua ya mwisho kabisa, hatua ambayo aliona ikivuka hapo angekuwa kichaa, mapenzi yaliuendesha moyo wake, yalimsumbua kupita kawaida na ndiyo maana alipogundua kwamba mwanaume aliyekuwa amemuona alikuwa Walter, alihisi kitu chenye ncha kali kikiuchoma moyo wake.

    “I must kill him,” (ni lazima nimuue)

    Huo ndiyo ulikuwa uamuzi alioufikia kipindi hicho, hakutaka kuona akimkosa Catherine kwa sababu ya Walter, alitamani kuendelea kulilinda penzi lake lakini si kuona likipotea na kuchukuliwa na mtu mwingine.

    Alichokifanya ni kuanza kufikiria ni watu gani ambao angewatumia kwa ajili ya kumuua Walter. Ilikuwa ni lazima afe kwani aliamini kwamba kama asingemuua basi ingekuwa ngumu sana kwake kuendelea na msichana huyo.

    Wazo ambalo lilimjia kichwani lilikuwa ni kuwamaliza kwa kuwekea sumu ndani ya gari alilokuwa akilitumia. Alijua kwamba ilikuwa ni lazima kwa mwanaume huyo kufika hospitalini hapo mara kwa mara hivyo kama angeweka sumu, wakati wanaingia ndani ya gari, kuwashwa na kiyoyozi kuwashwa basi sumu ienee ndani ya gari na mwanaume huyo kufa.

    “Yeah! I can use Hydrogen Selenide to kill him through air condition,” (Yeah! Naweza kutumia Hydrogen Selenide kumuua ndani ya gari lake)

    Huo ndiyo ulikuwa mpango wake, hakutaka kujua ni watu wangapi angewaua mara baada ya kuweka sumu hiyo katika gari hilo, kitu alichokuwa akihitaji ni kuona anammaliza mwanaume aliyetokea kuumiza moyo wake.

    Kuipata sumu hiyo kali halikuwa jambo jepesi, kulikuwa na ugumu sana na ilihitaji kupata barua maalumu kutoka serikali ambayo ingeeleza sababu ya yeye kuihitaji sumu hiyo ili kama kutaonekana hakukuwa na msingi wowote wa kupewa, basi asipewe na kama angepewa wakati wa kutumia ilikuwa ni lazima mtu wa serikalini awepo mahali husika.

    Aliuona ugumu huo hali iliyomfanya kuwasiliana na rafiki yake, Thomson ambaye baba yake alikuwa daktari mkuu katika Hospitali ya The Royal London, alihitaji Thomson afanye kila linalowezekana mpaka baba yake ampe sumu hiyo ya gesi na kwenda kuitumia kumuua Walter.

    “I will talk to him,” (nitazungumza naye)

    “I just need your help Thom,” (ninahitaji msaada wako Thom) alisema Edmund huku akionekana kweli kuhitaji msaada.

    “I will give you a hand,” (nitakusaidia)

    Wakakubaliana na kuondoka mahali hapo. Thomson hakutaka kwenda kumuomba baba yake sumu hiyo kwani aliamini kuwa ni lazima amkatalie, alichokifanya ni kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha anaiiba sumu hiyo hospitalini kwa kuchukua mtungi mdogo na kuondoka nayo.

    Hilo ndilo alilolifanya, siku iliyofuata akaenda katika hospitali aliyokuwa akifanya kazi baba yake kwa lengo la kumsaidia kumbe upande mwingine alikuwa na jambo jingine kabisa alilotaka kulifanya.

    Alipofika huko, akasalimiana na baba yake na muda wa kuondoka, akaanza kwenda maabara ambapo aliamini kwamba ni lazima gesi hiyo ingekuwa mahali huko.

    Hakuonekana kuwa na hofu, hata madaktari waliokuwa wakimuona akielekea katika maabara ile hawakuwa na hofu naye kwani hiyo haikuwa mara ya kwanza kwenda huko, alikuwa akifika mara kwa mara na kuingia katika maabara hiyo.

    Alisalimiana na watu mbalimbali mpaka alipoufikia mlango na kuingia ndani. Humo akakukatana na watu zaidi ya thelathini ambao walikuwa wakisomea uuguzi na walikuwa humo kwa ajili ya kuonyeshwa vitu mbalimbali kwa vitendo.

    Naye akajifanya kuungana nao, macho yake hayakutulia, yalikuwa yakiangalia huku na kule, alipoiona mitungi ya gesi na mingine midogo kama fire extinguisher zile zinazokaa kwenye pikipiki, akaona kwamba hiyo ndiyo ilikuwa nafasi yake.

    Wanafunzi wale walichukua dakika arobaini, walipomaliza wakaondoka na haraka sana Thomson kwenda kule kulipokuwa na mitungi ile. Kabla ya kuichukua, akaanza kuisoma ili kuipata gesi ya Hydrogen Selenide.

    “Haipo!” alisema mara baada ya kuangalia sana.

    “Nitrogen trioxide, Nitrosyl chloride, sasa nichukue ipi kama Hydrogen Selenide haipo?” alijiuliza, lakini hata kabla hajajijibu, akaichukua Nitrosyl chloride na kuuingiza ule mtungi mdogo ndani ya begi lake na kuondoka ndani ya maabara ile.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Akamfuata Thomson na kumkabidhi, akamwambia jinsi ambavyo ilitakiwa kutumika. Alimpa maelekezo kwamba ni lazima achukua mpira, aitoboe na haraka sana aingize mpira katika tundu la gesi ile kisha kuanza kuichukua kwa kuiweka katika kiyoyozi cha gari na kukaa humo, kiyoyozi kama kingewashwa, basi gesi hiyo ingetoka na kummaliza audui yake ndani ya gari.

    “Nashukuru sana!” alisema Walter na kumpa Thomson zawadi ya paundi elfu mbili ambazo ni zaidi ya milioni nne kama shukrani kwa kile alichomfanyia.

    ****

    Kila Muingereza alijua kwamba Walter na Walker walikuwa nchini Uingereza. Watu wengi walijazana katika Hospitali ya Queen Elizabeth kwa ajili ya kuwaona mapacha hao waliokuwa gumzo kila kona duniani.

    Wale waliokuwa katika miji mingine kama Liverpool, Newcastle, Manchester na sehemu nyingine wakaondoka kuelekea jijini London kwa ajili ya kuwaona mapacha hao waliokuwa na vipaji visivyo vya kawaida.

    Walikuwa ndani ya hospitali hiyo huku watu wengi wakiwa nje. Kila mtu alitamani kwenda kuwaona lakini hakukuwa na mtu aliyepewa nafasi, wengi wakaambiwa kwamba walitakiwa kusubiri mpaka watu hao watakapoondoka, wawapige picha kwa mbali lakini si kuwasogelea.

    Polisi walikuwa makini, kuwalina Walter na Walker haikuwa kazi ndogo hata kawaida. Watu walisumbua, walipata kazi kubwa ya kuwalinda kuhakikisha hakuna mtu mbaya yeyote ambaye anawasogelea na kuwafanya kitu chochote kile.

    "Tunataka kuwaona! Mbona jana nasikia watu waliowaona hapa hospitali ila leo mnatukatalia?” alihoji jamaa mmoja, alionekana kuwa na hasira.

    “Nyie subirini! Jana ni jana na leo ni leo!”

    “Haiwezekani bwana. Yaani kuwaona mnataka mpaka tufanye fujo?” alihoji jamaa huyo.

    Ilikuwa kazi ngumu kuwaona watu hao. Walter na Walker waliendelea kukaa hospitalini huku wakimfariji Catherine aliyekuwa ameanza kupata nafuu, ilipofika majira ya saa kumi na moja jioni, kama kawaida wakatoka tayari kwa kuondoka mahali hapo.

    Walipotoka nje, polisi wakafanya kazi ya ziada kwani kila mmoja alitaka kuzungumza nao huku wengine wakiwa na vitu vyao kwa ajili ya kusainiwa. Kwa mwendo wa taratibu, wakaanza kusogea kule watu walipokuwa na kuanza kusaini vitabu vyao huku wengine wakiwapiga picha.

    Waliwafurahisha watu, walipomaliza, wakaanza kupiga hatua na wazazi wao kuelekea katika maegesho ya magari kwa ajili ya kuondoka mahali hapo. Dereva alikuwa ndani ya gari hilo, alikuwa amelala, wakaufungua, hawakujali sana, walichokifanya ni kuufungua mlango wa gari hilo lililokuwa limefungwa vioo, hata kabla ya kuingia ndani, hapohapo wakaanguka chini, wakaanza kutoka mapovu na miili kuwatetemeka.

    Kila mtu aliyekuwa mahali hapo alishangaa, wazazi wao wakasogea kuangalia kulikuwa na kitu gani kilichokuwa kimewapata lakini nao waliposogea, wakaanza kusikia kivunguzungu, nao hapohapo wakaanguka kitu kilichomshtua kila mtu aliyekuwa mahali hapo, hakukuwa na mwingine aliyelisogelea gari lile kwani tayari kukaanza kusikika harufu fulani ambayo haikuwa ya kawaida.



    Edmund alidhamiria kufanya mauaji, hakutaka kufikiria utu, aliamini kwamba kama Walter angekufa basi ingekuwa rahisi kwake kuendelea kuishi na Catherine ambaye alikuwa akimpenda kwa mapenzi ya dhati.

    Sumu yake aina ya Nitrosyl chloride alikuwa nayo chumbani kwake, ilikuwa ni lazima kwenda kwenye gari la mapacha hao walioungana kwa ajili ya kuiweka na kisha kuondoka zake.

    Hakutaka kuchelewa, kwa kuwa siku hiyo Walter, Walker na wazazi wao walikuwa wakienda hospitalinikatika Hospitali ya Queen Elizabeth kwa ajili ya kumuona Catherine, naye akapanga kwenda huko kwa muda wake.

    Aliamini kwamba huko kungekuwa na watu wengi, hakutaka kwenda kikawaida, alifahamu jinsi polisi walivyokuwa wakivaa, suala la kutafuta sare wala halikuwa gumu kwani aliwasiliana na rafiki yake ambaye alikuwa akishona sare hizo kwa ajili ya kuigiza filamu mbalimbali nchini Uingereza, yeye akampelekea mavazi ya polisi ambayo kwa kuyaangalia kwa mbali, hayakutofautiana mpaka pale utakapoyachunguza zaidi.

    Akaingia ndani ya gari lake na kuondoka huku akiwa na mtungi huo mdogo. Hakuchukua muda mwingi akafika katika hospitali hiyo, ni kama watu walijua kwamba mapacha hao walioungana wangefika hapo, wengi walikusanyika kwa ajili ya kuwashuhudia tena.

    Edmund hakuteremka katika gari lake, alitulia huko huku moyo wake ukichoma kupita kawaida, baada ya kukaa kwa saa moja, akayaona magari yakianza kuingia hapo, akabaini kwamba gari moja lilikuwa limewabeba mapacha wale, hivyo akaanza kufuatilia.

    Watu wakaanza kusogea kule kulipokuwa na magari yale huku wakiwa na simu zao mikononi na wengine wakiwa na kamera, walitaka kupiga picha kila kitu kilichokuwa kikiendelea mahali hapo.

    Baada ya dakika kadhaa, mapacha hao wakateremka huku wakiwa na ulinzi mkubwa, kama kawaida yao wakaanza kuwapungia watu mikono huku wakipiga hatua kuelekea ndani.

    “Can you sign an autograph on my book, pleaseee?” (unaweza kusaini kwenye kitabu changu?) aliuliza msichana mmoja kwa sauti ya upole kabisa, japokuwa kulikuwa na ulinzi mkubwa, yeye alifanikiwa kupenya, na walinzi walipotaka kumtoa, Walke akawazuia.

    “Mine or his?” (yangu au yake?) aliuliza Walker.

    “Both of you,” (nyie wote)

    “Okey.” (sawa)

    Hilo halikuwa tatizo, wakafanya kama msichana huyo alivyotaka na kisha kupiga naye picha na kuanza kuelekea ndani ya hospitali hiyo. Bwana Cassian na mkewe, Naseku walikuwa na furaha kupita ajabu, hawakuamini kama watoto wao walikuwa wakikubalika kiasi hicho japokuwa walionekana kuwa na matatizo.

    Wakati watu wakiwa bize, haraka sana Edmund akateremka kutoka kwenye gari lake na moja kwa moja kuanza kusogea kule gari lililokuwa limewabeba mapacha wale lilipokuwa huku mkononi akiwa na mtungi wa gesi.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alipofika, akaangalia ndani, akamuona dereva akiwa anavuta sigara, akaanza kulisogelea gari zaidi, alipolifikia, akakigonga kioo, dereva akafungua.

    “Unajua kwamba unavunja sheria?” aliuliza Edmund huku akimwangalia dereva.

    “Sheria gani?”

    Akamuonyeshea bango dogo lililoandikwa kwamba hakukuwa na mtu aliyekuwa akiruhusiwa kuvuta sigara katika eneo la watu wengi likiwemo hospitali kama hiyo.

    Haraka sana dereva akaizima sigara yake kwani kwa jinsi Edmund alivyoonekana, jinsi alivyokuwa amevaa sare za bandia za kipolisi, aliamini kwamba mwanaume huyo alikuwa polisi.

    “Samahani sana.”

    “Hebu teremka, nenda nyumba ya gari nikukute huko. Nataka nipekue, unaweza kuwa na bangi au madawa ya kulevya humu,” alisema Edmund, kwa kuwa alikuwa amefanya kosa, haraka sana dereva akafungua mlango na kwenda nyuma, Edmund akaingia ndani, akachukua sumu ile na kuanza kuipulizia katika sehemu ya kiyoyozi, aliipulizia kwa wingi huku kiyoyozi hicho kikiwa kimezimwa, alipomaliza, akafunga mlango.

    “Una bahati sikukuta kitu. Sijakukataza kuvuta, kama utaendelea, hakikisha unafunga vioo, washa kiyoyozi na ndipo uvute, vinginevyo sitokuelewa,” alisema Edmund huku akiwa anamwangalia dereva huyo.

    “Haina shida.”

    Dereva akaingia ndani, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kufunga mlango, kioo kikashushwa, akachukua sigara nyingine, akaiwasha na kuanza kuivuta.

    “Alisema na kiyoyozi,” alisema na hapohapo kuwasha kiyoyozi.

    Hilo likaonekana kuwa kosa kubwa kwani hapohapo sumu iliyokuwa imepuliziwa humo ikaanza kutoka mfululizo. Ilikuwa sumu mbaya ambayo ilikuwa ikiingia mwilini mwa binadamu kwa haraka na kuharibu ini huku ikianza kuusimamisha moyo na kuziba mishipa ya damu.

    Dereva hakuchukua hata dakika moja, palepale alipokuwa, akatulia tuli, mwili ukaanza kukakamaa, mapovu yakaanza kumtoka mdomoni na hatimaye kutulia tuli.

    ***

    Kila mtu aliyekuwa ameliona tukio lile aliogopa, wote wakasogea nyuma kwani hali ilionekana kutokuwa nzuri. Watu walibaki wakiwaangalia Walter na Walker walivyokuwa wakihangaika pale chini walipokuwa na wazazi wao.

    Hakukuwa na mtu aliyetoa msaada zaidi ya watu hao kuanza kupiga picha kana kwamba walikuwa waandishi wa habari. Kwa kuwa ilionekana kama kulikuwa na gesi iliyokuwa imewadhuru, hapohapo wanaume wawili wakajifunga vitambaa puani na mdomoni, wakasogea kule walipokuwa watu wale na kuanza kuwasaidia, machela zikaletwa, wakapakizwa na kuanza kuingizwa ndani.

    “Nini kimetokea?” lilikuwa swali la kwanza alilouliza nesi.

    “Saidia kwanza. Tunahisi ni sumu!”

    “Sumu?””Ndiyo! Husikii harufu ya Nitrosyl chloride? Ni sumu hatari sana hii,” alisema mwanaume mmoja aliyekuwa akitoa msaada.

    Kila mtu akashtuka, dunia ikaingiwa na majonzi mazito, hakukuwa na aliyeamini kile kilichokuwa kimetokea. Kila mtu alikuwa na hofu, wengi wakaona kwamba huo ndiyo ulikuwa mwisho wa mapacha wale.

    Lawama zote zilikwenda kwa Waingereza, ilikuwaje washindwe kuzuia jambo hilo na wakati walijua kabisa kwamba watu hao walikuwa maarufu hivyo kungekuwa na watu wengi waliotaka kuwaua kwa kuwa tu waliwaoneka wivu?

    Kila mmoja akahisi kwamba kulikuwa na kiongozi mkubwa serikalini alikuwa amehusika katika tukio hilo la mauaji. Waziri mkuu nchini humo, Bwana Sinclaire hakutaka kuchelewa, haraka sana akawaita waandishi wa habari na kuwaomba msamaha kwa lililotokea lakini pia ilikuwa ni lazima kuhakikisha kwamba mtu aliyefanya tukio hilo akipatikana haraka iwezekanavyo.

    “Na hali zao?” aliuliza mwandishi mmoja.

    “Bado sijajua chochote kile kwa kuwa baada ya kupewa taarifa nikawaita kwa ajili ya kuzungumza nanyi,” alisema Bwana Sinclaire huku akiwaangalia waandishi waliokuwa wamemzunguka.

    Hospitalini hakukukalika, kila mtu alikuwa na hofu, sumu ambayo walikuwa wamepuliziwa ilikuwa ni sumu hatari ambayo ilikuwa ikitumika kuulia wanyama wakubwa msituni na samaki baharini.

    Kitendo cha kuwapata kidogo tayari ilionyesha nguvu zake kiasi kwamba walianguka na kupoteza fahamu huku hali ya miili yao ikianza kubadilika ghafla pamoja na wazazi wao.

    Madaktari walikuwa na kazi kubwa kuokoa maisha ya mapacha hao na wazazi wao. Haraka sana wakawapeleka katika chumba cha upasuaji na kuanza kuwahudumia haraka sana. Ilikuwa kazi kubwa kwani walitakiwa kwanza kuondoa sumu ile ambayo ilikuwa ikisambaa taratibu katika miili yao.

    Wakawatundikia dripu zilizokuwa na maji yaliyotiwa dawa ambazo zilikuwa na uwezo wa kuruhusu matone kumi na tano kwa dakika moja tu.

    “Hii itawasaidia!” alisema daktari mmoja.

    “Kweli?” aliuliza nesi.

    “Ndiyo! Ila hatutakiwi kuamini sana kwani kadiri dakika zinavyozidi kwenda mbele, mapigo yao yanazidi kushuka,” alisema daktari huyo.

    “Kwa hiyo wanaweza kufa?”

    “Uwezekano wa kupona ni asilimia thelathini na kufa ni asilimia sabini. Cha msingi ni kumuomba Mungu tu,” alisema daktari huyo, pamoja na utaalamu wake mkubwa lakini kwa sumu waliyokuwa wamepuliziwa watu wale, ilionekana kumshinda.

    Serikali ikaamua kuongeza madaktari wengi kumi kutoka katika hospitali nyingine. Ilikuwa ni lazima wapambane usiku na mchana kuokoa maisha ya watu hao kwani kama wangekufa katika ardhi yao ingekuwa aibu sana dunia nzima hivyo iwe isiwe ilikuwa ni lazima kupambana kuokoa hali zao.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Polisi jijini London walichanganyikiwa, hawakuamini kile kilichotokea kama kweli kilitokea katika ardhi ya Uingereza. Kila mtu alikuwa akizungumza lake, wengi waliona nchi hiyo ikiwa na uzembe mkubwa kiasi kwamba walishindwa kuweka ulinzi wa kutosha kuhakikisha vijana hao wanakuwa salama mpaka pale ambapo wangeondoka nchini humo.

    Haraka sana, mkuu wa jeshi la polisi nchini humo, Bwana Simon Pegg akazungumza na kitendo cha Usalama wa Taifa, Military Intelligence Section 6 kwa lengo la kutaka kujua kila kitu kilichokuwa kimetokea.

    Haraka sana maofisa wa Usalama wa Taifa wakaanza kufanya kazi hiyo. Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kwenda mpaka katika hospitali hiyo kwa lengo la kuangalia kwenye kamera kila kitu kilichokuwa kimetokea.

    Walipofika huko, wakapelekwa katika chumba kilichokuwa na televisheni ambacho kiliunganishwa na kamera thelathini na sita zilizokuwa katika hospitali hiyo.

    Walitaka kujua kila kitu kilichokuwa kimetokea tangu mapacha hao walipofika katika hospitali hiyo mpaka tukio la kuupatwa na sumu lilivyotokea. Hilo halikuwa tatizo, kila kitu kilikuwa kimerekodiwa na kilichofanyika ni kuonyeshwa kila kitu kilichotokea.

    Walianza kufuatilia. Dakika kumi kabla ya mapacha hao kufika mahali hapo wakaanza kuangalia mazingira jinsi yalivyokuwa. Hakukuwa na mtu yeyote ambaye walimtilia shaka, kila aliyekuwa mahali hapo alionekana kuwa na hamu kubwa ya kuwaona mapacha hao na ndiyo maana kila mmoja alishikilia simu yake tayari kwa kupiga picha.

    Baada ya dakika kadhaa, wakayaona magari yaliyokuwa kwenye msafara mfupi wa mapacha hao ukianza kuingia ndani ya eneo la hospitali hiyo. Kila mmoja alikuwa akiyaangalia kwa makini mpaka pale yalipokwenda kupaki.

    Waliwaona walipokuwa wakiteremka, lengo lao halikuwa kuwaangalia mapacha hao bali lengo lao kubwa ni kuangalia ni nani alikuwa amekwenda katika gari lile baada ya mapacha hao kuteremka.

    Wakati wameelekea ndani, wakamuona polisi mmoja akiteremka katika gari lake huku mkononi akiwa na kitu ambacho hawakuwa wakikifahamu kwa kuwa ilikuwa ni picha ya mbali kabisa.

    Polisi yule akaanza kutembea mpaka lilipokuwa gari lile walilokuwa mapacha wale na kuanza kuzungumza na dereva. Hawakujua walizungumza kitu gani lakini baada ya dakika moja wakamuona dereva akiteremka na kuelekea nyuma ya gari na polisi yule kuingiza kichwa kwa ndani.

    “Hebu vuta kwa karibu, vuta zaidi,” alisema Bwana Pegg ambaye naye alifika kwa ajili ya kuangalia.

    Picha ya karibu ikavutwa zaidi, halafu akamwambia arudishe nyuma na kisha kutakiwa kuvuta kile kitu kilichokuwa mkononi mwake, walitaka kujua kilikuwa kitu gani. Kilipovutwa, hakukuwa na mtu aliyeamini, ulikuwa mtungi mdogo wa gesi kali aina ya Nitrosyl Chloride iliyokuwa ikitumika kuulia samaki baharini na wanyama wakali.

    “Huyu ndiye aliyeweka hiyo gesi ambayo imekuwa sumu. Hebu mvute karibu. Ni polisi kweli huyu?” aliuliza.

    Jamaa aliyekuwa ameshikilia kipanya akaanza kuvuta picha kwa karibu zaidi. Walikuwa wakitaka kuona kama kweli huyo alikuwa polisi au la. Alipovutwa, waliangalia sare zake, hazikuwa origino kama za polisi wengine kitu kilichomaanisha kwamba mwanaume huyo ndiye aliyefanya tukio hilo la kuwamaliza mapacha hao.

    “Vuta sura yake, piga picha halafu anza kupeleka sehemu zote. Nahitaji ndani ya nusu saa mtu huyo awe amekamatwa,” alisema Bwana Pegg na hapohapo picha ya Edmund kuchapishwa na kuanza kupelekwa sehemu mbalimbali, hasa katika vituo vya polisi.

    Na kwa sababu waliipata picha ya sura yake, walichokifanya ni kutaka kupata data zote kuhusu mwanaume huyo ambaye waliamini kwamba kama alikuwa ni rais wa Uingereza basi ilikuwa ni lazima kujiandikisha kama rais wa nchi hiyo na hivyo kuwa na data zake zote.

    Wakaiingiza picha ile katika kompyuta ambayo ilikuwa na taarifa ya raia wote wa Uingereza na kuanza kumtafuta mwanaume huyo. Zaidi ya picha elfu moja zilikuwa zikipita ndani ya sekunde sitini na baada ya dakika tano, picha yake ikasimama na neno kubwa lililosomeka Match 100% likionekana vizuri kwamba picha ile iliyokuwa imeingizwa ilifanana kwa asilimia mia moja na picha iliyokuwa ikionekana.

    “Anaitwa Edmund Jefferson. Anaishi hapa Londo katika Mtaa wa Camberwell nyumba namba 297. Kikosi cha askari ishirini wanatakiwa kwenda huko haraka sana,” alisema Pegg na hivyo kikosi cha kwenda huko kupigiwa simu na kutumiwa picha ya mtu aliyekuwa akitakiwa na maelezo yote kuhusu yeye.

    ***

    Kidogo moyo wa Edmund ukajisikia amani, akahisi kwamba alifanikiwa kwa asilimia mia moja kufanya jambo lile lililompa uhakika kwamba mbaya wake, Walter alikufa katika gesi ile kali.

    Akaondoka hospitalini hapo, njiani, redioni ni taarifa za mapacha hao ndizo zilzokuwa zikisikika kila kona kwamba walikuwa wamekufa. Wakati dunia ikihuzika na kulia, kwake hali ilikuwa ni tofauti kabisa kwani moyo wake ulikuwa na furaha kupita kawaida.

    Alipofika nyumbani, hakutaka kubaki mahali hapo, ilikuwa ni lazima kuondoka nchini humo kwa kuamini kwamba mara baada ya kugundulika ilikuwa ni lazima kutafutwa kila kona. Akachukua baadhi ya vitu vyake na kuondoka zake huku lengo lake kubwa likiwa ni kuelekea nchini Ireland ambapo aliamini kwamba huko angeishi kwa amani kabisa.

    Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumpigia simu rafiki yake, Thom na kumshukuru huku akimwambia kwamba alikuwa akijiandaa na safari ya kuelekea nchini Ireland.

    “Nimefanikisha. Nashukuru sana,” alisema Edmund, akachukua begi lake lililokuwa na baadhi ya vitu na kuondoka mahali hapo.

    Akaingia ndani ya gari lake, akaliwasha, hakutaka kuaga, alipoingia barabarani tu, akasikia ving’ora vya polisi kwa mbali, akapishana nao, yaani wakati yeye akiondoka nyumbani kwao, nao ndiyo walikuwa wakiingia.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hamuwezi kunipata!” alisema Edmund huku akitoa tabasamuu pana ambapo alipokuwa akiangalia nyuma kupitia kioo cha gari cha pembeni, akawaona polisi wakiingia katika eneo la nyumba yao. Akaongeza gia na kukanyaga moto. Akapotea eneo hilo.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog